nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,860
- 5,803
NA GODFREY MUSHI
3rd August 2012
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) inawasaka makada wawili wa CCM, Waziri wa zamani, Joseph Mungai na Katibu Mkuu wa zamani wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Frederick Mwakalebela, kutokana na kukabiliwa na tuhuma za rushwa katika chaguzi za Chama cha Mapinduzi (CCM).
Mungai anakabiliwa na tuhuma za utoaji rushwa kinyume cha sheria ya Takukuru ya mwaka 2007 na sheria ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010.
Kaimu Kamanda wa Takukuru mkoa wa Iringa, Stephen Mafipa, alisema kuwa Mungai na Mwakalebela wanatafutwaili wafikishwe upya mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili, baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa kutupilia mbali rufani zao.
Mungai na wenzake wawili walikuwa wakiiomba Mahakama Muu kutolea uamuzi hoja mbili ambazo Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Iringa ilishindwa kutolea maamuzi katika kesi ya msingi.
Hoja ya kwanza kwa mujibu wa Mungai ni kwamba makosa yote 15 aliyoshitakiwa yeye na wenzake siyo ya jinai kutokana na kukosa maneno muhimu kisheria kama inavyotakiwa sheria namba 11 ya Takukuru ya 2007.
Aidha, taarifa hiyo inaitaja pia hoja ya pili ambayo imetupiliwa mbali na Mahakma Kuu ni kifungu cha 21 (1) (a) na kifungu cha 24 (8) cha sheria ya gharama za uchaguzi namba 6 ya mwaka 2010 ambacho Mungai na wenzake wanadai hakitengenezi kosa la jinai.
Awali, Mungai na makada wengine wawili wa CCM, akiwemo Katibu wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Mufindi, Fidel Cholela (41) na Moses Masasi walikuwa wakikabiliwa na mashtaka 15 ya kutoa rushwa na sheria ya gharama za uchaguzi ya mwaka 2010.
Inadaiwa kuwa Julai 08, mwaka huu, katika Kata ya Ihalimba, Wilaya ya Mufindi, Mungai na watuhumiwa wenzake walitoa hongo ya Sh.10,000 kwa Mwenyekiti wa CCM tawi la Vikula kama kishawishi cha kumpigia kura wakati wa zoezi la upigaji wa kura za maoni.
Mwakalebela anakabiliwa na tuhuma za rushwa katika chaguzi za CCM zilizofanyika mwaka 2010 wakati wa mchakato wa kura za maoni Jimbo la Iringa Mjini.
Mwakalebela anadaiwa kutenda kosa hilo Juni 2010 katika Kijiji cha Mkoga, Manispaa ya Iringa ambapo anadaiwa kutoa hongo ya Sh.100,000 kwa Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Hamisi Luhanga ili azigawe kwa wapiga kura 30 wa CCM ili wampigie kura.
CHANZO: NIPASHE