Parabolic
JF-Expert Member
- Dec 3, 2013
- 2,743
- 2,601
Lakini pia mjadala huu unaonyesha mvutano ulinzi wa haki za kiraia, huku athari zake zikiweza kugusa diplomasia na taswira ya nchi kimataifa.
============
Geneva- Uswisi. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetumia haki yake ya kujibu katika Kikao cha 61 cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, kujibu kauli zilizotolewa na Jumuiya ya Ulaya, pamoja na nchi za Uingereza, Uswisi, Sweden, Ireland, Ubelgiji na Norway, pamoja na asasi za kimataifa za Human Rights Watch na Amnesty International kuhusu matukio yaliyohusiana na Uchaguzi Mkuu wa Tanzania.
Akizungumza katika kikao hicho mjini Geneva Machi 2, 2026, Mwakili wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Geneva Uswisi, Dk Abdallah Possi amesema Serikali imesikitishwa na kile ilichokiita kauli zenye kuchagua matukio bila kuzingatia muktadha na chanzo chake, hususan madai yanayohusu vurugu zilizotokea Oktoba 29, 2025 wakati wa Uchaguzi Mkuu.
Tanzania ilikumbwa na vitendo vya vurugu vilivyolenga kuharibu vituo vya polisi, ofisi za serikali za mitaa, miundombinu ya usafiri wa umma pamoja na mali za watu binafsi. Serikali imesisitiza kuwa matukio hayo hayakuwa ya bahati mbaya, bali yalipangwa kwa lengo la kuvuruga mchakato wa kikatiba na kudhoofisha utaratibu wa uchaguzi.
“Tanzania inapinga vikali madai yaliyotolewa na baadhi ya washirika wa kimataifa, ambao kwa makusudi wamefumbia macho chanzo cha matukio hayo,” ameeleza.
Serikali imeeleza kuwa demokrasia inahitaji kulinda haki na kuheshimu utawala wa sheria, na kwamba vitendo vya vurugu haviwezi kuchukuliwa kuwa ni ushiriki halali wa kisiasa. Aidha, imeeleza kuwa ni wajibu wa kikatiba wa dola kulinda utulivu wa umma, mfumo wa kikatiba na usalama wa wananchi wake.
Katika kuimarisha uwazi na uwajibikaji, Serikali ilibainisha kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, aliteua Tume Huru ya Uchunguzi kwa mujibu wa sheria ili kuchunguza matukio yaliyojitokeza katika muktadha wa uchaguzi huo.
Tume hiyo, kwa mujibu wa taarifa, inafanya kazi kwa uhuru na imepewa jukumu la kubaini ukweli pamoja na kupendekeza hatua zinazofaa. Baada ya nyongeza ya muda mfupi, Tume inatarajiwa kuwasilisha ripoti yake ifikapo Aprili 3, 2026.
Serikali imeeleza kuwa matokeo ya Tume yanatarajiwa kutoa mwongozo kuhusu mipango ya maridhiano ya kitaifa pamoja na mageuzi ya kikatiba na kitaasisi yatakayofuata.