Bw. Waziri Mkuu Pinda

Iga

Senior Member
Dec 17, 2007
112
6
Bw. Waziri Mkuu Pinda:
Dar imekithiri uchafu

MBAGALA imeshughulikiwa kwa kasi ya ajabu ijapokuwa bado kuna kizaazaa cha hapa na pale kule.Ni dhahiri kuwa Dar kama unapatikana utashi wa kisiasa, menejimenti safi na viongozi wanaotambua kuwa usafi na mazingira bora ni sawasawa au hata zaidi ya rasilimali nyingine na kwamba usafi na mazingira bora yanaweza kututajirisha basi inaweza ikawa jiji kama Hongkong, Singapore, Shangai au Dubai hapa Afrika. Kinachonishangaza mimi ni kwamba sijawahi kuwasikia Waziri Mkuu wala Waziri husika na Mazingira kuzungumzia suala la uchafu uliokithiri Dar.

Je, katika mafaili yanayokwenda mezani kwa wakuu hawa ina maana kila moja linasifia Dar kwa usafi ?

Ninapenda kuwajulisha wakuu hao kwamba hali ilivyo ni kinyume cha hivyo. Na leo wakazi wa jiji hili wanawakumbuka Sumaye na Keenja sio kwa mengine ila kwa jitihada zao zilizochangia sio haba kuleta hali iliyofanana na usafi na ustaarabu jijini hapa.

La kusikitisha ni kuwa toka kuondoka awamu ya tatu hii awamu ya sasa imekuwa ni ya maneno matupu na wananchi wa Kunduchi, Kijichi, Kigogo, Vigunguti na madampo yasiyo rasmi jijini hapa wanazidi kuwinda na mabomu ya kimyakimya kama yale ya Mbagala huku wakuu wetu wakiwa hawana habari.

