Binti wa Miaka 12 Aliyeozeshwa Kinguvu, Afariki Akijifungua

Dr. Chapa Kiuno

JF-Expert Member
Sep 11, 2009
443
18


Nojud Ali, alikuwa ni mtoto wa kwanza wa kike aliyeolewa kuvunja tamaduni za Yemen na kuomba talaka, Mtoto Fawziya hakuwa na bahati kama yake alifariki wakati akijifungua..(Picha: AFP)

Binti wa miaka 12 aliyeozeshwa kinguvu kwa kijana mwenye umri wa miaka 25 nchini Yemen amefariki dunia akiwa leba baada ya kuhangaika kwa siku tatu kujifungua mtoto aliyefia tumboni.


Mtoto Fawziya Abdullah Youssef mwenye umri wa miaka 12 aliyekuwa ameolewa na kijana mwenye umri wa miaka 25 alifariki dunia ijumaa baada ya kupoteza damu nyingi sana wakati akijifungua.

Fawziya alifariki baada ya kutumia siku tatu ndani ya leba akihangaika kujifungua mtoto ambaye alizaliwa akiwa amefariki.

Fawziya alifariki kwenye hospitali ya wilaya ya al-Zahra katika jimbo la Hodeida lililopo kilomita 223 magharibi mwa mji mkuu wa Yemen, San'a.

Fawziya alikuwa na umri wa miaka 11 wakati baba yake alipomuozesha kwa kijana mwenye umri wa miaka 24 anayefanya kazi kwenye mashamba nchini Saudi Arabia, alisema Ahmed al-Quraishi, mwenyekiti wa taasisi ya kutetea haki za binadamu nchini Yemen inayoitwa Siyaj.

Al-Quraishi alisema kuwa aligundua kifo cha Fawziya hospitalini bila kutarajia wakati alipoenda hospitali kufanya uchunguzi kuhusiana na taarifa za watoto waliokimbia vurugu kaskazini mwa nchi hiyo.

"Hili ni mojawapo ya matukio mengi kama haya yanayotokea nchini Yemen" alisema al-Quraishi.

"Sababu kubwa ni ukosefu wa elimu na kuwalazimisha wasichana kuingia kwenye ndoa wakiwa na umri mdogo".

Wazazi masikini mara nyingi huwagawa mabinti zao wenye umri mdogo kwa malipo ya mahari kubwa sana.

Pia suala hili huchangiwa na tamaduni za muda mrefu ambapo watoto wa kike wanapozaliwa huahidiwa kuozeshwa kwa wajomba zao kwa imani za kuwalinda na mahusiano yasiyofaa.

Wanaume kuoa watoto wa kike wenye umri mdogo ni jambo la kawaida katika nchi ya Yemen ambayo ni masikini kuliko nchi zote za kiarabu na ambayo tamaduni za kikabila zinachukua nafasi kubwa katika jamii.

Kwa mujibu wa takwimu za wizara inayoshughulikia masuala ya jamii nchini Yemen, karibia robo ya wanawake wa nchini Yemen huolewa kabla hawajafikisha umri wa miaka 15.

Hata hivyo hakuna takwimu zinazoonyesha ni wanawake wangapi huolewa wakiwa na umri mdogo nchini humo kila mwaka.

 
Back
Top Bottom