Simulizi ya Kijasusi: Safari ya Gavin Luca

Simulizi ya Kijasusi: Safari ya Gavin Luca

FEBIANI BABUYA

JF-Expert Member
Joined
Mar 5, 2022
Posts
2,229
Reaction score
4,345
Season 2 ya IDAIWE MAITI YANGU

Gavin Luca

Katika Idaiwe Maiti Yangu, tulimfahamu Gavin Luca, lakini alibaki kuwa na hali ya kutatanisha. Hatukujua kama alikufa au alifanikiwa kuishi. Zaidi ya hayo, hatukuweza kugundua hatima ya nguvu zake wala mustakabali wa mtoto wake katika zile nguvu.

The Odyssey of Gavin Luca inakuja kutoa majibu ya maswali haya yote. Tutajua kilichotokea wakati ule, nini kilitokea kwa Gavin Luca, na ni nini kinatarajiwa kutokea siku zijazo.

Lionela, mtoto pekee wa Gavin Luca, anakuja kuwa kiumbe mwenye nguvu nyingi duniani, akitambua ukweli kwamba baba yake alikuwa mfu. Lakini je, ni kweli alikufa? Hatujapata uthibitisho wa kifo chake, na hakuna ishara ya uwepo wake.

Kama alikufa, kwa nini hakukuwa na dalili yoyote ya upanga wake au alama nyingine za uwepo wake? Kama alifanikiwa kuishi, alifanikiwaje kutoka kwenye hali kama ile? Yupo wapi sasa, na ni nini hatima yake?

Nini Kinaendelea Kuikumba Familia Hiyo Maarufu na Tajiri?

Je, kuna mtu alisahaulika katika The Immortals, au kuna siri nyingine nyuma ya pazia?

Nakukaribisha kuisoma hii simulizi inayofuata! Hautakiwi kuikosa simulizi hii kwa gharama yoyote ile.

Kabla ya kuisoma hii, hakikisha umeisoma Idaiwe Maiti Yangu, kwani ni sehemu ya kwanza ya hadithi hii.


Tunaanza rasmi kuzifunua kurasa zake.
Lionela-4.jpg
 
HADITHI: THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA (LIONELA)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
UKURASA WA KWANZA
ANZA NAYO................

MAHAKAMANI
Ndani ya mahakama kuu ya taifa kulikuwa na kesi nzito ambayo ilikuwa inaendelea siku hii maalumu kwa ajili ya kusikiliza na kumhukumu mwanaume mmoja ambaye alikuwa ametenda uhalifu usio elezeka kwa lugha ya kawaida na kila mtu akaweza kuielewa kwa usahihi.
Ndani ya mahakama ni watu wengi ambao walikuwa wamefika mapema wakiwa wanaisubiri kesi hiyo ambayo ilikuwa gumzo kwenye kila kona ya mitaa. Walikuwa wamejiandaa vyema huku wakiwa wanamsubiria mhusika mwenyewe ambaye ndiye kesi hiyo ilikuwa inamhusu aweze kufika ili kesi ianze. JOPA MAGOMA, ndiye mwanaume ambaye alikuwa anasubiriwa ndani ya mahakama tukufu ili aweze kusomewa mashtaka yake mazito ambayo yalileta msisimko mkali ndani ya jamii ndiyo sababu kesi yake ilikuwa inasubiriwa kwa hamu kubwa na watu wengi kila pembe.

Ndani ya muda mfupi, msafara wa gari za polisi na gari moja ambayo ilikuwa inatumika kubebea wafungwa iliwasili ndani ya mahakama hiyo huku kukiwa na ulinzi mkali mno kiasi kwamba hakuna mtu alikuwa anasogelea kirahisi ndani ya eneo hilo. Hata waandishi wa habari walijaribu kupenya penya na kupiga picha za kuibia ila hakuna ambaye alipewa uhuru wa moja kwa moja kufanya ambacho walikuwa wamemikusudia ili kuweza kuuza habari zao kwa ukubwa.
Kwenye ile gari ya wafungwa, alishushwa mwanaume mmoja ambaye alikuwa pande la mtu, alijazia vyema, afya haikuwa mgogoro kwa upande wake. Bwana yule kichwani alikuwa amenyoa upara ambao ulikuwa unang’aa isivyo kawaida huku akiwa na ndevu za kutosha kwenye mashavu yake na kidevuni, bila shaka zilitunzwa vyema.
Wakati wanamtoa mle ndani ya gari ndipo yalipatikana majibu sahihi kwamba huenda hakuwa mtu wa kawaida kama ambavyo wengi walikuwa wanamhisi. Alikuwa amefungwa minyororo mizito kwenye miguu yake huku kwenye mikono yake akiwa na pingu ambazo zilifungwa upande wa mbele. Kila baada ya hatua moja kulikuwa na askari wenye silaha nzito ambao walihakikisha bwana huyo anafika mahakamani salama na kupata kile ambacho alikuwa anastahili kukipata kwa yale ambayo aliyafanya.
Wakati anaingia ndani ya chumba cha mahakama, watu wote waligeuka kumwangalia bwana yule huku akiwa hana muda nao, alipelekwa mpaka kwenye kizimba, mahali ambapo alitakiwa kuwepo mpaka pale ambapo kesi yake ingefika mwisho. Bwana huyo hakuonekana kabisa kujali yale yote ambayo yalikuwa yanaendelea ndani ya lile eneo kwani aliona kama wanapoteza muda tu. Licha ya mawakili wake kujitahidi kupambana kuweza kumtetea lakini ilishindikana ila jambo la kushangaza ni kwamba yeye alikubali kwa mdomo wake kwamba mashtaka yote ambayo alikuwa ametajiwa pale, ni kweli alihusika nayo mwenyewe lakini hakuwa tayari kuomba msamaha jambo ambalo lilileta hisia zingine mpya ndani ya mahakama hivyo kazi ikabaki kwa jaji kufanya maamuzi ya mwisho kwani kila kitu kilikuwa wazi.

“Jopa Magoma, usiku wa tarehe kumi na tano ulihusika kwenye tukio la kumbaka mwanamke mwenye miaka kumi na tisa kisha ukamuua, unakubali mashtaka yako?”
“Ndiyo mheshimiwa jaji”
“Usiku mwingine wa tarehe ishirini tena ukahusika kwenye ubakaji na mauaji ambapo ulimbaka binti wa miaka kumi na sita kisha baadae ukambaka mama wa miaka arobaini na tano na haukuishia hapo tu ukafanikiwa mpaka kuwaua. Jopa Magoma, unakubali mashtaka haya?”
“Ndiyo mheshimiwa jaji”
“Una lolote la kusema kwa kile ambacho umekifanya kama kuwaomba msamaha ndugu na watanzania kwa ujumla kwa matukio yako yasiyo faa ambayo umeyafanya kiasi kwamba yameacha mapengo yasiyoweza kuzibika na maumivu makali kwa ndugu wa hao ambao umewafanyia ukatili?”
“Hapana, wote waliokufa walistahili kufa na kubakwa kama ambavyo nimefanya. Sijutii na wala siwezi kuomba msamaha mheshimiwa jaji”
“Mahakama imekukuta na hatia za kubaka na kuua kwa kukusudia ukiwa na akili timamu hivyo mahakama inakuhukumu kifo ambapo kabla ya kufa utapitia mateso makali ili iwe fundisho kwa watu wengine” jaji aliongea akiwa anaimaliza kesi hiyo huku akiinyanyua nyundo yake ili aweze kuigonga kuweza kuhalalisha hukumu ambayo alikuwa ameisoma mbele ya mahakama lakini ndipo ukatokea mshtuko mkubwa baada ya umeme kuzima ghafla.

Jopa, alikuwa ni mwanaume mwenye jeuri mbele ya mahakama, bwana huyo alihusika kwenye ubakaji wa wanawake watatu pamoja na kuwafanyia mauaji lakini akiwa mbele ya mahakama alikubali mashtaka yote na kugoma kuomba msamaha jambo ambalo lilifanya aipate hukumu ya kifo tena kwa mateso makali kabla ya kufa. Jaji mkuu akiwa yupo kwenye harakati za kuigongesha nyundo yake ndipo umeme ukakata.

Zilipita sekunde kumi tu umeme ukawa umerudi tena lakini wakati umeme unarudi, mwanaume yule hakuwa kwenye minyororo wala pingu. Jopa alikuwa huru kabisa akiwa amesimama nje ya kile kizimba mahali ambapo aliwekwa kwa mara ya kwanza. Kuwa huru halikuonekana kuwa jambo jema mle ndani, kila mtu alibaki ameduwaa asijue ni kitu gani kilikuwa kimetokea kwa wakati ule. Jaji alitoa amri ya kukamatwa kwa Jopa, ni kwa bahati ambao haikuwa upande wao.
Bwana yule hakuwa wa kawaida ndiyo maana alifungwa vizuri tangu mwanzo, alitua mguu wake mmoja kwenye kile kizimba kama anakipanda, alipinda kwa sarakasi ya nyuma ambapo alitua kwenye shingo ya askari aliyekuwa karibu yake akimjia kwa kasi, wakati anashuka naye chini aliivunja shingo yake mpaka ndani ya mahakama kukazuka kelele za hofu watu wakianza kuogopa. Alijivuta kwa nyuma na kugeuka kwa mguu wake ambao ulitua kwenye uso wa askari aliyekuwa pembeni akajibamiza ukutani kichwa kikapasuka.

Askari walianza kuongezeka mahali ambapo alikuwepo bwana huyo, mmoja alikuwa ameshika kiti cha mbao, alikirusha kwa nguvu zake zote ila kiliishia kupasukia kwenye mikono ya huyo bwana ambaye alimvuta askari huyo na kumtwisha ngumi yake moja kwenye shingo, shingo ilipinda akamtupa. Mwanaume mmoja ambaye alisimama kama shahidi wa upande wa bwana huyo alikirusha kisu kidogo kwa nguvu kuelekea kwa yule bwana na wakati anakidaka kilitua kwenye shingo ya askari mmoja ambaye alimkata kata kama karoti.

Aligeuka kwa nguvu zote miguu yake ikatua kwa askari wawili ambao walikuwa wanamjia lakini kisu kile alikirusha mbali huku akianza kukimbia kwa nguvu ambapo alipita kwenye vichwa vya wananchi ambao walikuwa wamenza kunyanyuka huku wakipiga makelele. Ile sehemu ambayo aliirushia kile kisu kulikuwa na askari wawili wenye silaha, wakati anakirusha kisu kile askari mmoja alikuwa mbele ya mwenzake akiwa amenyoosha silaha kuelekea alikokuwepo Jopa ila alionekana kusita sita kuiruhusu kwa sababu asije akashambulia watu wengine ambao hawana hatia.
Kule kusita kwake ilikuwa hatari kwake na kwa mwenzake kwa sababu ile nguvu ambayo ilitumika kurusha kile kisu ilikuwa sio ya kawaida. Kilizama kwenye shingo yake na kupita mpaka kwa askari aliyekuwa nyuma yake ambaye yeye kilimbaraza kwenye kifua kwa sababu alikuwa mrefu kuliko ambaye alikuwa mbele yake. Muda ambao aliutumia kuhangaika kuweza kuuguza yale maumivu na kuweza kukitoa kwenye mwili wake ndio muda ambao Jopa aliutumia kutembea kwa kasi kumuendelea pale ambapo alikuwepo hivyo wakati anafanikiwa kukitoa mwanaume huyo alikuwa amemfikia.
Alikutana na ngumi ya uso askari yule akainama chini akakutanishwa na goti ambalo lilimuinua tena kwa lazima akiwa anapiga kelele za kuomba msaada lakini hakuna ambaye angemsaidia wakati huo. Mwanaume huyo alimdaka kwenye shingo na kuinyofoa vibaya kisha akakichana kifua chake na kuupiga moyo kwa ngumi kali kiasi kwamba ulipasukia mwilini. Ile hali ndiyo iliwafanya watu watawanyike kama wamechanganyikiwa ili kuweza kuondoka lile eneo, wengi walianza kujutia kuja ndani ya lile eneo hiyo siku lakini nani angejua? Muda wao ulikuwa umefika.

