Vituko vya kuelekea uchaguzi 2010

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,137
WAZIRI wa Nishati na Madini, William Ngeleja amempa saa 24 Meneja wa Mamlaka ya Maji Wilaya ya Sengerema, Thomas Mwenda kuhakikisha kuwa mradi wa maji wa Nyamazugo unasambaza maji haraka kwa wananchi wa mji huu wa Sengerema na vijiji jirani.

Ngeleja ambaye ni Mbunge wa Sengerema alitoa agizo hilo juzi baada ya kufanya ziara ya kushitukiza kwenye mradi huo ambao uko umbali wa kilometa 17 kutoka Sengerema Mjini, na kukuta licha ya mradi huo kukamilika kwa asilimia 100 na kufungwa mashine mpya, lakini wananchi walikuwa wanapata huduma ya maji kwa mgawo.

“Naomba utueleze ni kwa nini bado kuna mgawo wa maji na huku mradi huu umeishakamilika? Wewe si umeoa na una familia? Nakupa masaa 24 kuanzia sasa (juzi) wananchi wa Sengerema wapate maji mara moja,” alisema Ngeleja akiwa kwenye bomba kuu la kusambaza maji katika mji wa Sengerema baada ya kuelezwa kuwa licha ya kukamilika, lakini kuna maeneo mengine ya mji hayapati maji.

“Mradi huu umeanza muda mrefu na umetumia fedha nyingi za walipa kodi, na kodi za wananchi na fedha za serikali haziwezi kuendelea kutumika chini ya kiwango, na huku ni kuwahujumu wananchi, hakikisha njia zote za maji zinafunguliwa na wananchi wapate maji haraka,”

“Tatizo hili mheshimiwa ni kubwa, maji yanapoingia hapa yana-overflow (jaa) na kumwagika, na wakati huo inabidi tuzime mashine, lakini pia siku za nyuma kulikuwepo na uwezo mdogo wa kuzalisha maji, lakini sasa hivi nitaendelea kufuatilia suala kwenye mtambo wake na njia za kusambaza maji ili nione kama kuna matatizo,” alisema meneja huyo na kuibua maswali zaidi kutoka kwa Ngeleja.

“Unasema uende kufuatilia sasa hivi kama kuna matatizo, ina maana wewe kama mtalaamu hujui kama kuna matatizo? Narudia tena achia maji full blast (kwa wingi), ukishindwa kutekeleza hili ndani ya saa 24, nasema uachie ngazi,” aling’aka Ngeleja.

Hata hivyo, Mwenda alikiri kuwa mradi huo ulitakiwa uwe umekamilika kuanzia Novemba mwaka jana, ambapo ulikuwa chini ya makandarasi Wedeco kutoka mkoani Shinyanga aliyepewa kazi ya kujenga na kutandaza mabomba na Genuine kutoka Mwanza aliyepewa kazi ya kufunga mitambo, lakini kazi hiyo haijakamilishwa.

Licha ya kupewa ufafanuzi huo, Ngeleja alisema serikali imetumia Sh milioni 900 katika kuujenga mradi huo wa maji kwa kufunga mtambo mpya na kuweka laini ya umeme na kuwa umekwishakamilika, hivyo sharti utoe huduma ya maji kwa wananchi na visingizio na maneno mengi hakuyahitaji kwa wakati ule.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya, Mathew Lubongeja aliyeongozana na Ngeleja, alisema kufika kwa Waziri huyo kwenye mradi huo kumemuondolea nafuu maana alikuwa anabanwa na madiwani na wajumbe wa Kamati ya Siasa ni kwa nini mradi huo hautoai huduma ya maji kwa wananchi licha ya kuwa umekamilika.
 
Back
Top Bottom