Mwizukulu wa Buganda
JF-Expert Member
- Nov 19, 2024
- 638
- 1,771
Kiongozi mstaafu wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe amesema kususia uchaguzi siyo suluhisho la kupambana na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwani hakijali chochote, bali njia pekee ni kupambana nacho kwenye sanduku la kura kwa kuhakikisha wananchi wanapiga kura nyingi za kukiondoa madarakani.
Zitto ameyasema hayo Oktoba 14, 2025 jijini Mwanza alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa kampeni wa mgombea ubunge Nyamagana kwa tiketi ya ACT Wazalendo, Ester Thomas, katika eneo la Dampo.
Amesema uchaguzi wa mwaka huu ni muhimu na kushiriki kwake kutawafanya wananchi waonyeshe hasira zao dhidi ya chama tawala ambacho kimekuwa madarakani kwa zaidi ya miaka 60.
Kabwe ambaye ni mgombea ubunge Kigoma Mjini, amedai anatambua kwamba wananchi wamekatishwa tamaa na matukio ya nyuma ya kuibiwa kura na kutangaziwa wabunge ambao hawakuwapigia kura, lakini akawataka wasikate tamaa na waonyeshe hasira zao kwa kupiga kura kwa wingi Oktoba 29, ili kukiangusha chama tawala.
Chanzo: Mwananchi