Wakati wanasogelea ulipokuwa mlango wa kuingilia ndani ndipo mlango ulifunguka nje wakatokezea watu ambao walivaa kama walinzi ambao walikuwa na silaha mkononi, raia wote walitandikwa risasi mpaka pale walipo isha ndipo risasi zikatulia. Jambo la kushangaza ni kwamba wale watu ambao waliwashambulia raia walikuwa ni miongoni mwa askari ambao walikuwa walinzi wa hiyo mahakama. Jaji alichoka.
Hakuwa mzee lakini umri wake kidogo ulikuwa umeenda jaji wa Tanzania, alikuwa amekaa pale pale kwenye kiti chake akiwa anashuhudia kila jambo ambalo lilitokea ndani ya mahakama yake. Tangu mambo yote yanatokea alikuwa ametulia tu kana kwamba hakuna jambo ambalo lilikuwa baya wakati huo. Utulivu wake ulisababisha yeye kuangalia kwa umakini hatua zote ambazo zilikuwa zimefanywa na watu hao.
“Usiendelee kufanya kosa lingine kij….” jaji hakupewa nafasi ya kuweza kuongea lolote, alipigwa na ngumu nzito kwenye shingo yake na mtu ambaye yeye hakumuona kwamba alikuwa amesimama nyuma yake mpaka akapoteza fahamu.
Wanaume hao ambao hawakujulikana kwamba walikuwa ni akina nani haswa na kwanini walikuwa wanayafanya hayo yote, walifanikiwa kufanya ukatili ndani ya mahakama kisha wakatoweka na jaji eneo hilo mahakama ikiwa wazi kwani wafanyakazi wote waliuawa, ni jaji tu pekee ambaye waliondoka naye akiwa mzima, ilionekana kabisa kwamba walikuwa wana uhitaji mkubwa na huyo jaji ndiyo sababu hawakuwa tayari kuweza kumuangamiza kirahisi.

Ndo kwanza kabisa tunaufunua UKURASA kwa kwanza wa simulizi hii. Tuna mengi ya kuyafahamu na kuweza kuyapatia majibu.

Twende sawa pamoja mwanzo mpaka mwisho.

Langu jina FEBIANI BABUYA.
Lionela-4.jpg
 
tuliza kipago ww New member kwa vile ni umejiunga leo JF..bila shaka humjui mtunzi basi fanya kubonyeza ID yake utaona story zake zote kisha soma story zake..karibu sana jamvini new member
Shukrani kwa kunisaidia kumjibu mkuu
 
HADITHI: THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA (LIONELA)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
UKURASA WA PILI
SONGA NAYO................

Jaji alishtuka baada ya muda kupita, ubaridi ndio ambao ulimshtua kwani mwili wake haukuwa na ushirikiano kwa sababu baada ya kushtuka tu alianza kutetemeka. Aliamshwa na maji ya baridi isivyokuwa kawaida ambayo ndiyo yaliufanya mwili wake kuwa kwenye ile hali ambayo alikuwa nayo wakati ule. Macho yake yalikuwa mazito, mwili ulikuwa umechoka huku akiwa na njaa kali ila haikuwa sababu ya kuyarudisha nyuma yote ambayo yalikuwa yametokea kule mahakamani.
Kumbukumbu zake zilirudi vizuri ndipo alishtuka baada ya kugundua kwamba hakuwa salama mpaka wakati huo, jambo hilo ndilo lilimfanya atahayari na kuanza kuangaza ndani ya hilo eneo ili kuweza kujua mahali ambapo alikuwepo kwani alijiona kabisa kuwa kwenye hatari kubwa ya kuyapambania maisha yake. Chumba ambacho alikuwepo kilikuwa kitupu kabisa zaidi ya sehemu tu ambayo yeye alikuwa ameketi, hakuona mtu hata mmoja na ndio wakati ambao akili yake ilirudi kwenye lile tukio ambalo lilikuwa limetokea ndani ya mahakama yake tukufu.

Moyoni alihofu kwa sababu hakujua kwamba ni nani alikuwa amemfanyia jambo lile, hakujua kabisa kwamba yule mtuhumiwa alikuwa ni nani haswa. Alishangazwa na bwana yule kufanya jambo lile mbele ya mahakama na kuua watu namna ile, hali hiyo ndiyo ilizidi kumpatia hofu kubwa kwenye moyo wake. Alitamani kuweza kumjua bwana yule kwamba alikuwa ni nani haswa kwenye maisha yake mpaka kuishia kwenye hali kama ile lakini hakufanikiwa kulipata jawabu lake kwa sababu muda huo haukuwa rafiki sana kwa upande wake akabaki na maswali ambayo hakuwa na uwezo wa kuyapatia majibu akiwa mwenyewe.
Ule ujasiri wa kufanya tukio kama lile tena mbele ya mahakama haukuwa wa kawaida, ulikuwa ni ujasiri ambao walikuwa wanauweza wanadamu wachache kwenye haya maisha ya kawaida. Hata walinzi wa mahakama walimshangaza, ilikuwaje wao ndio wakashiriki kwenye kutekeleza tukio kama lile? Maana yake ni kwamba walikuwa wanashirikiana na hao watu kwa muda mrefu? Hao watu ni akina nani na kulikuwa na nini haswa mpaka wakafanikiwa kuwafanya watu hao kukubali kulisaliti taifa lao na kufanya kazi na hao mabwana ambao bila shaka hakuwajua kabisa? Jibu lilibakia kuwa kizungu mkuti kwani alikuwa mwenyewe hata mtu wa kumuuliza hakuwepo humo ndani.
Jambo kubwa ambalo liliendelea kumtia hofu zaidi bwana huyo ni juu ya usalama wake na hatima yake kwa ujumla, aliletwa ndani ya hilo eneo asijue alikuwa anatakiwa kufanya jambo gani au kwanini alibakishwa akiwa hai. Huenda ni kazi yake ya kuhukumu watu ndiyo ilikuwa imemponza? Lakini kwanini iwe kwa mfungwa kama huyo ambaye aliua watu wengine wote? Ndipo aligundua kwamba jambo pekee la yeye kuweza kuijua sababu ya kuwa hilo eneo ni kusubiri mtu yeyote ambaye angekuja hapo ili aweze kuongea naye japo hakujua jambo hilo litawezekana kwa muda gani.

Akiwa anaendelea kujuta kwa mateso makali ambayo alikuwa anayapata hilo eneo ndilo mlango ulifunguliwa, kufunguliwa kwa mlango huo alimuona yule bwana mtuhumiwa wake akiwa anaingia ndani ya hilo eneo akiwa amezungukwa na wanaume wawili. Bwana huyo alikuwa amevaa suti ya blue lakini wale wengine wawili ambao wote walikuwa wamekaa upande wake wa kulia na kushoto, wao walikuwa ndani ya suti nyeusi ambazo ziliendana vyema na miili yao. Bila shaka alitambua kwamba huenda walikuwa ni walinzi wake.
“Unajua kwanini upo hapa mheshimiwa jaji?”
“Bila shaka sipo hata kuuawa kwa sababu mimi na wewe wote tunajua kwamba kama nilitakiwa kufa mpaka sasa nisingekuwa napumua”
“Huenda upo sahihi lakini kuishi kwako pia itategemea na aina ya mazungumzo ambayo utakuwa nayo hapa muda huu mheshimiwa”
“Unataka nini kutoka kwangu?”
“Kwanini unahisi nataka kitu kutoka kwako?”
“Kwa sababu kama ungekuwa unataka ni pesa usingetumia njia hii, wote tunajua hilo hivyo tufupishe mazungumzo, nenda kwenye hoja ya msingi moja kwa moja kwa sababu hapa nilipo nateseka na baridi na nina njaa kali sana natakiwa kwenda kula nyumbani”
“Mhhhh unawaza kwenda nyumbani?”
“Mimi ni mtu ambaye siku zote huwa nina amini kwamba lazima nipate njia ya kuishi hata kama nitakuwa kwenye mazingira ya namna gani, kwahiyo niambie sababu ya wewe kufanya haya yote ili uweze kukutana na mimi sehemu kama hii’
“Una kazi rahisi sana ya kuweza kuyaokoa maisha yako wakati huu ili nikuache hai, nahitaji unipatie jibu moja kwamba ipo wapi familia ya Gavin Luca”
“Samahani nahisi nimekusikia vibaya, umesema?” jaji alishtuliwa na jambo ambalo alilisikia kwenye kinywa cha huyo mwanaume kwa sababu lilikuwa jipya na kubwa mno kwake na hakutegemea kama angekutana na jambo la namna hiyo ndiyo maana waziwazi alionyesha hofu yake lakini bwana huyo hakuonekana kuwa na utani kwenye hilo jambo.
“Nina uhakika umenisikia vizuri, nina muda mchache wa kuwa na wewe kwenye hili eneo hivyo unaweza kunijibu haraka”
“Mhhhhhh naona mimi na wewe tuna mazungumzo marefu sana bwana Jopa, kama ungekuwa na namna nyingine basi usingeua watu wengi namna ile ili uweze kunipata mimi hapa, huenda nikawa msaada mkubwa kwako hivyo kwanza kabla ya kufungua rasmi haya mazungumzo, nataka unitoe kwenye hiki chumba na unipatie chakula ndipo tuongee kwa marefu juu ya jambo hili”
Jopa alimwangalia kwa umakini jaji huyo, alionekana kuwa mtu ambaye alijiamini ndiyo maana hakuwa na papara baada ya kusikia ambacho Jopa alitaka kukijua japo ni wazi kilionekana kumshtua kwa namna yake. Ilitolewa amri bwana huyo afanyiwe kile ambacho yeye alikuwa anakitaka kisha baada ya nusu saa maongezi yao yakawa yameanza upya kwa mara nyingine.
“Ni nani huyo ambaye anaitafuta hiyo familia?” lilikuwa swali la kwanza la jaji baada ya kuwa sehemu nzuri ambayo haikuwa inamuumiza kama ile ya kwanza.
“Mimi hapa”
“Hapana, nina uhakika sio wewe hapo, hakuna mtu ambaye anaitaka hiyo familia anaweza kuwa na jeuri ya kuonyesha sura yake hadharani tena kwa kujiamini namna ile. Ninajua kwamba wewe unatumika tu hivyo nataka kumfahamu huyo mtu ndipo tuendelee na haya maongezi”
“Una familia jaji, usifanye haya mambo kuwa magumu kwa sababu hivi ninavyo ongea na wewe, watu wangu wapo na familia yako muda wowote nitatoa amri hapa waue familia yako kwa sababu ya ujivuni wako ambao hauna umuhimu. Kuhusu nani kanituma au nafanya kazi kwa ajili ya nani hiyo sio biashara yako hivyo fanya yale ambayo yamekufanya wewe uwepo hapa vinginevyo sio muda mrefu utaanza kunipa lawama”
Mwanaume huyo wakati anaongea hivyo wote waligeukia ukutani sehemu ambayo ilikuwa imeunganisha na skrini kubwa. Ilianza kuonekana mijongeo ya video ikionekana watu kadhaa ambao walikuwa wamechangamana na walinzi wa jaji na hakuna mtu ambaye alikuwa amewashtukia nyumbani kwa bwana huyo jambo ambalo lilimpa wasiwasi mno hivyo alitakiwa kujibu kile ambacho aliulizwa, alimeza mate kwa shida, familia ilikuwa kila kitu kwake.
“Who are you people? (Nyie watu ni akina nani?)”
“Non of your business (Sio biashara yako)”
“Hiyo familia hakuna mtu hata mmoja ambaye anajua ilipo mpaka wakati huu ambao wewe unanihoji hapa”
“Whaaat?”
“Nina uhakika umekuja kwangu ukiamini utapata msaada jambo ambalo ulikuwa sahihi kabisa lakini huo msaada hauwezi kuupata kirahisi hivi leo leo kama ambavyo wewe unaonekana unatamani iwe japo mimi na wewe tunaweza kulifanikisha hili jambo pamoja”
“Nadhani bado haujanifahamu kwamba unadili na mtu wa namna gani bwana jaji ndiyo maana unayajibu maswali yangu kirahisi sana namna hii”
“Jopa hapa jambo la msingi sio mimi kujua kwamba nadili na nani bali ni aina ya taarifa ambazo wewe unazihitaji. Kufanikiwa kunijua tu mimi umefanya kazi kubwa sana ambayo ni hatua ya kwanza kwenye mafanikio yako ila jambo la kuipata hiyo familia ni jambo la pili ambalo linahusiana na mimi kwa udogo hivyo sio rahisi kama ambavyo huenda umepewa taarifa kwamba itakuwa”

Ukurasa wa pili unafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 

Attachments

  • downloadfile-200.jpg
    downloadfile-200.jpg
    80.9 KB · Views: 58
tuliza kipago ww New member kwa vile ni umejiunga leo JF..bila shaka humjui mtunzi basi fanya kubonyeza ID yake utaona story zake zote kisha soma story zake..karibu sana jamvini new member
Sawa kipago mwenzangu tuendelee kula mtori nyama tutazikuta chini
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom