Unaomba talaka, ukipewa unabembeleza tena ifutwe!

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
Mpenzi msomaji, bila shaka ungali unatafakari mada ya wiki iliyopita iliyohoji ‘kwanini nazaa watoto wa kike watupu, wakwe wananidharau?’ na endapo utakuwa na maoni yoyote usisite kuwasilisha kupitia email ya safu hii. Naam, leo nikumegee kisanga cha msomaji wetu mzuri ambacho nimeona nidodose machache kwa faida ya wengine wanaoweza kuangukia kwenye kashkash za aina hiyo ili wawe macho. Si unajua tena mwenzio akinyolewa wewe tia maji? Au siyo?
Nianze moja kwa moja na maelezo kwenye e-mail hiyo kama ifuatavyo;
“Habari dada Flora!
Kwanza nikupe pongezi kwa kazi nzuri unayofanya ya kuelimisha umma!Hakika jina lako nimeanza kulijua siku nyingi kupitia magazetini katika makala zako za "anti flo!" Hongera.
Sasa nikupe nami yangu nadhani utanishauri! Mimi ni Mtanzania ambaye nipo ng'ambo kimasomo. Nimeondoka Tanzania mwaka jana. Nyumbani nimemuacha mke wangu na mtoto mmoja. Wakati naondoka mke wangu akiwa na mtoto alikuwa hajamaliza chuo. Katika maisha mizozo haikosekani.
Mke wangu tulizozana na kunidai talaka, kubwa alilolalamika eti hakupenda mimi nikalale kunako ujenzi wa nyumba yangu(sight) ambako nilikuwa nimeweka vifaa vya kumalizia ujenzi ikiwemo milango na madirisha, pia bati. Huko bila hivyo vifaa huibwa! Alikuwa na uhakika kuwa nalala huko wala sio kwa mwanamke kwani katika ugomvi wetu hakuwa na dalili yoyote ya kuniona kuwa naenda nje ya ndoa!
Katika ugomvi ule nilikataa kumuacha, nikamuita kaka yake, akamsihi na dada yake lakini hakusikia, nikaenda kwa watu wa ushauri nasaha lakini hakusikia! Kwa vile naondoka na shinikizo lilikuwa kubwa, siku nasafiri nikampa talaka ingawa nilimwambia kuwa bado nampenda! Nilishangaa siku chache baada ya kuondoka akaomba turudiane! Sikuwa na kinyingo nilikubali. Mei 2010 nilirudi nyumbani likizo na nikaishi naye!
Siku moja simu yake ilipotea, nikamnunulia nyingine. Tukiwa nyumbani usiku alipigiwa simu na mwanaume ambaye alimuuliza kama alishapata simu nyingine na ameipata toka kwa nani?
Akasema kaninunulia XXX (Jina langu bila kuonesha kuwa ni mume wake!) Nikaanza kupata mashaka, nikamhoji kulikoni, akaniambia hakuna tatizo! Nikachukua simu yake nikagundua kulikuwa na sms yake ambayo sikuipenda.
Nikamuuliza mahusiano yao akaniambia hawana! Nikamwambia ampigie aweke loudspeaker amwambie kuwa simu ile ameninunulia mume wangu lakini aligoma! Mie nikakasirika nikamwambia simuamini na yote alikuwa ananidanganya!
Nikampigia kaka yake simu kumweleza kadhia hiyo na nikamwambia kwa kweli sasa niko tayari kuachana na dada yake! Akaniomba aongee na dada yake.
Mke wangu akamueleza maneno mengi aliyokosea kwa kaka yake. Akamtaka anieleze na mimi kisha aniombe radhi! Mke wangu akanieleza kuwa yule bwana wakati ule tuna mzozo walikuwa wanataka kufunga ndoa ila ameamua kuachana na huo mpango. Akaniomba radhi.
Nikamwambia mpigie simu uweke loudspeaker umueleze kuwa uko nami na wala hana mpango wowote naye tena, akafnya hivyo. Yule bwana alionekana kuwa alikuwa na mambo anataka kueleza, nikachukua simu nikamwambia aridhike na hayo maelezo akasema sawa. Baadae alituma sms kuomba radhi. Nikaendelea na maisha na mke wangu.
Julai nikasafiri tena kuja masomani, mke wangu akamaliza chuo ikawa anatafuta kazi. Akanipa pasword yake ya email ili niangalie kuwa kuna majibu ya kazi ametumiwa. Nikaangalia, nilishangazwa sana mke wangu alivyokuwa akiwasiliana na huyu bwana kabla hajanidai talaka, kumbe walishakuwa na maelewano ya kimapenzi na ndio maaana alinidai talaka.
Nilishangaa kuwa aliniomba turudiane ilhali bado anaendelea kuwasiliana naye kimapenzi. Nilipata moyo kuona email yake ya mwisho aloituma anayolalamika kwa mke wangu alivyomkataa hilo kidogo lilinipa moyo. Nikamueleza mke wangu, akaniomba radhi kuwa hayo yamepita. Nikakubali!
Sasa kimepita kitambo bila kuajiriwa na tunaish kwa kusaidiwa kidogo na ndugu pamoja na kufundisha part time nilikomtafutia ingawa sio fani yake! Maisha ni magumu!Kazi tunaomba hatufanikiwi! Pango kwa sasa nasaidiwa kulipa na ndugu zangu!
Hivi karibuni aliwasiliana nami kuwa kuna kazi kwenye kampuni fulani hapo bongo linalojishughulisha na vinywaji. Ingawa hakunishauri ameniambia kuwa aliunganishiwa na binti rafiki yake. Sharti lao uwe hujaolewa na uwe tayari kufanya kazi popote. Mke wangu ameomba bila kunishirikisha na sasa amepata ameambiwa atapangiwa kazi nchi jirani. Mimi nimemkataza nikamwambia kama ni maisha magumu basi narudi nyumbani baada ya mwezi mmoja kutoka sasa!
Amekataa ushauri wangu na kuniambia kuwa sina uwezo wa kumkataza atakwenda hata kama sitaki! Nikawasiliana na ndugu zake, mmoja wao akaniambia alimshauri asichukue uamuzi wowote kabla ya kuongea nami ili tukubaliane lakini haikuwa hivyo! Dada yake alionekana kuwa anataka kuwe na ridhaa yangu ndio aondoke vinginevyo asiondoke.
Lakini mke wangu amegoma! Kinachonishangaza ni kuwa hata kazi hajapangiwa, aende kwa gharama zake, akaangalie kazi atakayopangiwa akiridhika asaini mkataba! Kuna mengi nahoji hapo!
Anti flo ukiumwa na nyoka ukiona ukuti unaogopa, hatuna maelewano na mke wangu kwa hili. Bado nampenda na nahitaj niishi naye.
Nifanyeje? Sitaki kumruhusu, Mazingira ya kazi nayaelewa hasa unapojieleza kuwa hujaolewa. Ndoa ni heshima, leo ukiikana kwa kisingizio cha kupata kazi, tunaelekea wapi? Naomba ushauri wako”. Hivi ndivyo anavyomaliza dukuduku lake msomaji wetu huyu.
Naam. Bila shaka msomaji wangu wa safu hii umempata mwenzetu huyu namna anavyopambana kuokoa penzi lake. Tokeo maelezo yake pale mwanzoni, inaonekana kuwa bibie huyo hampendi kwa dhati bwanamdogo huyu. Na ndiyo maana akatafuta kisingizio kile cha mumewe kwenda sight kulinda vifaa na hapo hapo akazusha mzozo na haraka akadai talaka.
Ushahidi wa wazi ni pale mume huyu alipofuma mawasiliano ya simu ya bibie na mwanaume wa nje. Alipombana alikiri kuwa alikuwa na mpango wa kuoana naye baada ya talaka ile. Hata hivyo yapo mambo yamejificha kuhusu mahusiano ya bibie na mwanaume huyo wa nje. Kwanini aliomba talaka na alipopewa, siku chache baadaye bibie akaghairi na kuomba amrejee mumewe?
Haidhuru, mume alikubali kurudiana. Lakini bado swali lingine ni kwanini mke huyu bado anataka kuishi mbali na mumewe kwa kufanya kazi nje ya nchi?(nchi jirani). Swali ni je, kutokana na mwelekeo wa bibie alioonyesha kuwa hana ukaribu sana na mumewe, akienda kufanya kazi hiyo ndoa itakuwa salama?
Kusema ukweli. Kijana huyu yuko njia panda na yafaa sasa mwenyewe apime. Amruhusu mkewe akafanye kazi na wakati huo huo amfuatilie kuona ndoa iko salama au la. Kipimo hicho ndicho kitakachomwezesha kuchukua maamuzi mengine magumu kama ataona udanganyifu ule wa awali bado unajirudia.
Hayo ndiyo maoni yangu lakini pia wasomaji wengine wanaombwa kuchangia mawazo kunusuru ndoa ya mwenzetu huyu. Swali langu hapa ni je, mtu aliyeoa au kuolewa ambaye kabla alikuwa na mahusiano na mtu fulani, je, ni rahisi kuua mahusiano hayo? Au kwa maneno mepesi; Ukipata chungu kipya cha zamani utakitupa? Tutajadili wiki ijayo. Pia tuma maoni yako tuzungumze.
fwingia@yahoo.com
flora.wingia@guardia.co.tz
 
Mi nafikiri jamaa anampenda sana mkewe......ila apige moyo konde.....hata biblia inasema usimuache mke wako isipokua kwa uzinzi tuu....PIGA CHINI MWANAWANE...ATAKUUA HUYO MWANAMKE NA ELIMU YAKO IWE HAIKUKUSAIDIA CHOCHOTE....SISTA DUU TU HUYO NA SIYO MKE KAMA UNAVYODHANI.....UKIIPENDA CHUKUA...KAMA UNAMPENDA SANA KUWA TAYARI KUFA...
 
hivi sheria za kidini zinasema akizini umuache?
Mi nafikiri jamaa anampenda sana mkewe......ila apige moyo konde.....hata biblia inasema usimuache mke wako isipokua kwa uzinzi tuu....PIGA CHINI MWANAWANE...ATAKUUA HUYO MWANAMKE NA ELIMU YAKO IWE HAIKUKUSAIDIA CHOCHOTE....SISTA DUU TU HUYO NA SIYO MKE KAMA UNAVYODHANI.....UKIIPENDA CHUKUA...KAMA UNAMPENDA SANA KUWA TAYARI KUFA...
 
Ampige chini kama mzee Mandela mwenyewe alimpiga chini mkewe itakuwe yeye bana...achukulie kama daladala ukikosa moja unapata nyingine.
 
Back
Top Bottom