Simulizi: Mwanafunzi Mchawi (A Wizard Student)

Simulizi: Mwanafunzi Mchawi (A Wizard Student)

SEHEMU YA THELATHINI

....Dorice aliendelea Julia huku matone yake ya machozi yakiwa damu. Ghafla akajikuta ana uwezo wa ajabu ambao hajawahi kuufikiria kuwa nao hata siku moja. Alijibadilisha sura na kuwa kiumbe wa kutisha, macho yalikuwa kama ya paka, uso wake ukawa mweusi tii kama mkaa, kucha zake zikawa ndefu sana na meno yake mawili yalichomoza nje ya kinywa chake. Mansoor alicheka kicheko kikali cha kutisha huku sauti ya kicheko chake ikiambatana na mwangwi. Radio zikapiga mfululizo Dorice akatoweka ghafla na kumuacha Mansoor.

Pete aliyokuwa amevalishwa Dorice ilimpa uwezo mkubwa na wa ajabu. Alipata uwezo wa kupotea na kujibadilisha kadri atakavyo lakini sharti kubwa alilotakiwa kufanya ilikuwa ni lazima arudi tena kwa Mansoor baada tu ya kumaliza kazi yake inayompeleka duniani.

Dorice alikuwa ametokeza katika eneo lenye Giza Giza lilitawaliwa sauti za wadudu. Palikuwa na utulivu mkubwa sana , kwani eneo lile halikukaliwa na mtu yeyote zaidi ya ndege, wadudu na wanyama wadogo wadogo. Dorice alibaki anajishangaa, alijiuliza amefika vipi eneo lile akiwa peke yake bila Mansoor.

"Ina maana nimekuwa na nguvu za kijini?" Alijiuliza Dorice. Ghafla upepo mkali ukapuliza eneo lile, Dorice alitazama huku na kule ili kujua nani alikuwa mgeni wake kwa wakati ule. Ghafla Mansoor akajitokeza akiwa anacheka kicheko cha kutisha sana kisha akapiga hatua za taratibu kumsogelea Dorice.

"Kwanini umefika huku?" Aliuliza Mansoor kwa ghadhabu.
"Sijui nimefikaje" alijibu Dorice.
"Muda wako wa kuondoka kwenye himaya yangu bado Dorice, nilikuwa na jaribu kukupa ladha ya vile utakavyokuwa baada ya wakati kutimia" alisema Mansoor.
"Kwahiyo unataka nirudi?"
"Ndio.. Tunarudi wote".

"Hapana Mansoor sitaki kurudi tena Kule" alisema Dorice.
"Ni lazima urudi maana bado sijakupa maelekezo"
"Hayo maelekezo nipe hapa hapa"
"Haraka haraka ilimfanya chura apate ngozi ya mabaka"
"Hata hivyo siwezi kurudi".

Yalizuka mabishano makali baina ya Dorice na Mansoor kwani Dorice hakutaka kurudi kwenye himaya ya Mansoor tena. Alitaka aachwe huru na arudi kwao, lakini mkongwe ni mkongwe tu licha ya mabishano Yale Mansoor aliibuka mshindi baada ya kumchukua Dorice kinguvu kwa kutumia uwezo mkubwa wa kijini alionao. Katika eneo walilokuwepo ukatokea upepo mkali na kuwavuta wote wawili kisha ndani ya muda mfupi walijikuta wametokea katika himaya ya akina Mansoor. Dorice alikasirika sana.

*****

"Mama mbona sikuelewi" aliuliza mlinzi kwa hofu huku akimtazama Mama Eddy kwa woga.
"Wewe!" Alisema mama Eddy akiwa amevimba kama mbogo huku akimsonta mlinzi yule kwa kidole chake na kumfanya mlinzi yule atawaliwe na hali ya sintofahamu.
"Nimefanya nini mama?".

"Kaa mbali na Eddy... Nakusisitiza Tena kaa mbali na Eddy la sivyo utakiona cha mtema kuni paka shume wewe!"alisema Mama Eddy huku akipiga hatua na kutaka kuondoka.

