Asalaam za siku nyingi wana JF.
Nilipotea kwa muda mrefu humu jamvini hii ni kutokana na shughuli za ujenzi wa taifa.
Leo napenda kuzungumzia kwa kifupi kuhusu mwenendo wa siasa zetu za hapa bongo. Hatua tuliyofikia kisiasa ni mbaya sana hatuna tofauti na wanyama, tunafanya siasa za uhasama, siasa za kulipiza kisasi, siasa za kudharau utu wetu wenyewe, imefikia hatua ya kuwatumia marehemu waliotangulia mbele za haki.
Ukweli ulio wazi, baadhi ya ndugu zetu wa CCM wamejivua utu hawawaheshimu ndugu zao waliotangulia kana kwamba wao hawaelekei huko. Juzi nilimsikia kada mmoja wa chama kipya cha ACT kupitia Star TV akisema, "ana uhakika Chacha Wangwe RIP aliuawa na Chadema", nikajiuliza polisi wako wapi na yeye alikuwa wapi kupeleka ushahidi huo mahakamani wakati wa kesi hadi kupelekea Deusi Mallya kufungwa kwa zaidi ya miaka mitatu. Leo tena nimesikia Antony Diallo mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mwanza anataka kumtumia Mallya huyo huyo aliyefungwa kwa kesi ile ile kuendelea kumtumia marehemu Wangwe.
Hizi siasa za kutumia marehemu zimetoka wapi? nani mwanzilishi wake? na zinatupeleka wapi.
Naomba kuwaasa wana CCM wanapoanza kufukua makaburi wasije kujilaumu hapo baadaye wakati makaburi ya ndugu zao yatapoanza kufufuliwa.
Niwakumbushe tu kama CCM wako tayari kutuambia nani alisababisha kifo cha Kolimba, nani alimuua Sokoine, kina nani wako nyuma ya kifo cha Imran Kombe. Kwani Karume Sr. aliuawa na nani? Tukiachilia mbali vifo vyenye utata kama vya (RIP) Malima, Prof Shaba, Dr. Mvungi, Prof. Harub Othman, Prof. Chachage, na wengine wengi, CCM wanaweza kututhibitishia baba wa taifa alikufa tarehe ngapi? Ni maswali mengi ya kujiuliza lakini ukiangalia kwa undani hayana msingi wowote. Tuache kutonesha vidonda.
CCM kama chama au mtu yeyote anayefanya siasa za marehemu aache mara moja kuwatumia marehemu ndugu zetu wapendwa kwenye siasa zao chafu. Kama kuna mtu anapenda sana kutumia marehemu basi awatumie wazazi wake au ndugu zake waliotangulia mbele ya haki. Inasikitisha.
Naomba kuwasilisha.