Sarkozy na Ndege Ya Bei Mbaya Kwa Mkewe.

Junius

JF-Expert Member
Mar 11, 2009
3,181
139
* Inaitwa ‘Carla One’ ni kama ile ya Air Force One, imenunuliwa kwa zaidi ya sh. bilioni 105

Na Noor Shija

KILA mtu ana namna ya kumfurahisha mpenzi au mke wake. Hivyo ndivyo ilivyo pia kwa Rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa ambaye ameamua kumfurahisha mkewe kwa kununua ndege ya Rais yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 105, na kuipa jina la mkewe Carla kwa kuiita ‘Carla One’.

Ndege hiyo ya kifahari na yenye madoido mengi ni aina ya Dassault Falcon 7X ikiwa ni kubwa kuliko ya kiongozi yeyote wa nchi za Ulaya.

Mwaka jana Rais Sarkozy alipuuza mporomoko wa kiuchumi duniani na kuagiza katika serikali yake, zitumike pauni milioni 240 za Uingereza (zaidi ya sh. bilioni 507) kwa ajili ya kununulia ndege tatu za safari za Rais.

Ndege hizo tatu moja ni aina ya Airbus A330-200 kwa ajili ya safari ndefu, na mbili kwa ajili ya safari fupi.

Rais Sarkozy anakuwa kiongozi wa kwanza katika nchi za Ulaya kuwa na ndege kubwa na ya kifahari. Ndege hiyo ni ya pili baada ya ile ya Rais Barack Obama wa Marekani, aina ya Boeing 747-200 inayoitwa Air Force One.

Carla Bruni ni mke wa wa tatu wa Rais Sarkozy, ambapo mke wa kwanza wa kiongozi huyo ni Marie-Dominique Culioli aliyeolewa Septemba 23, 1982 na kuachika akiwa na umri wa miaka 53. Baadaye akaolewa Cecilia Cigner-Albenis aliyekuwa rafiki wa karibu wa mke wa kwanza Marie.

Rais Sarkozy mwaka 2007 aliamua kumuacha Cecilia ambaye kwa kipindi hicho alikuwa na umri wa miaka 50, na mwaka jana alimuoa mwanamitindo Carla ambaye kipindi hicho alikuwa na umri wa miaka 40. Kiongozi huyo ana umri wa miaka 54.

Wakati wa harusi yao mwaka jana, Rais huyo aliweka wazi kuwa mkewe mpya na mwanamitindo maarufu atampa ndege nzuri ya kifahari itakayomsafirisha sehemu mbalimbali duniani.

Ndege hiyo ambayo bado haijaanza kutumika ina viti vya ngozi na sehemu ya kufanyia kuchulia mwili. Mtaalamu wa masuala ya anga wa Ufaransa, Jean Guisnel, alisema kuwa ndege hiyo ina vifaa muhimu kwa ajili ya ofisi ya Rais.

Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, ndege hiyo pia ina ofisi ya katibu muhtasi wa Rais, chumba cha mikutano kwa ajili ya watu 12, viti vya abiria 60, chumba cha kulala cha Rais na bafu maalumu kwa ajili ya kiongozi huyo.

Vituko vya kuonyeshana ufahari pia viliwahi kutokea wakati wa chakula cha usiku kilichoandaliwa na Carla Bruni, wakati rafiki wa karibu wa Rais Sarkozy, Jacques Seguela kwa kueleza kuwa mtu yeyote aliyeshindwa kumiliki saa aina ya Rolex hadi alipofika umri wa miaka 50, aandike ‘maumivu’ katika maisha yake.

Seguela alitoa matamshi hayo huku akieleza kuwa, kila mtu akiwemo Rais Sarkozy na mkewe Carla katika chakula hicho cha usiku walikuwa wamevaa saa aina ya Rolex ambayo gharama yake ni kubwa.

SOURCE:MZALENDO.
 
Back
Top Bottom