Aliyetokomea na mamilioni UVCCM aibukia Dodoma

Sumasuma

JF-Expert Member
Jun 23, 2011
342
110
Habel Chidawali, Dodoma
MTUHUMIWA wa uporaji wa fedha za Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara amejitokeza na kukiri kuzipokea akisema sehemu ya fedha hizo anazitunza kwenye akaunti yake.

Akizungumza jana, mtuhumiwa huyo, Omary Kariaki ambaye kwa sasa ni Diwani wa Kata ya Kwadero, Kondoa kwa tiketi ya CCM alisema hakuondoka na Sh26milioni kama ilivyoripotiwa jana na gazeti hili kwani baadhi ya fedha hizo zilikuwa ni ahadi ambazo hadi sasa walioahidi hawajatoa na badala yake alipokea Sh6 milioni tu.

Kariaki ambaye alikuwa Katibu wa UVCCM Wilaya ya Simanjiro alisema kati ya fedha hizo, amebakiwa na Sh2 milioni alizozihifadhi benki.

“Ni kweli ndugu yangu mimi nilianzisha harambee hiyo na kuchangisha kiasi cha fedha kati ya Sh4 milioni au sita hivi, sikumbuki vizuri... lakini nyingine zilikuwa ni ahadi ambazo hadi leo sijazipata,” alisema Kariaki huku akidai kwamba alilipia ukumbi ilikofanyika harambee hiyo kiasi cha Sh4 milioni.

Alidai kuwa sababu ya kuondoka na fedha hizo na bila ya kuaga ni ugomvi baina ya Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka na Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Ole Millya na kuongeza kuwa anasubiri kuambiwa kama upepo wa kisiasa umetulia Arusha ili azipeleke kwa vijana hao.

Harambee hiyo iliyofanyika mwaka juzi iliongozwa na aliyekuwa Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Shamsi Vuai Nahodha ambaye kwa sasa ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na jumla ya Sh26milioni zilipatikana.

“Ukumbi tuliofanyia ni kwa Mwenyekiti wa UVCCM na tulilipa fedha hizo na yeye anajua, lakini nyingine hatukuwahi kuzikusanya hadi leo. Ugomvi wa Ole Sendeka na Ole Millya ndiyo ulionifanya nisikabidhi fedha hizo,’’ alisema.
Diwani huyo alisema mara baada ya harambee hiyo, kuliibuka makundi mawili ya wanasiasa hao kuhusu mambo aliyodai kuwa ni ya ubunge na kusababisha mvutano.

Alipotakiwa kueleza ni lini atakabidhi fedha hizo, alijibu: “Kama makundi yametulia basi mimi nitatoa fedha hizo katika akaunti yangu na kuwapa mara moja, lakini kweli niliondoka ovyo katika kituo changu maana hakukuwa na usalama wa kutosha.’’

Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma, Paza Mwamlimwa alisema baada ya kusoma habari hizo katika toleo la jana la gazeti hili, ameanza kulifuatilia akiahidi kulitolea maelezo hapo baadaye.

Taarifa zinaonyesha kuwa Kariaki aliwahi kuwa Katibu wa Uhamasishaji wa Vijana mkoa wa Dodoma kabla ya kuteuliwa kuwa Katibu wa UVCCM Bukoba Mjini na kisha wilaya ya Simanjiro.

Mwenyekiti wa UVCCM wilayani humo, Kiria Laizer alisema fedha hizo zilizochangwa kwa lengo la kutunisha mfuko wa maendeleo ya vijana Simanjiro na ziliyeyuka muda mfupi baada ya harambee hiyo.

Katika harambee hiyo, Nahodha alichanga fedha taslimu Sh2 milioni.

Ilielezwa kwamba wageni wawili waliohudhuria shughuli hiyo kwa mwaliko wa mtuhumiwa huyo ambao walitambulishwa ukumbini kuwa dada wa Rais Jakaya Kikwete, walichangia Sh400,000.

Kwa mujibu wa kumbukumbu rasmi za shughuli hiyo, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Henry Shekifu ambaye sasa ni Mbunge wa Lushoto (CCM), alichangia Sh500,000.

Viongozi wengine waliohudhuria na kiasi walichochanga kwenye mabano ni Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Khalid Mandya (200,000), Ole Sendeka (Sh1.5 milioni) na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Manyara, Lucas Ole Mukusi (Sh100,000).

“Baada ya mgeni rasmi (Nahodha) kunikabidhi mfuko wenye fedha usiku ule pale ukumbini, nilimwita (mtuhumiwa jina tunalo) na kumkabidhi mbele na wajumbe wawili wa kamati ya utekelezaji wilaya na tangu siku ile, sijawahi kumwona wala kupata mawasiliano naye,” alisema Laizer.

Aliwataja Wajumbe wa Kamati ya Utendaji walioshuhudia makabidhiano hayo kuwa ni Bonny Shongo na Paul Sipitet.

“Siku tatu baadaye tulimtafuta (mtuhumiwa), bila mafanikio na tulipompata kwa njia ya simu alidai yuko Mjini Arusha kwa shughuli binafsi lakini baada ya muda mfupi alitutumia ujumbe mfupi wa simu akitutaka kutafuta mtu mwingine (wa kujaza nafasi yake) kwani yeye ameondoka,” alisema Sipitet.


Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro alisema tayari ameziagiza ngazi husika (UVCCM), kuchukua hatua kulingana na kanuni na taratibu zao na pia kutoa taarifa polisi ili hatua za kisheria zichukuliwe.

“Sisi kama Serikali, chama kikichukua hatua na kuwasilisha taarifa, nitaagiza polisi wachukue hatua za kisheria kwa kuchunguza na kumtia mbaroni mtuhumiwa. Nakushauri pia uwasiliane na katibu wa CCM wilaya ambaye ndiye mlezi wa jumuiya zote za chama ngazi ya wilaya,” alisema Mandya.

Mkuu huyo wa wilaya alisema baada ya ofisi yake kutopata taarifa za utekelezaji wa amri yake ya mhusika kuchukuliwa hatua hadi sasa, ameamua kuuandikia barua rasmi uongozi wa UVCCM na chama wilaya kudai utekelezaji wa agizo lake kutokana na wahusika kuonekana wazito katika jambo hilo.:A S 465:
 
Kwani kafanya lipi la ajabu? Magamba wizi, ufisadi na utapeli si ndio sera zao rasmi?
 
Haaa anaendeleza jadi yao,kashakula hela huyo tena ni diwani khaaaaa,ingeua ni cdm washamfukuza!
 
Dalili za kuanguka hizo, hadi watu wanakimbia na hela za chama, eti zimewekwa akaunti ya mtu binafsi kweli? uvccm hawana akaunti!!! ukumbi unalipiwa milioni 4, ukumbi gani huo? tena ukumbi unamilikiwa na kiongozi??? huu ni utapeli kweli kweli?
 
Toka lini nyoka akazaa mjusi, ni moja ya sera za magamba kutafuna. Chukua Chako Mapema. Kigumu chama cha mapinduzi...KIGUMU.
 
Kama ukumbi umelipiwa sh mil 4 na ukumbi wenyewe unamilikiwa na Mwenyekiti wa UVCCM, basi WAMESHIRIKIANA WOTE KULA HIYO HELA!!

Swali: Baada ya mwenyekiti kujulishwa na katibu wake kuwa watafute mtu wa kuziba nafasi yake, kwanini hakumuuliza fedha zilizokusanywa zilipo? Mbona amenyamaza mpaka juzi baada ya tuhuma hizi kuibuliwa? Yeye mwenyekiti Bw. Kiria Laizer anaweza kuudhibitishia umma uhalali wa malipo hayo makubwa wa ukumbi tena wa Mererani?

Huu ni ufisadi wa kienyeji/kijinga sana na ni aibu kwa UVCCM ambayo ilipaswa kuonyesha njia kwa mustakabali wa CCM ya baadae.
 
Hiyo ndio hali halisi CCM. Mtu anakwiba halafu anabembelezwa hakuna cha Polisi wala mahakamani. Na bado tunaendelea kuwaamini na kuwapa nchi yetu waiongoze
 
Kweli jamaa wizi ni jadi yao, yaaani ukumbi milioni 4!! tena Simanjiro!! Jamaa mjanja sana huyo kasepa na hela kaenda kugombea udiwani Dodoma... Chukua Chako Mapema (CCM)...
 
Back
Top Bottom