Viongozi wa dini wakemea ushoga

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
Viongozi wa dini nchini, wamelaani vikali kauli ya Rais wa Marekani Baraka Obama, Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron iliyoungwa mkono na Rais Mpya wa Malawi, Joyce Banda ya kutambua kisheria ndoa za jinsia moja.

Viongozi hao wa dini wakizungumza kwa masikitiko, walisema kukubali na kutekeleza kauli hizo ni balaa na laana kwa nchi kama si ulimwengu mzima.
Wa kwanza kulaani hali hiyo ni Askofu Msaidizi wa Kanisa Katoliki Jimbo la Bukoba, Mhashamu Methodius kilaini, aliyesema kuwa viongozi wa

Bara la Afrika wanajipendekeza katika nchi za Marekani na Uingereza kwa kuwaunga mkono kuhusu suala la ushoga ambalo ni kinyume na mila na desturi za Mwafrika na hata kwa Mungu.

Alisema viongozi wa aina hiyo hawana tofauti na wanaojiuza kwa wenye mali ili azma zao za kuendelea kuwepo madarakani zikamilike.
Mhashamu Kilaini aliyasema hayo wakati akizungumza na NIPASHE Jumapili kwa lengo la kutoa ufafanuzi juu ya kauli ya Rais wa Malawi ya kuruhusu mashoga kutambuliwa kama watu wengine na sheria za nchi ziwatambue bila kuathiri uhuru wao.

Naye Sheikh Mkuu wa Tanzania Mufti Shabani Bin Simba, mbali na kulaani kauli hizo, aliwataka wananchi wa Malawi wasikubali kauli ya Rais wao na waipinge kwa njia zozote zile.

“Bila kuzipinga kauli hizi, zitatengeneza balaa kubwa. Kwa kuwa viongozi wengine wa Afrika hakuna aliyetoa tamko lolote, lakini ninawaomba walaani sana, hii tunakaribisha laana na kumchukiza Mungu,” alisema.

Siku chache baada ya kauli za viongozi wa nchi za Magharibi kwamba zitawaondolea misaada nchi mbazo hazitambui haki za mashoga na wasagaji,

Rais wa Malawi Banda, kwa mara ya kwanza baada ya kuapishwa kuwa rais wa nchi hiyo, alitamka hadharani kuwa, nchi yake italazimika kubadili sheria inayopinga mapenzi ya jinsia moja, hivyo kuruhusu ndoa za jinsia moja.

Kauli hiyo ya rais wa Malawi ni ya kwanza Barani Afrika kubariki mapenzi ya jinsia moja, nchi ambayo ilikuwa mstari wa mbele kupinga mapenzi ya aina hiyo na kusababisha mahakama nchini humo kuwahukumu kifungo cha miaka 14 jela, hukumu iliyotolewa mwaka 2010 kwa wanaume wawili, Tionge Chimbalanga na Steven Monjeza waliotaka kufunga ndoa.

Hukumu hiyo ilitolewa kipindi cha utawala wa Rais Bingu wa Mutharika, hali ambayo ilimsababishia msukosuko mkubwa kutoka kwa mataifa ya Magharibi ikiwa ni pamoja na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon kwenda Lilongwe na kuhutubia Bunge la Malawi katika mkutano wa dharura kabla ya kukutana kwa faragha na Mutharika.

Baada ya Moon kuondoka nchini Malawi, wapenzi hao wawili waliachiwa huru, hali iliyotafsiriwa kuwa Katibu Mkuu huyo alikwenda kuweka shinikizo zito kwa utawala wa nchi hiyo.

Akizungumzia zahma hiyo, Mhashamu Kilaini aliwataka Waafrika kutokubali kudhalilishwa utu wao na wawe mstari wa mbele katika kukemea, kuwakataa viongozi wa aina ya Banda.

“Hawa viongozi wanajipendekeza kwa watu wa Magharibi wakidhani kuwa watawatetea na kuwasimamia ili waendelee kukaa madarakani kwa vile wanafuata matakwa yao…ni sawa na kujiuza na kuuza haki zetu,” alisema.

Mhashamu Kilaini alisisitiza kuwa mambo hayo hayaendi tu kinyume na maadili ya Waafrika, bali pia na utu lakini na taratibu za uumbaji wa Mungu.
“Unajua bwana, Mungu aliumba mtu mke na mume, ukienda kinyume na hayo unakwenda kinyume na uumbaji wa Mungu…kwa mila zetu Waafrika,

ukiona ng’ombe anafanya hivyo, utamchinja na kumuuza na kupata fedha, maana kwa kufanya hivyo unaondoa balaa na nuksi katika familia walipo wanyama hao,” alisema.

Kwa mujibu wa Mhashamu Kilaini, dunia inaelekea Sodoma na Gomora, na kusisitiza kuwa haya yanayoendelea ulimwenguni yanamkasirisha Mungu, na kama binadamu wakiyabeba bila ya kuyakemea, laana itakuwa juu yao.

Hata hivyo, msimamo na kauli ya Rais wa Malawi umekuja wakati ambapo nchi yake inatarajiwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa Umoja wa Nchi za Afrika (AU) utakaofanyika mwezi Julai, mwaka huu.

Aidha, msimamo huo unatuma ujumbe mzito kwa viongozi wa Umoja wa Afrika (AU), na ni mawazo ya Wamalawi na Waafrika kwa ujumla kufikiri kwamba umoja huo hauwezi kumaliza mkutano huo bila kulijadili suala hilo nyeti ambalo linagusa tamaduni na dini zao.

Hata hivyo, katika nchi nyingi za Kiafrika mapenzi ya jinsia moja hayaruhusiwi na ni kosa kisheria kujihusisha nayo.
Nchini Uganda, Mbunge mmoja aliwasilisha muswada ambao unataka watu wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja wapewe adhabu ya kifo, lakini

baada ya mataifa makubwa kuingilia kati na kukosoa kauli hiyo na hata kutishia kusitisha misaada yake, baadaye Mbunge huyo alibadili muswada wake na kutaka wafungwe kifungo cha maisha jela.

Waziri Mkuu wa Uingereza, Cameron, ndiye aliyekuwa wa kwanza kujitokeza hadharani kwenye mkutano wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Uswis hivi karibuni na kutamka kwamba, nchi yake itasitisha misaada kwa nchi zote duniani ambazo hazitambui haki za mashoga. Baada ya Cameron

kutamka hayo, Rais Obama wa Marekani naye akatangaza kwamba, taifa hilo kubwa litatumia uwezo wake wote ikiwamo misaada inayotoa kwa nchi mbalimbali kuhakikisha haki za mashoga zinatambuliwa na kuthaminiwa duniani.

Obama alikwenda mbali zaidi kwa kutumia rungu la misaada yake inayotoa kwa nchi mbalimbali duniani, huku ikitenga dola za Marekani milioni tatu sawa na Sh. bilioni 5.1, kwa ajili ya kufanikisha mkakati huo.

Awali Obama alisikika akisema, daima amekuwa mgumu kukubali kwamba wanaume na wanawake wenye uhusiano wa mapenzi ya jinsia moja nchini Marekani wangetendewa haki na jamii kwa kutambua uhusiano huo na kwamba amekuwa akipitia kile anachokiita mabadiliko ya kimtazamo kuhusu suala la ndoa za jinsia moja.

Alisema amejadili suala hilo na familia, marafiki na majirani kwa muda mrefu na kutilia maanani wafanyakazi wenzake na askari ambao wamejikita katika uhusiano wa mapenzi ya jinsia moja na hatimaye amekuja na hitimisho kwamba ndoa zilizozoeleka hazikidhi matarajio ya wote.

Mbali na viongozi wa dini na watu wa kada tofauti kupingana na viongozi hao wa Magharibi, lakini pia mpinzani wa Rais Obama katika uchaguzi wa rais wa mwaka huu, Mitt Romney wa chama cha Republican, amesema bado anabakia kupinga ndoa za watu wa jinsia moja.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

 
Back
Top Bottom