Simulizi Ya Kweli:Nilimuoa Jini Nikamsaliti

SEHEMU YA 32

Subira alimweleza kilichotokea muda mfupi, mumewe kumshangaa na kumwona si mkewe. Mzee Mukti aliamini kazi aliyotumwa na Nargis ilikuwa imekwisha, alishusha pumzi na kusema:
“Mmh! Mambo mazito, inaonekana uwezo wangu umefikia mwisho.”
“Mungu wangu sasa itakuwaje?”
ENDELEA...
“Kwani anasemaje?”
“Kama nilivyokueleza anashangaa hata picha za harusi yetu na kuuliza ile picha kama ni yake huoni kama naumbuka mwenzio?”
“Mmh! Kweli kazi ipo.”
“Mzee wangu fanya uwezavyo ili mambo yawe sawa nakuahidi kukupa chochote ukitakacho.”
“Nina ushauri mmoja.”
“Ushauri gani?”
“Nakuomba umuachie mume wake?”
“Eti nini?” Subira alishtushwa na kauli ya mzee Mukti.
“Njia rahisi ya kumaliza suala hili ni kuachana na mumewe lakini zaidi hapo nauona mwisho wake ni mbaya.”
“Sikubali nimeishapoteza fedha nyingi kwa ajili ya kulinda ndoa yangu, lazima niipiganie,” Subira hakukubali kirahisi.
“Lakini si unajua Thabit ni mume wa Nargis?”
“Hata kama, mimi ni mwanadamu na yule ni jini hivyo mwenye nafasi kubwa ni mimi kwa vile ndoa ya halali ni mwanadamu kwa mwanadamu.”
“Unajua mwenye haki ni huyo jini na sasa hivi ana nguvu mara mbili ukishindana naye utakufa unajiona.”
“Bora nife lakini sikubali lazima nipambane.”
“Nakuhakikishia kama kwangu umeshindwa hakuna sehemu yoyote utakapopata msaada.”
“Siamini, wewe si mganga wa mwisho nitahakikisha namrudisha mikononi mwangu,” Subira alisema kwa hasira.
“Sawa, lakini kwa ushauri wangu achana na mume wa Nargis yatakukuta makubwa.”
“Leo ndiyo umeyaona hayo?”
“Subira acha ubishi hata huo utajiri ni wa huyo mwanamke.”
“Hakuna ni wa Thabit si wa jini wako.”
“He! Ameisha kuwa jini wangu! Subira ninayokueleza haya ni kwa ajili ya kukupenda, lakini kama huyo jini angekuwa na roho mbaya angeweza kutuua wote.”
“Umejuaje?”
“Kuna siri nzito nilikuficha juu ya yule jini, ndiye aliyerudisha mali zilizopotea na ndiye aliyemponya Thabit kwa vile ni mume wake. Amekosa kuniua zaidi ya mara nne na kunieleza kama ninataka usalama wangu na wako basi tumrudishe mumewe mikononi mwake la sivyo atatupoteza wote.”
“Mzee Mukti, wewe si ulinieleza kuwa wewe ni kiboko ya majini?”
“Ni kweli lakini imeonekana Nargis ana nguvu za ziada tofauti na mwanzo tulivyomfanya.”
“Ndiyo maana nikasema wewe si mganga wa mwisho kama uwezo wako umeishia hapo wapo wenye kukuzidi.”
”Sawa, lakini nakuomba kwa usalama wako achana na Thabit kwa vile mwenye mali amerudi kama alikulaza kwenye kaburi anaweza kukufanya chochote anachotaka.”
“Sikubali nipo radhi kufa lakini nimrudishe mume wangu.”
“Kila la heri.”
Subira akiwa amechanganyikiwa alibeba mkoba wake bila kumuaga mumewe na kutoka nje. Alikumbuka kuna mganga mmoja anasifika sana maeneo ya Bunju, aliingia kwenye gari na kuondoka. Alipofika Bunju hakujua yupo wapi, ilibidi ampigie shoga yake ambaye alikuwa akiwafahamu waganga kila kona.
“Nenda mpaka Bunju mwisho kisha ulizia Moboja, ni maarufu sana.”
Baada ya kuelekezwa vile alisogea pembeni ya barabara kulikokuwa na vijana wenye bodaboda. Aliteremsha kikoo na kumwita mmoja aliyekuwa amesimama pembeni.
“Samahani kaka naomba nikuulize.”
Yule kijana alisogea hadi kwenye gari la Subira na kuuliza:
“Unasemaje Sister?”
“Eti unamjua mganga anayeitwa Moboja?”
“Si yule anakaa mpakani?”
“Hata najua, kuna mtu kanielekeza anakaa Bunju.”
“Mimi namjua yule wa mpakani?”
“Labda ndiye yeye si mwanamke?”
“Ndiyo.”
“Basi atakuwa yeye.”
“Basi nenda mpaka ukikaribia daraja linalotenganisha Bunju na Bagamoyo, kata kulia kuna njia ndogo lakini gari linafika fuata barabara hiyo mpaka mbele utaona nyumba ina kitambaa chekundu juu ya mti kama bendera ndipo hapo.”
“Asante kaka yangu,” Subira alisema huku akimpatia elfu mbili kisha aliwasha gari na kuondoka kuelekea kwa mganga.
Alifuata barabara mpaka alipokaribia kwenye daraja alikata kulia na kuifuata njia alipofika mbele aliona nyumba yenye bendera nyekundu. Aliamini ni pale alipoelekezwa alisimamisha gari. Aliteremka na kuelekea kwenye nyumba kwa kuingia mlango wa uani ambako alikuta kuna wagonjwa waliokuwa wakipata matibabu na wengine wakiwa kwenye foleni ya kumuona mganga.
Baada ya kuwasalimia alikaa pembeni kusubiri zamu yake, baada ya dakika arobaini aliitwa ndani kwenda kuonana na mganga. Baada ya kukaa na kusalimiana alitulia kumsikiliza.
“Karibu.”
“Asante.”
“Una tatizo gani?”
“Ndoa yangu imeingia katika matatizo baada ya jini mmoja kutaka kumchukuwa mume wangu. Naomba msaada wako ili kuhakikisha mume wangu hachukuliwi kwa gharama yoyote. Tena ukifanikisha kumbakisha mume wangu nitakupa zawadi kubwa ambayo hutaisahau maishani mwako.”
Baada ya kumweleza mganga alitulia kwa muda na kuchukuwa mtandio mwekundu na kujifunika usoni ili ampigie ramli. Aliwasha udi na kuufusha kisha aliuweka chini ya kitambaa na kuvuta moshi wake baada ya muda alisikika akiguna peke yake na kusema kwa sauti nyembamba.
“Ewe mwanadamu una shida gani?”
“Nataka kuchukuliwa mume wangu.”
“Mbona unasema uongo?”
“Kweli huu ni mwaka wa tano nipo ndani ya ndoa yangu.”
Inaendelea
 
SEHEMU YA 33

“Aliwasha udi na kuufusha kisha aliuweka chini ya kitambaa na kuvuta moshi wake baada ya muda alisikika akiguna peke yake na kusema kwa sauti nyembamba.
“Ewe mwanadamu una shida gani?”
“Nataka kuchukuliwa mume wangu.”
“Mbona unasema uongo?”
“Kweli huu ni mwaka wa tano nipo ndani ya ndoa yangu.”
SASA ENDELEA...
“Mbona kuna aliyeanza kuwa katika ndoa kabla yako?”
“Ni kweli, lakini naomba msaada wako.”
“Sasa nimsaidie nani mwenye mali au wewe?” Mganga aliuliza.
“Kivipi?” Subira hakumwelewa mganga.
“Mwenye mume ametoka hapa kuomba nisiiguse ndoa yake la sivyo atanifanya kitu kibaya.”
“Lakini wewe si mganga, hawezi kukutisha.”
“Ni kweli lakini si wakuharibu mambo ya watu.”
“Kwa hiyo huwezi kunisaidia.”
“Sina msaada zaidi ya wewe kumwachia mume wake, zaidi ya hapo utatafuta matatizo.”
“Kwa hiyo umeshindwa?” Subira aliuliza.
“Sijashindwa bali huo ndiyo ukweli, hebu angalia pembeni yako,” mganga alisema akiwa bado amejifunika kichwani.
“Nini?” Subira aliuliza huku akigeuka kuangalia pembeni yake lakini hakuona kitu.
“Mbona hakuna kitu, kuna nini?”
“Umeangalia vizuri?”
“Ndiyo.”
“Mbona mimi naona.”
Kauli ya mganga ilimfanya Subira ageuke tena kuangalia pembeni japokuwa mwanzo hakuona kitu chochote. Alipoangalia pembeni kwa mara ya pili hakuona kitu aligeuka ili amuulize mganga aliyemuona alimchezea akili baada ya kazi kumshinda. Macho yake yalishtuka baada ya kumuona mtu tofauti na mganga aliyekuwa amekaa mbele yake.
“He!” Alishtuka na kushika mkono kifuani kwa mshtuko.
“Unashtuka nini?” aliyekuwa mbele yake alimuuliza.
“Ha...ha...pana, ni...ni...sa...mehe.”
“Nikusamehe nini?”
“Ni...ni...me...me...ku...wa si...si...sikii,” Subira alipata kigugumizi cha ghafla.
“Sikiliza Subira nina imani kote ulipopita umeelezwa vizuri mimi ni nani na nina nguvu gani. Najua una tamaa ya mali, sikiliza sasa hivi sitaki shari na wanadamu ndiyo maana sitaki kukufanyia lolote baya. Sasa nieleze unataka nini ili uachane na mume wangu?” Subira aliulizwa kwa sauti ya upole tofauti na alivyotegemea.
“Si...si...taki chochote,” alijibu huku akitetemeka.
“Sema ukweli ulio ndani ya moyo unataka nikupe nini uachane na mume wangu, kwa ulichonifanyia nilikuwa ninawezo wa kuua au kukugeuza kiumbe cha ajabu. Lakini namshukuru Mungu amenipa subira na akili ya kuushinda mtihani huu. Mpaka unahangaika kwa waganga ulijua kabisa Thabit ni mume wangu na utajiri aliona ni mimi nimempa lakini ulijitoa akili .
“Ni kweli mimi ni jini na mwanaume niliyemchagua katika viumbe wanadamu ni Thabit baba wa watoto wangu Zumza na Zamzu. Hivi kweli hata akili ya kawaida tu, mfano wewe usafiri kwenda kwenu kujifungua nyuma aje mwanamke amchukue mumeo kwa nguvu za kichawi utajisikiaje?”
“Nitajisikia vibaya.”
“Utakubali kumwachia mumeo mpenzi?”
“Hapana.”
“Utafanyaje?”
“Nitapambana ili kumrudisha.”
“Nina imani jibu unalo, nafahamu ungekuwa wewe mtu huyo ungemuua hata kwa risasi, hali hii Thabit mume wangu wa halali umetaka kuniua vipi angekuwa mumeo mimi ni mwizi?”
“Ni...ni...sa...samehe dada yangu,” Subira alipiga magoti.
“Nataka kukueleza jambo moja dogo, ili ninalokupa ni onyo la mwisho. Naomba uachane kabisa na mume wangu. Nakuahidi ukiachana na mume wangu nitakupa zawadi nzuuuri.”
“Nimekuelewa dada yangu, sasa nikitoka hapa niende wapi?”
“Ooh! Swali zuri, kuna nyumba nimekutafutia utakaa hapo maisha yako yote masharti yake usiiuze tu. Kwa sasa utakwenda kumueleza ukweli Thabit kuwa wewe si mkewe kisha utaondoka, ukiondoka usirudi tena kazini, nimetafuta wafanyakazi wengine.”
“Sawa, hapo uliponitafutia nitapajuaje?”
“Ukitoka ofisini kwa Thabit kabla ya kuvuka mlango fumba macho ukitoka nje tu utajikuta kwako.”
“Sawa.”
Ghafla Subira alishangaa kujikuta mbele ya mganga ambaye muda huo alikuwa akinyanyua kitambaa alichojifunika kupiga ramli na kunyoosha mkono kuchukua maji. Alijinyoosha kuonyesha alichoka sana kisha alisema:
“Dada ondoka, kazi yako nzito, nilikuwa nakufa najiona angeendelea dakika tano ningekufa.”
“Angeendelea nani?”
“Binti hebu ondoka ukizidi kukaa hapa utanitafutia matatizo,” mganga alizungumza kwa wasiwasi huku akimeza funda la maji na kujishika shingoni kama mtu aliyekabwa.
“Kwani umepatwa na nini?” Subira alijikuta akimshangaa mganga.
“We’ mwana umetumwa? Hebu ondoka, kumbe ulipotoka ulimshindwa umekuja kunitafutia matatizo bure nikifa familia yangu utaitunza wewe?”
“Mmh! Makubwa.”
Subira alijikuta akichanganyikiwa asijue nini kimetokea, kwani muda mfupi alikuwa akizungumza na Nargis na ghafla tena akawa anazungumza na mganga, alijiuliza kile ni nini. Kwani baada ya kuzungumza na mganga ghafla akaja Nargis mara tena akarudi mganga.
Japokuwa alijiona kama yupo ndotoni lakini maneno ya Nargis yalikuwa na ukweli hivyo alitakiwa kuyafuata kwa usalama wa maisha yake. Hakutaka kuendelea kuwa pale kwani kila dakika mganga alipandisha hasira. Alinyanyuka na kutoka nje na kwenda kwenye gari lake na kurudi moja kwa moja ofisini kufanya aliyoelezwa na Nargis.
Aliendesha gari mpaka ofisini na kwenda moja kwa moja ofisini kwa Thabit na kuingia. Thabit alipomuona alishtuka na kumuuliza:
“Subira ulikuwa wapi?”
“Thabit naomba unisamehe.”
“Nimekusamehe, kaendelee na kazi.”
“Hapana kuna kitu nataka kuzungumza na wewe.”
Inaendelea
 
SEHEMU YA 34

Aliendesha gari na kwenda moja kwa moja ofisini kwa Thabit na kuingia ndani. Thabit alipomuona alishtuka na kumuuliza:
“Subira ulikuwa wapi?”
“Thabit naomba unisamehe.”
“Nimekusamehe, kaendelee na kazi.”
“Hapana kuna kitu nataka kuzungumza na wewe.”
“Kitu gani?”
SASA ENDELEA...“
Kuhusu mimi na wewe.”
“Kitu gani hicho?”
“Eti mimi na wewe tupo vipi?”
“Subira swali gani hilo?” Thabit alishangaa.
“Thabit naomba kuanzia leo uendelee na mkeo Nargis, mimi si mkeo.”
“Kwani wewe ndiye unayeongoza maisha yangu kwanza nani kakupa jeuri ya kusema hivyo?”
“Na kazi ndiyo mwisho.”
“Mbona sikuelewi, kama umeamua mwenyewe sawa.”
Subira alishangaa na kuamini kila chenye mwanzo kina mwisho, kwa hali ile ilionesha Thabiti alirudi katika hali yake ya kawaida. Hakuongeza neno alinyanyuka na kutoka nje ya ofisi. Kabla ya kuvuka mlango wa kutoka nje alifumba macho na kutoka, ghafla alijikuta kwenye nyumba nzuri. Hakuamini alibakia amesimama kama mgeni, mara alisikia hodi.
Hakujibu haraka, aliusogelea mlango na kuufungua, alishtuka kumuona Nargis akiwa amesimama.
“Ka...ka...ribu,” aliingia wasiwasi.
“Asante,” Nargis alisema huku akiingia ndani.
“Ka...karibu,” Subira alimkaribisha huku akitetemeka.
“Acha woga, hukuogopa ulipotaka kuniua uniogope nikiwa hivi.”
“Sa...sa...mahani dada Na...na...”
“Nargis,” Nargis alimalizia jina lake.
“Karibu dada.”
“Asante,” Nargis alijibu huku akikaa.
“Dada mimi ndo’ nafika hata sijui nyumba ikoje,” Subira alizungumza kwa unyenyekevu.
“Utajua kwa vile ni kwako, mi si mkaaji nimekuja kukumbusha tena achana kabisa na mume wangu ukijitia kiburi cha nazi kushindana na jiwe sitakuua nitakugeuza nzi wa chooni maisha yako yote yatakuwa kwenye kinyesi.”
“Dada nakuapia kuanzia leo sitamfuata mumeo, nashukuru kwa kunisamehe kwa ubaya wote niliokufanyia.”“Hilo si la muhimu kwangu zaidi ya kukukanya kwa mara ya mwisho.”
“Nakuahidi sitamsogelea tena, hivi nimetoka kumweleza pia kuacha kazi.”
“Nashukuru kama umenielewa.”
Baada ya kuachana na Subira, Nargis alirudi moja kwa moja ofisini kwa Thabit ili kuhakikisha kama kweli dawa za Subira alizopewa na mganga zimefanya kazi. Baada ya kufika eneo la ofisi za Thabit alitembea taratibu. Alijishangaa alivyokuwa mwepesi kila alivyotembea tofauti na siku za nyuma.
Alimsalimia mlinzi ambaye alimpokea na kujikuta akimuuliza.
“Shemeji ni wewe?”
“Ni mimi John.”
“Karibu.”
“Asante, mheshimiwa yupo?”
“Ndiyo.”
Wakati huo Nargis alikuwa ameishamweka jini sehemu ya mapokezi mwenye sura ya Subira ili asiwachanganye watu. Alipomuona alimkaribisha.
“Karibu binti wa mfalme.”
“Asante,” Nargis alijibu huku akiingia ofisini kwa Thabit.
Wakati huo Thabit alikuwa ameinama akiishangaa picha yake na Subira ambayo ilimshangaza sana kila alivyojiuliza alikosa jibu. Alijiangalia mkononi na kutandaza vidole kuangalia pete aliyoachiwa na mpenzi wake haikuwepo. Alijuliza kipi kimepita kwani alishindwa kuelewa nini kinaendelea.
Moyo wake ulijaa wasiwasi na kujiuliza kama mkewe Nargis angetokea siku ile na kukuta hali ile lazima angeonekana msaliti. Alipata wazo la kuziondoa picha zote alizokuwa amepiga na Subira wakionekana wapenzi kitu ambacho yeye kwa akili zake alikuwa hakumbuki kabisa kama aliwahi kuwa na uhusiano na mwanamke yeyote zaidi ya Subira.
Akiwa bado katika dimbwi la mawazo aliisikia sauti ya Nargis siku alipokuwa akiondoka kwenda kwao ujinini kujifungua: “Thabit naondoka nikiwa nimekuachia utajiri mkubwa ambao hutaumaliza mpaka unakufa, unajua kiasi gani nilivyopigana na majini wenzangu na wanadamu kukulinda.
Nina dhambi ya kuua majini na wanadamu kwa ajili yako. Nimewatia wanadamu na majini vilema ambavyo watakufa navyo kwa ajili yako. Thabit naondoka nakuacha peke yako, kwa utajiri ulionao una mtihani mzito kwa wanadamu kila mwanamke atakutaka wapo watakaokuendea kwa waganga ili wakupate. Kipindi changu cha kujifungua sitaweza kutoka mpaka miaka kumi hivyo sitakuwa karibu na wewe tena.
“Mpenzi naomba usinisaliti nimechoka kubeba dhambi za wanadamu na majini kwa ajili yako. Nakuomba baada ya kuondoka kaa mbali na wanadamu, mafuta niliyokuachia siku ukinikumbuka sana jipake usiku wakati wa kulala utaniota usingizini lakini hatutaonana mpaka miaka kumi ipite,” Nargis alisema kwa hisia kali.
“Nakuahidi kuwa muaminifu kwako, sitakusaliti nakupenda sana Nargis, nilitamani niwapokee wanangu wakati wa kuzaliwa lakini sina jinsi. Nenda mpenzi wangu ukijua nakupenda kuliko kiumbe chochote kilichoumbwa na Mungu. Nakuahidi kukusubiri hata kwa miaka mia moja,” Thabit alimuahidi Nargis.
“Kweli Thabit?” Nargis alimuuliza Thabit huku akimkazia macho yake makubwa lakini yenye urembo wa ajabu.
“Kweli kabisa.”
“Hutanisaliti?” alimuuliza tena.
“Siwezi.”
Baada ya kuyakumbuka maneno ya zaidi ya miaka kumi iliyopita alijikuta mapigo ya moyo yakimwenda mbio na kujiuliza Nargis akitokea na kuona zile picha alizopiga na Subira atamuona mnafiki na muongo. Wazo lilikuwa kuzitoa picha zote na kuzichoma moto.
Akiwa katika mawazo mazito alisikia mtu akibisha hodi, alitulia bila kujibu huku macho yake yakitua kwenye picha kubwa ya Subira akiwa katika tabasamu pana iliyokuwa mbele yake ambayo siku ile lilikuwa tabasamu baya kama amemuona mtoa roho mbele yake.
itaendelea
 
Kwakweli sijapenda mwandishi uliposema kuwa Mzee Dumidunzi atampa Nargis kitu chenye uwezo robo ya Muumba. Hapana tena sema Astaghafirullah hakika uwezo wa Mungu hakuna kiumbe chenye uwezo wa kuufikia hata chembe ya mchanga wala nukta.
 

Similar Discussions

Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…