Bajeti ya Serikali yapigwa panga

Mallaba

JF-Expert Member
Jan 30, 2008
2,554
47
NI KWA AJILI YA KUFIDIA NAKSI YA BILIONI 640

Mwandishi Wetu

HALI mbaya ya uchumi imeilazimisha Serikali kufumua bajeti yake ya mwaka wa fedha 2010/11 kwa kupunguza matumizi ya Wizara ili kufidia upungufu wa Sh670.4 bilioni zilizotegemewa kupatikana kutokana na makusanyo ya kodi katika mwaka huu wa fedha.

Uamuzi huu ambao umetokana na kupungua mapato ya ndani ya mwaka huu wa fedha, umesababisha Serikali kupiga panga fedha za miradi ya maendeleo na za matumizi ya wizara zote.

Taarifa za kuaminika ambazo Mwananchi Jumapili imezipata, zinaeleza kuwa fedha hizo zinapunguzwa kutoka katika kila wizara kwa viwango tofauti kulingana na bajeti ya wizara husika, ili kufidia makusanyo ya kodi yaliyokusudiwa na kulipia mahitaji ya fedha za mishahara na kuwalipa makandarasi wa Barabara.

Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustaffa Mkullo, alipoulizwa kuihusina na hali hiyo alisema taarifa ya hali ya uchumi wa nchi alishaitoa hivi karibuni kwenye chombo kimoja nchini, hivyo hahitaji kuitoa tena.

"Nilitoa taarifa kwa wenzenu wa gazeti (sio Mwananchi) sasa siwezi tena kuirudia," alisema.

Habari hii inakuja wakati Serikali imeelezwa kuwa imetuma barua kwa nchi wafadhili kuziomba ziweze kuchangia miradi ya maendeleo katika bajeti yake.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Wizara ya Fedha na Uchumi (Hazina), imekuwa ikifanya vikao mbalimbali vya kujadili tathmini ya hali ya uchumi na mwelekeo wa utekelezaji wa bajeti tangu Desemba mwaka jana.

Katika vikao hivyo vilivyofanyika Januari 11 hadi 24 mwaka huu ilibainika kuwa kuwepo kwa upungufu wa mapato kwa mwaka huu wa fedha unafikia Sh670.4 bilioni.

Kutokana na hali hiyo, Serikali imelazimika kupunguza fedha za matumizi kwa wizara zake, kiasi cha Sh480.51 bilioni ili kufidia upungufu huo.

Vile vile, itapunguza fedha za matumizi, kiasi cha Sh153 bilioni ili kuziba pengo la gharama za mishahara.

Taarifa zaidi zinasema kuwa, Serikali inahitaji kiasi cha Sh258 bilioni kulipa madai ya wakandarasi wa barabara na mkandarasi aliyekarabati Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, huku fedha hizo zikielezwa kuwa mikataba yake ilifanyika nje ya bajeti ya mwaka 2010/11.

Kwa mujibu wa chanzochetu cha habari, katika mkutano wa makatibu wakuu wa wizara, uliofanyika hivi karibuni kuliibuka mjadala juu ya kwanini malipo ya kandarasi ya barabara yaonekane kuwa ni ya dharura wakati kuna wizara ambazo pia zinadaiwa na wakandarasi.

Mvutano mwingine ulihusu kiwango cha fedha za matumizi ya wizara zilizopendekezwa kupunguzwa, kuwa ni kikubwa na kuwa hali hiyo itazifanya wizara kushindwa kuendesha shughuli zake kwa kipindi kilichobaki cha mwaka wa fedha.

“Kulitolewa mapendekezo kuwa badala ya serikali kupunguza kiwango hicho cha fedha kutoka katika kila wizara, inatakiwa iibane Mamlaka ya Mapato Nchini (TRA) kuziba mianya inayosababisha kushindwa kufikia malengo ya makusanyo ya mapato,” kilisema chanzo hicho.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Profesa Beno Ndulu akizungumza na waandishi wa habari mwanzoni mwa mwezi huu alisema hali ya uchumi wa nchi ni nzuri na kwamba Serikali ina hazina ya kutosha ya fedha.

Hata hivyo, pamoja na mjadala huo mkali, Mwananchi Jumapili imebaini kuwa Wizara ya Fedha imesema Serikali haina budi kulipa deni hilo la kandarasi ya barabara linalofikia Sh250 bilioni ili kuendelea na kazi ya ujenzi wa barabara kabla ya kuanza kwa msimu wa mvua.

Pia wizara hiyo imesema hali ya uchumi imeathiriwa na mgao wa umeme unaoendelea, na hivyo kuathiri mwelekeo wa kuongezeka kwa ukusanyaji wa mapato.