Nina maswali machache kwa waziri mkuu:
1. Je, makampuni yaliyopewa kazi ya kuchangia usafi wa jiji si makampuni ya wababaishaji na wachovu wa hali na mali ?
2. Je, hawawezi kupatikana wakandarasi wenye uwezo wa kuifanya kazi yenyewe kikamilifu na kuridhisha serikali na wananchi ?
3. Hawa wenye makampuni yanayojidai kufanza usafi jijini wakati yanachafua ni kina nani ? Walipewa kandarasi na nani na kwa namna gani ?
4. Kuna vigezo na sifa muhimu zinazotakiwa ili mtu apewe kazi ya usafi wa jiji na nani anayevikagua na kupitisha ?
5. Je, dampo la Kigogo likihamishiwa huko wakuu wetu mnakoishi nyie, wake zenu na watoto wenu kweli mtalala ?
6. Hivi tunahitaji misaada toka nje kuweka jiji letu katika hali ya usafi ?
7. Hivi rais si anakuwa Alinacha kama sio msanii wa kimataifa kusikika akitaka jiji liwe na mvuto kwa utalii huku hakuna anayejali hali ya usafi wa jiji lenyewe ?
8. Hivi mkuu unaelewa kwamba asilimia 70 au zaidi ya nyumba kati ya jiji haina mifumo ya kuondoa maji chafu na vinyesi kwenda panapostahili na badala yake vinyesi hivyo vinaelea katikati ya eneo la CBD ?
9. Hivi wataalamu wetu wa mifumo ya kupitisha maji ya mvua na maji chafu wana elimu na ujuzi unaostahili ? Kama wanazo sifa zinazostahili inakuwaje hapa Dar ambako bahari na makazi na maofisi ni pua na mdomo ? Itakuwaje mkihamia Dodoma ?
10. Kwamba serikali na chama vingehamia Dodoma mngetupunguzia vyoo kujaa kama mmeshindwa kukarabati mifumo iliyopo mnabaki hapa ya nini ?
11. Kipindupindu kimeanza magharibi ya Tanzania na kwa hali hii tusubiri siku mbili tatu kabla hakijaingia mashariki ?
12. Ni busara gani iliyotumika kcuhagua watu wanaotaka kujionesha badala ya kusimamia jiji kuwa safi na mazingira salama na bora kuwa ndio viongozi wa mambo ya mazingira ?
13. Hivi hii siku ya mazingira si wamewekewa mataahira wanaodhani usafi na utunzaji mazingira ni jambo la siku moja kwa mwaka. Hivi wao wenyewe wanaofanya na kuhakikisha usafi na mazingira bora ni kitu cha kila siku si wanatusanii na kuthibitisha dhana yao kwamba sisi ni feki kwelikweli ?
14. Wizara 30 nchini tena hapa jijini lakini jiji linashindwa na miji kama Arusha, Moshi, Mwanza, Iringa hivi hii sio ishara ya uchafu ulioko katika vichwa vya baadhi ya wale tunaowaita viongozi wetu. Maana hali ya nje kwa taaluma ya saikolojia ni kielelezo cha kutosha cha kile utakachokiona nje. Kwa hiyo uchafu, harufu mbaya na uoza tunaouona katika mazingira yetu ni ushahidi tosha kuwa vichwa vyetu pia vina uchafu, harufu mbaya na uoza kama huu hu u wa huku nje. Katika hali chagueni na mchague wallahi hakuna kitakachobadilika ?
15. Je, huu uchafu wa mazingira unaosababishwa na sauiti za matangazo na kammpeni zisizo na nidhamu wala ustaarabu tena zinazofanywa na makampuni makubwa yenye heshima na majina hapa nchini, unajulikana kwenu wakubwa au ni sisi tu tunaoishi huku vichungani ndio tunaokosa starehe ya usingizi tulivu ?
16. Huu uchafu wa magari na mitambo mingine uliozagaa jijini ndio umekuwa badala ya bustani na maua ?
17. Hii hali ya kuwa na vijiji kutokana na giza kubwa usiku katikati ya jiji ndio maendeleo?
18. Hivi takataka za kompyuta na vifaa vingine vya elektroniki wakuu mnajua vinakotupwa au wizara ya mazingira inamruhusu ndugu waziri kukaa nyuma ya kiyoyozi kwa saa zote za kazi bila kuyaona na kujifunza mazingira yake ? Au hii ndio mojawapo ya zile wizara za ziada za mtu kupewa zawadi lakini hakuna kazi ya kufanya ?
19. Hivi jiji linashindwa kweli kuwa na utaratibu ama peke yake au kwa kutumia makampuni yenye sifa na uwezo wa kuwa na matrela ya kubeba kontena kubwa zinazochukua taka zilizochambuliwa- chupa peke yake, karatasi peke yake, nailoni peke yake na kadhalika ? Kisha kwa kushiriikiana na nchi zilizoendelea katika shughuli za 'recycling' kama vile Norway, Japan, Switzerland, Seychelles, Mauritius kuwa na mitamba ya kurecycle takataka kuwa mali ? Ni laki ngapi ya wakazi wa jiji hili watapata ajira kutokana na hilo? Au kuna ukweli kuwa wanaotaka kuleta mitambo ya recycling nchi hii wanalazimishwa eti kuwafanya baadhi ya viongozi wa serikali kuwa wabia wao na wao hawakubal hilo?
20. Na swali la mwisho Bw. Waziri Mkuu hivi wewe na serikali yako mnajua kwamba usafi na mazingira bora peke yake unaweza kuuza jiji na nchi yetu kiasi cha matatizo yetu madogomadogo ya ndani kwisha kabisa ? Mna mipango, mikakati na malengo gani kwa hili au hili halistahili kufanyiwa strategic planning na management mheshimiwa?
21. Kuna mengi ambayo kweli tuanweza kuwa hatuwezi kuyafanya lakini kuna kama hili la usafi na kutunza mazingira kama kweli tutalishindwa tufahamau hata tukienda nchi za wazungu na suti za bei kubwa kuliko zao watakuwa wanatudharau na kusonya tazama nani hawa nimeacha 'y' kwa ustaarabu wanajua kuvaa suti lakini kwa usafi bure kabisa.
22. Kuna mwandishi mmoja alikuwa akizungumzi a uwezekano wa kugawa JKT wakati fulani huko nyuma. Kama ninakumbuka sawasawa bwana huyo alisema kuwa JKT inaweza kuwa na sehemu ya Uzalishaji mali, Masuala ya Ulinzi na Usalamu, Ufundi na uhandisi na pia idara ya huduma za kijamii. Akapendekeza Idara ya Kijamii iwezeshwe kufanya usafi wa miji yetu na wawe wanalipwa vizuri tu kuliko kuwa na wababaishaji wanaochafua badala ya kusafisha miji yetu. Kwa kuwa wana-JKT watakuwa wakiingia na kutoka kila mwaka hatutakuwa tena na tatizo la usafi na utunzaji mazingira katika miji yetu hadi mwisho wa dunia. Inavyoelekea masikio ya viongozi wetu wote kwa hili yalizibwa na macho yao yalifumbwa na hakuna dalili kuwa kuna aliyesikia au kuelewa lolote. Pengine huyo mwandishi yuko miaka 50 mbele ya pale walipofika viongozi wetu na kwa hali hii ninaamini ninaelewa kwanini tutatendelea kuwa masikini na ombaomba kwa miaka mingini 50 ijayo!

HILI NAOMBA LIBAKI KWENYE MTANDAO HADI MWISHO WA DUNIA KUTHIBITISHA UDUNI WA VIONGOZI WETU WA SASA NA WATAKAOKUJA KAMA HALI HII ITAENDELEA KUWA HIVYO.

TAFADHALI TOVUTI NISHUHUDIE!

Iga,
Tanzania
 
Back
Top Bottom