mamayoyo1
JF-Expert Member
- Jul 25, 2018
- 1,011
- 1,019
Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) karibuni linatarajia kuzindua safari mpya za kwenda Afrika Kusini, ambapo ndege ya kwanza kuruka kwenda jijini Johannesburg itaruka Julai mwaka huu.
Mkurugenzi Mkuu wa ATCL, Ladislaus Matindi amesema kuwa watatangaza nauli na kuanza kutangaza safari hizo watakapoanza kuuza tiketi.
Hatua hii kubwa ya kuendelea kupanuka kwa shirika hilo inakuja ikiwa ni miezi miwili tangu lilipozindua safari mpya za kwenda Harare nchini Zimbabwe na Lusaka nchini Zambia.
Safari ya kwenda Afrika Kusini itakuwa ni safari ya tano ya kimataifa kuzinduliwa na ATCL baada ya Harare, Lusaka, Bujumbura na Entebbe.
Baada ya kuzindua safari hiyo, Matindi amesema kuwa shirika hilo litajiandaa na safari za kwenda Mumbai (India) na Guangzhou (China) ambapo maandalizi yake yamefikia katika hatua nzuri.
Ameongeza kuwa safari hizo zitazinduliwa mara tu mazungumzo na mamlaka kwenye nchi hizo yatakapokamilika.
Kwa sasa shirika hilo linalofufuka baada ya kutofanya vizuri sokoni kwa miaka mingine lina ndege nane ambazo ni, Bombardiers Q-400s tatu, Airbus (A200-300) mbili, Fokker50, Fokker28 na Boeing 787-8 Dreamliner.