Wafahamu historia ya Tom Mboya wa Kenya?

Wa Mjengoni

JF-Expert Member
May 4, 2010
480
128
Tom Mboya alipigwa risasi katikati ya Nairobi. Ni miaka ipatayo 41 tangu siku ya tukio hilo. Ni tukio ambalo liliishtua Nchi ya Kenya, Afrika Mashariki na dunia kwa jumla.

Ni siku ambayo Tom Mboya aliyekuwa mwanasiasa maarufu na waziri katika serikali ya Rais Jomo Kenyatta wa Kenya alipouawa jijini Nairobi mchana kweupe akiwa anatoka katika duka moja la dawa katika moja ya mitaa maarufu ya jiji hilo.

Tom Mboya, mmoja wa mawaziri maarufu wa Kenya na aliyekuwa anatoka katika Kabila la Waluo (Wajaluo), aliuawa kwa kupigwa risasi na Nahashon Isaac Njenga wa Kabila la Gikuyu, siku ya Julai 5, 1969.

Kabila la Waluo linashika nafasi ya pili kwa wingi wa watu nchini humo, likitanguliwa na Wagikuyu ambalo ndilo lilitoa rais wa kwanza wa Kenya, Jomo Kenyatta.

Mboya, ambaye jina lake kamili ni Thomas Joseph Odhiambo Mboya, alikuwa ni mmoja wa waasisi wa Chama cha Kenya African National Union (Kanu) kilichotawala nchi hiyo tangu ilipopata uhuru mwaka 1963 hadi mwaka 2002 kiliposhindwa katika uchaguzi mkuu.

Wakati anauawa, Tom Mboya, alikuwa ni Waziri wa Mipango ya Uchumi na Maendeleo. Pia alikuwa ni mmoja wa wanasiasa waliokuwa wanapewa nafasi kubwa ya kuja kuwa rais wa nchi hiyo baada ya Kenyatta.

Mboya alizaliwa Agosti 15, 1930 huko Kilima Mbogo karibu na Mji wa Thika katika maeneo ambayo wakati ule yalikuwa yanaitwa White Highlands.

Alisoma na kupata elimu ya juu, akaenda Uingereza na kurejea Kenya mwaka 1956 akafanya kazi na kujiunga na siasa. Wakati huo Waingereza walikuwa wanajaribu kulidhibiti wimbi la wapigania uhuru wa Mau Mau, waliokuwa wanataka ardhi yao na uhuru wa Kenya.

Aliajiriwa na Halmashauri ya Jiji la Nairobi, akajiunga na Chama cha Wafanyakazi cha African Staff Association na kuchaguliwa kuwa rais wa chama hicho ambacho kikaitwa Kenya Local Government Workers Union.

Aliingia katika bunge ambalo miongoni mwa wabunge 50, Waafrika walikuwa nane tu.

Katika medani ya kimataifa, akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa All-African Peoples’ Conference nchini Ghana, ambao uliitishwa na Kwame Nkrumah. Wakati huo Mboya alikuwa na umri wa miaka 28 tu.

Mnamo1959, alianzisha mchakato wa kupeleka Waafrika kusoma nchini Marekani, ambapo wanafunzi 81 walihusika.

Barack Obama Sir, baba wa Barack Obama, Rais wa sasa wa Marekani, alikuwa rafiki mkubwa wa Mboya na Mluo mwenzake, yeye hakuwemo katika kundi hilo la kwanza kwani alikwenda katika Jimbo la Hawaii, Marekani.

Juhudi hizo za Mboya zilimfanya Rais John Kennedy wa Marekani mwaka 1960, kujumuisha pia wanafunzi kutoka Uganda, Tanganyika (Tanzania) na Zanzibar, Rhodesia ya Kaskazini (ambayo sasa ni Zambia) Rhodesia ya Kusini (sasa ni Zimbabwe) na Nyasaland ambayo sasa ni Malawi.

Mradi huo uliwezesha wanafunzi 230 wa Afrika kupata masomo nchini Marekani mwaka 1960 ambapo mamia zaidi walifuatia mwaka 1961.

Yote hayo yalizidi kumpa Mboya umaarufu mkubwa machoni mwa umma na akazidi kushika nyadhifa za juu kila kukicha.

Ni katika Mtaa wa Independence Avenue (ambao sasa ni Moi Avenue), mchana wa Julai 5, 1969 ambapo Nashon Isaac Njenga Njoroge alimpiga risasi na kumuua akiwa anatoka katika duka moja la madawa.

Mboya, aliyekuwa na umri wa miaka 39, alikufa papo hapo.
Baada ya kukamatwa kwake, Njoroge alisikika akisema: “Kwa nini hamuendi kumuuliza bwana mkubwa?”

Mtu huyo aliyeitwa ‘bwana mkubwa’ kamwe hakufichuliwa, jambo ambalo linaaminika mpaka leo kwamba Mboya aliuawa baada ya kuonekana angekuwa tishio kwa rais wa nchi hiyo.

Katika tukio hilo, Kabila la Wagikuyu lililaumiwa sana hasa la Waluo kwa kifo hicho ambacho kilizua vurugu kubwa nchini humo hususan wakati Kenyatta alipohudhuria mazishi ya Mboya huko Kisumu. Watu wengi walikuwa wanaamini Kenyatta alikuwa anahusika katika kifo hicho.

Mboya aliacha mke (Pamela) na watoto watano. Alizikwa katika kaburi maalum kwenye Kisiwa cha Rusinga. Kaburi hilo lilijengwa mnamo mwaka 1970.

Pamela, ambaye baadaye alizaa mtoto mmoja aitwaye Tom Mboya Jr na kaka wa marehemu Tom Mboya aitwaye Alphonce Okuku, naye alikufa mwaka 2009 wakati akitibiwa huko Afrika Kusini.
Source: Global Publishers
Karibu tumjadili Mwanasiasa huyu.
......
 
Nakumbuka hayo mauaji ya Mboya kwenye gazeti moja la kiingereza nimelisahau jina lake. Siku zile tulikuwa primary school lakini tukijitahidi kusoma gazeti hilo.

Tom Mboya alikuwa very creative na maarufu sana na umaarufu wake ndiyo uliomponza. Mzee wa watu aliogopa angenyang'anywa madaraka na kijana kwa hivyo akaamua amuondoe kabisa.

Nakumbuka kama kulikuwa na Scotland Yard waliletwa Kenya ili kusaidia uchunguzi na kuziba midomo ya watu kwani mazungumzo yalikuwa wazi kwamba ni fulani ndiye aliyeamrisha mauaji hayo yafanyike. Badala yake inasemekana walimtrace yule jamaa na kumkuta Japan ambako aliletwa Kenya kwa kushtakiwa.

Sijui kama yule jamaa yuko hai au amefariki gerezani.
 
Hakika Tom Mboya kwa Tanzania ni muhimu kukumbukwa, kwani ktk harakati za wafanyakazi kudai haki zao zidi Waajiri wa kikoloni Tom Mboya alikua mstari wa mbele kuongoza Chama ca Wafanyakazi kudai haki zao na kupinga unyanyasaji uliokua umekithiri. Hivyo Tom na hakina Rashidi Mfaume Kawawa na wanaharakati wengine wa wakati huo lazima tuwwakumbuke. Katika mchakato Vyama Vya Wafanyakazi(Trade Unions) kwa sasa vimekosa nguvu kwa kukosa Viongozi shupavu kama hakina Tom.
 
Back
Top Bottom