Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) imesema, Uwanja wa Ndege wa Bukoba, Mkoa wa Kagera ni salama kwa asilimia 100.
Dar es Salaam. Wakati yakiibuka madai ya usalama duni wa Uwanja wa Ndege wa Bukoba, Mkoa wa Kagera baada ya ajali ya ndege ya Precision Air, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA), imesema uwanja huo ni salama kwa asilimia 100.
Si uwanja wa Ndege wa Bukoba pekee, bali na vingine 57 vinavyoendeshwa na mamlaka hiyo ni salama kwa usafiri wa anga.
Kauli hiyo ya TAA inakuja ikiwa ni siku nne baada ya kutokea ajali ya ndege ya Precision Air, Jumapili ya Novemba 6, 2022 iliyotumbukia katika Ziwa Victoria na kusababisha vifo vya watu 19.
Kutokana na ajali hiyo, maoni mbalimbali yameibuliwa ikiwemo usalama duni wa viwanja na kasoro katika mifumo ya uokozi.
Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Alhamisi, Novemba 10, 2022 Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mussa Mbura amesema usalama wa viwanja hivyo unatokana na kufuata viwango vya kimataifa.
"Hatuna rekodi ya tatizo au kukosekana kwa usalama katika Uwanja huo wa Ndege (Bukoba) na mambo mengi yanayoendelea yamezungumzwa baada ya ajali.
"Hatujawahi kupokea malalamiko ya uwanja huo kabla kutoka kwa yeyote na hilo halijawahi kuelezwa kwa yeyote," amesema.
Kwa mujibu wa Mbura, viwanja hivyo vilifanyiwa uchunguzi na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Duniani (ICAO).
Taarifa ya uchunguzi ya Shirika hilo, amesema imeipa Tanzania alama 67 kati ya 60 zinazohitajika kwa mujibu wa viwango vya kimataifa.