AZIMIO NAMBA 13:
"Serikali izihusishe Kamati za Kudumu za Bunge kwenye hatua za awali za maandalizi ya Mikataba mikubwa ya kibiashara na ya muda mrefu ili kuondokana na utaratibu uliopitwa na wakati kwamba Mikataba ya Kibiashara ni siri, hata kwa walipa kodi wenyewe. Aidha, Serikali ihakikishe kuwa, Kamati zote za Bunge zinapitia Mikataba mikubwa ya kibiashara na ya muda mrefu chini ya Sekta zao ili kuliondolea Taifa mizigo isiyo ya lazima."
HATUA ZILIZOCHUKULIWA:
Tarehe 24 Aprili 2008, Ofisi ya Waziri Mkuu ilimwandikia barua Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumfahamisha kuhusu utekelezaji wa awali wa baadhi ya Maazimio ya Kamati Teule yaliyopitishwa na Bunge. Katika barua hiyo, utekelezaji wa Maazimio Namba 13, 15, 16, 21 na 23 yalitolewa taarifa. Hata hivyo, kwa madhumuni ya Taarifa hii, ninapenda kurejea kwa muhtasari maelezo kuhusu utekelezaji wa Maazimio hayo.
Kuhusu Azimio Na. 13, Serikali imechambua Azimio hili kwa kina na imekubali kimsingi kwamba, Mikataba yote muhimu ya Serikali itakuwa inawekwa kwenye Maktaba Maalum ya Bunge ili Kamati za Bunge lako Tukufu ziweze kupata nafasi ya kupitia Mikataba mikubwa ya Kibiashara na ya muda mrefu chini ya Sekta zao na kushauri ipasavyo.
Kuhusu kuzihusisha Kamati za Kudumu za Bunge kwenye hatua za awali za maandalizi ya Mikataba mikubwa ya Kibiashara na ya muda mrefu, Serikali imeanza kufanya tafiti katika Mabunge ya Nchi za Jumuiya ya Madola ili kupata uzoefu zaidi utakaosaidia katika utekelezaji wa suala hili.