Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 2,814
- 11,991
Hayo yameelezwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, Agosti 26, 2023 Mkoani Kilimanjaro alipokuwa akizungumza katika Hafla ya Jubilei ya miaka 50 ya Shule ya Sekondari Uru iliyopo mkoani hapo ambapo amesema katika kutekeleza mageuzi hayo Serikali inawahitaji Wadau ili kwenda sambamba katika mageuzi hayo.
Prof. Mkenda ameeleza mchakato mzima wa ukusanyaji maoni ulihusisha Wadau mbalimbali ambao walitoa mchango mkubwa katika kupatikana kwa rasimu hizo, hivyo Serikali imeona umuhimu kwa Wadau hao kushiriki kuweka mikakati ya utekelezaji.
“Rasimu ya Mapitio ya Sera na mabadiliko ya Mitaala zitakapopitishwa rasmi na mamlaka husika na kuwa tayari kwa ajili ya utekelezaji, tutakutana tena na kushirikisha taasisi zote za dini za Kiisilamu na Kikristo pamoja na sekta binafsi kuona ni vipi tunajiandaa kwa pamoja katika kutekeleza mageuzi haya ili na nyie mchangie katika hilo kwa sababu tunawahitaji sana,” ameelezea Waziri Mkenda.
Kiongozi huyo ameongeza kuwa kazi ya kufanya mabadiliko ya Mitaala imefanyika kwa kipindi cha miaka miwili kwa kushirikisha Wadau ambapo amesema maandalizi ya Mtaala wa somo la dini umeshirikisha madhehebu yote ambayo kwa pamoja yalikubaliana kwamba ni mtaala sahihi, huku akiwataka Wadau kutembelea Tovuti ya Taasisi ya Elimu Tanzania ili waweze kuiona mitaala hiyo pendekezwa na kama kuna lolote lisilo sawa.
Kuhusu kuanza kwa Mtaala wa masomo ya amali Waziri huyo amesema unaweza kuanza kutekelezwa katika shule tisa za ufundi zilizopo nchini ambazo tayari zilishatembelewa, kufanyiwa tathimini pamoja na kutengewa fedha kwa ajili ya kutoa mafunzo ya ufundi uhandisi. Amezitaja shule hizo kuwa ni Tanga, Moshi, Ifunda, Iyunga, Musoma, Mtwara, Bwiru, Shinyanga na Chato kwamba utaratibu umewekwa kuwawezesha wahitimu kuendelea na Elimu ya Juu.
Akizungumzia uwekezaji katika sekta ya elimu amesema katika uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita fedha nyingi zimetolewa ambazo zimewezesha ujenzi na ukarabati wa miundombinu ambayo imetoa fursa kwa watoto wanapomaliza elimu ya msingi kujiunga kidato cha kwanza kwa mara moja tofauti na zamani ambapo ililazimika kusubiri awamu ya pili na pia hakuna tena zoezi la wazazi kulazimishwa kutoa michango ya ujenzi ili kuwezesha watoto kupata madarasa.
“Hiki ni kiashiria cha namna uwekezaji mkubwa unavyofanywa na Serikali, tunaona fedha zinatengwa, shule zinajengwa zinakamilika wanafunzi wanaingia hakuna tena kukimbizana na wazazi kuhusu michango, ingawa kwa hiari wazazi wanaweza kuchangia maendeleo ya elimu,” amefafanua Waziri huyo.
Kwa Upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo la Moshi, Mhashamu Baba Askofu Ludovick Minde amemshukuru Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda kwa kusimamia vyema sekta ya elimu na maono ya Skt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu na ujuzi utakaowawezesha kujitegemea na kuchangia katika uchumi wa Taifa.
Kwa upande wake Katibu wa Elimu Msaidizi Jimbo Katoliki la Moshi, Padri Peter Asantebwana amesema kuwa katika mabadiliko ya mitaala wao kama Wadau wakubwa wa elimu wanaiomba Serikali isiwasahau katika mageuzi hayo kwa kuwasaidia kuwapatia vitabu, vifaa vya kufundishia na kujifunzia ikiwemo vifaa vya maabara ili nao waweze kutekeleza kwa ufanisi na weledi katika kuwapatia elimu bora watoto wa Kitanzania.