Waziri Masha apasuliwa bomu

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
headline_bullet.jpg
Wananchi wamtajia polisi washiriki ujambazi
headline_bullet.jpg
Aonya iko siku viongozi watapigwa mawe



Masha%286%29.jpg

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha.



Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrence Masha, ametajiwa majina ya polisi wawili waliohusika katika mauaji ya watu 14 na kuwajeruhi wengine 18 kisiwani Ukerewe, mkoani Mwanza.
Watu hao waliuawa na majambazi katika kisiwa kidogo cha Izinga Januari 17, mwaka huu, walipokuwa wakijaribu kuzuia boti iliyotumiwa na majambazi waliovamia kisiwa hicho na kupora mali za wafanyabiashara.
Wananchi hao walimweleza Waziri Masha juzi wakati akiwahutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Bwisya kuwa kuna askari wawili, akiwemo aliyekuwa mkuu wa polisi wilayani Ukerewe na askari mmoja waliyemtaja kwa jina moja la Mrisho, kuwa walishiriki katika tukio hilo la uhalifu.
Wananchi hao walisema kuwa pamoja na kutuhumiwa askari hao hawakuchukuliwa hatua zozote, badala yake walihamishwa katika vituo vyao vya kazi tu.
Baada ya wananchi kumtajia majina ya polisi hao, Waziri Masha alisema serikali haitakubali kuharibiwa sifa na watu wachache wanaokiuka maadili ya kazi yao, na akawaagiza viongozi wote, ikiwemo kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya na mkoani Mwanza, kufanya uchunguzi dhidi ya askari wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo vya ujambazi.
Alisema kuwa askari wamaeajiriwa kwa ajili ya kulinda raia pamoja na mali zao na siyo kufanya vitendo vya uhalifu na kuonya kuwa askari yeyote atakayebainika kufanya vitendo hivyo, atawajibishwa kisheria ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.
“Viongozi wenzangu, nafikiri mmeyasikia. Siyo rahisi mtu huyo huyo anatajwa kila sehemu...hapa lazima kuna tatizo,” alisema na kuongeza: “Lazima mfuatilie na hatua zichukuliwe. Iko siku tutapigwa mawe na wananchi wakichoka.”
Masha aliwataka watu wanaoendesha vitendo vya uhalifu visiwani humo kujisalimisha mara moja na kuaacha kazi hiyo kwa kile alichoeleza kuwa serikali imejipanga vilivyo kukabiliana nao.
Pia aliwataka wananchi kutoa ushirikiano wa karibu kwa Jeshi la Polisi kwa kuwataja watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu katika maeneo yao.
Alisema kuwa serikali ilisikia kilio cha muda mrefu cha wananchi wa Ukerewe kupitia kwa Mbunge wa jimbo hilo, Balozi Gerturude Mongella, cha kuimarisha ulinzi katika visiwa hivyo na kuamua kuunda wilaya ya kipolisi katika kisiwa cha Ukara ili wananchi waishi kwa amani na utulivu.
Akizungumza katika mkutano huo, Balozi Mongella aliishukuru serikali kwa uamuzi huo na kufafanua kuwa kama askari watakaopelekwa katika wilaya hiyo ya kipolisi watawajibika ipasavyo, watasaidia kwa kiasi kikubwa kukomesha vitendo vya uhalifu ambavyo vimekuwa kero ya muda mrefu kwa wakazi wa visiwa hivyo.
“Napenda kuishukuru serikali kupitia kwa Rais wetu na Waziri Mkuu na wewe mwenyewe (Masha) kwa kusikia kilio hiki cha wana-Ukerewe, kwa kweli nimefarijika sana na ninakuomba umfikishie salaam zangu Rais wetu,” alisema Mongella.
Hata hivyo, Mongella aliitaka serikali kuboresha maisha ya askari polisi pamoja na askari wa Jeshi la Magereza hususan kuwajengea nyumba bora ili wawe na maisha mazuri, hali itakayowapa moyo wa kufanya kazi na kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Katika hatua nyingine, Masha aliliagiza Jeshi la Polisi, Magereza na serikali wilayani Ukerewe kushirikiana kujenga kituo kikuu cha polisi katika wilaya ya kipolisi ya Ukara, badala ya kutegemea bajeti ya serikali.
Waziri Masha alitoa agizo hilo baada ya kukagua jengo la mahakama ya mwanzo katika katika kijiji cha Bwisya, ambalo linatumika kama kituo cha polisi.
Alisema mazingira aliyoyaona katika eneo hilo hayaridhishi kabisa kwa sababu jengo hilo ni bovu na chakavu na kuviagiza vyombo hivyo kushirikiana ili kujenga kituo hicho mapema iwezekanavyo.
Alisema mafundi katika ujenzi huo watatoka katika Jeshi la Magereza kwa lengo la kuharakisha ujenzi huo.
Alisema kuwa kituo hicho kilipangwa kujengwa kwa bajeti ya mwakani, lakini akasema hali aliyoishuhudia hairuhusu kusubiri bajeti ijayo. “Hatuwezi kuchezea maisha ya wananchi kwa kusubiri bajeti ya serikali, hivyo ninawaagiza Polisi, Magereza na uongozi wa wilaya kuhakikisha kituo hicho kinajengwa mara moja na serikali kuu itashiriki kikamilifu,” alisema.
Akisoma taarifa ya wilaya, Mkuu wa wilaya hiyo, Queen Mlozi, alisema katika tukio la mauwaji ya watu 14 katika kisiwa cha Izinga, tayari watu 40 wamekamatwa na kulipongeza Jeshi la Polisi kwa operesheni iliyofanywa katika kisiwa hicho.



CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom