Tanzania kupeleka wanajeshi Darfur

Ngongo

JF-Expert Member
Sep 20, 2008
18,800
30,725
SERIKALI itapeleka askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika eneo Darfur, kujiunga na vikosi vingine vya askari wa Umoja wa Mataifa (UN), kulinda amani katika eneo hilo.


Akizungumza baada ya kukutana na Kamti ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, alisema hayo jana.


Membe alisema Kamati hiyo ya bunge imeridhia hatua ya kupeleka askari Darfur na kufafanua kuwa bataliani moja itapelekwa kuungana na askari wengine 17,000 waliopo mjini humo.


"Serikali itapeleka askari Darfur kujiunga na wengine 17,000 waliopo mjini humo, Ni bataliani moja itakayokwenda," alisema Membe.


Alisema uamuzi huo umeridhiwa pia na Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na kwamba askari hao wanatarajiwa kuondoka nchini mapema mwezi Machi.


"Uamuzi huo umeridhiwa pia na Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na kwamba askari hao wataondoka nchini kuanzia Machi mwaka huu,"alisema.


Alibainisha kuwa wizara yake imewasilisha kwa kamati hiyo taarifa ya mafanikio katika utendaji wake na utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM)na kuanisha maeneo mbalimbali aliyoyaita ya ushindi.


Aliainisha maeneo hayo kuwa ni pamoja na kufanikisha mazungumzo ya amani nchini Kenya, kuongoza nchi za Afrika kukataa mahakama ya kimataifa isimshtaki Rais wa Sudan, Mohamed Hassan Al Bashir kwa madai ya kufanya makosa ya kivita Darfur na kupinga ma[induzi na kuwaondoa viongozi wa kijeshi Mauritania na Guinea kwa mujibu wa kanuni za Umoja wa Afrika.


Membe alisema Kamati hiyo imeipongeza serikali na Rais Jakaya Kikwete katika utekelezaji wa mambo hayo aliyoyaelezea kuwa ni mafanikio katika nafasi ya uenyekiti wa Umoja wa Afrika.


Alisema kuwa wakati muda wa uongozi wa Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa AU ukimalizika Februari mosi mwaka huu ataacha changamoto tatu kubwa kwa mwenyekiti ajaye.


Changamoto hizo ni suala la Somalia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Zimbabwe pamoja na uundaji wa Serikali ya Umoja wa Afrika.


Katika hatua nyingine, Membe alisema serikali imepokea mapendekezo ya kamati hiyo yanayokataa muundo wowote wa ushirikiano wa Afrika Mashariki utakaoruhusu ardhi ya Tanzania kutumika kwa manufaa ya shirikisho.


Alisema kamati hiyo imeitaka serikali kuwa makini na suala la ardhi ambalo ni rasilimali na urithi pekee wa wananchi wa Tanzania na vizazi vyao na kwamba atalifikisha suala hilo katika vyombo husika.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom