Mungu hakuletwa kama usemavyo, Mungu alikuwepo katika kila jamii, lugha, jamaa, taifa na dunia kwa ujumla.
Unachojaribu kueleza ni kuwa watu walichanganya utamaduni na ubinafsi katika Kumtafuta na kumuabudu huyu Mungu.
Pia jamii moja kutaka kujitofautisha na jamii nyingi kulingana na mazingira na maumbile ndivyo vilivyopelekea Mungu aonekane kagawanyika.
Ukweli ni kwamba Mungu ni yule wa wote mwenye uweza japokuwa jamii zimemmilikisha Fulani zimemmilikisha na baadhi ya mataifa kumtaifisha huku baadhi ya watu kumbinafsisha. Jambo hili limefanya jamii nyingi kuchanganyikiwa.
Mfano wa watu waliojaribu kumbinafsisha Mungu ni pamoja na Waisrael ambao kupitia kitabu cha historia yao ambacho wengi hukiita kitabu kitakatifu "BIBLIA". Husema;
Mungu wa Ibrahimu, Isaka na yako, huku ni kumbinafsisha Mungu wa wote. Na ikiwa Mungu angekuwa wa Mtu mmoja mmoja basi ni wazi asingeweza kuwa wa Ulimwengu mzima.
Vitabu vya Biblia hasa Agano la kale, viliandikwa kiokombozi zaidi. Ukombozi pekee uliokusudiwa ulikuwa ni ukombozi wa taifa la Israel katika dunia hii. Hata alieandika vitabu vya mwanzoni kabisa alikuwa ni Mwanamapinduzi au Mkombozi wa awali wa taifa hilo. Mwanamapinduzi huyo na mwanaharakati ambaye aliitwa Nabii ili kwa malengo mahususi ndiye aliyeanzisha Vuguvugu kwa taifa hili ambalo lipo katika msuguano mpaka leo.
Nabii Musa mwanamapinduzi ndiye aliyeandika vitabu vitano vya awali katika biblia, aliandika vitabu hivyo kwa mtindo wa ubinafsi kwa taifa lake.
Nasema kwa Ubinafsi nikiwa namaanisha kabisa kutokana na baadhi ya visa vilivyomo katika vitabu vyake.
Aidha kuna kisa cha Yakobo na Esau ambacho kinaonyesha dhahiri lengo la mwandishi wa vitabu hivyo. Yakobo ambaye ndiye Israel aliutwaa ukubwa kwa Esau ambaye ni Baba wa waEdomu. Kisa hicho cha kusisimua kinaonyesha lengo kamili la mwandishi ambalo ni ubinafsi kwani Yakobo hakuwa na khaki yoyote ya kupata baraka ama kurithi katika familia ya Isaka. Musa akiwa mwanzilishi wa Kitabu cha Biblia kwa maandishi yake ndiye mtu aliyeleta mgogoro wa Uwapo wa Mungu.
Mfano wa Pili ni Wa Isaka na Ishimael.
Ubinafsi wa mwandishi katika kutetea asili ya mababu yake aliweza kuudhihirisha. Kisheria Mtoto wa kwanza hasa wakiume ndie anayetakiwa kuwa mrithi wa Mali.
Mtunzi Musa alijua kabisa Ishmael sio wa Taifa lake hivyo kumtukuza lilikuwa ni jambo baya sana kwake. Ukisoma kwa makini aya za kisa kile unaona jinsi Mungu alivyokuwa upande wa Ishmael.
Kama mtoto wa nje yaani wa mtumwa hajri hawezi kuwa Mrithi ilikuwaje kwa Yakobo na Wake zake wanne ambao kila mmoja alipata gawio katika nchi ya Kanani.
Biblia inasema kuwa Ibrahimu atabarikiwa na kuwa taifa kubwa lakini mtoto wake mmoja ambaye ni Ishmael ambaye ni wakwanza anafichwa kabisa pamoja na watoto zake wengine kwa mkewe Ketura. Watoto hawa wa ibrahimu Historia yao inawekwa kapuni na mwandishi Wa kitabu cha Mwanzo katika Biblia. Huku watoto wa Yakobo(Israel) wakiibuka kidedea katika historia. Moja ya sababu kubwa ni kuwa Mwandishi Musa alitoka katika moja ya makabila ya Israel hivyo huenda aliandika kwa ubinafsi au kwa kutojua ama kufuatilia vizuri historia ya vizazi vingine vya Ibrahimu.
Jambo jingine ambalo Musa alililenga si kumtangaza Mungu kama baadhi ya watu wadhaniavyo. Musa alishindwa kuandika mambo ya Msingi ikiwemo Asili ya mwanadamu. Ameelezea juu juu chimbuko la mwanadamu kana kwamba hakuona umuhimu wake. Pengine tusimlaumu kwa kutoelezea chimbuko lake kwani huenda hata yeye hakujua au hakuwa na taarifa muhimu zenye manufaa.
Musa alishindwa kuelezea Kwa kivipi Watoto Wa Adamu walivyopata wake zao.
Pia watu wengine walitoka wapi ambao Kaini aliogopa wasije wakamuua.
Mwandishi huyu pia alitumia lugha ambayo kimsingi huweza kumletea utata mtu mwenye akili ndogo au kubwa. Kwa mfano kitendo cha kusema Nyoka akamdanganya Hawa bado kinautelezi katika fikra za watu wengi.
Iweje nyoka amdanganye hawa wakati hakupewa uwezo kama binadamu aliye mfano wa Mungu.
Lugha ya mafumbo ya kitabu cha Mwanzo huwagawa watu katika makundi mbalimbali. Wapo wanaoachwa solemba kwa akili ndogo na wapo wanaotoa tafsiri kulingana nauwezo mkubwa wa akili zao.
Kwa mfano ikiwa wapo wanaofikiria kuwa nyoka alikuwa ni Shetani huku wakijiona wapo sawa basi hata wale wanaoona Tunda lilikuwa ni uchi au sex huenda nao wakawa sawa.
Musa hamtaji Shetani Mara kwa Mara jambo ambalo linazua utata. Mara nyingi hutumia watu Kama wachawi, waganga, wanajimu n.k. Jambo ambalo hakuna anayeweza kuthibitisha kuwa huu ni Uchawi au ni muujiza. Na upi ni Mungu na upi ni washetani. Kwa bahati mbaya wote husema wanamtumia Mungu. Hivyo kila upande humwona mwenzake ni Mchawi atumiwaye na Shetani.
Musa alijikita kuelezea Historia ya taifa lake na kusahau historia ya mwanadamu. Ndio maana naweza kusema Musa alisahau iwe kwa kujua au laa kusimulia habari muhimu za asili ya mwanadamu.
Dunia ipo hivi Leo kwasababu ya Musa, japokuwa kuna Imani nyingi lakini nyingi zinaamini kulikuwa na Adamu na Hawa.
Historia ya mwanadamu ikiwekwa sawa ndio ukweli kuhusu Mungu kuwepo haitakuwa na Mashaka.
Mungu yupo sema waandishi ndio huongozwa na athari mbalimbali katika kumwelezea hivyo hujikuta wakiacha maswali mengi kwa kuacha kusimulia baadhi ya matukio ya Msingi.
Musa alikuwa na athari ya elimu za kimisri hivyo lazima umakini uwepo katika kusoma habari zake na lengo lake na nafasi yake.