Wachambuzi wa uchumi, Serikali kulazimika kupunguza bajeti yake kunatokana na kuwepo kwa matumizi mabaya na utoaji holela wa misamaha ya kodi iliyosababisha kushuka kwa kiwango cha ukusanyaji wa mapato.

Habari zilizopatikana kutoka mkutano wa wahisani na watendaji wa Serikali kuhusu utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka wa Fedha wa 2010/2011, ulifanyika hivi karibuni zinaeleza kuwa Serikali ina upungufu wa Sh600 bilioni kutoka kwenye bajeti ya Sh11 trilioni, iliyopitishwa na Bunge mwaka jana.

Kati ya Sh11trilioni, Sh6 trilioni zilitarajiwa kukusanywa kutoka vyanzo vya ndani vya mapato na kiasi kilichobaki kingetokana na fedha za wafadhili.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, John Haule, hivi karibuni alinukuliwa na vyombo vya habari akiwatoa hofu wananchi kwamba Serikali haina mpango wa kuwa na bajeti ndogo kukabiliana na hali hiyo.

Alisema Serikali inatarajia kuwa na mkutano wa kutathmini utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2010/11 ambao utatoa picha ya hali halisi ya uchumi wa taifa nchini.
 
Tatizo la serikali ya sasa ni kutopenda kunguza matanuzi yao; kunapokuwepo tatizo la fedha wao hukimbilia kwenye kupunguza matumizi ya maendeleo. Mtu anajiuliza bila kuwekeza kwenye maendeleo ya uchumi, hizo fedha za kodi zinazo wawezasha hao viongozi na watendaji wakuu serikalini kujitanua zitapatikana wapi?
 
Hii serikali kweli inawafanya watu mazuzu ile mbaya! Hivi si wiki chache tu wamesema imevunja record ya mapato ambayo haijawahi kutokea nchini? Na wana kiasi kikubwa cha akiba ya dola??? Leo tena imekuwa mapato madogo yanayopatikana TRA?

Duh kama kuku wanasahau baada ya dk 10 walichosema! Na bado yale madeni ya benk ya Stanbic sijui wameshaanza kulipa au ndo wajukuu wataubeba mzigo huo na mengine wanayokopa kila siku?? Hamna plan yoyote ya maana kama suala la umeme halieleweki na ni sehemu muhimu sana kuchangia mapato hayo!

Kwa kweli tunahitaji mawazo mbadala kwa nguvu zote. Tunahitaji vichwa vinavyothubutu kuchukua hatua kwa mipango iliyofanywa miaka mingi na sio mipango, mikakati, mipya ya kila siku inayosemwa na watu wasiotekeleza ishakuwa jadi yetu sasa!
 
umeona? kupunguza maendeleo ni sawa kwao bali kujipunguzia marupurupu na chai zao hapana.
Tatizo la serikali ya sasa ni kutopenda kunguza matanuzi yao; kunapokuwepo tatizo la fedha wao hukimbilia kwenye kupunguza matumizi ya maendeleo. Mtu anajiuliza bila kuwekeza kwenye maendeleo ya uchumi, hizo fedha za kodi zinazo wawezasha hao viongozi na watendaji wakuu serikalini kujitanua zitapatikana wapi?
 
mwongo ziku zote ni mwepesi sana wa kusahau.
kwani unadhani Ahadi mlizotolewa na JK bado anazikumbuka? la hasha jamaa alishasahau zamani sana hata kama kulikuwa na uchaguzi.
kazi kwenu
Hii serikali kweli inawafanya watu mazuzu ile mbaya! Hivi si wiki chache tu wamesema imevunja record ya mapato ambayo haijawahi kutokea nchini? Na wana kiasi kikubwa cha akiba ya dola??? Leo tena imekuwa mapato madogo yanayopatikana TRA?

Duh kama kuku wanasahau baada ya dk 10 walichosema! Na bado yale madeni ya benk ya Stanbic sijui wameshaanza kulipa au ndo wajukuu wataubeba mzigo huo na mengine wanayokopa kila siku?? Hamna plan yoyote ya maana kama suala la umeme halieleweki na ni sehemu muhimu sana kuchangia mapato hayo!

Kwa kweli tunahitaji mawazo mbadala kwa nguvu zote. Tunahitaji vichwa vinavyothubutu kuchukua hatua kwa mipango iliyofanywa miaka mingi na sio mipango, mikakati, mipya ya kila siku inayosemwa na watu wasiotekeleza ishakuwa jadi yetu sasa!
 
Ndio tujifunze kuwa na wizara chache na kupunguza matumizi yasiyo ya lazima.
 
Back
Top Bottom