Vinavyofaa ni vichache

Amani Dimile

JF-Expert Member
Joined
Jul 27, 2022
Posts
243
Reaction score
399
Kwahiyo kila mtu awe makini kuuongoza moyo wake kabla ya moyo wake kuamua kumuongoza yeye. Ni kweli moyo umeumbiwa tamaa, lakini sina hakika kama tamaa zimeumbwa kwa ajili ya moyo.

Ukweli dhahiri ambao hatukufunzwa shuleni ni kwamba, si kila utakachokitamani kitakufaa, hivyo ili ufanikiwe kimaisha na kusonga mbali ni lazima ukubali kwa hiari yako kuwa sio kila hitaji la moyo wako basi litatimizwa kama unavyofikiri.

Mungu alituumba na macho akatuumba na mdomo pia. Naamini si kila kitu tutapata nafasi ya kukila kwa mdomo vingine acha tuvile kwa macho.

Mpumbavu ni yule ambae anausikiliza moyo wake unataka nini na kuupatia kila unachotaka bila kujiuliza mara mbili mbili.
Tunavyovitamani ni vingi ila vinavyotustahili ni vichache, na kama unapinga hii kauli basi pinga mpaka pale utakapojikuta kwenye shimo la majuto ili hali huna mjukuu.

Ukomo ndio unaotufanya tuishi, hivyo muungwana yeyote ni lazima awe na kikomo katika kila anachokitaka.

Usiruhusu hisia zako zikuongoze sababu hisia ni jambo la mpito ila matokeo ya hisia zako huenda yakadumu milele na milele.

Maamuzi yanayofanywa kwa hisia yana majuto mengi kuliko ahueni, kaa chini tafakari kisha chukua hatua.

Hata hivyo nahisi nimeongea vingi sana ila kama niliyoyaongea hayana maana kwako basi yaache, huenda shairi hukutungiwa wewe yanini ulichezee pambio.

Binafsi naamini kama nyoka huyu angeusoma huu ujumbe kabla hajakutana na tajiri wa rangi basi asingethubutu kufungua kinywa chake kujaribu kumla.

Vinavyotamanisha ni vingi ila vinavyofaa ni vichache


Ahsante sana kwa kunisikiliza, wenu katika kalamu
Amani Dimile


 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…