Tuache kuutangaza vibaya Uwanja wa Taifa

Magezi

JF-Expert Member
Oct 26, 2008
3,359
692
Hatimaye klabu za Simba na Yanga, jana zilicheza mechi yao ya kukamilisha ratiba ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwenye Uwanja wa Uhuru.

Ni imani yetu kwamba baada ya mechi hiyo, walau tambo zilizokuwa zikitolewa awali baina ya mashabiki wa klabu hizo mbili kuhusiana na mechi za jana zitakuwa zimepungua, hasa baada ya kila upande kujua ukweli wa timu gani kati yao inacheza soka safi zaidi uwanjani.

Klabu hizo kongwe zilihitimisha ratiba ya ligi jana kutokana na ukweli kwamba kabla ya kushuka dimbani, Simba walishajihakikishia ubingwa wa ligi hiyo huku Yanga wakiwa pia wameshajihakikishia nafasi ya pili.

Hata hivyo, sisi hatuzungumzii sana mechi hiyo iliyochezwa jasna na kuvuta hisia za wapenda soka wengi nchini. Badala yake, tunataka kuzikumbusha mamlaka husika kuwa ziache kuutangaza vibaya uwenja wetyu wa kisasa wa Taifa.

Awali, sote tunakumbuka kwamba Simba na Yanga ziliamua kuachana na uwanja huo mpya (Taifa) na badala yake kutaka kuutumia Uwanja wa Uhuru.

Sababu za Simba na Yanga kuukimbia Taifa zilielezwa bayana na waendeshaji wa Ligi Kuu, Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF), kwamba klabu hizo zilikuwa zikiumizwa na makato makubwa ya asilimia 40 ya watakachovuna, tofauti na Uwanja wa Uhuru ambao makato yake ni nafuu.

Baadaye, Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, iliingilia kati na kuzisihi klabu hizo zicheze mechi yao Uwanja wa Taifa na kwamba suala la makato, lingetafutiwa ufumbuzi.

Kweli. Tunaamini busara ilitumika na ndiyo maana mechi ilichezwa jana, badala ya awali ambapo ilitakiwa ichezwe Aprili 11, kwenye Uwanja wa Uhuru. Sisi tunapongeza maafikiano hayo.

Lakini, wakati zikiwa zimesalia siku mbili kabla ya mechi ya jana, zilitangazwa taarifa ambazo sisi tunaona kwamba si nzuri kwa maslahi ya Taifa.

Ilielezwa kwamba mechi ya Simba na Yanga isingechezwa tena usiku kama ilivyotangazwa awali kwa sababu ya ‘matatizo ya mfumo wa umeme’ ndani ya uwanja huo.

Kwa tunavyofahamu, Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, imekuwa ikijitahidi kwa kila hali kuutangaza uwanja wa Taifa ili ikiwezekana, timu zitakazokwenda kucheza fainali za Kombe la Dunia zitakazoanza Juni 11 nchini Afrika Kusini zivutiwe na hatimaye zije kuweka kambi nchini.

Serikali imekuwa ikifanya hivyo kutokana na imani kwamba, ujio wa timu maarufu za mataifa mbalimbali kama Brazili, Hispania, Ufaransa au Nigeria, utatupa manufaa ya kiuchumi, kwani Tanzania itatangazwa dunia nzima kupitia wachezaji nyota wa timu hizo.

Lakini, kitendo cha kuiambia dunia kwamba uwanja huo wa Taifa una ‘matatizo ya mfumo wa umeme’ ni kuharibu jitihada za kuutangaza.

Sisi tunaona kwamba, ingetumika busara nyingine ya kueleza sababu za kubadili muda wa mechi hiyo.

Mathalan, sisi tunahofia kwamba, nchi yenye wachezaji nyota kama Argentina, yenye mwanasoka bora wa dunia na kocha Diego Maradona, kamwe haitakuwa tayari kuweka kambi katika uwanja wenye ‘matatizo ya mfumo wa umeme’.

Tunadhani kwamba, taarifa kama hizi ambazo husambaa dunia nzima na kuharibu sifa njema ya uwanja wetu ziepukwe na ikiwezekana, uwasilishaji wake uwe ukizingatia maslahi ya soko.

Tunaamini kwamba muuza vitumbua yeyote akisema hadharani kwamba vitumbua vyake vina mchanga, basi ajiandae kuvila mwenyewe. Ni dhahiri kuwa wateja watamkimbia.
Nasi, kama kweli tuna dhamira ya dhati ya kuzivutia timu zitakazokwenda kushiriki fainali za Kombe la Dunia, basi tuache kuutangaza vibaya Uwanja wa Taifa.

Vinginevyo, kwa mtindo huu wa kutangaza kwamba una ‘matatizo ya mfumo wa umeme’, basi tujiandae kuutumia wenyewe kwa mechi za Simba dhidi ya Yanga, au hata Moro United dhidi ya Prisons!

CHANZO: NIPASHE
 
Inashangaza kuona mtu anatunga uongo ili ku-justify uzembe. Kwa nini TFF waseme uwanja mpya una matatizo ya umeme wakati wakijua ni uwongo? Tatizo ni makato na issue iko wazi? Mijitu hii hii utasikia baadaye inalalamika eti timu za nje zima kataa kuja wakati wenyewe mmewaambia uwanja wenu unamatatizo ya mifumo ya umeme?? TFF mmeanza kuwa wababaishaji!!!
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom