Sunday, 15 May 2011 10:46
Habel Chidawali, Dodoma
Mwananchi
SHIRIKA la Umeme Nchini (Tanesco), liko katika wakati mgumu baada ya mawaziri na watendaji wengine wa serikali kulibana kuhusu utendaji wake usioridhisha, huku likipewa muda kujitathmini na kuja na mikakati madhubuti ya kujiendesha. Hayo yanakuja huku kukiwa na taarifa kuwa Tanesco inakabiliwa na ukata mkubwa wa fedha huku likizidi kushutumiwa kwa utendaji wake mbovu na usioridhisha.
Akizungumza na Mwananchi Jumapili mjini Dodoma jana, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adamu Malima alikiri kuwa Rais Jakaya Kikwete alishatoa maagizo kwa shirika hilo kujitathmini na kutoa majibu jinsi gani wanavyoweza kujiendesha na kutoa maagizo kwa serikali kuacha kuweka mkono katika shirika hilo. Jana Malima alikiri kuwa kweli Tanesco imeyumba katika utendaji wake wa kazi, lakini akasema serikali ilishatoa maagizo kwa shirika hilo lijitathmini lenyewe bila ya kuingiliwa na mtu mwingine.
Alisema hali ilivyo kwa sasa hakuna ubishi kuwa Tanesco inawaumiza wananchi katika baadhi ya huduma zake licha ya kuwa kila siku Shirika hilo linalalamika kuwa hali ni mbaya kiuchumi.Unajua hilo ni kweli kwamba tuliwaagiza wajitathmini na hata ndani ya semina hii elekezi Mheshimiwa Rais amewataka wajitathmini, na katika kipindi kifupi watoe majibu ya namna gani wanataka kuliendesha Shirika na sisi (serikali), rais ametupa maagizo ya kuacha kuingiza mikono yetu ndani ya Shirika hilo , alisema Malima.
Bila ya kutaja ni muda gani waliopewa Tanesco kwa ajili ya kujitathmini kabla ya kutoa majibu serikalini, Malima alisema agizo hilo limekuwa ni la muda mrefu kwani hata rais alipotembelea Wizara hiyo mwanzoni mwa mwaka huu aliagiza hivyo. Malima alisema kuwa shirika hilo limekuwa likilalamikiwa kwa mambo mengi ikiwemo huduma za kuunganishwa umeme pamoja na ubora wa nguzo wanazotumia katika kutandaza nyaya, na kwamba bei ya nguzo hizo pia ni juu lakini cha kushangaza kila siku shirika linalia hakuna fedha.
Vitu vingine ambavyo hata ninyi mnajua ambavyo Tanesco wanavyolalamikiwa ni pamoja na gharama kubwa za kuunganisha umeme ambazo ni kero kwa mtu wa kipato cha chini haiwezekani kwa hali ya kawaida mtu wa kipato cha chini kutoa Sh 450,000 kwa ajili ya maunganisho, alisema Malima. Mfano mimi ni Mchumi najua namna gani bei hiyo ilivyokubwa, lakini kitu kingine ambacho hata ninyi hamjakijua bado ni kitendo cha Tanesco kuwalipisha wateja nguzo za umeme lakini bado nguzo hizo zinabaki kuwa mali ya Shirika hilo, huu ni uonevu mkubwa, aliongeza kusema. Mbali na hilo Malima alirusha lawama kwa taasisi zilizopewa dhamana ya kusambaza nguzo za umeme kuwa licha ya kuziuza kwa bei ya juu lakini nguzo hizo hazina ubora.
Alitolea mfano kuwa zamani nguzo zilikuwa zikiuzwa kwa bei ya chini lakini pia zilikuwa ni imara ambazo ziliweza kumudu kuwa ardhini kwa zaidi ya miaka 15, lakini kwa sasa zinaweza kukaa kwa miaka miwili tu. Hivi zamani mlikuwa mnaona kwamba nguzo zilikuwa zinakaa kwa zaidi ya miaka miwili bila ya kuharibika, lakini siku hizi nguzo zikikaa miaka miwili ukijaribu kukanyaga unakua unga, alisema.
Kwa mujibu wa Malima hayo ni moja ya mambo waliyoagizwa Tanesco kuyaangalia na kutoa majibu serikalini kama wanataka ziwekwe nguzo za chuma au zege, lakini cha muhimu ni lazima nguzo hizo ziwe na ubora unaotakiwa. Katika hatua nyingine, Serikali imekanusha madai kuwa imetoa kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya Tanesco baada ya kuonekana kuwa na hali mbaya kiuchumi.
Malima alisema hakuna mpango wowote ndani ya serikali wa kuisaidia Tanesco kifedha na badala yake Tanesco wanatakiwa kijitathimini wenyewe. Kauli ya Malima imekuja siku chache baada ya kuwepo kwa taarifa kuwa serikali imewekeza mabilioni ya fedha ndani ya Shirika hilo ambalo linaonekana kuyumba hali inayopelekea kuzidiwa kwa madeni likitaka kujinusuru.
Elizabeth Suleyman anaripoti kuwa baadhi ya wanafunzi wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wameitaka Serikali iache kuingiza siasa na utendaji wa Shirika la umeme Tanzania (Tanesco), kwani husababisha maendeleo ya shirika hilo kurudi nyumba. Kauli hiyo imekuja, kufuatiwa kuwepo kwa malalamiko ya wananchi hao wakilalamikia mgao wa umeme ambao umekuwa ni tatizo kubwa katika nchi, na haijulikani tatizo hilo litakwisha lini.
Wakizungumza jana jijini Dar es Salaam, katika kipindi cha malumbano ya hoja kinachorushwa na kituo cha ITV, wanafunzi hao walisema serikali inapoamua kuingiza siasa ndani yake, inasababisha utendaji wa shirika hilo kuyumba. Wananchi wanaweza kuilalamikia Tanesco ndiyo wazembe katika utendaji, kumbe tatizo lipo kwa serikali kutokana na kuingiza siasa na kazi kitu ambacho ni kibaya sana, walisema wanafunzi hao na kuongeza: Serikali inapaswa iiachie Tanesco, ijiendeshe yenyewe katika utendaji wake na sio kuliingilia kwa kuingiza siasa ndani yake, kwani kwa kufanya hivyo ni kulifanya shirika lionekane halina wataalamu wenye ujuzi,alisema. Kwa upande wake mwanafunzi wa chuo hicho Hongera Timotheo alisema ni vema wananchi wakaacha kuitupia lawama Tanesco badala yake waelekeze jicho lao kwa serikali, kwani ndiyo inayosababisha matatizo ya umeme hayaishi.
Mie siamini kwamba, ndani ya tanesco hakuna wataalamu wenye ujuzi, najua wapo tena wakutosha ila wanakwamishwa na serikali kuwaingilia kati katika kila wanachotaka kufanya,alisema Tomotheo. Naye mwanafunzi mwingine, Emmanuel John aliongeza kuwa ili tatizo la umeme Tanesco liweze kupungua ni vema, wakahakikisha wanakuwa na wataalamu wa kutosha katika utendaji wao. Alisema, wataalamu wanapukuwa wengi itasaidia mikakati inayowekwa kuwa yakudumu na hatasababisha shirika hilo kushindwa kujiendesha.
Lakini kama shirika litaendelea kuwa na wataalamu wabovu, utendaji wa shirika hilo utaendelea kuyumba na mwisho wake uchumi wa nchi utashuka na viwanda vingi vitakufa,alisema John na kuongeza Kama nchi itaendelea kuwepo na tatizo kubwa la mgao wa umeme, na kusababisha Tanesco kuingiza umeme wa dharura, ni wazi tutapoteza wawekezaji wa kuja kuwekeza kwasababu hakuna atakaye kubali kuja kuwekeza kwenye nchi yenye giza,.
Alisema, iko haja ya shirika kuhakikisha inapanga mikakati yenye dira na itakayoleta mafanikio kwa watanzania kwa kutumia njia mbadala za kuongeza vyanzo vya maji, ili kupata umeme wa kutosha.