Ghazwat
JF-Expert Member
- Oct 4, 2015
- 23,718
- 66,267

Watu 50 wakiwa na watoto wadogo wamenusurika kufa, baada ya kupotea ndani ya Pori la Akiba la Selous kwa siku saba, huku wakikosa chakula na maji na kulazimika kula kinyesi cha ng'ombe, damu na mikojo ya binadamu
Watu hao ambao ni wafugaji walikuwa wakihama na mifugo yao inayokadiriwa kufikia Ng'ombe 1,780, kondoo 200 na punda 6, kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya ya Rufiji mkoani Pwani, yakiwemo Chumvi na Muhoro walielekea Morogoro, ambako walidai ndiko yalipo makazi yao
Tukio hilo ambalo si la kawaida kutokea katika pori hilo lilianzia Jumatano iliyopita wakati wafugaji hao, walipoanza safari ya kuelekea Malinyi mkoani Morogoro, wakiongozwa na wenyeji wao, waliyemtaja kwa jina la Mzee Mzigua, ambaye hata hivyo wanadai aliwalaghai na kuwatelekeza
Wafugaji hao walisema walitembea kwa siku tano ndani ya pori hilo, wakitarajia kufika Malinyi, yaliko makazi yao. Lakini hali ilikuwa tofauti baada ya mwenyeji wao huyo kuwalaghai kwa kuwapitisha njia zisizo sahihi
Walisema waliishiwa chakula na maji ya akiba na mwisho walijikuta wanatokea ndani ya pori la Akiba la Selous, huku hali zao zikiwa zimedhoofu kutokana na njaa na kiu cha maji
Wakiwa safarini mwenyeji wao huyo, aliwataka kila mmoja alipe fedha ikiwa ni ujira wake kwa kuwaonyesha njia. Walidai kuwa walimpa fedha nyingi, wengine walimlipa shilingi milioni mbili, shilingi milioni moja na wengine Sh 500,000 wakitarajia angewasaidia
Walitembea usiku na mchana ndani ya pori hilo, wakipishana na wanyama wakali kama Simba na Nyati, hivyo kuhatarisha usalama wa maisha yao na watoto wao
Hali ilizidi kuwa mbaya zaidi baada ya kutimia siku ya tano wakiwa ndani ya pori hilo, pale walipoishiwa chakula na maji hivyo kuwalazimu kuanza kuchinja ng'ombe na kunywa damu kwa ajili ya kukata kiu, pia walikula kinyesi chao ili kupunguza njaa
Yule mwenyeji wao aliwatelekeza baada ya kuona hali zao zimekuwa mbaya, alitokomea kusikojulikana, akiwaacha wasijue pa kwenda hivyo kulazimika kutelekeza mifugo yao ili kunusuru kwanza maisha yao
Hadhalika wengine walilazimika kunywa mikojo yao na mingine kuwanywesha watoto wao kunusuru maisha yao hali iliyowafanya kuathirika kiafya na kushindwa kuendelea na safari, wengine walianguka na kupoteza fahamu
"Sisi tulitaka kurudi nyumbani Morogoro huku tulikuja kununua ng'ombe tukaambatana na huyo mwenyeji wetu na mtoto wake, tunajua mpaka nyumbani kwake "alisema kiongozi wa msafara huo wa wafugaji hao aliyejitambulisha kwa jina la Lisesi Cherahani Bela na kuendelea.
Baada ya kuona hali inakuwa mbaya zaidi, alitafuta eneo ambalo lina mtandao wa simu na kufanya mawasiliano na watu mbalimbali, ambapo akifanikiwa kuwasiliana na watu wa Kigoma na kuomba msaada, ambapo watu hao waliwasiliana na Wahifadhi wa Hifadhi ya Taifa ya Mikumi na kuwasiliana na wahifadhi wa Pori hilo la Selous, ambapo walianza kazi ya kuwasaka na hatimaye kuwakuta katika eneo la Mlima Luhombelo, lililopo katikati ya Pori hilo wakiwa tayari wameshadhoofika kiafya
Askari hao wa wanyamapori waliwapatia uji na maji na kuwapa huduma ya kwanza wale wengine ambao walikuwa na hali mbaya
Baada ya taarifa hizo za kupotea kwa wafugaji hao, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Gaudence Milanzi alifika katika eneo hilo juzi, akiambatana na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) Martin Leibooki, Meneja wa Pori la Akiba la Selous, Henock Msocha na maofisa wengine wa wizara na pori hilo
Milanzi alisema Serikali inaangalia namna ya kuwasaidia wafugaji hao, kurejea katika hali zao kiafya pamoja na kuwasaidia kutafuta mifugo yao ili waweze kurejea katika makazi yao na kuendelea na shughuli zao.
Chanzo : HabariLeo