Sakata la IPTL
Umoja wa Ulaya warejea ukoloni mamboleo
¬ Wasimamisha misaada ya maendeleo
¬ Wasaliti washangilia
¬ Serikali yatakiwa kuyashitaki makampuni na mabenki
UMOJA wa Ulaya kwa pamoja na baadhi ya nchi wanachama wake moja moja zimeamua kusitisha au kusimamisha kwa muda utoaji misaada kwa Tanzania kwa madai kwamba haziridhishwi na mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi ndani ya serikali ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
Nchi zilizotajwa ni Sweden, Finland, Norway, Marekani na Uingereza. Ni katika nchi hizi mabenki na makampuni ambayo kwa namna moja au nyingine yanahusika katika mgogoro wa ufisadi wa IPTL yana makao makuu yake. Na ni katika nchi hizo kwamba makampuni yaliyoko kwenye mgogoro yalifungua kesi mbalimbali na kudai mabilioni ya fedha dhidi ya kampuni ya VIP Engineering and Marketing na serikali ya Tanzania kuhusu mambo mbalimbali yanayohusiana na mradi wa kufua umeme wa IPTL na hasa suala la akaunti ya ESCROW. Kiasi cha dola za kimarekani milioni 125 zilikuwa zimewekwa katika akaunti ya ESCROW iliopo Benki Kuu ya Tanzania (BOT).
Tumemuona Balozi wa Uingereza akiamsha bendera nyekundu kwa madai kwamba anatetea maslahi ya Benki ya Uingereza ambayo eti ilinunua madeni ya IPTL na hivyo inadai fedha zilizokua zimewekwa kwenye Akaunti ya ESCROW.
Kampuni ya IPTL lilikuwepo siku zote na benki ya Standard Chartered inajua matatizo yote ya ufisadi yaliyoibuliwa katika Mahakama mbalimbali pamoja na ripoti za maofisa wafilisi wa muda wa kampuni ya IPTL hapa nchini. Ikitokea kwamba IPTL na washirika wake wakatiwa hatiani, je kwa vipi Standard Chartered itakwepa mashtaka?
Katika nyakati tofauti Mahakama za Kimataifa na mahakama za kawaida katika nchi za Magharibi zimetoa hukumu na maelekezo kwa kampuni zinazoshitakiana. Baadhi ya maelekezo ya mahakama ya New York ni yale yanayosema kwamba kesi nyingine zingelifunguliwa Tanzania kwa sababu mahakama yake ina uwezo wa kusikiliza mashauri hayo.
Mahakama nyingine Uingereza iliagiza fedha hizo zibaki kwenye akaunti ya ESCROW mpaka mfumo mwafaka wa ukokotoaji utakapopatikana. Hakuna mfumo wa ukokotoaji unaoweza kupatikana nje ya wahusika katika IPTL ambao ni wale walionunua hisa za Mechmar ambayo ilikuwa na asilimia 70% na VIP Engineering and Marketing iliyokuwa na asilimia 30%.
Na hicho ndicho kilichofanyika baada ya PAP ambayo ilinunua hisa za Mechmar katika IPTL kununua hisa za VIP Engineering and Marketing na kukubali kubeba madeni halisi ambayo IPTL itakuwa inadaiwa, kuongeza uzalishaji wa umeme kutoka megawati 100 kufikia megawati 500 na pia kupunguza bei ya umeme ambao kampuni hiyo inaiuzia TANESCO.
Awali Mahakama za usuluhishi za kimataifa kama ICSD ambapo shauri kati ya TANESCO na IPTL lilipelekwa kufafanuliwa ni kiasi gani IPTL iliwekeza ili kiasi cha capacity charge kieleweke. Uamuzi wa Mahakama hiyo ulimaliza ubishi kati ya TANESCO na IPTL na kuweka kiwango cha malipo ya dola za kimarekani milioni 2.6 na hivyo kuweka wazi kuhusu malipo kwenye akaunti ya ESCROW yanatoka wapi. Kufuatana na nyaraka zilizopo, fedha zote zilizoingizwa kwenye Akaunti ya ESCROW zilitokana na IPTL kuuza umeme TANESCO kwa kiasi kilichokubaliwa.
Jambo ambalo limesababisha hatua hizo kuchukuliwa, zinahusu jinsi fedha zilizohifadhiwa katika akaunti maalum ya ESCROW kutokana na malipo ya mauzo ya umeme iliyoyafanya kampuni ya IPTL kwa TANESCO zilivyoidhinishwa kuchukuliwa.
Kuna baadhi ya watu wasaliti na hata ya baadhi ya vyombo vya habari kushangilia jambo hilo la Umoja wa Ulaya kurejea kutoa misaada kwa masharti ya kisiasa. Wakati mageuzi ya kiuchumi yana anza katikati ya miaka ya 1980, sera za kurekebisha uchumi ambapo Tanzania ilianza kupata misaada kutoka mashirika ya fedha duniani yaani IMF na Benki ya Dunia, ilikuwa lazima misaada ya kiuchumi kutolewa kwa masharti ya nchi husika kutekeleza masharti ya kisiasa.
Baadhi ya masharti ya kisiasa yalikuwa kwamba ni kuachana na itikadi na sera za Ujamaa na Kujitegemea, kuwanyang'anya mawaziri madaraka na kuyaweka mikononi mwa watendaji wakuu na warasimu serikalini na pia kukubali mfumo wa vyama vingi vya siasa na tafsiri ya utawala bora ambayo inatolewa na mashirika ya kimataifa kwa muktadha wa siasa na itikadi za kiliberali.
Kutoa misaada kwa masharti ni jambo ambalo nchi nyingi za Afrika na nyinginezo katika maeneo ya nchi changa zilikuwa zinayakataa. Sababu ya kukataa ni kwamba kila nchi ina historia yake, utamaduni wake, na mchakato wake katika kupata, kulinda na kuboresha uhuru wake na kutengeneza mazingira ya kupata maisha bora kwa watu wake.
Kwamba kila nchi na kila taifa hupitia majaribu yake ambayo kwa namna moja au nyingine yanatengeneza makovu na vilevile mafunzo kuhusiana na kwa vipi taifa linajiamirisha na kujitengenezea ustaarabu wake bila kudhibitiwa na nguvu kutoka nje.
Vita ya kupambana dhidi ya kuwekewa masharti katika kupata mikopo na misaada imepiganwa na viongozi wetu akiwemo Mwalimu Julius Nyerere ambapo katika nyakati tofauti aliwahi kuhoji tangu lini Shirika la Fedha la Dunia (IMF) liligeuka kuwa wizara ya fedha ya nchi wanachama?
Katika hali isiyo ya kawaida nchi za Umoja wa Ulaya zimeanza kuinua vichwa na kutaka kurejesha mfumo wa masharti katika kutoa misaada yake. Kama ni kuamua kusitisha kutoa misaada kwa sababu za kiuchumi na kifedha au kutokana na kubadilisha mikakati ya mahusiano ya kiuchumi kati ya nchi na nchi, hilo linawezekana. Na wakati mwingine inawezekana kabisa kupunguza kutoa misaada kutokana na mtikisiko wa uchumi duniani kama ilivyotokea kati ya mwaka 2007 mpaka 2011.
Lakini ni jambo la kishenzi kusimamisha kutoa misaada kwa sababu ya tukio moja ambapo nchi husika zina maslahi katika jambo hilo na hasa kwa kuzingatia kwamba mabenki na mashirika ya nchi hizo kwa namna moja au nyingine yanahusika katika kutengeneza mgogoro.
Ni jambo la ajabu kwamba wakati watu wanashikilia suala la akaunti ya ESCROW ya IPTL kuwa na utata, mkataba wenyewe hauna chembe ya utata na unatamka wazi kwamba fedha zilizowekwa kwenye akaunti ya ESCROW ni mali ya IPTL na serikali ya Tanzania wakati Benki Kuu ni wakala anayetunza akaunti hiyo.
Kwa vipi nchi za Magharibi ambazo zinajua ukweli wa kuhusika kwa mabenki na makampuni yao katika mgogoro wa kifisadi wa IPTL zinatoa shutuma kwa Tanzania na kutoa masharti ya kupata misaada badala ya kushirikiana na Tanzania kuziweka kizimbani kampuni na benki zinazohusika katika mgogoro wa kifisadi wa IPTL?
Katika madai na hukumu zilizokwisha kutolewa nje ya nchi, udhalimu wa IPTL ulikuwa unaibuliwa hasa kuhusiana jinsi wakurugenzi wa kampuni hiyo kwa kushirikiana na mabenki ya nje na wakora walivyokuwa wanatumia njia za kihalifu kuparanganya mahesabu na kufanya kama vile IPTL imekopeshwa fedha kumbe hayo ni madeni hewa ambayo inabebeshwa IPTL.
Wanaonufaika ni wakurugenzi binafsi wa Mechmar na wakurugenzi wa mabenki ya kimataifa.
Kwa mfano tangu mitambo ya IPTL ilipoanza kufua umeme, kiasi kikubwa cha fedha zaidi ya dola milioni 200 zilikuwa zimelipwa kwa IPTL kabla ya kufunguliwa akaunti ESCROW Benki Kuu ya Tanzania.
Fedha hizo zilikuwa ni kiasi kinachotosha kulipa madeni ya IPTL. Kwa vipi wakurugenzi wa IPTL na Benki ya Standard Chartered waliamua kutotumia fedha iliyopatikana kulipa madeni kwa wadai ni kitendawili.
Lakini habari za uhakika zinasema kwamba wakurugenzi wa kampuni ya Merchmar ambayo ilikuwa na hisa nyingi katika IPTL kwa kushirikiana na wakurugenzi wa Benki ya Standard Chartered waliamua kuzungusha fedha walizolipwa na TANESCO badala ya kulipa deni. Kwa upande mmoja watakuwa wamepata faida binafsi na kwa upande mwingine watakuwa wameongeza madeni kwa IPTL na kuchelewesha kupanua uwezo wa IPTL kufua umeme zaidi kwa kutumia gesi badala ya mafuta mazito na kupunguza gharama za uzalishaji.
Sakata la IPTL halikuanza leo ambapo Umoja wa Ulaya na baadhi ya wanachama wake wameamua kusitisha misaada. Tangu awali bendera nyekundu ilishaonyeshwa kwamba kampuni ya Mechmar ambayo ilikuwa inamiliki asilimia 70% ya hisa zote katika IPTL kwa kushirikiana na mabenki na makampuni ya uhandisi yaliyoko Umoja wa Ulaya yalikuwa yamesuka njama za kifisadi kwa madhumuni ya kuhamisha mtaji kutoka Tanzania kwa kubuni madeni hewa na kuzidisha viwango vya uwekezaji ili TANESCO ilipe kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya Capacity charge.
Benki zilizohusika ni benki ya Standard Chartered ya Uiengereza yenye matawi yake Hong Kong, Malysia na Tanzania na kampuni ya Uhandisi ya Watsilla ya Uholanzi na Finland ambayo ilikuwa na kazi ya kusanifu, kufunga na kusimamia mitambo hapa nchini. Kwa nyaraka zilizopo mabenki na makampuni hayo yamehusika kwa kiasi kikubwa katika kukuza mgogoro wa IPTL na kusababisha hasara kubwa kwa maslahi ya Tanzania.
Benki na kampuni hizo kwa nyaraka tofauti yalikuwa yanaghushi nyaraka na kushuhudia uongo kuhusiana na gharama halisi za kununua mitambo na kutoa huduma nyingine za kiufundi na pia kuhusiana na uchukuaji na urejeshaji madeni kwa njia za ujanjaujanja.
Habari za kampuni ya IPTL kuwa na mkakati wa kifisadi ndani na nje ya nchi zilianza kujitokeza tangu mwaka 2002 ambapo kampuni ya VIP Engineering and Marketing ya wazawa ikiwa na asilimia 30% katika IPTL iliyoingia ubia na kampuni yaMechmar ya Malysia kupeleka kesi mahakamani ikitaka itolewe amri ya mahakama ya kuifilisi IPTL ili ubia ufikie kikomo na kila mmoja alipwe haki zake kwa kulingana na hisa alizokuwa nazo na pia faida iliyopatikana.
Kwa upande mwingine mkataba huo unaelekeza namna ya kuingiza pesa zitokanazo na mauzo ya umeme kwa TANESCO, kutoa pesa kwa ajili ya kuwekeza pesa hizo katika miradi mbalimbali na kwa vipi faida itakayopatikana inakwenda kwa nani.
Katika gazeti moja la kila juma (siyo Taifa Imara) liliandika makala iliyosomeka kwamba, "BOT iliwekeza dola za Marekani milioni 22 nchini Ufaransa, iliwekeza shilingi bilioni 48, katika Hati Fungani (Treasury Bills) za siku 182 na shilingi bilioni 8, zilikuwa salio katika akaunti zilizowasilishwa baada ya uwekezaji kufanyika"
Waandishi wa makala hiyo inayozungumzia BOT kutumia kiasi cha pesa za akaunti ya ESCROW kuwekeza katika masoko ya mitaji ndani na nje ya nchi ni jambo ambalo limo katika mkataba wa kuanzishwa kwa akaunti ya ESCROW. Vinginevyo fedha hizo zingekuwa na faida gani kama zingebaki kuwa mtaji mfu (dead capital).