Mwana Mpotevu
Platinum Member
- Sep 7, 2011
- 3,295
- 2,505
Waandishi Wetu
KAMATI ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama imembana Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ikimtaka aeleze ni kwa nini vitabu vya bajeti ya wizara hiyo vimechelewa kufikia wajumbe wa kamati hiyo.
Hatua ya kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa imekuja siku chache baada ya baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Miundombinu kuikataa Bajeti ya Wizara ya Uchukuzi, ikihoji sababu za bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka 2011/12 kutekelezwa kwa kiwango cha asilimia 40.
Juzi jioni, taarifa zilizopatikana kutoka kwenye kikao cha kamati hiyo ya mambo ya nje zilisema wajumbe walichukizwa na hatua ya wizara hiyo kuchelewa kuwapatia vitabu kwa mujibu wa taratibu.Taarifa hizo zilisema, Lowassa alihoji sababu za msingi za wao kuchelewa kupata vitabu hivyo siku mbili kabla na badala yake kuvipata siku ya mkutano.
Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo aliliambia gazeti hili kwamba wajumbe waligomea bajeti hiyo kutokana na kuchukizwa na kitendo hicho cha kucheleweshwa kwa vitabu na kutokuonyesha madeni ya wizara.
Pia wajumbe hao walichukizwa na hatua ya ujumbe huo wa wizara hiyo kuchelewa kufika katika kikao hicho.
Hata hivyo, Lowassa alipotakiwa kutoa ufafanuzi juu ya suala hilo alikataa na kumtaka mwandishi athibitishe taarifa hizo kwa mtu aliyezitoa... Siwezi kusema lolote kuhusu hilo na wala mimi sijui. Mwulize aliyekupa taarifa, yeye ana maelezo zaidi lakini siyo mimi.
Chanzo hicho cha habari kilisema kamati hiyo pia ilihoji kuhusu uwasilishaji wa michango ya wanachama wa mifuko ya hifadhi ya jamii, ikiwemo NSSF.
Hata hivyo, baadaye kamati ilipitisha bajeti hiyo ya Sh80 bilioni na kumtaka Waziri Membe na ujumbe wake kuwasilisha mapema vitabu vyao katika siku zijazo ili wajumbe waweze kuhoji utekelezaji wa mikakati ya Serikali.
Source: Mwananchi (Leo)
MY TAKE: Bila ubishi, kambi ya EL ambayo inaongoza kamati ina malengo ya kuwafanyia kweli wale wote ambao ni wapinzani wao kisiasa. Bado Sitta zamu yake inakuja.