Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Shadrack Masija, amewataka wananchi wote wenye sifa za kupiga kura kujitokeza kwa wingi kushiriki Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, 2025 kwa amani utulivu na bila hofu yoyote.
Kamanda Masija amesema hayo Oktoba 27,kushiriki 2025 uchaguzi ni haki ya msingi ya kila Mtanzania, hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuitumia fursa hiyo kikamilifu kwa lengo la kuchagua viongozi watakaoliletea taifa maendeleo.
Soma: SACP Safia Jongo: Vyombo vya dola vimejipanga kuhakikisha usalama wa wapiga kura Oktoba 29
Aidha aliwaambia waendesha bodaboda na bajaji katika soko la Sabasaba, Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, kutokubali kutishwa au kurubuniwa na kauli za uchochezi kutoka kwa watu wasiolitakia mema taifa.
Alisema kuwa Jeshi la Polisi limejipanga kikamilifu kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa usalama wa hali ya juu na kila mwananchi anashiriki bila bughudha.
Aidha, Kamanda Masija alisisitiza kuwa taarifa zinazosambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii zinazodai kutakuwepo vurugu au uvunjifu wa amani katika maeneo ya kupigia kura hazina ukweli wowote wananchi wanapaswa kupuuza taarifa hizo na kuendelea kuamini vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo vimejipanga kulinda maisha na mali zao wakati wote wa mchakato wa uchaguzi.
Kwa kuhitimisha, alitoa onyo kali kwa watu au makundi yenye nia ya kuchochea vurugu au kuvuruga amani wakati wa uchaguzi, akisema Jeshi la Polisi halitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yao. Alitoa rai kwa wananchi kuendeleza mshikamano, kudumisha umoja wa kitaifa na kushiriki uchaguzi kwa amani ili kuiweka Tanzania katika ramani ya dunia kama nchi ya mfano wa demokrasia na amani barani Afrika.