Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,319
- 33,125
Tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 12 jioni katika Kijiji cha Komkonga, Kata ya Kabuku, Barabara ya Chalinze-Segera, baada ya wananchi kuzuia magari yanayopita barabara hiyo, na kutishia uhai wa yeyote ambaye angethubutu kuingilia harakati zao.
Akizungumza na Tanzania Daima ofisini kwake jana, Ofisa Upelelezi wa Mkoa wa Tanga, Japhari Mohamed, alisema hali ilikuwa tete mahali hapo baada ya gari kumgonga na kumuua mtembea kwa miguu aliyejulikana kwa jina la Mohamed Idrisa (30).
Alisema Idrisa aligongwa na basi aina ya Isuzu, mali ya Kampuni ya Tahmeed, yenye namba za usajili KAY 177 A iliyokuwa ikiendeshwa na Athuman Abbas (34).
Ofisa upelelezi huyo alikiri Zitto kunusurika na kipigo, lakini akasema haikujulikana mara moja mwanasiasa huyo alikuwa anaelekea wapi.
Alisema kilichotokea ni kwamba baada ya Zitto kufika eneo la tukio, alishuka kwenye gari alilokuwamo, akaanza kuwasihi wananchi hao waliokuwa na hasira na jazba.
Ni kweli Zitto alikuwa mmoja wa abiria waliokumbana na adha ya wananchi kufunga barabara aliamua kushuka kwenye gari lake na kwenda kuwasihi, jambo ambalo hakufanikiwa hata kidogo, huku wananchi wakikataa kumsikiliza.
Kutokana na hali hiyo, wananchi walimwambia hawataki siasa bali wanamtaka Rais Jakaya Kikwete au Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Meja Jenerali mstaafu, Said Kalembo, alisema Mohamed.
Alisema baada Zitto kuelezwa maneno hayo, aliamua kuondoka na kwenda moja kwa moja kwenye gari lake kwa ajili ya kujiokoa na dhahama hilo.
Alisema wananchi hao walikuwa wanashinikiza kuwekwa matuta katika eneo hilo kwa madai kuwa wamechoshwa na ajali za mara kwa mara zinazotokea eneo hilo.
Alisema polisi wa kituo cha Kabuku walishindwa kuwatawanya wananchi hao na kulazimika kuomba msaada kutoka mkoani ambako askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) walifika na kutumia mabomu ya machozi.
Katika ghasia hizo mtu moja alijeruhiwa, baadhi ya magari kuvunjwa vioo huku watu 35 wakikamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Kamanda huyo alisema ni kosa la jinai wananchi kufunga barabara kuu kinyume cha sheria.
Gazeti hili lilipomtafuta Zitto kuhusu tukio hilo jana, hakupokea simu; mwandishi akamwandikia meseji kumuuliza habari za tukio hilo; mbunge huyo naye akajibu kwa kifupi: nimenusurika kupigwa mawe wapi?
Mwandishi akamjibu kwa meseji: Imetumwa stori kutoka Kabuku, Tanga. Zitto hakujibu tena.
Hata hivyo, mmoja wa watu waliokuwa na Zitto katika safari hiyo, aliliambia gazeti hili kwa simu jana kwamba kina Zitto walipofika eneo la tukio walikuta foleni ndefu ya magari yapatayo 400 yaliyokuwa yamezuiwa na wananchi hao kwa mawe na magogo.
Ndipo Zitto akashuka kwenye gari lake, akitaka kuzungumza na wananchi hao. Akamwendea mkuu wa kituo cha polisi cha Kabuku kumsihi amruhusu ahutubie wananchi hao, lakini mkuu wa kituo alikataa kwa kuhofia usalama wa Zitto.
Kwa mujibu wa mtu huyo, vile vile, wananchi wenyewe waligoma kumsikiliza Zitto, ambaye alijitambulisha kama waziri kivuli; wanakijiji wakasema wanamheshimu, lakini wanataka kumsikiliza mkuu wa mkoa. Wakamtaka Zitto arudi kwenye gari lake alale. Polisi nao wakamshauri Zitto aondoke.
Chanzo hicho cha habari kilisema hata hivyo Zitto aliweza kuzungumza na wananchi wachache waliokuwa karibu naye, huku akiwa amezingirwa na polisi, lakini walimpa ujumbe huo huo.
Mnamo saa nne za usiku ndipo askari wa FFU walipowasili mahali hapo na kutawanya wananchi kwa mabomu na kuondoa vizuizi ili magari yaweze kupita.
CHANZO: TANZANIA DAIMA