Askari adaiwa kuua mfanyabiashara
*Barabara Tunduma zafungwa kwa saa 9
*Wananchi wavunja magari JWTZ,ofisi RC
*Mbio za Mwenge wa Uhuru zasitishwa
* Risasi zarindima, kituo chazingirwa
MJI Mdogo wa Tunduma uliopo mpakani wa Tanzania na Zambia jana uligeuka uwanja wa vita baada ya mamia ya wananchi kuandamana, kurusha mawe na kushambulia magari kushinikiza Jeshi la Polisi kuwajibika baada ya mmoja wa askari kudaiwa kumuua kwa kumpiga risasi mfanyabiashara wa kitongoji cha Sogea Bw. Frank Mwachembe (34).
Mfanyabiashara huyo aliuawa kwa kupigwa risasi ubavuni saa nne usiku wa kuamkia jana na askari aliyefahamika kwa jina la PC Justin, mita chache kutoka nyumbani kwake.
Wananchi hao wakiwemo wafanyabiashara wa mji huo wa Tunduma, walikuwa wakiandamana kuelekea kituo cha Polisi wakiwa na mawe kwa nia ya kumuua askari anayedaiwa kusababisha mauaji hayo huku wakisema jeshi hilo limekuwa
likiacha majambazi na kuwaua raia wasio na hatia.
Hata hivyo askari huyo baada ya tukio hilo alitoweka na hajulikani alipo hadi sasa.
Hatua hiyo ilisababisha barabara kuu ya Tunduma kufungwa kwa takribani saa tisa kutokana na vurugu hizo ambapo mbio za Mwenge wa Uhuru uliokuwa ukimbizwe eneo hilo zilisitishwa.
Inadaiwa kuwa askari huyo alikuwa akifuatilia tukio la ujambazi ulitokea Tunduma hivi karibuni na mara alipoona gari la mfanyabiashara huyo lenye namba za usajili T 888 AEA, Toyota Cheaser ambalo alikuwa akiendesha mfanyabishara huyo alianza kulifukuzia kwa nia ya kulikamata.
Taarifa zimeelezwa kuwa wakati askari huyo akilifukuza gari hilo akiwa ndani ya gari Suzuki Escudo, namba T 559 AFA, marehemu naye aliongeza mwendo akidhani kuwa alikuwa akifukuzwa na majambazi ndipo, alipoanza kumfyatulia risasi.
Hali hiyo ilisababisha marehemu aongeze mwendo zaidi kwa kuhofia usalama wake na baadaye gari lake kukutwa na gari hilo ambalo lilikuwa ni la kiraia na askari huyo kumuua mfanyabishara huyo mita 50 kutoka nyumbani kwake.
Mara baada ya kufanya mauaji hayo inadaiwa kuwa askari huyo aliliondosha gari lake kwa mwendo kasi na kuelekea Tunduma na kudondosha bastola eneo
ambalo marehemu aliuawa.
Muda mfupi baada ya kufanya mauaji hayo baadaye lilikuja gari ya Polisi Landrover Defender likiwa na machela ndani na kuuchukua mwili wa marehemu kwa nia ya kuupeleka katika kituo cha Afya cha Tunduma.
Akizungumzia tukio hilo Mwenyekiti wa Serikali za Mtaa wa Sogea, Bw. Ali Mwafongo alisema kuwa yeye alipata taarifa za kutokea kwa tukio hilo saa nne za usiku aliposikia milio ya bunduki.
Bw. Mwafongo alisema asubuhi kulipopambazuka waliletewa taarifa kuwa kuna mtu ameuawa na baadaye walipofika eneo la tukio walielezwa kuwa jirani yao ameuawa na askari Polisi na baadaye kufuatilia kituo cha afya ndipo walipobaini kuwa aliyefariki ni jirani yao Bw. Frank.
Tukio hilo lilisababisha wananchi hao kufanya maandamano ambapo kikosi cha Askari wa Kutuliza Ghasia (FFU) walianza kurusha mabomu ya machozi pamoja na risasi za moto
kwa nia ya kuwatawanya wananchi waliokuwa wakifanya maandamano hayo.
Hali ambayo ilisababisha hasira kwa wananchi ambao walianza kurusha mawe na kuvunja vioo vya magari.
Magari mawili moja la Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa lilivunjwa
vioo vya mbele.
Mmoja wa ndugu wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Bw. Joseph Mwasote, ametaka iundwe tume kuchunguza kifo hicho.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya Bw. Advocate Nyombi alisema alikuwa kwenye mbio za Mwenge wa Uhuru na kuona mawe yamepangwa barabarani ndipo kusitisha mbio hizo na kwamba wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.
SOURCE: MAJIRA