Udom siasa au mradi binafsi?

JACADUOGO2.

JF-Expert Member
Dec 13, 2010
930
217
Elimu siku zote huchukuliwa kuwa mhimili wa maendeleo na ufanisi wa taifa lolote liwalo. Huu ni ukweli usio na walakini ndani yake. Cha ajabu ni kwamba elimu yetu (taaluma) imechanganywa na siasa! Wengi wanaliona hili na hakuna anayefungua mdomo kusema hili. Wanaofanya hivyo tuelewe fika kuwa mfumo wetu wa elimu hauwagusi wao. Tazama elimu ya sasa ya awali, msingi na ya upili, ni aibu tupu!

Ni kiongozi gani wa kitaifa mtoto wake anasomea shule za kata (vituo vya kukulia)? Naomba nizungumzie kifupi kuhusu chuo kikuu cha Dodoma/ The University of Dodoma (UDOM). Naipongeza serikali kwa kubuni, kusimamia na kuhakikisha chuo kinajengwa na kudahili wanafunzi kwa ajili ya elimu ya juu. Lakini sanjari na machache mazuri yaliyopo napata ukakasi na kukanganyikiwa kwa mengi mabaya yanayofurukuta ndani yake; kwa kugusia kidogo baadhi yake ni; mafunzo kwa vitendo (Field), maji, uchafu, mfumuko wa bei, matumizi ya dola (Polisi), malazi, rushwa, elimu duni, mikopo, dharau, magofu, siasa na taaluma, kulazimishwa kozi/ vitivo.


Kwanza; mafunzo kwa vitendo (Field): siamini kuwa humu duniani kuna masomo ya elimu ya juu yanafanyika bila wanafunzi kwenda mafunzo kwa vitendo (Field) na utafiti (Research). Ni ajabu kwa chuo kama hiki kudai kuwa baadhi ya kozi hazina mafunzo hayo na kuwa hazistahili kufanya mafunzo hayo. Shinikizo la mgomo wa 2009 Februari 15 ulisaidia kwa kiasi chake, baadhi ya kozi kupewa mafunzo hayo japo kwa shingoupande. Sijui mgomo wa Disemba 20 – 22, 2010 utaleta ufumbuzi gain katika hili. Tusubiri! Haiingii akilini kuona chuo kinakataa vitu vya msingi kama hivi kwa kisingizio cha kukosekana hela. Je, wao ndio wanaotudhamini? Au wao waliposoma hawakuwa na mafunzo hayo? Inashangaza mno vyuo vingine kwa kozi hizo hizo wana mafunzo kwa vitendo ilihali UDOM kukiwa na vikwazo na mikono ya wenye nguvu! Ieleweke mbele ya umma kuwa mwanachuo bila ya field kuna mapungufu makubwa mno!

Pili; Suala la maji: Ni aibu kwa taasisi kama hii yenye zaidi ya wakazi 20,000 kukosa maji kwa zaidi ya siku tatu mfululizo. Wakubwa wakifanya ziara kwenye huu mradi wao (UDOM) siku hiyo maji yatafunguliwa na kutiririshwa ili waone kuwa hali ni shwari. Ieleweke kuwa jumuia ya wana-UDOM si watoto wa kupewa pipi ya kijiti. Hapa si wote wanasomea au ni wanasiasa. La! Dodoma awali ni jangwa, kisha unakosa maji kwa siku kadhaa, tuishije? Kama majengo haya ya kitalu yanajengwa kwa kasi hivi kwa nini maji ya kutosha yakosekane ndani yake?tatizo fedha au utekelezaji? Naamini kinagaubaga kuwa hili lina mkono wake na linakwamishwa mahala au makusudi ama kwa ajili ya maslahi binafsi.

Tatu; Kukithiri kwa uchafu: UDOM imekuwa kama kituo cha kujaribishia ufugaji wa bata na nguruwe. Hainikai akilini kuona msomi (hata kama ni mtu baki) kuishi na kinyesi na kuchukulia kuwa ni sehemu ya maisha yake. Inastaajabisha na kutia aibu kuona majengo yaking’aa ukijani na weupe kwa juu huku mfumo taka ukiwa hobela hobela. Ingia vyooni; hakuna maji ya kuondlea vinyesi. Tazama mabomba ya maji taka, kila leo yanapasuka na vinyesi kuzagaa kama mafuriko yaliyovamia kijiji kuwasulubu wakazi. Kwa hali ilivyo utawahurumia wanaofanya usafi mabwenini (Hostels). Hali ni mbaya! Mbaya!! Mbaya ajabu!!! Ukipita eneo moja kwenda lingine ni harufu tupu. Mitaroni ni harufu kali na haiyumkini kusikia watu wakilalamakufurwa matumbo. Wachina wameshindwa nini kutatua tatizo hill? Je, sababu ni malipo au uzembe? Hili liangaliwe kwa umakini na kwa undani wake.

Nne; Mfumuko wa bei: Bei ya vitu hapa chuoni inakatisha tamaa. Nenda kwenye maduka na mgahawani (Cafteria), utazizima kwa simanzi la machozi! Ni ulanguzi juu ya ulanguzi! Wizi juu ya wizi! Kanda ya kaskazini iliyopewa nafasi ya kubebwa kuwekeza humu chuoni inatunyonya na kutuibia mali yetu kwa kiwango kisichomithilika. Kila wakijisikia bei inapanda na hakuna kuhoji. Hii ni kwa vile mikono ya wakubwa imo humo. Lakini tujiulize na kujijuza, je, wagogo na wengineo hawana mtaji wa kuwekeza hapa chuoni? Kwa nini iwe kanda ya kaskazini tu? Hapa lazima kuna jambo. Nakumbuka suluhu moja ya kupungua bei ya usafiri ilikuwa ni mgomo na bei ilishuka toka 350/= hadi 250/=. Maduka hayo hayo bei tofauti kwa nini? Waliambiwa wawekezaji kuwa hela ya wanafunzi haina kazi ama ndiyo sehemu ya kusaka utajiri kwa nguvu? Mabadiliko yanahitajika, tena ya haraka sana.

Tano; Kero ya malazi chuoni: Sanjari na kuwa majengo mengi tena ya kisasa, suala la malazi kwa wanachuo ni tatizo na ni kero kubwa. Chumba cha watu wane hulazimishwa vitanda ili waishi watu sita. Tena kubebana (yaani mtu mmoja kulala na rafiki yake). Hili limehalalishwa na kuwa utamaduni wa kudumu. Hivi magofu kama yale ya chuo cha ualimu na chuo cha lugha na sanaa (Humanities) yanafanya kazi gain? Nadhani yamejengwa kwa ajili ya maonesho tu na si kutumiwa na wanachuo. Hali inaonesha kuwa Tanzania ili haki ifikiwe lazima maandamano na migomo isiyokoma. Lakini kwa nini watu waandamane na kugoma kudai haki yao, huku wenye kuishikilia wakijua kuwa si vyema kuhodhi haki ya mtu. Waswahili husema “ Pua jeuri dawa yake mafua”. Nguvu ya umma itasema na kuamua muda ukifika.

Sita; Majengo mengi ni magofu: Ni jambo la kuhuzunisha kuona rasilimali kubwa ya taifa ikiharibiwa kwa kujenga magofu. Naita magofu kwa vile majengo yaliyopo hayakidhi kiwango. Mfano ni chuo cha ualimu, nyumba nyingi yakiwemo madarasa (Theatres) yanavuja kana kwamba yalijengwa enzi za Ujerumani. Na nionavyo mengi yataishia njiani kabla ya miaka ishirini ijayo. Unakataa! Ingia ndani uone nyufa kwenye kuta. Angalia mikanda iliyowekwa kufunika nyufa. Wachina hawajashindwa kujenga majengo imara, bali wanazidiwa na siasa. Fikiria jengo halijaisha tayari linatumika. Mifano ni mingi yakiwemo majengo ya Humanities and social sciences mpya (Haiti) na madarasa yake (Lecture rooms).

Saba; Rushwa ya chinichini: Umasikini si chanzo pekee cha rushwa na ieleweke kuwa “ maji hufuata mkondo”. Haiwezekani mwanachuo uripoti majuma mawili kabla na mwenzako aje baada ya muda huo apate chumba na wewe usipate. Kwenye vitabu kama vile “ The Beautiful One Is Not Yet Born” , “A Man Of The People” na “An Enemy of the People” tunaona jinsi mfumo (System) ulivyoharibika toka mizizi hadi majani. Hii ishara ya walezi wa mabweni (Wardens) kuhalalisha rushwa na kuharamisha utu ni kiashirio tosha cha uhalali wa rushwa hapa chuoni. Na ndivyo hali inavyoelekea kuwa, maana adha tupatazo ili tupate huduma zinajibainisha kama wasemavyo “ mwenye macho haambiwi tazama”.

Nane; Elimu duni chuoni: Ni afadhali kusoma chuo kikuu huria kuliko kuwemo kwenye kororo ya UDOM. Aibu tupu! Si madarasani, si utawala. Robo tatu ya wahadhiri ni wa shahada au shahada za uzamili. Wengi hawajiamini na ole wako ulete mtazamo mpya, utakiona mwisho wa muhula (Semester). Ama utapigwa “Supplementary” ama “Carry over”. Na hii imekuwa kaida (Fashion) ya matokeo ya chuo hiki. Si ajaa kusikia kozi fulani wamekamatwa 20, 50, 100, 300…..kawaida! Njoo kwenye elimu itolewayo, haikidhi haja wala kuendana na kiwango cha shahada. Si utani kwa aliyesoma shule za serikali ana uelewa wa juu kuliko mafunzo ya zimamoto yatolewayo hapa (Extremes). Hivi elimu ni GPA au ni uelewa wa ulichokisoma na kuweza kukifanyia kazi? Hapa tunachezewa maisha mithili ya mkulima aliyesikia mbegu akingoja majaliwa ya Mola mvua ioteshe mazao yake. Serikali na vyuo vijipange na kuweka malengo na siyo siasa na mbwembwe.

Tisa; Kero ya mikopo: Katika uombaji wa mkopo, haya huwa ni makubaliano kati ya bodi (HESLB) na mwanachuo. Inashangaza kuona kwenye hela wanajua kuchangamkia viongozi, lakini ikosapo hujiengua na kudai hawahusiki na bodi. Mbona migomo ya 2008 na 2009 ilikuwa ikifuatwa na kutolewa kwa malipo ya wanachuo? Hivi kama tatizo ni bodi kwa nini serikali isiutazame uongozi wa akina Nyatega? Au wanawaogopa? Hivi kama bodi imeridhia kukupa hela kwa nini ikupangie kiasi cha kukupa kwa muhula? Na kwa nini icheleweshe hela wakati tayari wanakuwa tayari wanajua idadi ya wanafunzi na idadi ya hela wanayotakiwa kutoa? Huu ni uzembe wa aina yake! Umma uelewe kuwa 75% ya wanavyuo wanaokopeshwa hutumia mkopo huo huo kulipia ada na gharama nyinginezo. Kwa hiyo si jambo la kutumia sheria (Law) bali mantiki (Logic) kusoma nyakati na kuamua. Kuna mantiki gain kutoa hela kwa semester moja mara mbili? Hizo zingine zinaachwa kwenye akaunti ya nani na ni kwa nini? Hii sit u ni bodi bali ni injini ya maisha ya wanachuo. Ijipange vizuri zaidi. Tuache siasa na mbwembwe kwenye taaluma, tutapiga hatua mbele zaidi. Najua wengi wa viongozi wetu hawajui machungu ya kuishi bila hela huku ukila mlo mmoja maarufu kama “pasi ndefu” (Lampard) kwani wao walisomeshwa bure ilihali wakipinga sisi tusifanyiwe hivyo miaka 50 sasa ya uhuru wetu wa bendera!

Kumi; Kero ya dharau: “Akutukanaye hakuchagulii tusi”. Hili halina ubishi wala porojo. Ilivyo hapa chuoni kila mtu ana nguvu na mamlaka yake. Si mlezi, si mhadhiri, si mkuu wa idara…..ilimradi tu kwa vile anahodhi madaraka. Tembea uone waliolewa na madaraka na kujiegemeza sehemu Fulani. Hapa chuoni tatizo la Rubagunya na Mlacha, SAK ni kero si tu kwa wanachuo bali hata kwa watumishi! Kila mmoja analia, ila anashindwa afanye nini? Hana pa kuanzia. Hakuna kusikilizwa. Kwenye mgomo wa Februari 15, 2009 na hatimaye Rais Jakaya Mrisho Kikwete kuja 17.2.2009; Rubagunya aliwaita wanachuo wanaodai haki yao kuwa ni “wanaharamu”. Naye Mlacha ana kauli moja tu “ Unanizidi urefu, ujinga na umasikini…..nitakutimua chuo”. Kwa vile yeye ni Professor. Sawa, lakini “ hakuna marefu yasiyokuwa na ncha”. Ieleweke wazi kuwa hapa hawakai wanafunzi wa shule za awali (Chekechea) wala wanafunzi wa shule ya msingi bali watu wazima tena wengine ni wakubwa (wazazi). Kwa matusi na dharau zao hizo wajue kuwa ipo siku nguvu ya umma itawahukumu. Lakini yote kwa yote tunamuachia Mungu.

Kumi na moja; Utumiaji wa polisi: Inasikitisha kuona jeshi la polisi kujifanya mbwa awindaye sungura kwa amri ya mmiliki wake! Tarehe 15 Februari 2009 kwenye maandamano yaliyoanzishwa na chuo cha ualimu na kutukutanisha eneo la Chimwaga, polisi walitumika kutawanya wanachuo pasi na kosa lolote. Wengi waliumia na kupoteza vitu vyao. Mgomo wa Desemba 20 – 22, 2010, polisi walipiga, walinyang’anya watu vitu vyao(Mfano; simu, wallet na fedha), kurusha mabomu hovyo hadi mabwenini kana kwamba watu walikuwa wanafanya mapinduzi ya nchi. Lakini hawa vibaraka wajue kuwa Tanzania ya sasa siyo ile 1970, ni wakati mpya! Maandamano ya amani yakitokea viongozi hudai kuwa ni haramu, bali yale ya kuunga mkono ulaji wa mapanki, ushiridi na bajeti hushadidiwa na watu hurusiwa watembee umbali watakao wao. Fikiria kwa mfano kauli ya James Msekela (Mkuu wa mkoa wa Dodoma) aliyotoa haitofautiani na Issa Machibia aliyotoa tarehe 29.11.2007 kufunga shule ya Musoma Technical huku mkuu wa shule (Lawrence Mwita) akisulubiwa. Je, mbona haki ilipatikana? Dodoma yatashindikana kweli? Tanzania hakuna haki bila mgomo na maandamano.

Kumi na mbili; Siasa na taaluma: Kuna dhana iliyojengwa na kukuzwa, sijui na akina naini kuwa chuo hiki ni cha kisiasa. Binafsi siliongelei kwa upande wa wanachuo, maana kwa chaguzi mbili za viongozi wa wanachuo hapa chuono (2009 na 2010) wagombea walihusishwa na nguvu ya umma (CHADEMA) na CCM. Sikatai siasa bali UDOSO (Serikali ya wanafunzi) haina chama cha siasa. Kama baadhi walijitolea kuchangisha hela zao kwa ajili ya urais na mtu Fulani, hiyo ni haki yao kama makada wa chama husika. Tatizo linakuja kwamba jinsi hali ilivyo na inavyoendeshwa hapa siasa imechukua nafasi kubwa mno! Mfano baada ya kustaafu, Mkapa aliwekwa mkuu wa chuo kikuu cha Dodoma na kwa vile hakimhusu, huja chuoni akijisikia tu. Fikiria pia kupeana shahada kulikoibuliwa. Dili ni kuingia tu kwenye siasa, mara unapewa digrii kama mgawo wa zawadi Fulani. UDOM imekuwa ni daraja la kutokea kukwea kwenda juu. Dr. Gharib Billal (Makamu wa rais) aliibukia huko kama mwenyekiti wa bodi ya chuo,; kwa sasa Shamsha Vuai Nahodha (Mwenyekiti mpya). Usishangae kuibuka rais wan chi 2015. Ni kawaida tu.

Mwisho; Kulazimishwa kitivo: Wengi wanaacha masomo ama kuhairisha mwaka kutokana na kudahiliwa vitivo ambavyo wao hawakuviomba. Mwaka 2008, chuo kilipokea makupuo (Cluster) mawili maarufu kama “makontena”. Waliotangulia septemba walau, bali waliobaki wengi walijikuta ama wakirudi nyumbani au kusoma tu hicho walichoshinikizwa. Mfano, mtu aliomba kusomea ualimu anajikuta amepangiwa kikorea au kiarabu. Ukiuliza unaambiwa, tumekusaidia. Hivi hii ni sehemu ya kutoa msaada? Sijui. Ifike mahali uimla wa viongozi wetu uishe maana nguvu ya umma ndiyo itaongea. Kwa nini mtu asibadilishiwe kitivo? Ama haujui kuwa haya ni maisha ya mtu? Ubabaishaji una kikomo chake. Tena mkanganyo wa mwongozo wa masomo (Prospectus) ni kero kubwaajabu. Hivi wanaoziandaa ni akina nani? Mbona kila siku mapungufu yale yale? Ama tuamini wananukuu na kuamisha (Copying and pasting)? Vijukuu na vitukuu wetu watakuja kufukua makaburi yetu kuangalia kama Maulana alituwekea akili kichwani au la! La sivyo watachapa makaburi yetu viboko. Fikiria UDOM mwanachuo mwaka wa kwanza hadi anatoka hajawahi kupewa “ prospectus” wala “School Regulations Guide”. Ndiyo chuo chetu. Hapa ni chota kama siyo chukua chako mapema kwani siku ukombozi (Uhuru) wa pili ukija hapatakuwepo cha Msalia Mtume wala Mwokozi Yesu tusaidie.
Mbaya zaidi mpaka leo hatujajua dhamira na malengo makuu juu ya ujio wa Nape Nnauye UDOM 24/05/2011. Alikuja kwa madai kuwa anakagua nyufa na mipasuka ndani ya mabweni. Je, yeye (Nape) ni engineer wa UDOM? Akadai vilevile kuwa anakagua sewage system. Je Nape ni bwana afya wa UDOM? Tunaomba ufafanuzi juu ya hili.
Tutafakari na tusome nyakati. Hii ni nchi yetu, sote tuijenge imara la sivyo muda si mrefu hali. Mimi, wewe, yule pamoja na nguvu ya umma tunaweza. Kwa pamoja tudai haki zetu za msingi ikiwa ni pamoja na KATIBA MPYA na siyo viraka ndani ya katiba. Ieleweke kuwa Tanzania ni ya watanzania wote na siyo mtu fulani, watu fulani au jamii fulani au tabaka fulani la watu!!!!!!!!!!

JACADUOGO


“TO GOD BE THE GLORY”
 
aisee!! uliyosema ni kama vile ulikua akili mwangu, maana kadhia iliyopo huku chuoni, mmh!!!!! tuombe uzima tu na Mungu atusaidie tumalize salama.
Mkubwa umesahau kidogo kuongelea ishu ya Huduma za Afya kwani nalo ni tatizo, tatizo..
Big up kwa kueleza ukweli!! meseji senti
 
mwanangu eeee nakupongeza kwa hotuba yako ndeeefu umesema kweli kuhusu suala la field na maji thanx but kama mwanafunz wa udom skubaliani na wewe kuhusu mambo yafuatayo

MALAZI
ebwana ee hatulali watu sita kwenye chumba cha watu 4 mfano sisi twalala wawili tu vitanda 4 hapo umedanganya umma jirekebishe

BEI
ishu ya bei mbona ni kazi ya UDOSO serikali yetu tulioichagua na mara kwa mara hupita kukagua bei na kushusha

UCHAFU
mwanangu toka nije sjaona bomba lililopasuka bali nimeona yakiziba na kumwaga kinyesi na hili ni ushenzi wetu sisi wanafunzi nafkiri unajua, "kutoflash" manake sometime maji yatoka lakini mtu avizia hamna mtu chooni atimiza haja zake

VITIVO
braza eeh umesahau hao wanaotupwa kwenye vitivo wana div three?? Udom si beba beba?? Si rahisi eti una one then upangiwe kitivo usichochagua

MAJENGO
bro kwenye nyufa mbona hujazungumzia tatizo la tetemeko la ardhi linalotokea mara kwa mara ng'ong'ona

RUSHWA
hapo nakupa tano mwanaaaa mawaden wa udom wamezidiiiii utafkiri hawalipwi mishahara

DHARAU
oya mwanangu mbona ishu ya kina mlacha ishatatuliwa chuo kimekua dicentralized kila college itajitegemea na uongozi wake hakutakua na kiongozi mwenye mamlaka makubwa

THANKS؛؛؛؛؛؛؛؛ NI MIMI MRUGARUGA ASKARI SHUPAVU WA MKWAWA
 
Back
Top Bottom