By
Jamvi Habari
August 29, 2018
– Wasababisha iamuliwe kuilipa Benki ya Standard Chartered ya Hong Kong zaidi Bilioni 338.8/- pamoja na riba na gharama za uendeshaji kesi
-Walaumiwa kuweka mbele maslahi binafsi na kuacha kuisaidia nchi kushinda kesi
– TANESCO haikupaswa kushtakiwa na benki hiyo kwa kuwa haina mkataba nao, IPTL walishasaini kinga ya kisheria kwa madai yote dhidi ya serikali kwenye suala hilo kuwa wao ndio wahusika ‘Indemnity Deed.’
– Zitto Kabwe aibuka, aikingia kifua Serikali aitaka isikubal kulipa
MASUALA TATA
1. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kushindwa kuzichukua na kuzisimamia kesi miaka minane mfululizo
2. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na TANESCO kuacha kutekeleza matumizi ya hati ya kinga (Indemnity Deed) iliyotolewa na IPTL/PAP
3. TANESCO/Mwanasheria Mkuu kutowashirikisha IPTL/PAP katika mashtaka yanayowahusu
4. TANESCO kuendelea kuitumia kampuni hiyo hiyo ya uwakili kwa mabilioni ya fedha na kuendelea kushindwa kesi
NA Hamis Kufakunoga, Dsm
LICHA ya serikali kutumia mabilioni ya shilingi, kuwalipa wanasheria kuiwakilisha nchi katika mashauri mbalimbali yanayoikabili kupitia taasisi mbalimbali zinazoshtakiwa katika mahakama za kimataifa, bado tija ya utumiaji wa wanasheria hao imekuwa ndogo.
Inadaiwa hakuna manufaa kwa nchi, badala yake wengi wa wanasheria wanaopewa kazi za kuwakilisha serikali wamekuwa wakizitumia kazi hizo kibiashara zaidi na kuwaza watapata nini, kuliko kuwaza njia bora ya kuweka mazingira ya ushindi wa kesi hizo.
Mapema Aprili mwaka huu, gazeti hili liliandika juu ya hatari ya wanasheria wa kampuni binafsi kuendelea kutafuna mabilioni ya serikali kupitia shirika la umeme nchini (TANESCO), katika kuliwakilisha kwenye mashauri yakiwemo ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi Migogoro ya Uwekezaji (ICSID), ambapo TANESCO inashtakiwa mashauri kadhaa na Benki ya Standard Chartered Hong Kong (SCBHK).
Licha ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuishauri TANESCO kutoendelea na kesi hizo na badala yake kujikita katika kutafuta fedha za kulipa, kwani uwezekano wa kushinda ni mdogo jambo ambalo ni nafuu kwa TANESCO na nchi.
Kwani serikali isingelipa fedha yoyote hususani kwenye kesi zote zinazoihusisha dhidi ya benki hiyo kutokana na makubaliano ya kisheria (Hati ya kinga na dhamana – Indemnity Deed), baina ya serikali na IPTL yanayoitaja kampuni hiyo kuhusika na ulipwaji na gharama zitakazopelekwa dhidi ya serikali katika jambo lolote linalohusiana na fedha za akaunti ya ESCROW.
Aidha, sambamba na CAG kutoa ushauri huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli, tayari ameshaweweka msimamo dhidi ya utaratibu wa serikali kutumia mawakili binafsi kuitetea katika mashauri mbalimbali, kunaigharimu serikali kwa kuilipisha kiasi kikubwa cha fedha hasa mashauri ya kimataifa na mengi ya mashauri hayo kuifanya serikali kushindwa.
Hivi karibuni Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi Migogoro ya Uwekezaji (ICSID), imeikataa rufaa ya TANESCO iliyokuwa ikiwakilishwa na wanasheria wa kampuni ya Crax Law Partners wakishirikiana na RK Rweyongeza & Co. Advocates kupinga hukumu ya kuilipa Benki ya Standard Chartered takribani Sh. Bilioni 338.8 (USD 148.4 Million).
Kutokana na hukumu hiyo, TANESCO inatakiwa kulipa fedha hizo kama ilivyoamriwa katika hukumu ya mwaka 2016 ambapo fedha hizo ni madai ya malipo ya umeme baina ya TANESCO na Kampuni ya IPTL iliyopewa zabuni ya kufua umeme wa dharura kuanzia Mei 26, 1995.
Kwa kile kinachoitwa kuwa IPTL ilikuwa ikidaiwa na benki hiyo ya Hong Kong, kutokana na mkopo iliochukua kutekeleza mkataba kati yake na TANESCO, ambao kwa mujibu wa hukumu hiyo TANESCO imeagizwa kulipa gharama zote za uendeshaji wa shauri hilo ikiwemo ada ya kesi na malipo ya wajumbe wa kamati waliolisikiliza.
Taarifa za kuaminika zilizopata kuandikwa na gazeti hili, zinaeleza katika ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG), ilieleza kuwa mnamo Septemba 2010, TANESCO ilishitakiwa na Benki hiyo kulipa kiasi cha Dola za Kimarekani milioni 258.7, kilichotokana na madai ya malipo ya uzalishaji umeme pamoja na fidia ya kutolipa madai ya uzalishaji umeme na uharibifu uliosababishwa na TANESCO kutoilipa IPTL kwa wakati.
Ilisema maamuzi ya mwisho yaliyotolewa Septemba 12, 2016 yaliitaka TANESCO kuilipa SCBHK, ikijumuisha fidia ya kiasi cha Dola za Kimarekani 148.4 (Fedha zilizokuwepo katika akaunti ya ESCROW ).
Baada ya hukumu, TANESCO ilipinga maamuzi hayo kwa kukata rufaa Mahakama ya ICSID, kisha kuwasilisha utetezi wake Agosti 21, 2017 ambapo baadaye SCBHK iliwasilisha pingamizi juu ya utetezi wa TANESCO.
Tangu kipindi hicho, TANESCO imekuwa ikitumia gharama kubwa za uendeshaji kesi hiyo, ambapo jumla ya Sh. bilioni 7.58 zimetumika ikiwa ni jumla ya Sh. bilioni 3.65 kwa mwaka wa fedha 2014/2015 na Sh. bilioni 3.93 kwa mwaka wa fedha 2015/2016 .
“Hata hivyo, suala hili litarejeshwa kwa mamlaka za kisheria za ndani ambapo utekelezaji wake kisheria utazingatia uwezo wa kulipa wa TANESCO, ambapo licha ya kiasi kikubwa cha fedha zinazotumika kwenye kesi hiyo, hakuna uhakika wa kushinda,” umenukuliwa taarifa ya CAG.
Ripoti inaeleza TANESCO inapaswa kuandaa mpango wa utafutaji fedha za ziada ili kujiandaa ikitokea maamuzi ya kesi yakiipa ushindi SCBHK, TANESCO iwe tayari kulipa fedha hizo kwa wakati, ambapo hata hivyo ulipaji fedha itakuwa ni kitanzi kwa serikali ambayo haihusiki kwa namna moja ama nyingine.
Taarifa zaidi zinaeleza wakati wa mgogoro wa IPTL, kampuni ya PAP iliingia makubaliano na serikali ili ijipatie mamilioni yaliyokuwepo kwenye akaunti ya ESCROW, kwa kuingia makubaliano ya kisheria yanayojulikana kwa jina la ‘Deed of Indemnity,’ chochote kikitokea iwe kesi au madai wa kudaiwa ni IPTL na si serikali, katika hati ya kisheria iliyosainiwa Oktoba 27, 2013 mbele ya Harbinger Sing Sethi, kama Mwenyekiti na mtendaji mkuu wa IPTL na James Makandege kama katibu na mshauri mkuu wa kisheria wa kampuni ya IPTL.
‘Indemnity Deed,’ hiyo (Hati ya Kinga) inaitaja kampuni ya IPTL kuwa ndiye atakayebeba mzigo wote wa madeni, hasara, malalamiko ikiwemo uwepo wa kesi baina ya Tanesco na benki hiyo kesi ambazo kimsingi Tanesco haiwahusu kutokana na ukweli kwamba shirika hilo la umma la uzalishaji umeme halijawahi kuwa na mkataba wowote wa kibiashara na benki hiyo.
Utafiti wa kitaalam wa gazeti hili unaonyesha kuwa badala ya mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali, kuishauri Serikali kupitia TANESCO kuanza kutunza kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kuilipa benki hiyo pekee, pia CAG angeshauriana na ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kufanikisha utekelezaji wa hati hiyo ya kinga ‘Indemnity Deed,’ ambayo inaiweka serikali salama bila kulipa hata senti moja ya fedha na mzigo huo wa malipo kuwaangukia Sethi na wenzake kama alivyofanya mwanasheria mkuu kwa kuanzia.
Aidha, miongoni mwa mambo yanayoleta mashaka kwa ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kupenda kutumia wanasheria binafsi katika masuala hayo kunazua swali kuu lenye utata, wa kwanini tangu mwaka 2014 walipoanza kushtakiwa na benki hiyo, ofisi haijaichukua kesi na kuiendesha yenyewe ili kupunguza gharama na kutoa ushauri sahihi kwa serikali.
Swala lingine linalozua ukakasi katika ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kwa kipindi chote cha kati ya mwaka 2013 zilipotolewa fedha za ESCROW hadi 2016, ilipotolewa hukumu ya benki hiyo kulipwa mabilioni hayo, kwanini ofisi haikushughulikia utekelezwaji wa hati hiyo ambayo ingeiacha serikali bila kuiingiza hasara yoyote (Indemnity), badala yake ofisi na wanasheria wake binafsi wakaendelea kuishauri serikali kuitia TANESCO kukata rufaa huku ikijua kuwa haina kesi ya kujibu na badala yake anayepaswa kulipa kiasi hicho cha fedha ni kampuni ya IPTL.
Kadhalika swala lingine linalotia ukakasi kwenye jambo hilo, kwanini kwa kipindi chote cha kuanzia mwaka 2013 hadi 2016, TANESCO na ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali haikuishirikisha kampuni ya IPTL kama mdau muhimu kwenye sakata hilo kutokana na ukweli kampuni hiyo ndio mnufaika wa mamilioni yaliyokuwemo kwenye akaunti ya ESCROW, tayari ilishasaini hati ya kinga (Indemnity Form) kuikinga serikali.
Uchunguzi wetu umeendelea kuibua maswali mengi ikiwemo inawezekanaje shirika hilo la umeme nchini na ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kwa kipindi chote cha zaidi ya miaka minane iwe inawakilishwa na wanasheria wa kampuni moja tu na wabia wake katika mashauri mbalimbali na mengi ya mashauri hayo kuangukia pua kwa serikali kushindwa, kisha kuiongezea nchi deni la taifa mpaka hivi karibuni ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kufikia kuinyang’anya kampuni hiyo kesi yake dhidi ya kampuni Symbion.
Naye Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi wa Chama cha ACT- WAZALENDO Zitto Kabwe, alikuwa ni miongoni mwa wabunge waliolivalia njuga sakata la ESCROW bungeni, ameonyeshwa kushangazwa na serikali kuendelea kusumbuliwa na jambo hili wakati ni jambo lililo wazi na muhusika wa kulipa ama kutaifishwa mali zake yupo wazi kabisa na si serikali.
“Nashangaa kwanini mpaka sasa serikali inahusishwa na jambo hili, anayedaiwa hapa si serikali, anayedaiwa na anayetakiwa kulipa ni IPTL/PAP ambao ndio wamechukua hizi fedha…Serikali haipaswi kulipa hata senti tano, Indemnity itumike,’’amenukuliwa Kabwe.
Mmoja wa wanasheria maarufu nchini ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini ameipongeza ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali kwa kubadili mambo mengi ya kimfumo katika ofisi hiyo, amempongeza Rais Magufuli kuanzisha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, ambayo ipo chini ya mwanasheria mkuu wa serikali kwa sasa imepewa wajibu wa kuitetea na kuiwakilisha nchi katika mashauri yote yanayoikabili.
“Hawa wanasheria wenzetu hawana uzalendo, linapokuja suala la kesi kama hii kitu muhimu kwao wanachokiwaza ni kiasi gani cha fedha watapata na si vinginevyo, mwanasheria mzalendo kamwe asingeishauri serikali kukata rufaa kwenye jambo jepesi kama hili ambalo tayari lina Indemnity,’’ amenukuliwa wakili mmoja mashuhuri nchini na kuongeza:
“Serikali hapa iwe makini na isikubali kulipa hizi fedha, kama wakati fedha za ESCROW zikitolewa kulikuwa na makubaliano baina ya serikali na waliopewa fedha kampuni ya PAP kuwa chochote kitakachotokea mbeleni kwanini wao wasiwe ndio wadaiwa, kwanini hawa wanasheria wasishauri iwe hivyo badala ya kuiingiza nchi kwenye hasara za namna hii.”
Alisema isifike mahala taaluma ya sheria iwe ya msaada kwa nchi na si watu wachache wawe wanaiingizia matatizo nchi, hapa nadhani ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali iwe makini na isikubali kutumbukia katika mtego wa kulipa mamilioni ya shilingi kwa watu, ambao serikali haihusiki hata kidogo.
“Kisheria aliyekuwa anadaiwa si TANESCO bali ni PAP na IPTL, ambapo serikali ilishayamaliza tangu awali kuhusiana na mambo hayo, kwani kuna makubaliano ya kisheria ambayo yako wazi,” alisema.
Alisisitiza kuwa AG mstaafu na wanasheria wa TANESCO walitakiwa wajikumbushe kitu kidogo kwenye shauri hili, wangekumbuka tu kuwa hakuna mkataba wa serikali na benki hiyo, wanachodai kwa serikali ni nini.
“Lazima tuwe wakweli kwenye mambo ya msingi, ambayo kwa namna moja au nyingine serikali ilikuwa inatoa fedha nyingi pasipokuwa na sababu za msingi na sasa haiwezekani,” aliongeza Mwanasheria huyo na kuendelea kumpongeza Rais Magufuli kwa kitendo chake cha kuunda upya timu ya mawakili wa serikali watakaokuwa wanaitetea serikali katika mashauri mbalimbali yanayoikabili iliyo chini ya mwanasheria mkuu wa serikali.