Alitembea kwa hatua chache tu kisha akamgeukia tena mlinzi na kumuonya vikali kuwa asiwe karibu na Eddy. Mlinzi yule hakuelewa mwanamke yule ana maana gani kumwambia vile. Alibaki na maswali mengi kichwani mwake huku akimsindikiza kwa macho mwanamke yule aliyejongea taratibu machoni mwake baada ya kuingia ndani ya jumba la kifahari la Mr Alloyce. Mlinzi aliachana na mwanamke yule kisha akaendelea na kazi zake za kupunguza maua.

Mama Eddy aliingia ndani na kumkuta Mr Aloyce akiwa ameketi kwenye sofa huku uso wake ukidhihirisha furaha kubwa aliyonayo moyoni mwake. Alifurahia sana kurudi kwa mkewe katika familia yao ili waendelee kuijenga na kuidumisha furaha yao ikiwa ni pamoja na kutafuta tiba ya tatizo la mtoto wao wa pekee.

"Mwanangu yuko wapi?" Aliuliza Mama Eddy huku akitabasamu. Baba Eddy alinyanyua kichwa chake na kupaza sauti yake akimwita mwanaye. Bila kuchelewa Eddy alirudi sebuleni na kumkumbatia mwanamke yule aliyedhani ni mama yake.

"Mama bora umerudi.. Tulikuwa wapweke sana humu ndani!" Alisema Eddy na kumfanya mwanamke yule atabasamu kwa furaha.
"Nimerudi mwanangu" alisema mwanamke yule. Familia ile ikarejewa na furaha iliyokuwa imepotea ndani ya muda mfupi uliopita.

Wakiwa wameketi sebuleni pale kwa utulivu wa hali ya juu, ghafla simu ya Mr Aloyce iliita, akaitoa mfukoni na kuangalia nani alimpigia. Alipotazama tu akaona namba aliyoisevu "Shem Dar" akashtuka kidogo kisha akapokea.

"Ndio..ndio shemeji!" Alisema.
"Nipo njiani na sio muda nafika hapo nyumbani" ilisikika sauti ya Dada yake Mama Eddy.
"Unakuja hapa kwangu?"
"Ndio.. Si ulisema kuna matatizo!"
"Mh Haya karibu"

Baada ya mazungumzo hayo simu ikakatika ndipo Mr Aloyce akaona si vyema kumficha mkewe kuhusu jambo lile. Akamweleza kila kitu kuhusu chanzo cha Dada yake kufika nyumbani kwao.

"Ulimwambia kuna tatizo gani?" Alisema mama Eddy kwa mshangao.
"Nilimwambia tu kuna tatizo na sikumweleza ni tatizo gani. "
"Vizuri! Akija hapa usimweleze chochote kuhusu suala la Eddy" alisema Mama Eddy. Kauli hiyo ilimshtua Mr Aloyce kwani hakuona haja ya kumficha shemeji yake kuhusu jambo lile.

"Kwanini nisimwambie? Hujui kama anaweza kutusaidia.. Pengine hata kwa ushauri..." Alisema Baba Eddy.
"Nimesema usimwambie chochote.." Alisema Mama Eddy na kuinuka kitini kisha akaondoka sebuleni pale na kuwaacha Mr Aloyce na Eddy.

Mr Aloyce alibaki na mshangao sana kwani alikumbuka jinsi ambavyo Mama Eddy wanavyopatana na kuelewana kama mapacha iweje Leo amfiche matatizo yake?. Alishindwa kuelewa sababu akabaki kimya kitini pale.

*****

Mama Pamela na mwanaye waliendelea kuusubiri usingizi uwachukue ili kupambazuke haraka. Usingizi ulichelewa sana kuwachukua lakini haukuwaacha kabisa. Baada ya kuusubiri kwa muda mrefu wakiwa na hofu kupita kiasi hatimaye usingizi ukawapitia. Kila mmoja alilala fofofo kutokana na uchovu pamoja na mihangaiko mingi iliyosababishwa na mauzauza ya usiku ule.

Hatimaye kukapambazuka lakini bado wanafamilia ile walikuwa wapo katikati ya usingizi. Mlango wa chumba iligongwa na kumfanya mama Pamela ashtuke usingizini na kusikiliza nani aligonga.

"Mama" sauti nyororo ya Doreen ilipenya masikioni mwa Mama Pamela ikiwa na wingi wa adabu na upole uliokithiri. Bila kusita mama Pamela Aliitikia wito na kumsikiliza Doreen anahitaji nini.

"Hauendi kazini? Pia Dada Pamela haendi shule?" Aliuliza Doreen.
"Hatuendi... Wote tupo likizo.." Alijibu Mama Pamela .
"Sawa mama.. Nilifikiri mmesahau.. Ngoja niendelee na kazi"
"Hebu njoo kwanza.." Mama Pamela alimwita Doreen na kutaka aingie chumbani.
"Abee mama" Doreen aliitika kwa heshima na kusogelea karibu kabisa na kitanda cha Mama Pamela.

"Hivi usiku ulilala salama?"
"Ndio kwani vipi?" Aliuliza Doreen kwa mshangao.
"Mh! Kweli?"
"Ndio.. Kwani nini kilitokea"
"Duh basi kama ulikuwa salama sawa... Hakuna tatizo!" Alisema mama Pamela.

Doreen alijifanya kushangaa kupita kiasi, lakini hakuuliza zaidi. Aliachana nao na kwenda jikoni kuandaa chai.Alichemsha maji na kuweka majani ya chai. Na baada ya kuhakikisha imechemka vizuri akaiipua vizuri kisha akatemea mate halafu akaiweka kwenye chupa ya chai huku akicheka.

"Mtakoma mwaka huu..." Alijisemea Doreen kisha akapeleka chai mezani. Akarudi jikoni na kuchemsha maini ya ng'ombe lakini alipokuwa akichemsha maini yale alichanganya na maji Fulani yaliyokuwa kwenye kichupa Fulani kidogo.

"Na mtakula sana uchafu wangu... Huu mkojo tu! Bado vingine vinakuja" alisema Doreen kwa sauti ya chini.Maini Yale yalichemka vizuri na kutoa harufu ya kuvutia sana. Baada ya kuyaivisha vizuri akachukua mayai ns kuyakaanga vizuri kisha akapeleka mezani na kuandaa vizuri.

Majira ya saa tatu asubuhi Mama Pamela na mwanae waliamka. Wakaoga na kwenda chumba cha kulia chakula.
"Doreen kumbe umeshaandaa kila kitu" alishangaa Mama Pamela.
"Ndio mama! Karibuni" Aliitikia Doreen.
"Asante.." Alisema mama Doreen huku akiketi na kusogeza karibu mikate, akaipaka blueband.

"Mbona wewe huji kula?" Alimuuliza Doreen.
"Mimi tayari.. Hivyo ni kwaajili yako na dada Pamela"
"Oh sawa.. Mwite Dada yako aje kula maana ni mvivu kweli" alisema mama Pamela huku akianza kukishughulikia chakula kile. Punde tu Pamela naye akaenda mezani pale na kuanza kula.

Wakati huo Doreen alikuwa pembeni yao akiwatazama jinsi wanavyokula chakula kile kichafu. Aliwasikitikia sana moyoni mwake lakini wao walimmwagia sifa tele kwa utamu wa chakula kile. Kila mmoja alimsifu Doreen kwa kumwambia ni fundi wa Mapishi.

"Doreen mwanangu.. Nataka nikuulize kitu" alisema Mama Pamela huku akimeza funda moja la chai na kutua kikombe taratibu kwenye meza nzuri na safi ya kioo. Kauli ile ilimshtua kidogo Doreen na kumfanya amuulize vizuri mama Pamela.
"Kitu gani mama?"

ITAENDELEA.......
 
SEHEMU YA THELATHINI NA MOJA

...Doreen alimsikiliza kwa Umakini mama Pamela ili ajue ni swali gani analotaka kuuliza. Mama Pamela alikaa vyema kisha akakohoa kidogo na kumtazama Kwa makini Doreen.
"Niulize Tu mama" alisema Doreen.

"Hivi ni kitu gani unapenda nikufanyie ili moyo wako ufurahi? Maana nimependa sana heshima na adabu uliyojaaliwa." Alisema mama Pamela.

"Kiukweli mama Mimi napenda sana unitafutie shule.. Ili niweze kusoma na kufikia malengo yangu" alisema Doreen.
"Shule tu? Wala usijali wiki ijayo nitakuwa tayari nimetafuta shule kwa ajili yako.."

"Nitafurahi sana mama..."
"Unapenda shule ya kutwa au bweni?"
"Yoyote tu itanifaa" alisema Doreen.
Suala lile lilimfurahisha sana Doreen, aliendelea kuishi kwa kunyenyekea sana ndani ya nyumba ile, lakini katika ulimwengu mwingine alikuwa ni mtu jeuri na katili kwa familia ile. Kila Mara aliliwinda sana titi la Pamela, alitamani kulipata kwa udi na uvumba lakini kwa bahati mbaya ilikuwa vigumu kulipata. Alitumia kila namna lakini bado hakuelewa sababu ya kushindwa kulipata titi la Pamela.

Hasira zilimuwaka sana Doreen pale alipoingia chumbani kwa Pamela usiku na kutaka kumkata titi lake. Alikuta Pamela amelala usingizi mzito sana, akampulizia dawa ili usingizi ule uzidi kuwa mzito zaidi kisha akamsogelea taratibu akiwa ameshikilia panga Kali lililofungwa kaniki nyeusi na nyekundu.

Doreen alitamka maneno ambayo aliyajua mwenyewe kisha akamfunua shuka Pamela na kusogeza kisu chake karibu na titi la Pamela. Hakuwa na hofu kama kazi yake haitofanikiwa kwani alikuwa anajiamini na alikiamini kile alichokifanya. Lakini kwa bahati mbaya sana kila alipotaka kumgusa Pamela na upanga ule, Doreen hakuona chochote kitandani pale. Alijaribu tena na tena lakini bado hali ikaendelea kuwa vile vile. Doreen alikasirika sana, akatupa chini upanga ule mlio wake ukamshtua Pamela usingizini.

Doreen alishtuka sana baada ya Pamela kushtuka usingizini, akakimbia haraka na kujibanza kwenye kona moja ya chumba kile kisha akatamka maneno Fulani ya kichawi halafu akatulia kimya.

Pamela aliangaza macho huku na kule chumbani mle lakini hakuona kitu, akainuka kitandani na kuwasha taa kisha akaangalia kila sehemu ya chumba kile lakini hakuona chochote. Akatoka na kwenda msalani, alipokuwa anajisaidia haja ndogo akahisi kuna mtu anamfuata nyuma yake Pamela alishtuka na kuogopa sana kisha akakumbuka jambo muhimu la kufanya kama alivyoambiwa na baba yake. Pamela akasali kwa sauti ya chini na kwa imani kubwa sana kisha akajisaidia na kurudi kitandani, akalala bila kuzima taa.
Doreen alikasirika sana baada ya kumkosa Pamela kwa Mara nyingine. Akaamua kurudi chumbani kwake kupitia kona ile ile aliyokuwa amejibanza.

Doreen alitokea chumbani kwake akiwa na hasira sana. Alijituliza kimya akiwa amekaa chini sakafuni huku akiwa ameshika tunguli na hirizi mkononi mwake. Aliamua kuita mizimu ya kwao ili iweze kumsaidia katika hali ngumu aliyonayo.

Ndani ya sekunde chache alitokea mwanamke mmoja Mzee sana. Kichwa chake kilikuwa kimejaa mvi lakini hakuvaa nguo yoyote isipokuwa kaniki nyeusi aliyovaa kiunoni pamoja na shanga nyingi sana alizokuwa amevaa kiunoni mwake na shingoni. USO wake ulikuwa na makunyanzi mengi sana yaliyokuwa yametawaliwa na vitu kama unga unga mweupe. Alipotua tu chumbani kwa Doreen, nyumba nzima ilitikisika kwani alikuwa ni mtu mkubwa sana katika himaya ya uchawi ya akina Doreen.

"Karibu! Karibu! Mama mtukufu! Mkuu wa wachawi wote! Mwenye nguvu kuliko wote duniani!" Doreen alimkaribisha mgeni wake yule kwa heshima kubwa sana. Yule bibi hakutoa sauti yoyote zaidi ya Kuitikia kwa kichwa tu huku akimsogelea Doreen kwa kutumia makalio yake.

"Doreen! Tangu tumekutuma huku duniani hujawahi kuniita isipokuwa Leo.. Najua una jambo zito linalokusumbua"
"Ndio! Ndio! Mtukufu"
"Sasa inabidi tutoke humu maana si mahali sahihi"
"Sina pingamizi Bi Tatile! Kipenzi cha wachawi wote" yule Bibi alimshika mkono Doreen kisha taratibu kwa kutumia makalio yao wakasogelea kona ya kushoto kwao. Kisha wakatoweka ndani ya jumba lile. Lakini kitandani kwa Doreen waliacha mwili wa Doreen pekee na hata kama angeamshwa kwa kipindi kile basi asingeweza kuamka .

Safari ya wawili wale kwa kutumia usafiri wa ungo huku dereva akiwa Bi Tatile iliwafikisha mpaka eneo la makaburini ambapo walitua na wakaketi hapo kisha wakaendelea na kikao chao kifupi kilichotokea kwa dharula.

"Sema mjukuu wangu.. Mimi ndo Tatile binti Matatila mwenye uwezo wa kubadili nyasi za kijani zikawa nyeupe.."
"Mtukufu lile suala la kupata titi naona linakuwa gumu sana kwangu.. Nimekamilisha kila kitu lakini bado hilo tu.. Tafadhali naomba unisaidie kwa hili..."

"Ha ha ha hah Doreen wewe una uwezo mkubwa sana wa kukamilisha hilo.. Unaweza ukafanya hivyo haraka sana ila kuna jambo moja tu! Unatakiwa ufanye."
"Jambo gani mtukufu? Niambie tu maana nimechoka kuhangaika" alisema Doreen.

****

Majira ya saa kumi na moja jioni Dada wa Mama Eddy aliwasili nyumbani kwa Mr Aloyce. Alipokelewa vizuri sana na Bwana Aloyce pamoja na Eddy lakini ilikuwa tofauti sana kwa mama Eddy kwani alimkaribisha Dada yake kama vile alimkaribisha adui yake ndani ya nyumba. Suala hilo liliibua maswali mengi sana kwa Mr Aloyce pamoja na mgeni wao.

"Mama Eddy.. Nakuomba chumbani Mara moja..." Alisema Baba Eddy kisha akaingia chumbani. Mama Eddy alimfuata mumewe ili amsikilize kile anachotaka kumweleza.
"Mke wangu... Mbona unaniabisha kwa shemeji yangu?"
"Kivipi?"
"Dada yako amekuja lakini unamsalimia kama hutaki vile.. kwanini?" Aliuliza baba Eddy kwa mshangao.

"Nimejisikia tu.."
"Hapana mke wangu usiwe hivyo... Nakuomba basi onesha kumjali mgeni tena nduguyo wa damu.."
"Siwezi kumjali mchawi mkubwa yule..." Alisema mama Eddy akiwa anajishumburua midomo yake kwa dharau.
"Unasemaje? Dada yako mchawi kivipi?"
"Amemroga mwanangu..."

"Umejuaje au nawewe mchawi? Maana haiwezekani umtuhumu mwenzio mchawi wakati huna uhakika?" Alisema Baba Eddy kwa hamaki. Hakutaka kuamini kile alichokisa mkewe.
"Leo hii unaniambia mimi mchawi? OK sawa... " alisema Mama Eddy na kwenda sebuleni kwa hasira.

Alisimama wima akiwa ameshika mkono kiunoni huku akimtazama dada yake kwa dharau.
Dada yake alipigwa na butwaa sana, alibaki anamshangaa mdogo wake kwa vitendo vya dharau anavyomfanyia.
"Wewe!" Alisema Mama Eddy.
"Naomba utoke kwenye nyumba yangu.. Ulichomfanyia Eddy kinatosha..."
"Mimi?"

"Kumbe naongea na nani kama sio wewe mpumbavu..." Alisema Mama Eddy akidhihirisha chuki kubwa aliyonayo moyoni mwake. Eddy alimtazama mama yake kwa mshangao sana akiwa haelewi sababu ya mama yake kumfanyia unyama ule dada yake wa damu. Hakuna aliyefahamu ukweli kuwa yule hakuwa mama Eddy halisi.

"Mama... Mama mkubwa amekosa nini?"
"Hebu kelele huko na wewe.. Hujui kama huyu ndo aliyekuroga?"
"Sio huyu mama..." Eddy alimtetea.
"Hebu ondoka hapa.. Kwanza hayakuhusu.." Alifoka Mama Eddy.
"Sasa na mimi naondoka na mamkubwa.. Sibaki hapa?" Alisema Eddy.
Wakati huo Mr Aloyce alifika sebuleni pale na kuanza kumuomba msamaha mgeni yule asiye na hatia....

ITAENDELEA.....
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom