Bibi Mikopo
Senior Member
- May 15, 2015
- 177
- 33
MASWALI YAULIZWAYO MARA KWA MARA KUHUSU UREJESHAJI WA MIKOPO ELIMU YA JUU
Swali: Mwajiri anapaswa kufanya nini baada ya kuajiri wahitimu wapya?
Jibu: Kwa mujibu wa Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (SURA 178), mwajiri anapaswa aijulishe Bodi kwa maandishi kuhusu waajiriwa wapya ambao ni wahitimu wa vyuo vya elimu ya juu ndani ya siku ishirini na nane (28) tangu tarehe ambayo wahitimu hao wameajiriwa naye.
Swali: Nini kitafuata baada ya kuwasilisha HESLB orodha ya wahitimu walioajiriwa?
Jibu: Baada ya kupokea orodha ya waajiriwa kutoka kwa mwajiri, Bodi itabainisha wafanyakazi walionufaika na mikopo ya elimu ya juu. Baada ya hapo, mwajiri atapaswa kuhakikisha kuwa makato ya kila mwezi kutoka kwenye mishahara ya wadaiwa wa mikopo yanawasilishwa Bodi ndani ya siku kumi na tano (15) baada ya tarehe ya kila mwisho wa mwezi.
Swali: Nini kitatokea endapo mwajiri ataacha kukata mshahara wa mfanyakazi baada ya kuelezwa na HESLB kwamba mfanyakazi huyo ni mdaiwa wa mkopo?
Jibu: Iwapo mwajiri atashindwa kukata ama kukata mshahara wa mdaiwa wa mkopo na kushindwa kuwasilisha makato hayo Bodi ndani ya muda uliopangwa, atatozwa asilimia kumi (10%) ya kiasi cha deni lililopaswa kulipwa kwa kila mwezi ambao makato hayatawasilishwa.
Swali: Ni lini mnufaika wa mkopo anapaswa kuanza kurejesha mkopo wake?
Jibu: Mkopo huanza kulipwa inapomalizika miezi 24 baada ya kuhitimu masomo ya elimu ya juu au baada ya kusitisha masomo.
Swali: Je, ajira ya mdaiwa wa mkopo ni jambo linalozingaliwa katika urejeshaji wa mikopo?
Jibu: Wanufaika wote wa mikopo ya elimu ya juu wanapaswa waanze kurejesha mikopo mara baada ya miezi 24 baada ya kuhitimu. Lengo la muda huu ni kuwawezesha kutumia elimu waliyoipata kujiajiri au kuajiriwa na hivyo kupata kipato.
Swali: Ni asilimia ngapi hutozwa kama tozo la kutunza Thamani ya fedha kwa kila mdaiwa wa mkopo?
Jibu: Madeni yote ya mikopo hutozwa asilimia sita (6%) kama tozo la kutunza Thamani ya Fedha (Value Rention Fee) kwa mwaka.
Lengo la tozo hii ni kutunza thamani ya fedha dhidi ya mfumuko wa bei ili mkopo uwe na thamani sawa wakati utakapotolewa kwa mwanafunzi mwingine mwenye uhitaji katika siku zijazo.
Swali: Ni hatua zipi za kisheria zitachukuliwa kwa wadaiwa ambao hawatarejesha mikopo yao?
Jibu: Mdaiwa yeyote ambaye, bila sababu za msingi atashindwa kulipa mkopo atachukuliwa hatua za kisheria. Aidha, mambo yafuatayo yatafanyika:
a) Atapata adhabu ya kulipa asilimia kumi (10%) ya mkopo wake wote;
b) Taarifa zake zitawasilishwa kwenye taasisi zinazosimamia taarifa za wakopaji wanaotaka kukopa kutoka taasisi za fedha zinazotoa mikopo na kuzuiliwa kukopa kutoka kwenye Taasisi za Fedha;
c) Atazuiliwa kupata ufadhili wa Serikali kwa ajili ya masomo ya Uzamili au Uzamivu katika chuo chochote cha Elimu ya Juu ndani na nje ya nchi;
d) Taarifa zao zinawasilishwa kwa wadau mbalimbali kama Mifuko ya hifadhi za Jamii ili hatua stahiki zichukuliwe;
Swali: Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kampuni zingine binafsi za ukaguzi wana wajibu gani katika urejeshaji wa mikopo?
Jibu: Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali (CAG) na makampuni mengine binafsi ya Ukaguzi yana majukumu mawili:
a) Kuhakikisha waajiri wanatekeleza matakwa ya Sheria kwa kuwasilisha orodha za wahitimu wa elimu ya juu walioajiriwa kwa Bodi ya Mikopo; na
b) Kuhakikisha makato ya fedha kutoka kwa wadaiwa yanawasilishwa kwa wakati.
Swali: Mnufaika wa mkopo anapaswa kufanya nini ili kulipa deni lake?
Jibu: Mara baada ya kuhitimu masomo au kusitisha masomo yake kwa sababu yoyote ile, mnufaika anapaswa aitaarifu Bodi kwa maandishi mahali alipo na hali ya ajira yake na kuanza kurejesha mkopo wake.
Swali: Makato huwasilishwaje HESLB?
Jibu: Kwa wanufaika waajiriwa, hukatwa asilimia kumi na tano (15%) ya mshahara wa kila mwezi.
Aidha, mnufaika anaweza kulipa kiwango cha chini cha shilingi 100,000/= kila mwezi.
-------------------------
Kwa maoni:
info@heslb.go.tz
au repayment@heslb.go.tz
info@heslb.go.tz
au repayment@heslb.go.tz