Ukata wamkwamisha Waziri Kawambwa

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,080
Kawambwa%2827%29.jpg

Waziri wa Miundombinu jana, Dk. Shukuru Kawambwa.



Wizara ya Miundombinu imenyooshewa kidole kwamba ndiyo imekwamisha miradi ya barabara kwa kushindwa kutoa kiasi cha Sh. bilioni 300 ambazo ni madeni ya wakandarasi ili wakamilishe miradi ya barabara nchini kwa mwaka wa fedha unaomalizika (2009/10).
Hali ndiyo ilimkabili Waziri wa Miundombinu jana, Dk. Shukuru Kawambwa, alipokuwa akiwasilisha rasimu ya makadirio ya matumizi ya wizara yake mbele ya Kamati ya Bunge ya Miundombinu jijini Dar es Salaam jana.
Kwa hali hiyo sasa wizara hiyo inaingia mwaka mpya wa fedha ikiwa na mzigo wa deni la jumla ya Sh. bilioni 300, zikiwamo zilizopaswa kulipwa kukamilisha miradi ya ujenzi wa miundombinu ya barabara nchini katika mwaka wa fedha wa 2009/10.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, Anne Kilango Malecela, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa deni hilo limejulikana baada ya Waziri Kawambwa, kusoma rasimu ya bajeti ya wizara yake jana.
“Rasimu ya bajeti iliyowasilishwa na mheshimiwa waziri, inaonyesha wizara inadaiwa Sh. bilioni 300, zikiwamo za makandarasi,” alisema Kilango alipotakiwa na Nipashe kueleza kilichojiri katika kikao hicho cha jana.
Hata hivyo, hadi tunakwenda mitamboni jana jioni, kikao hicho chini ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Bunge, Mohammed Missanga, ambaye ni Mbunge wa Singida Kusini (CCM), kilikuwa kikiendelea, ambapo wajumbe wa kamati hiyo walikuwa wakiendelea kuijadili rasimu ya bajeti ya wizara hiyo.
Kilango alisema deni hilo linaleta sababu nyingi za kuiondoa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) katika lawama za kukwamisha utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu ya barabara na kuzielekeza lawama hizo kwa wizara hiyo.
“Hapo siyo Tanroads inayokwamisha utekelezaji wa miradi ya barabara, bali wizara ina deni,” alisema Kilango, ambaye ni Mbunge wa Same Mashariki (CCM).
Kutokana na hali hiyo, alisema haoni sababu za kuinyooshea kidole kila mara Tanroads kuhusu kukwama kwa ujenzi wa miradi hiyo na kusema kwamba, japo wakala huyo wa serikali ina upungufu, “Lakini siyo mbaya kiasi hicho”.
Naye Missanga aliunga mkono kauli ya Kilango na kusema: “Hilo (la kutoilaumu Tanroads kukwamisha ujenzi wa miradi hiyo) halihitaji mjadala. Jinsi ambavyo mabishano na vyombo vya habari yanavyofanyika ndivyo unavyokuza jambo.”
Katika hatua nyingine, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, imeridhia uundwaji wa Mfuko wa Misitu kwa ajili ya kurejesha misitu katika maeneo ilikovunwa.
Uanzishwaji wa mfuko huo utaigharimu serikali Sh. bilioni 26 zitakazopatikana katika makusanyo ya fedha za misitu.
Uamuzi huo umefikiwa baada ya kamati hiyo kukutana na viongozi na watendaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii katika ofisi ndogo za Bunge, jijini Dar es Saalam jana.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Hassan Rajab Khatib, ambaye ni Mbunge wa Amani, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa kamati imeridhia uundwaji wa mfuko huo kwa vile kwa sasa misitu imekuwa ikivunwa, lakini maeneo ilikovunwa yanabaki wazi.



CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom