Uhalifu Mlima K`njaro waongeza umasikini

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,314
33,108
Uharibifu kili.jpg

Diwani wa Kata ya Machame Mashariki, Rajabu Nkya, akiwa karibu na mti ulioangushwa na wapasuaji haramu wa mbao katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro na hivyo kusababisha uharibifu mkubwa wa mazingira katika mlima huo.


Uhalifu wa ukataji miti na upasuaji wa mbao katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro ambao umefumbiwa macho na mamlaka husika, umezidi kudidimiza Mkoa wa Kilimanjaro katika lindi la umaskini.
Wataalamu wa maji mkoani humo wanaeleza kwamba kiwango cha maji ardhini (water table), kinazidi kushuka wakati ambao pia chanzo kikuu cha maji ambacho ni Mlima Kilimanjaro kikiendelea kuteketezwa.
Wakizungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti, wananchi wa vijiji vinavyozunguka hifadhi ya mlima huo walisema katika miaka ya hivi karibuni wameshindwa kuendesha kilimo cha mbogamboga kwa kuwa mito na mifereji imekauka hivyo wanakosa maji ya kumwagilia mashamba yao.
Mkazi wa Kijiji cha Kifuni, Kata ya Kibosho Magharibi, Peter Boniface, aliiambia NIPASHE kwamba hali hiyo inaongeza umaskini kwa wananchi ambao wanategemea kilimo kama njia kuu ya uchumi.
“Kwa sababu mifereji yote imekauka, kwa sasa tunaziba maji kwenye mto unaotiririsha maji kidogo kazi hiyo inafanyika usiku kucha halafu alfajiri mwanakijiji anayekuwa ameziba maji hayo anaenda kuyafungulia kwa sababu yanakuwa mengi kiasi ndipo anamwagilia shamba lake, ijapokuwa haitoshelezi uwamgiliaji,” alisema.
Alisema hata maji ya kutumia nyumbani wanalazimika kununua ya bomba kwa kuwa vyanzo walivyokuwa wakitegemea vimekauka.
Katika maeneo mengine hali ni hiyo hiyo ambayo imesababisha mgawo wa maji katika Manispaa ya Moshi hususan kwa wakazi wa Pausa na Soweto ambao hawapati maji kwa saa 24 kama ilivyokuwa imezoeleka.
Ofisa Maji wa Bonde la Pangani, Philipo Patrick, alisema maji yamepungua kwa kiasi kikubwa kwa sababu ya shughuli za kibinadamu na mabadiliko ya tabianchi.
Alitoa mfano kwamba mwaka jana mvua zilinyesha chini ya wastani hivyo kuathiri mtiririko wa maji hadi kwenye bwawa la Nyumba ya Mungu linalotumika kuzalisha umeme.
“Wiki ya 38 ya mwaka jana hadi wiki ya pili ya mwaka huu, maji katika bwala la Nyumba ya Mungu ni mita za ujazo 683.53 kiasi ambacho kinaweza kuzalisha umeme, lakini tumewaandikia wadau wa bwawa hilo ikiwemo Tanesco kuwajulisha juu ya hali hiyo, tumewaandikia pia wakulima kupitia vyama vyao juu ya kuendelea kupungua kwa maji ili pengine kupunguza migogoro baina yao na wafugaji,” alisema.
Alisema upungufu wa maji unaendelea kusababisha madhara makubwa ya kijamii na kiuchumi kwa kuwa wananchi watashindwa kulima kwa uhakika.
Hata hivyo, alisema upungufu huo unaongeza uharibifu zaidi kwa kuwa wananchi wanalima hadi kwenye vyanzo vya maji jambo ambalo ni hatari.
Akizungumzia Ziwa Jipe, alisema linakaribia kabisa kutoweka kwa sababu limemezwa na magugu maji.
Akizungumza na NIPASHE, Meneja Umwagiliaji wa Kiwanda cha Sukari cha Tanganyika Plantation Company (TPC), Mhandisi Brighton Nyamgege, alisema upungufu wa maji unaongeza gharama za uzalishaji kwa kuwa kiwanda kinatumia megawati tano za umeme kila siku kwa ajili ya kuendesha pampu zinazovuta maji yanayomwagilia mashamba ya miwa.
Alisema mito mingi imekauka hivyo kiwanda kinalazimika kutumia maji ya chumvi yanayotokana na mto Kikuletwa unaotoka Arusha ambayo wanayachanganya na maji ya visima yanayochimbwa na kiwanda ili kupunguza chumvi.
Hata hivyo, pamoja na kwamba kiwanda kinajiendesha kwa kutegemea pampu; mwenendo wa maji wa kila siku unaonyesha kwamba kiwango cha maji ardhini kinapungua.
“Kwa hivyo tumeanza kuchimba visima vidogo vidogo ili tuvute maji kidogo ambavyo vinamwagilia hekta 50 hadi 60… awali tulikuwa tunatumia visima vikubwa vilivyokuwa vinatumia pampu za kuvuta lita za ujazo 500 kwa saa,” alisema.
Alifafanua kwamba kiwanda kimekuwa kikifuatilia hali ya maji kila siku ili kuepuka athari zozote zinazoweza kutokea.
Alisema mito mikubwa iliyokuwa tegemezi kwa TPC kama Kikavu, Karanga na Weruweru, inatiririsha maji chini ya kiwango ambapo mita za geji zinazoruhusu umwagiliaji ni 498, lakini hivi sasa ni 456 ambazo hazifai kwa shughuli za kilimo.
Wakati hali ikizidi kuwa mbaya, mamlaka zinazosimamia Mlima Kilimanjaro zimeshindwa kudhibiti wahalifu wanaoingia msituni na kukata miti ovyo kwa ajili ya kupasua mbao, ambayo imekuwa ni biashara ya baadhi ya viongozi wa meneo yanayopakana na msitu.



CHANZO: NIPASHE
 
KINAPA uhalifu huu Mlima Kilimanjaro haukubaliki


KATUNI(614).jpg

Maoni ya katuni


Jana na leo tumeandika habari za kina kuhusu uhalifu mkubwa unaofanywa na watu wanaokata miti kwa ajili ya kupasua mbao katika msitu wa Mlima Kilimanjaro. Uhalifu huu uanaelezwa kuwa umekuwa unaendelea kwa muda mrefu sasa kana kwamba Mlima huo hauna mwenyewe.
Tumesema kuwa watu wanaingia msituni, wanakata miti na kupasua mbao kisha kuzisafirisha hadi Moshi mjini kuziuza; pia wapo wanaolisha mifugo (ng’ombe na mbuzi) ndani ya msitu na matokeo ya vitendo vyote hivi ni uharibifu mkubwa wa mazingira.
Athari za uharibifu huu unaonekana wazi katika maeneo mengi ya mkoa wa Kilimanjaro, wilaya zote za mkoa hizo ambazo zinapakana na mlima huo, yaani Rombo, Moshi Vijijini, Hai na Siha, zimeshuhudia mabadiliko makubwa ya tabia nchi, kama vile ukame wa muda mrefu, kukauka kwa mito, vijito na chemichemi ambavyo vilikuwa vyanzo vya maji ya matumzi ya binadamu, mifugo na kilimo.
Mito mikubwa katika maeneo hayo ambayo ilikuwa ikitiririsha maji mwaka mzima, kwa sasa imebakia kuwa mapito ya maji wakati tu wa masika au tuseme mafuriko. Athari ni kubwa kiuchumi kitaifa na kwa mkazi mmoja mmoja wa mkoa wa Kilimanjaro.
Ni jambo la kusikitisha kwamba pamoja na umuhimu wa mlima huu kiuchumi kwa taifa, lakini zaidi kwa uhai wa wakazi wa mkoa wa Kilimanjaro, vitendo vya hujuma za kuuteketeza vinafanywa machana na usiku bila mamlaka zinazosimamia hifadhi ya mlima huu kuchukua hatua zozote za kukabiliana na uharibifu huo.
Wapo wakazi wa maeneo hayo walioshuhudia kwamba wamekuwa wakitoa taarifa za uhalifu huu kwa mamlaka husika lakini wamekatishwa tamaa kwani hakuna kinachotokea kudhibiti hali hiyo.
Mamlaka ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA) ina wajibu namba moja kulinda mlima huu, kwa maana ya uoto wake wote wa asili ikijumuisha misitu, wanyama na mlima wenyewe, kuna askari walioajiriwa kwa kazi hiyo, kwa bahati mbaya, hawa wamebakia kulinda malango makuu ya kungia kwenye mamlaka hayo, huku uhalifu wa kutisha ukiendeshwa ndani ya hifadhi.
Itakumbukwa kwamba miaka ya mwisho mwa tisini, kulikuwa na matukio makubwa ya milipuko ya moto msituni, hasa eneo la uwanda ambako kuna majani na wanyama. Matukio haya yalielezwa kuchangiwa na shughuli za binadamu kama kurina asali na uwindaji. Operesheni nyingi zilifanyika kwa kuwashirikisha jamii zinazozunguka mlima, na mafaniko makubwa yalifikiwa. Tunajiuliza ule moyo wa kuendesha operesheni hizo ulikwenda wapi? Kuna nini miaka ya sasa.
Athari za kufyeka misitu zimekwisha kuathiri wakazi wa mkoa huu wa mapana yake, vipo viwanda vinavyohaha kupata vyanzo vya maji kwa ajili ya kuendesha shughuli zake kwa kuwa mito iliyokuwa inategemewa ama imekauka kabisa au kiasi cha maji kilichopo hakikidhi mahitaji, wengine sasa wanakimbilia kuchimba visima kwa gharama kubwa.
Wakulima waliokuwa wanalima mbogamboga kwa kumwagilia nao wako hoi, maji yamekuwa adimu mno. Hayapatikani na wakazi ambao walizoe tu kujichotea maji kwenye vyanzo mbalimbali sasa wanawajibika kunununua maji kwa bei kubwa. Mathara haya yote ni matokeo ya ufyekaji wa miti kwa ajili ya mbao.

Tunaamini Mlima Kilimanjaro bado ni muhimu kwa uchumi wa taifa, tunaelewa kuwa mlima huu ni nguzo kuu ya uhai wa wakazi wa mkoa huo, lakini kubwa zaidi, mlima huu na vyote vinavyofungamanishwa nao, yaani misitu, wanyama, majabali ya mawe na barafu iliyotanda kileleni mwa mlima, ni urithi wa taifa kwa vizazi vya sasa na vijavyo; kuachia watu wachache tu wafyeke miti msituni kama watakavyo, tunasema si haki na hali hii si ya kuvumlia hata kidodo.
Ni matumaini yetu kuwa mamlaka zinazohusika na mlima huu zitatambua wajibu wao katika kuulinda na kwa maana hiyo hatua zitachukuliwa kuhakikisha kuwa vitendo vyote vya uhalifu wa kuteketeza msitu kwa kisingizio cha kupasua mbao vitakomeshwa mara moja. Mwenye kutaka kufanya biashara ya mbao apande miti yake na kisha aivune kwa wakati wake. Uhalifu didhi ya mlima Kilimanjaro haukubaliki.



CHANZO: NIPASHE
 
Back
Top Bottom