Riwaya : Kiroba Cheusi

Riwaya : Kiroba Cheusi

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,637
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA KWANZA
1
PALISHAKUCHA.
Pakuche mara ngapi?
Ni vile tu huyu Morena alilala chakari. Asubuhi hii ya saa nne, kwake ilikuwa ingali liamba. Alilala kifudifudi. Fofofo..
Ghafla, kuna mtu alimtoa katika ule ufofofo. Akamkera. Alimkera hasa!
Kivivu, aliinua shingo yake, akakigeuzia kichwa chake upande mwingine. Akasonya
Angali na mawenge ya usingizi. Si hayo tu, bali pia uvivu ulimjaa. Vikampa hali ya kutaka kuendelea kubadili uchago kila dakika, licha ya jua la asubuhi kuhanikiza nuru ya kutosha mle chumbani mwake.
Akilini, aliutaka utulivu kwa gharama yoyote ile. Japo apate kukimalizia hicho kipande cha usingizi. Wala hakujua kingekwisha saa ngapi. Alitaka kulala. Kulala tu mpaka pale mwili wake utakapomruhusu kutalikiana na kitanda.
Aliyemkera, akamkera tena.
“Eeh mchicha matembele majani ya kundeee… eeh mchicha tembeleee… eeh mchicha tembele majani ya mabogaaa”
Huyu muuza mboga ndiye aliyemgutua toka usingizini, kwani alikuwa akichuuza biashara yake ya mboga za majani karibu na dirisha la Morena. Dirisha lililokuwa upande wenye kichochoro kilichopakanisha chumba alichokuwemo na nyumba ya jirani.
Mchuuza mboga alisimama hapo kichochoroni pamoja na wateja wake waliokuwa wakichagua mboga toka kwenye tenga. Wakafanyiana mizaha ya hapa na pale iliyosindikizwa kwa vicheko vya juu na chini.
Kelele zao zikamfanya Morena ajihisi kama mtu anayepigiwa zumari sikioni. Akasonya tena. Msonyo mrefu uliobeba uzito wa makumi ya maneno. Maneno aliyotamani yawasilishe hisia zake kwa sauti ya kuhutubia umati. Alichefukwa.
Naam! Ikawa kama vile huo msonyo wake ulimuhimiza mchuuza mboga akolezee tena kibwagizo chake maradufu. Akamvumilia kidogo huku akiinua tena shingo yake na kuzisikiliza sauti za wateja wake. Akaitambua moja, ya mtoto wa mpangaji mwenzake.
“Somoe! We Somoe!” akaita kwa sauti ya kukaripia na Somoe mwenyewe akaginiza kwa sauti ya juu.
“Abeee!”
“Embu niondoshee huo mnada wenu hapo dirishani”
Morena akatoa amri yake kwa sauti ya chini kidogo huku akiyabana mate yaliyomjia ghafla kinywani. Hakuona pa kutemea. Akakunja ndita kadhaa usoni. Kwanza alikereka kwa kule kugutuliwa usingizini; pili, ile adha ya kujaa mate ilimkalfisha nafsi. Na mwisho, ombi lake kwa Somoe lilipita kimya kimya kama kivuli.
Muuza mboga naye kama mtu aliyefinywa alianza tena kuchuuza biashara yake kwa sauti. Safari hii Morena hakusubiri mbivu ziwe mbovu. Alitoka kitandani. Akasimama na kuikaza khanga yake kifuani. Ngoja nikamshikishe adabu! Akajiapiza.
Alipita katikati ya chumba chake, akivipamia vitu vilivyotupwa sakafuni shaghalabaghala; hapa nguo, pale viatu na makorokoro yake mengine chungu nzima.
Alihangaika na kitasa kwa takribani robo dakika wakati akiufungua mlango ambao ni dhahiri ulikuwa mbovu. Pale nje ya mlango wa chumba chake aliitafuta ndala yake moja na asiione, akaivaa hiyo moja iliyokuwepo na kuanza safari ya kuelekea nje.
Alimpungia mkono mpangaji mwenzake aliyepishana naye, akishindwa hata kuijibu sawasawa salamu aliyopewa, kwa kule kuyakonga mate kinywani. Aliukusanya mdomo wake akautanguliza mbele mithili ya mdomo wa bata.
Akatoka nje na kuyatema upenuni mwa nyumba. Akayafukia kwa mguu uliokuwa peku.
Haikuleta maana; kuivaa ile ndala moja na kisha kwenda kuyafukia mate kwa mguu uliopeku. Ila ndiyo falsafa ya maisha, kupata na kukosa; wanaokosa ndio wenye kutumika na kusulubika.
Twaibu! Morena aliiongoza miguu yake kuelekea ule upande wenye uchochoro. Alimfungia kibwebwe muuza mboga kana kwamba alitaka tena kwenda kulala akishamfukuzia mbali.
Alipoifikia ile kona inayoelekea uchochoroni, akausikia mlio wa bodaboda, mlio uliomgeuza shingo. Aliyemuona akamfanya ayasahau yote yaliyomtoa nje. Akakigeuza kiwiliwili kizima kumtazama mgeni aliyewasili.
Alikuwa rafikiye, Fatumata Mzinga. Somo yake wa kufa na kuzikana.
Alitulia akimtazama namna anavyoshuka toka kwenye bodaboda, mwili wake tipwatipwa uliogawanyika kike kisawasawa ukitibwirika. Na mshukaji nwenyewe akaongeza sifa za mkwezi kuudandia mnazi. Aliujaza madoido ule mtibwiriko!
Wanaume waliokuwa upande wa pili wa barabara palipo na karakana ya fenicha wakameza mate ya tamaa, wengine walijikohoza na wengine walikaribia kuviranda vidole. Umbile lake lilileta hali ya kubahashika pasi hiyari.
Wakaingia ndani, Morena akitangulia na Fatumata akimfuatia. Mle ndani Fatumata akayaanzisha maongezi mara tu baada ya kuufunga mlango na kwenda kuketi kitandani.
“Nilijua nikifika kwa Mzee Hizza n’takuta wanatembeza daftari la rambirambi” akazungumza akimtaja baba mwenye nyumba aliyopanga Morena.
“Aaah! kwa lipi?” Morena akauliza huku akiumba uso wa mshangao.
“Yale mapombe makali makali uliyogida jana. Mwanamke unakunywa kiama” Akampigia saluti. “Nikajua utaunguza hadi utumbo maana ile mijibaba jana ilikuvulia kofia ujue! Chupa ya tisa jicho kodo!... kope zimekusimama kama miiba ya nungunungu” Fatumata aliongea akitoa macho na kuchezesha mikono kuyasindikiza maneno yake.
Morena akacheka. Alicheka vile mwenzake alivyomsifu na kumsagua kwa pamoja.
“Tena mbona ungenikuta nimelala kama si muuza mboga mmoja mpuuzi alonikatishia usingizi wangu” Morena akalalamika akiutafuta mswaki wake kwenye stuli pana iliyokuwa na vitu vya kila aina; vipodozi, misumari, kalamu mbovu, dawa zilizokwisha muda wake mpaka karatasi za vocha zilizotumika. Stuli ilijaa hobelahobela!
Akaupata mswaki.
Pasipo dawa aliuchomeka mdomoni na kutoka nje. Alimuacha Fatumata anapitisha macho kwenye kipande cha gazeti kilichotumika kufungia dagaa mchele waliokwishaliwa tangu juzi.
Dakika moja Morena alirejea ndani, akautupia mswaki wake juu ya ile stuli.
“Kwanza nambie jana uliondoka na nani kwani… hukuokota garasa kweli?” Fatumata akamdodosa Morena aliyekuwa anaukagua uso wake kwenye kipande cha kioo.
Kioo kilichokuwa kimetundikwa kwenye msumari ukutani. Aliutazama uso wake, akazitazama nywele zake ndefu zilizopakwa rangi mbili tatu tofauti kiasi cha kufanana na mtu aliyejitwika jogoo kichwani.
Morena akacheka kwanza, kama ilivyo haiba yake. Alicheka akigeuka na kumtazama Fatumata kwa bashasha.
“Mimi huyu, niliyenyonyeshwa mataputapu. Nikalewe zile bia zenu za mafungu” akasonya. “Bia ya tisa nikikurembulia jua nimekuhurumia saaana”
“Kijukuu cha mwana harashi wewe!” Fatumata akashadidia akifinyanga kile kipande cha gazeti na kumtupia Morena, huku akitoka kitandani na kuketi sakafuni. Akatandaza miguu yake huu mashariki ule magharibi.
“Hizi kazi zetu ukijifanya unajua kulewa utakopesha kiuno hicho kila siku” akamjibu na kuendelea “Nimeingia kulala humu saa moja asubuhi” Morena akaachana na kioo na kukifuata kitanda.
“Eh! Nipe… nipe… michapo” Fatumata akasherehesha akipunga mikono hewani.
“Kitu Bokilo” Morena akatamka kwa mbwembwe akinyanyuka na kuketi sawa pale kitandani huku akilitaja jina la mwanaume aliyeondoka naye usiku uliopita.
“Yule Bokilo Mzaire?” Fatumata akauliza kishabiki, akitenga mikono kiunoni.
“Mzaire dada, mutu ya vitenge na bazee” Morena akafanya mbwembwe zake tena akipaza sauti.
“Pedeshee la Bukavu, Kinshasa na kati ya Lubumbashi, mutu ya suruali pande sita” Fatumata akaumalizia utambulisho.
“Kwani zile ni suruali? Kwa upana ule tuyaite mashuka tu dada”
Kikafuata kicheko kirefu cha kugongesha mikono, kisha wakarejea kwenye mjadala wao.
“Alikupeleka wapi? Maana wangu yule majinuni na akili zake za kuhesabu alijua kuninywesha tu. Tumefika kule Bondeni loji kwenye mbuyu akalala puh!”
“Ndani puh!” ikawa zamu ya Morena kushangaa.
“Puh! Nilitamani kumchumia mikwaju nimtandike fimbo za kitambi anijue mie nani” Fatumata hakusemea utani, alimaanisha kiasi cha kumchekesha mwenzake.
“Pole mwaya, mie kwanza alinipeleka gesti moja nzuri balaa maeneo ya Kigogo. Akanianzia na ahadi za mtaji wa biashara, nikaongeza bakora… chapa! chapa!” akakung’uta vidole. “Akaniahidi nyumba nzima. Dada upo?” Morena akalivuta neno la mwisho kwa mikogo mingi, Fatumata akiwa bado amemtumbulia macho.
“Nyumba nzima! Bokilo Mzaire huyo? Ulimvalia na njinjili?” Fatumata akauliza kwa midadi akijishikashika kiuno kumaanisha shanga zivaliwazo na wanawake kiunoni.
“Mie tena, nilimfungia hizi” akafunga dole gumba na kuviacha vinne hewani. “Sio watoto wa siku hizi wanaovamia fani na zigo la shanga ka’ fundo la msuli” Morena akamfanya Fatumata acheke mpaka machozi.
“Asubuhi kaacha elfu 50 kasema baadaye atan’tumia bajaji tukale kuku sekela mahali”
“Usinambie!” Fatumata akamaka. “Ngekewa hiyo dada. Mungu akitaka kukupa-” Fatumata akatamka akikomea njiani kwanza kisha kwa pamoja wakamalizia.
“Hakuandikii barua” wakamalizia kwa sauti za kuimbia irabu.
Wakacheka cheko lingine refu kisha wakatulia, wakiyaanza maongezi mengine.
Ilikuwa kawaida yao, kukutana namna hii na kuzungumzia maisha yao ya ukahaba almaarufu kama uchangudoa. Wangetambiana juu ya wanaume waliowaopoa, pesa walizopata na pengine hata ahadi hewa za hiki ama kile. Lakini pia, mara nyingine ingekuwa huzuni tupu, wangekutana kufutana machozi, kupeana pole na kusaidiana kwa suluba na madhila waliyokumbana nayo.
“Embu kaoge tutoke kwanza, twende mahali nikakupe akili za maisha leo” Fatumata sasa akaweka umakini kwenye mazungumzo yao.
“Kuna nini tena?”
“Kaoge tutoke mwe! hii mijumba yenu isiyo na silingibodi mtu akijamba hapa panya wa chumba cha tatu kule anasikia” Fatumata aliposema hivi Morena alicheka, na wapangaji waliokuwa nje nao wakasikika wakicheka. Dongo lile kuhusu nyumba walilisikia kama walivyoyasikia maongezi mengine yote.
“Kwako kuna nini?”Morena akasaili akinyanyuka toka kitandani.
“Hivi sijakwambia, baada ya ile harusi ya binamu, nyumba imejaa watu kama soko”
“Usinambie!” Morena akamtolea macho.
“Mwenzangu, ukipita nje utasema kuna meza ya muuza mitumba ndani… embu kaoge tutoke bwana” Fatumata akalijibu swali na kumuhimiza tena Morena ajihimu.
Alipotoka kuoga Morena alirejea chumbani kwake. Pasi kujali uwepo wa rafiki yake, akaitupilia mbali ile khanga moja iliyokuwa imesitiri maungo yake na kuanza kuranda mle chumbani akijipaka mafuta, akitafuta nguo ili mradi alikuwa na hekaheka za hapa na pale.
Morena alikuwa mrefu wa kadiri, ungemtazama kwa haraka haraka ungedhani ni mwanamke wa kisomali. Vile alivyojaaliwa nywele ndefu laini na wajihi mwembamba kiasi wenye pua iliyonyooka. Watu wengi walihisi Morena alikuwa na usomali ndani yake.
“Haya shanga ushatupa kule, kwanza huo mkufu kiunoni hauchuji?” Fatumata alimtupia swali mwenzake akimtazama vile alivyokuwa akimkatishia mtupu kama mwanga, huku akiuvaa huo mkufu wake.
“Dhahabu yenye gramu zake hii sio cheni zenu za vyuma chakavu ukinunua leo mtondogoo kutu imekutoa mapunye” Morena akajibu akianza kuvaa nguo zake.
“Hivi ulidunduliza miezi mingapi? halafu umenikumbusha Bintuni na cheni lake la kuhongwa”
“Yule nusura tumpeleke India kwa matibabu, sijui aliuokota wapi mcheni mzito kama mnyonyoro wa geti” Alidakia Morena na kuzua kicheko kingine mpaka kwa wapangaji waliokuwa koridoni wakidoea mazungumzo yao.
Morena alipomaliza kuvaa na kujipara, akajipulizia manukato yake. Manukato ghali kidogo kulinganisha na kipato chake cha kuungaunga.
Pamoja na uduni wa maisha yake na uzito wa majukumu aliyokuwa nayo, Morena hakuacha kujitafutia vitu alivyovipenda kwa dhati. Hata kwa kudunduliza senti moja kila siku, angeweka bila kusita wala kuchoka, aliamini haba na haba hujaza kibaba. Morena alipenda vidani vya dhahabu, na aliyapenda manukato.
Akamgeukia Fatumata.
“Haya twen’zetu sasa” akatamka huku akiufuata mkoba wake na kuweka sawa baadhi ya vitu vyake.
Wakatoka pamoja mpaka nje ambako walianza kutembea pole pole huku wakishauriana pa kwenda. Papo hapo, Fatumata akichombezea hizo akili za maisha alizotaka kumgawia mwenzake. Aliuremba mpango wake kiasi cha kumtia kiwewe mwenzake.
“Hili dili lililonifungisha safari likitiki… tutaununua huu mtaa mzima somo!” Fatumata akamfanya Morena adondoshe mguno.
“Ngoja tufike basi Kha!” akamtoa papara huku akijiandaa kuvuka barabara kuelekea mahali ziliposimama bodaboda.
Taratibu wakakaza mwendo kuwahi kupeana hizo akili za maisha. Wasijue tu namna ambavyo akili hizo zingekuja kuigharimu furaha yao maishani.
2
JUA la saba mchana liliwaka hasa!
Liliwakutia mgahawa maarufu wa Vitukoutata, maeneo ya Vingunguti. Kila mmoja alikwishaagiza chakula chake. Wakakishambulia chakula hicho haraka haraka, kana kwamba walikuwa wamekikamia.
Morena alikuwa wa kwanza kumaliza kula. Akamwita mhudumu amletee maji ya kunawa. Maana, mchuzi wa kongoro ulikwishamganda mikononi. Ikawa kero kwake. Wakati mhudumu anafika na beseni lake mkononi, Fatumata naye akawa amemaliza chakula chake. Akajiunga kwenye kunawa.
“Shing’ ngapi?” Fatumata aliuliza huku akikimbilia kutoa kijiti cha meno kwenye kichupa chake mara tu baada ya kumaliza kunawa.
Morena yeye alihangaika kuyachokonoa magego yake kwa ulimi.
“Vishalipiwa mbona!” Yule mhudumu alijibu akitabasamu, akiufurahia pia mshangao wa wanawake wawili mbele yake.
Wakatazamana kwa bashasha. Wakaendelea na mambo yao pasipo hata kusaili ni nani aliyewalipia. Nyakati zingine ofa kama hizi zilikuwa za kawaida kwao, hasa akiwepo Fatumata Mzinga. Wangelipiwa chakula, nauli na huenda wangepata ahadi za kupelekwa huku na kule kisha kuzungumza biashara.
Wateja wao walikuja kwa njia mbalimbali.
“Tawire! Haya leta habari habibti” Morena alijiweka sawa tayari kumsikiliza rafiki yake.
“Unamkumbuka yule bwana alonileteaga dili ya mawese?” Fatumata akaianzia mbali habari yake. Akakitupa kando kijiti cha meno.
“Bwana we hayo ya nani anafanya nini utanichanganya tu, hao mabwana zako wauza mawese nawajua kumi na…” Morena akajibu, akimfanya Fatumata amtukanie ukoo wake, akaliunga na tusi lingine la nguoni na Morena asijali.
“Kimboka” Fatumata alipolitaja jina Morena akadakia.
“Yule mpuuzi. Haya kafanyaje?” akauliza kwa sauti ya mkwara.
“Hujasamehe tu!”
“Muuza mawese yule aliyetaka kutulaza ndani kwa bia zake za mafungu.” Akasonya.
Uso wa Morena haukuwa na masihara hata kidogo. Alimpindishia mwenzake midomo.
“Tukio la mwaka juzi bado linakupandisha mavi ya kifua tu! Punguzaga vinyongo unenepe shaa!… embu sikia, Kimboka ana dili la mamilioni somo!”
Akayatumbua macho kimbeya.
Aliianza tena habari yake kwa madaha. Akimfanya Morena aukunje uso na kumeza mate mithili ya mtu aliyelambishwa kitu kichachu.
“La kuuza mawese yake?” Akauliza kwa dharau akibetua midomo.
“Sio mawese jamani!”
“Kumbe!?”
“Madini!” Alilitamka neno madini kwa sauti ya chini akikisogeza kichwa chake mbele zaidi ili Morena amsikie vizuri pamoja na kule kunong’ona.
Morena alitoa macho kana kwamba alichotamka Fatumata kilikuwa kitu cha kutisha mno. Akauliza kwa sauti ya mshangao. “Madini?”
“Mdomo huo mwanamke, shiii!” Fatumata akamuwahi, akimtaka apunguze sauti.
Morena akafunga mdomo wake wa kiganja chake cha kuume huku bado jicho likiwa limemtoka pima. Taratibu akamtazama mwenzake kama zumbukuku.
“Jela unaijua lakini Fatumata?”
“Jela ya nini?”
“Jela hizi za Segerea, Ukonga sijui Butimba?”
“Mie nilimsikia anaongelea biashara ya madini, sasa jela inahusikaje?”
“Mmh! Madini mwenzake utapeli Fatu, lakini haya! Kila la kheri kwenye huo mpango wako. Mie n’taendelea kuibia wanaume kwa mtaji huu chini mpaka siku yangu ikifika.” Alizungumza akiutazama huo mtaji wake.
“We huzitaki pesa?”
“Nazitaka ndio, ila hizo mishe mishe za lala apache alolo amka Bakhresa, Bongo hii, haya!”
“Mbona unan’tisha na sijamaliza, unajua nimekuita sababu kuna lingine na ndio hilo linaloniumiza kichwa?” Fatumata alimtazama mwenzake kwa uso mkavu usio hata na chembe ya utani.
Morena naye akamtazama kwa umakini kidogo, moyo ukimtokota. Alishaingia woga ghafla. Akauliza mboni za macho zikicheza kulia na kushoto kwa kasi ya ajabu. “Kitu gani?”
“Kuna kiroba cheusi hicho tukishikamana tunatoka huku uswazi”
“Eeeh!”
“Punguza mchecheto basi!”
“Haya niambie kuna nini kwenye hicho kiroba?” Morena akajiweka sawa, akitazama huku na kule kana kwamba alihofia watu wangewasikia wakiongelea mambo ya viroba.
“Ndio maana n’kakutoa kule kwenu.” Fatumata alimzodoa mwenzake, akiucheka ule mchecheto wa Morena. Huku akitaka kuziweka sawa akili za mwenzake, Fatumata aliendelea. “Sikia, wiki iliyopita, siku ile tuliyokesha Kiwalani sijui unaikumbua…”
“Tunakesha mara ngapi uko Kiwalani? We n’ambie moja mbili tatu basi!” Morena aliona anachelewa kuijua habari yenyewe.
“Haya twende, nililala kwa Kimboka pale, unajua tena kusikia mamilioni kidogo niingie wehu, sasa vile jasiri haachi asili….” Fatumata hakumalizia, Morena akamdaka.
“Ukaiba?”
“Hebu bwana we kha!” Fatumata alianza kukerwa na kule kukatishwa katishwa kila mara.
“Sikuiba, nilikuwa nafanya doria, nikatokezea stoo moja uchwara umo ndani. Na hapo ndio paliponifanya nikuite hapa n’kupe akili za maisha.” Alijieleza huku mwenzake akiitikia tu chapuchapu. Kichwa kikienda juu chini juu chini mara kadhaa.
“Nilikuta viroba hivi…” Alivikutanisha vidole vyake vya mikono yote kwa pamoja akimaanisha kumi.
“Enhee!” Morena akaendelea kuitikia.
“Nikafungua kimoja kidogo dogo. Nilichokiona sasa aaah!” Fatumata akanesa nesa akifuatisha maneno aliyoyatamka kwa kupanda na kushuka.
Morena hakumdaka, alimfuata kwa macho alivyonesa kulia na kushoto akingoja kuisikia habari kamili.
“Almasi!” Fatumata alimalizia mithili ya mtu aliyeubwaga mzigo mzito kupitiliza.
“Almasi!? Unazijua almasi wewe au unazisikia tu? Ukute uliona vipande vya chupa ukajua almasi.” Morena hakumwamini kabisa.
“Nimekuja mjini na lori za mpunga huku waitukei inatikisa dunia naanzaje kutoijua almasi? Mungu na Mtume vile ni almasi pyuwa!” Fatumata alisisitiza, akipitisha kidole cha shahada shingoni na kukinyooshea juu kuapia.
“Sasa?” Morena akaomba dira ya mwito.
“Nataka n’kitaifishe kimoja, tunakimbilia zetu Zambia au Msumbiji hapo, tunakula maisha huku tunasikilizia kwanza, kisha tunarejea kulijenga taifa. Naamini hata hela ya kumlipa tutakuwa tumepata.”
Morena alimtazama mwenzake kama vile alikuwa anaisoma hiyo ramani ya kufika Zambia usoni pa somoye. Kisha, akaguna akipiga kofi moja hafifu hewani.
“Shosti hebu tuagize bia ya baridi kwanza, hiki unachoongea ni kama vile koo limekukauka sana mwenzangu. Ukurupuke na kiroba cha watu uko, ukimbie nacho wapi sijui, ujifiche siku mbili tatu, urudi kuishi maisha ya kawaida? Narudia tena na tena hivi unaijua jela wewe? Unaijua almasi?” Morena hakuelekea kukubaliana na mwenzake.
“Umaskini matusi somo! Mie nimeuchoka. Na tatizo lako uoga umekuzidi pia. Hapo ulipo, umri unaenda bado umebanana mule kwenye chumba kimoja chenye dirisha moja. Mwili unaporomoka huo hata gari ya mtumba huna!” Fatumata aliuongea ukweli unaochoma nafsi.
“Kwa hiyo?” Morena akabweta.
Maneno ya Fatumata yalimkwangua roho. Hata hivyo, wazo la kukiiba kiroba halikumwingia.
“Maisha ukitaka kuyapatia lazima kuna mbilinge upitie.” Akamshawishi tena.
Mwenzake wala hakumsikiliza. Aliangaza huku na kule kama mtu anayetafuta kitu.
“Psiiiii! We kaka!” Morena alimwita mhudumu aliyepita karibu yao. Akamwagiza. “Niletee maji madogo ya baridi.”
Naye Fatumata akadandia. “Na mie niletee.”
Mhudumu alipoondoka wakatazamana tena.
“Kwa hiyo?” ikawa zamu ya Fatumata. Akiutafuta msimamo wa mwenzake.
“Wahenga walisema, mchuma janga….” Morena hakumalizia.
Fatumata naye alimkatisha. “Umeanza mambo yako, Kiswahili chenyewe ulipata mswaki huko shule. Ungewaelewa sana hao wahenga ungekuwa na mijidigriii leo. Si wanasemaga elimu ndio ufunguo wa maisha?”
Akamsuta mwenzake, akimpindishia midomo upande.
Morena akacheka.
Akili za rafiki yake zilikuwa za mafungu mafungu kama zake tu, ingawa kidogo yeye alimzidi mwenzake wepesi wa kuelewa. Aliwaza. Fatumata na umbole sheshe alilokuwa nalo, ungempa karatasi akuandikie hata hilo jina lake la Fatumata, si ajabu ungeitisha umati wa Mtume ukusaidie kusoma! Katu, asingekosea kama angeamua kumuita shogaye mbumbumbu mzungu wa reli.
“Kimboka anajua ulikiona hicho kiroba?” Morena aliuliza. Wakati huo, mhudumu alirejea na chano chenye chupa za maji na bilauri. Walipokaribishw
a, waliendelea na maongezi yao.
“Kimboka anajua?” Morena akalirudia swali lake.
“Angekuwa anajua nisingekuja hapa. Najua hajui na mle ndani mwake anaingiza dazeni kwa dazeni ya wanawake. Hivyo, anaweza asijue kabisa nani kamkwapulia. Huoni godeni chansi hiyo?” Fatumata akasisitiza.
“Naona na kizungu cha kuongelea uko Zambia ushajifunza tayari. Mambo ya golden chance, sijui good morning – how are you teacher – I am fine – thank you au siyo eeeh?” Morena alitamka akiigiza lafudhi ya Kizungu.
Wakaangua kicheko, wakigonga viganja vyao.

***
Haya, mwisho wa kicheko…?
Madada ndo wameshasuka mkakati wa kuuaga umasikini kwa kumzunguka Kimboka. Watafanikiwa? Njoo tena hapa tuwafuatilie…
 
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA PILI
ILIPOISHIA:
“Naona na kizungu cha kuongelea uko Zambia ushajifunza tayari. Mambo ya golden chance, sijui good morning – how are you teacher – I am fine – thank you au siyo eeeh?” Morena alitamka akiigiza lafudhi ya Kizungu.
Wakaangua kicheko, wakigonga viganja vyao.
INAENDELEA:
****
PAKA ndiye wa kumpa sumu. Kumpa mbuzi ni kumdhulumu.
Swadakta! Morena alikuwa kama mbuzi aliyekabidhiwa sumu. Fatumata alimdabika kisawasawa na ile habari ya kuiba kiroba cha almasi kwa Kimboka.
Hakuyazoea mambo haya. Hakuwa na mkono mrefu. Haikuwa haiba yake kuchukua ambacho si chake. Kisebusebu. Roho ilimchonyota. Pesa aliitaka. Aliitaka sana tu na ushawishi wa Fatumata ulivyomvika nguvu, Morena akayavua mashaka na kuamua kujitosa.
Siku ile, walizunguka mjini kama watalii. Baadaye, walikwenda kula nyamachoma na bia za ofa kwa Bokilo, mteja wa Morena. Walipotoka huko, walirudi Vingunguti, kwa Morena. Wakalala hapo. Senti mbili tatu alizoshika toka kwa Bokilo zilimpa jeuri ya kuupumzisha mwili kwa siku hiyo.
Morena Malizozo alikuwa msichana wa miaka ishirini na saba tu. Lakini, kwa sababu ya pombe na hekaheka za kujiuza ili aweze kuyamudu maisha, ungeweza kusema alikuwa anaikimbilia miaka arobaini tangu alione jua.
Waama, shida zilimkongoroa. Ila, hazikuufuchama uzuri wake wa asili. Katikati ya dhiki zake, ulimbwende wake uliwaka kama kandili hafifu gizani. Isingehitajika darubini kung’amua ni wapi uzuri wake ulikopotelea. Ni dhahiri, maisha yalimpigisha kwata.
Utoto wake ulidhulumiwa na majukumu mazito aliyobebeshwa angali mtoto. Akiwa binti mdogo, asiyejua lila wala fila ya ulimwengu. Usichana wake ulishambuliwa na utu uzima uliomjia ukiwa umevikwa koti la umasikini.
Morena hakuwa na elimu wala ujuzi wowote wa maana. Angeupata wapi na ufakiri uliung’ang’ania ukosi wa maisha machungu aliyoyavaa tangu angali tumboni. Elimu ya darasa la saba aliyokuwa nayo, aliimaliza kwa mbinde, ikimuachia uwezo wa kusoma, kuhesabu na kuandika tu.
Alikuwa na kesi za shule kila siku; utoro, uchafu, ujinga, kukosa pesa ya michango ya hiki na kile. Shule aliiona chungu, mawio hadi machweo.
Alipozaliwa, Morena aliwakuta ndugu zake watatu waliomtangulia. Akawashuhudia wengine watatu waliozaliwa baada yake. Kila mtu na baba yake. Wakakua wakijifunza kujitunza na kujiongoza.
Mama yao aliyekuwa muuza pombe za kienyeji, aliwaletea baba tofauti kila uchao. Mwishowe, wakazoea kuita baba kila mwanaume aliyezama chumbani kwa mama yao. Neno baba likakosa thamani mbele yao. Likapungua uzito. Hatimaye, kupoteza maana.
Hakuyapenda yale maisha yao hata kidogo, lakini ndiyo vile mtu hajichagulii pa kuzaliwa. Maisha ni kama chakula kilichofunikwa na kawa. Hujui ni chakula gani hadi kawa lifunuliwe; hujui kina ladha gani mpaka uchote ukionje. Unayafunua maisha ukishazaliwa, unayaonja ukianza kuyaishi!
Basi angesoma ili ajikwamue, lakini angejikwamuaje na kilabu cha pombe kilimsubiri kila alipotoka shule. Kama si kilabu, basi angepewa chano kubwa la mahindi ya kuchemsha akalitembeze stendi ya mabasi. Angerudi akiwa hoi, hoi bin taabani. Mwili wote ukiushtakia uchovu wa kutwa nzima. Angejiunga na mama yake kuuza pombe mpaka usiku mnene. Dakika mbili tatu za kuinamia daftari ili apate kujisomea, angesinzia, angetopea usingizi mpaka adhana ya alfajiri.
Mzunguko wa maisha yake, ukawa hivi kila iitwapo leo.
Kuna wakati alitamani kuyakimbia maisha yale. Alitafakari kwa kina katika ule umri wa miaka tisa. Akaona pengine amtafute baba yake mzazi, huyo Mzee Malizozo. Aliwaza, labda angeliiona ahueni katikati ya ile dhiki.
Kama ambavyo mlilala handingwa handingwa mwenye macho haambiwi kula, ndivyo ilivyokuwa kwa Morena kusubiri mama yake amueleze mwenyewe alipo baba yake. Haikutokea!
Usiku mmoja, baada ya kufunga hesabu za pombe, akajitosa. Akamwuliza mama yake, mahali alipo baba yake. Alichojibiwa, kilimkalfisha.
Mama yake mzazi alimporomoshea matusi ya nguoni. Akamtukana kiasi cha kutosha. Akitishia kumpa laana ya maisha endapo angemsaili tena kuhusu baba yake. Morena akalala usiku ule akiutazama ukuta machozi yakimtiririka. Hakuliona kosa lake. Akalazimika kuzibana hata kwikwi za kilio akichelea kuambulia kipigo toka kwa mama yake.
Aliumia zaidi kwa kuwa hata ndugu wachache aliowafahamu upande wa mama yake, ilisemekana si ndugu wa damu. Hakujua alikotokea mama yake, naye hakutaka kusailiwa juu ya hilo. Alisononeka zaidi, kujua yeye pia angefuruka na kuzeeka pasi kujua asili wala fasili yake.
Lahaula!
Ikawa mwanzo na mwisho wa Morena kumfikiria baba yake. Hakuthubutu tena kumuulizia fakaifa kumtaja kwa bahati mbaya. Maisha yakaendelea.
Morena alivunja ungo alipofikia miaka kumi na miwili. Matiti machanga yalianza kusimama. Umbile la kuvutia likaanza kuchomoza. Miluzi ya hapa na pale ikamsindikiza. Walevi kilabuni wakaanza kumshikashika.
Alijua amekua!
Mabadiliko aliyoyaona hakuyaelewaelewa. Lakini sasa, nani angemweka kitako amweleweshe? Hakuna. Alipambana nayo mwenyewe alivyojua, kimya kimya.
Maisha nayo yalimpiga danadana. Hakuwa na hakika ya sare ya shule, wala mahitaji mengine muhimu. Alibangaiza kwa kudokoa kidogo pesa za mama yake. Mama mwenyewe, wala hakuwa na habari na shule. Kitu pekee alichokifanya, kilikuwa kumwandikisha Morena shuleni. Mengine, atajuana nayo Morena mwenyewe.
Mara moja moja sana, mama yake angekumbuka kumpa mafuta ya mgando ya kujipaka mwilini. Tena ambayo, mara zote ni kwenye chupa iliyo mbioni kubakia tupu. Morena angeikwangua hadi mgando wa mwisho. Kukwangua kwenyewe kungeambatana na maumivu ya viganja vyake, kuingiza vidole hadi kwenye sakafu ya chupa ya mafuta. Chupa yenyewe, aliyopewa kwa masimango.
Si kwamba mama yake hakumudu gharama za hapa na pale katika kumhudumia. Hata kidogo. Aliingiza kipato japo kidogo, kupitia biashara yake ya pombe. Ila sasa, alitumia kipato hicho kuwahonga vijana kadha wa kadha pale kijijini. Aliwahitaji, wamtimizie haja za mwili wake.
Jambo hili lilimuumiza vilivyo Morena. Afanyeje sasa, ilhali huyo ndiye mama yake? Afadhali basi, Morena aliwaza, walau angewafahamu ndugu wengine wa mama yake. Hao wachache aliowafahamu, kila mmoja alitingwa na hamsini zake. Hivyo, Morena aliendelea kuwaza, mkono asioweza kuukata, yampasa aendelee kuubusu.
Kuna nyakati, Morena aliikosa hata pesa ya sabuni. Shule nayo, haikumweka salama dhidi ya viboko kila alipokwenda akiwa na nguo chafu. Si tu uchafu, bali pia, uchakavu. Viboko vikawa sehemu ya maisha yake ya shule. Leo, angekula vya viatu vichafu na vichakavu. Kesho, vya kukosa ada ya mtihani. Keshokutwa, kwa kukosa kalamu na madaftari. Mtondo, kwa kukosa vitabu alivyoagizwa na walimu kuvinunua. Mtondogoo, kwa kusinzia darasani kutokana na kukesha akimsaidia mama yake kuuza pombe kilabuni.
Angelala kwa saa mbili tatu tu baada ya pilika za kutosha kuhangaishana na wateja walevi kilabuni. Jumlisha adha za hapa na pale alizokabiliana nazo kila siku. Kuamka alfajiri, kutafuta kuni za kuchemshia chai iliyonyweka mara moja moja sana. Zaidi, angechemsha uji, na kuutia chumvi. Angeunywa kabla ya kwenda shule.
Pamoja na mchakamchaka huo wa maisha, Morena alimaliza elimu ya msingi. Hakuchaguliwa kuendelea na masomo ya sekondari. Hilo alilitegemea. Alifahamu fika, kufaulu kwake kungekuwa miujiza.
Akaendelea na maisha yasiyokuwa na muamana juu yake.
Siku moja yakamkuta!
“Umeshakuwa mtu mzima sasa mwanangu na wewe tafuta hela ya matumizi tusaidiane majukumu. ” Mama yake alimtolea uvivu siku aliyomwomba pesa ya kununulia gagulo mnadani.
Alimuelewa. Roho ikamuuma hasa. Alijua alichopaswa kukifanya ili kusaidia hayo majukumu mle ndani. Mama yake akasitisha rasmi kumpatia hata ile pesa ndogo ya mafuta.
Tayari alikwishatimu miaka kumi na nne. Chuchu za kisichana zikachomoza kifuani. Waama, zikitishia kuitoboa fulana hohe-hahe aliyoivaa. Mama anamwambia atafute pesa zake. Azipate wapi sasa? Njia moja rahisi ya kujiingizia kipato ikamjia kichwani.
Kulala na wanaume, apate wake ujira.
Alianza taratibu. Siku za mwanzo zilikuwa za maumivu makubwa kwenye viungo vyake. Hakuwa na namna. Baada ya shughuli, alijibanza maliwatoni akijikanda. Machozi yalimdondoka pasi ajizi. Akajikaza. Alifahamu anapaswa kukomaa. Akakomaa kweli, akazowea. Ikafikia wakati, alimudu kulala na wanaume zaidi ya watatu, usiku mmoja!
Nyakati zingine, alisononeka. Ah! Mungu wangu mpaka lini? Nyakati zingine angejiuliza kwa nini hakuzaliwa kwenye familia zenye ahueni kama wenzake? Kwa nini maisha yalikuwa hivi kwake? Hakukuwa na wa kumpa majibu, fakaifa hata wa kumpa maneno ya kumtia moyo wa kupambana na madhila yale peke yake. Hakuwepo! Pepo kwake ilikuwa nyeusi ti!
Kipindi hicho, mama yake alikwishaanza kuumwa hiki na kile. Akawa mtu wa kuuguzwa. Wakahisi ameukwaa UKIMWI. La hasha! Walipima na kupima. Hawakuona walichokihisi. Aliendelea kuugua tu. Mara alalamike mgongo, mara miguu, ama kichwa. Ili mradi, hakuna magharibi iliyopita asiwe katika hali ya kunung’unikia maumivu.
Ikasemwa mitaani amefanyiwa ushirikina. Tabibu mmoja akawaambia, kinachomsumbua zaidi, ni msongo mkali wa mawazo. Hili la msongo hawakulimaizi. Walichagua kuamini katika ushirikina. Ilikuwa rahisi kwao kulielewa hilo kuliko kuambiwa mawazo yakizidi huleta ugonjwa. Potelea mbali! Ikabaki kusemekana mpaka leo hii, usiku huu. Morena alipokuwa ameitumbulia macho dari pasipo kuitambua akilini. Mama yake huko alikokuwa alikuwa mgonjwa wa kuchechemea.
Alifanya yote aliyoyafanya hapa mjini, ili kila wiki atume pesa kidogo nyumbani kwao. Wadogo zake wajikimu na walio shuleni wasome. Kamwe, hakutaka na wao waishie alikoishia yeye. Aliifanya kazi yake dhalili katika mazingira magumu mno, aliifanya kazi ngumu iliyomuondolea utu na heshima kwa jamii ili tu wadogo zake wapate elimu.
Elimu aliyoamini ingewakomboa toka katika lindi la ufakiri.
Morena alilengwa na machozi wakati alipokumbuka alipotoka na kutazama pale alipokuwa sasa. Akajikuta tu tamaa ya kushirikiana na Fatumata kuiiba hiyo almasi ikimtekenya kupitiliza huku ujasiri ukimpapasa mbavu polepole. Aliuchoka ufakiri, naye akataka kuijaribu bahati yake.
Akiamini tu, huenda ni kweli mgagaa na upwa hali wali mkavu!
Laiti tu angejua!
***Mnh! Kwa hali hii ataacha kutamani kuiba kiroba cheusi kweli?? Hebu twende naye!!
 
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA TATU...
ILIPOISHIA:
Morena alilengwa na machozi wakati alipokumbuka alipotoka na kutazama pale alipokuwa sasa. Akajikuta tu tamaa ya kushirikiana na Fatumata kuiiba hiyo almasi ikimtekenya kupitiliza huku ujasiri ukimpapasa mbavu polepole. Aliuchoka ufakiri, naye akataka kuijaribu bahati yake.
Akiamini tu, huenda ni kweli mgagaa na upwa hali wali mkavu!
Laiti tu angejua!
INAENDELEA:
3
MORENA alibadili uchago na kujilaza kiubavu. Huko alikogeukia alilala akimtazama Fatumata aliyekua ametopea usingizini. Alimtazama tu na kutabasamu. Huyu alikuwa ni rafikiye wa utotoni mpaka sasa utu uzimani.
Mwenzake ahueni ndogo ya maisha ilishamtembelea, alitangulia kuja mjini. Lile umbile lake murua walau lilimjalia kupata wa kumpa vya kumuwezesha hata kupanga upande mzima wa vyumba vya uani, ila kichwani ndiyo vile alikuwa mtupu kuliko mtungi uliotoboka.
Mungu hakupi vyote!
Usiku ule alilala usingizi wa kuvizia. Ilipotimu alfajiri ya saa kumi na moja akawa wa kwanza kudamka. Akaketi kitandani huku moyo wake ukiwa bado unamsokota. Alichotaka kukifanya hakikuwa sahihi, lakini mangapi yasiyo sahihi amekwishayafanya hadi sasa? Hata leo hii aliogope hili la kuiba? Akawaza, akawazua!
Aligeuza shingo polepole na kulitazama dirisha. Akalitanua pazia na kulitazama anga la Karima. Kwa dakika zile alizoketi pale aliushuhudia ulimwengu ukipambazuka na ule utusitusi wa alfajiri ukikimbizwa na ujio wa siku mpya. Alijikuta tu akitamani maisha yake yabadilike kirahisi namna ile, kama pambazuko lile.
****
Pilika pilika za kuashiria kumekucha zilikwishaanza. Sauti za wapangaji jumlisha na miburuzo ya viatu, achilia mbali honi za pikipiki kwa baiskeli vilifanya utulivu ufungashe virago na kwenda masafa ya mbali zaidi.
Morena alikuwa bado kitandani kwake pale pale. Safari hii akiwa peke yake. Fatumata alikwishaamka na kuelekea msalani. Mlango ukafunguliwa na Fatumata akaingia akirusharusha miguu huku mikono ikiwa imekikamata kibofu chake kana kwamba kilitaka kuchomoka. Alizunguka kama tiara.
Akaenda, akarudi, akapunga mikono hewani na kukishikilia tena kibofu chake. Alilalamikia haja ndogo iliyokuwa imembana kupitiliza.
“Ah! Kwani chooni kuna nini!?” Morena alimwuliza, akimshangaa. Papo hapo akijisikia kucheka kwa namna ule mwili wa Fatumata ulivyokuwa ukitikisika. Ufundi wa Mungu ulidhihirika.
“Kuna foleni na mtu ‘uko ndani sijui anajisaidia kamba… basi aah!” Aling’aka.
Morena aliinyoosha shingo mbele. Akachungulia kule mlangoni. Kwa vile mlango ulikuwa wazi, alimwona mpangaji mwenzake aliyekuwa akizoa taka mlangoni pake.
“Mama Sara eti chooni kuna nani jamani?” Morena aliuliza akisotesha matako ili kuteremsha miguu sakafuni.
“Sinasudi huyo na bwana yake wanakoshana uko masaa… Si unajua kuna watu wanajikuta wazungu kila mwisho wa mwezi!” Mama Sara alijibu akiwa amegeuka kabisa kumtazama Morena ambaye sasa alishateremka toka kitandani na kwenda kusimama karibu na mlango.
“Wazungu wako Masaki ’uko wanakogea masinki, sasa maji ya kujaa kisadolini nayo ya kukogeshana?” Alisonya akimgeukia Fatumata. “Chukua kopo chini ya uvungu hapo ujisaidie!”
Morena alitoka pale mlangoni. Aliikamata korido akielekea huko msalani. Aliwakuta wapangaji wenzake wamefura. Kila mtu akisema lake, huku misonyo ikiwamba eneo zima.
Aliutazama mlango wa msalani. Khanga na taulo vilining’inia mlangoni hapo.
“We Sinasudi hebu toa basi hicho kikaragosi chako humo ndani watu waoge bwana!” Morena aligomba kwa sauti ya juu hasa, ikipokea ushirikiano mkubwa toka kwa wale wapangaji wengine pale nje. Walishambulia kwa maneno na wengine wakifanya mizaha iliyowavunja mbavu.
Zikapita dakika kadhaa, ile khanga ikavutwa kwa ndani, na lile taulo likafuatia. Watu wote waliukodolea macho mlango. Sinasudi alitangulia kutoka, akifuatiwa na mwanaume nyuma yake. Hakusemezana na mtu licha ya wapangaji wenzie kumsindikiza na maneno ya kukera.
Ni kama hakuwasikia, nao wakaachana naye na kuendelea na shughuli zao. Haikuwa mara ya kwanza kwa Sinasudi kuwakera wenzake namna hii kila mpenzi wake alipomtembelea. Kero kama hizi zilikuwa sehemu ya maisha yao katika nyumba yao ya kupanga ambayo choo na bafu vilikuwa sehemu moja.
Zilikuwepo kero zingine kedekede. Leo, wangesutana kwa umbeya. Siku nyingine, wangeshikana mashati na kutoleana maneno makali wakigombea foleni ya kukinga maji bombani ama zamu za kununua umeme. Wakati mwingine wangeamka na ugomvi wa zamu za kusafisha choo chao kiasi cha watu kuapizana kutozikana. Na baada ya siku mbili tatu ungewakuta wakisogoa na kuteta kama si wao.
Morena alirudi chumbani kwake huku koridoni wachache wakiendelea kuzoza.
“Mmemalizana?” Fatumata akamsaili wakati akiingia chumbani.
“Tushamsuuza na bwana’ake huyo mwenye komwe ka’ kifuu cha kutwangia dawa, akija hatuhemi dada!” Alisonya akimfanya Fatumata acheke wakati akiliweka uvunguni lile kopo lenye mkojo.
Morena alikifuata kitanda. Akaketi hapo, mwayo ukimvamia na kumtangazia njaa.
“Sasa inakuwaje?” Aliuliza akipiga mwayo mwingine kiasi cha kumletea cheche za machozi machoni.
“Tunywe hata chai kwanza, kisha ndio nikupe mpango mkakati.” Fatumata naye akapiga mwayo alioubembeleza kwa kupiga piga mdomo wake kwa kiganja.
“Ila wasiwasi wangu ni mambo yakienda kombo! Mie n’na mama mgonjwa mwenzio, nikipotea miezi tu nitaiua familia kwa njaa.” Alijitetea Morena.
“Kwahiyo ukifa na wao watakufa? Wadogo zako washakuwa watu wazima wale nao waanze kukata viuno sasa msaidiane majukumu!” Fatumata alimjibu kimasihara na asijue kauli kama hiyo ndiyo iliyomfikisha mwenzake kwenye maisha haya aliyonayo.
Morena akatikisa kichwa kwa masikitiko huku akinyanyuka toka pale kitandani. Akaenda zake kutafuta staftahi.
Jioni ya siku ile, Kimboka, mpenzi wa Fatumata aliwapigia simu akiwataka waende Wanyama Hotel, Sinza. Wakati wakijikwatua, Fatumata akaamua kumweleza Morena mpango mzima utakavyokuwa. Waliongea kwa sauti ya chini kidogo kuepuka kusikika hadi nje.
“Mmh! Daudi Chochoro? Yule anaweza kukaa na siri kweli?” Morena alionyesha shaka mara tu alipotajiwa huyo dereva teksi ambaye wangemtumia katika shughuli nzima.
“Sasa nani mwingine wa kumtumia? Daudi mtu poa sana, tutamkatia jiwe ili aogope kusema maana atajua akijichanganya tu tutasombwa wote.” Fatumata alijaribu kumtoa hofu.
“Kwa hiyo ukinibeep tu ndio nizunguke ukirushe au ukibeep itamaanisha umeshakirusha?” Morena aliachana na kazi ya kupaka wanja akamgeukia mwenzake, akiuliza maswali aliyotaka yamtulizie nafsi yake.
“Nitakuwa nimeshakirusha yaani wewe na Chochoro mkisikia ndindili ndindili…” Aliuigiza mlio wa simu, akaendelea. “Wewe zunguka nyuma chukua kiroba kimbilia teksi ya Daudi na yeye aondoe gari moto… Hakuna kusimama mpaka muwe na uhakika mko salama. Ikibidi mzunguke kidogo mjini kupoteza maboya kama kuna mtu anawafuatilia.” Fatumata aliongea kwa ujasiri.
“Hatariii! Kama muvi la misukosuko vile!” Morena alihisi matumbo yakimcheza.
“Yaani msikosee Morena, mi n’tahakikisha siachi alama yoyote na nyie ndio kabisa mhakikishe mmetoka salama.” Fatumata alisisitiza akizidi kumtia mwenzake hali ya mshawasha.
Walipomaliza kujipara, waliita bajaji tayari kwa safari yao.
***Kimenuka, wabongo wanasema... dili litatimia? Njoo kesho tuwafuatilie.
 
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA NNE....
ILIPOISHIA:
“Hatariii! Kama muvi la misukosuko vile!” Morena alihisi matumbo yakimcheza.
“Yaani msikosee Morena, mi n’tahakikisha siachi alama yoyote na nyie ndio kabisa mhakikishe mmetoka salama.” Fatumata alisisitiza akizidi kumtia mwenzake hali ya mshawasha.
Walipomaliza kujipara, waliita bajaji tayari kwa safari yao.
INAENDELEA:
Walianzia starehe zao Wanyama Hotel. Wakati wengine wakiburudika, kwa Morena havikulika vikashuka. Alikuwa na wahaka uliompeleka msalani kila dakika. Alijisikia kuhara, wala asihare fakaifa kushuta tu. Moyo haukudunda kawaida tena, ulikwenda mara mbili ya mshale wa sekunde. Ta! Ta! Ta! Ta!
Alichachatika! Wizi haukuwa hulka yake abadani. Pombe zilizotapakaa mezani aliziona kama chupa za sumu. Hazikunyweka!
Usiku wa saa sita kasoro vichapo kadhaa, starehe zao zilifikia ukingoni. Kimboka alikuwa anayumba kwa ulevi huku akiwa na mpenzi wake ubavuni. Kwa mahaba ya uongo na kweli, alioneshwa mpaka sehemu za kukanyaga wakati akilifuata gari lake. Morena yeye alizuga kuaga kuwa anarejea kwake Vingunguti.
Marafiki wa Kimboka nao walinyanyuka. Baadhi yao, kwa safari za kurudi makwao na wengine wakiwa na nia ya kuhamia kiwanja kingine cha starehe. Kila mmoja alikuwa anaondoka eneo lile. Fatumata alimtazama Morena akimkazia macho. Macho ya kusisitizia mipango waliyoongea.
Moyo wa Morena ulidunda dabali, ni kama vile aliyahisi matatizo, na kuzinusa dalili mbaya; hakuwa huru nafsini hata kidogo. Ujasiri mdogo aliokuwa nao ulimwezesha kutembea japo kwa kujikanyaga kanyaga kana kwamba alihisi kuna watu walioyaona mawazo yake.
Alikwenda kujibanza mahali, akitaka kuhakikisha kwanza watu wote aliokuwa nao wameondoka. Kisha taratibu alijichomoa toka kwenye eneo alilokuwa amejibanza. Akasimama kwenye njia iliyopita nyuma ya ile hoteli.
Ukimya mkubwa uliotamalaki eneo hilo ulimdabua kidogo. Ulikuwa ukimya uliomfanya akiogope hata kivuli chake. Aliangaza huku na kule akiitarajia teksi aliyokuwa anaisubiri. Walikwishakubaliana mawasiliano pekee yawe ile beep na kwamba dereva teksi, Daudi Chochoro, angepita saa sita kamili kumchukua Morena hapo alipokuwa. Waende sehemu waliyopanga kujibanza.
Morena aliitazama tena simu yake kwa minajili ya kujua muda.
00:47 pm
Maandishi ya saa yake kwenye simu yalimfanya azidi kupungukiwa subira. Zilikwishapita dakika arobaini na tangu muda wa makubaliano. Kulikuwa na tatizo gani? Akawaza mamoja kwa makumi ndani ya muda huo mfupi.
Ni vipi kama Daudi Chochoro amebadili mawazo? Akawaza tena ilhali hofu nayo ikizidi kumtomasa maungoni na kumchachafya.
Wakati akiangaza huku na kule, miguu nayo ilianza kumwuma. Alishasimama pale kwa muda mrefu wa kutosha kutembea hata nusu kilometa. Alipotaka kuchutama alimwona mtu akija upande ule aliokuwa amesimama. Mtu huyo alikuwa peke yake. Alikuja kwa mwendo wa taratibu. Mavazi na umbile lake vilimjulisha kuwa ni mwanaume, tena kipande cha mtu.
Morena alimeza mate kwa nguvu mno mithili ya mtu anayejaribu kuimeza sarafu ya shilingi hamsini. Ghafla tu, vinyweleo vilimsimama. Alighairisha hata zoezi la kuchutama. Alihisi baridi ya hofu ikipenya hadi kwenye mifupa. Alipomwona mtu yule akihama upande wa njia aliyokuwepo na kuja upande huo aliokuwa amesimama yeye, aliuhama huo upande huku akigeuka nyuma mara kadhaa kutazama alikotoka.
Alionekana kama mtu aliyekuwa akivizia jambo!
Hili lilimwongezea mashaka zaidi Morena. Alitamani kupiga yowe na sauti yake ikamsaliti. Kwa nini apige yowe? Akili ilimhoji na kumtia ganzi. Akayafinya macho yake na kuyapunguza upana wake wakati akiyakaza yamtazame vema yule jamaa aliyekuwa anazidi kumkaribia. Bado alikuwa na ule mwendo wa kuvizia, mwendo uliomfanya Morena amuone yule jamaa na kivuli chake kama watu wawili tofauti!
Nafsi yake ilimtuma kupiga hatua moja kurudi nyuma. Hiyo hatua moja ikazaa hatua zingine za pole pole. Hatua za minyato. Mapigo ya moyo yakikimbia kwa kasi ya ajabu. Alihisi yalikaribia kukitoboa kifua na kuchanja mbuga nje ya mwili wake.
Afanaleki!
Alitishika. Alitishika si kidogo.
Hapana huyu si mtu mzuri! Morena alijiambia kwa sauti ya kichwani huku akimtazama jamaa kwa wasiwasi. Wakati huo, alikwishagotea kwenye ukuta wa nyumba iliyotazamana na ile hoteli.
Alimwona yule jamaa akichomoa mkono toka kwenye mfuko wa jaketi kubwa alilokuwa amevaa. Morena hakusubiri kuona kilichochomolewa. Aliinama haraka. Akavua viatu vyake. Akatimua mbio.
Alikimbia kwa kasi ndogo. Mara moja aligeuka kutazama nyuma. Pengine alitaka kuhakiki kama uamuzi wake wa kukimbia ulikuwa sahihi. Akashuhudia mwendo wa yule jamaa nao ukiwa umebadilika toka mwendo wa pole pole na kuwa mchaka mchaka. Morena alihamanika.
Anakimbizwa, uwii!
Hakugeuka tena. Alikimbia kwa kadiri miguu yake ilivyonyonga, akitamani kuiuliza kama aliwahi kula chochote na kuinyima. Alikimbia hadi alipoifikia njia panda iliyogawanyika mara nne; ile aliyotokea, iliyoelekea mbele yake na mbili zilizokuwa kushoto na kulia kwake. Akapiga breki za ghafla akiwa anahema na asijue ashike njia ipi.
Aliweweseka kwa hofu lakini ikamlazimu kuuvaa ujasiri wa kukopa. Akageuka kutazama kwanza kule alikotoka. Patupu!
Hakukuwa mtu tena wala kivuli. Kaenda wapi? Akachoka. Hii kwake haikuwa ishara njema kwenye mpango wao. Aliliona bwawa la mikakati yao likinyemelewa na ruba.
Alihamanika. Alipepesa macho kutazama kule alikotoka. Pamoja na kuwepo kwa mwanga wa taa toka nyumba hii na ile. Bado giza dogo lililokuwepo katikati ya barabara hii iliyokuwa kimya, lilimchezesha kwata. Ujasiri wa kurudi alikotoka ulichanja mbuga na kutokomea.
Sasa?
***Mnh! Hata mi' sijui...hapa tuje kesho tu kujua kilichofuata, Daah!!
 
RIWAYA: KIROBA CHEUSI
MTUNZI: LAURA PETTIE
SEHEMU YA TANO.......
ILIPOISHIA:
Aliliona bwawa la mikakati yao likinyemelewa na ruba.
Alihamanika. Alipepesa macho kutazama kule alikotoka. Pamoja na kuwepo kwa mwanga wa taa toka nyumba hii na ile. Bado giza dogo lililokuwepo katikati ya barabara hii iliyokuwa kimya, lilimchezesha kwata. Ujasiri wa kurudi alikotoka ulichanja mbuga na kutokomea.
Sasa?
INAENDELEA:
4
MORENA alikata shauri kusonga mbele. Kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kurudi pale alipokuwa amesimama mwanzo. Aliangaza akizitazama zile njia nne kwa awamu. Kibaridi cha usiku nacho kilimpuliza na kuiparaza ngozi mpaka utumbo. Kuna majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumtaja Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.
Akaamua tu kukamata njia iliyokuwa mbele yake, akiwa amejikumbatia, mkono wa kulia ukiwa na viatu vyake huku ule wa kushoto ukiwa na simu yake. Akaivuka njia panda, akiwa yeye na kivuli chake. Alitembea tu na asijue aendako.
Si kwamba hakuzoea kuwa nje usiku kama huu. La hasha! Katika mikikimikiki yake ya kujiuza alikwishazunguka nje usiku mnene zaidi ya huu.
Vingunguti, Buguruni, Yombo ama Kariakoo hii saa saba kasorobo usiku, pilika pilika za hapa na pale zingetosha kumfanya akae mahali aagize hata mchemsho wa miguu ya kuku kusukumia wasaa. Ila huu mtaa alioibukia ulikuwa kimya mno, kimya kupitiliza.
Hatua kadhaa mbele akamwona mtu kwenye moja ya mageti yaliyokuwa mbele yake. Kwa haraka haraka akahisi ni mlinzi. Mkombozi!
Alimkimbilia. Akasimama mbele yake wakati mlinzi yule naye akiacha kuingia ndani na kusimama kizingitini. Alimtazama Morena juu chini.
“Kaka yangu n’na shida!” Alianza kujieleza.
Ile hali ya kuhema ilifanya mabega yake yapande na kushuka kiasi cha kuonekana wazi kuwa alikuwa katika hali ya taharuki. Yule mwanaume getini, alimtazama Morena kwa mashaka kisha akatazama kule alikotokea. Ni dhahiri alitaka kuhakiki kwanza kama Morena alikuwa yu mtu mwema, ama pengine kujiridhisha kuwa hakuwa ameongozana na mtu mwingine yeyote.
Morena alimeza mate kwa taabu akiwa kimya. Huenda aliomba dua amri ya kuendelea kujieleza itoke na kumhakikishia usalama wake. Yule mwanaume akamkunjia uso.
“Shida gani?” Alisaili kwa sauti kali. Alifunga geti, akasimama kumwelekea bibie.
Morena aliomba hifadhi ya muda hata pale ndani ya geti ili aweze kuwasiliana na ndugu yake kwa usalama.
Yule mwanaume hakumwelewa. Alimtandika maswali ya haraka haraka ambayo Morena alijitahidi kuyajibu ili tu apate hifadhi aliyoihitaji. Uongo na ukweli vikichanganywa kuitafuta huruma. Akaipata.
Alipopewa stuli ili aketi hapo getini kwa ndani, Morena alipata amani ya kumpigia simu Fatumata. Ghadhabu na hofu vilikumbatiana wakati akisubiri simu yake ipokelewe.
Simu iliita hadi kukatika. Aliitoa sikioni. Akaitazama kwa hasira.
Yule mwanaume alimtazama kana kwamba alitaka kuthibitisha kuwa Morena hakuwa mwongo. Akaipiga tena simu ya Fatumata safari hii akimwomba Mungu simu ipokelewe. Ikaita kwa sekunde tatu nne.
Kimya!
Alisubiri kidogo tena.
Kimya!
Alihisi ile ilikuwa siku ya kufa nyani, kila mti pruuu mpaka maka. Akainua macho. Alimtazama yule mlinzi, ambaye naye alikuwa anamtazama kwa umakini.
“Hapokei simu!” Alitamka kwa huzuni akinyanyua mabega juu na kuyashusha.
“Sasa?” Mlinzi alimtupia swali kwa sauti ya kuhimiza jibu.
Morena akatapatapa. Kwa nini? Hakuwa na pesa yoyote ya maana zaidi ya shilingi elfu mbili alizokuwa amezitia kwenye sidiria. Makubaliano yao yalikuwa teksi ije impitie pale alipokuwa akiisubiri mwanzo kisha impeleke huko pa kusubiria kuuchukua mzigo halafu imrudishe nyumbani. Si hivi mambo yalivyoonekana kuparaganyika ghafla!
Hasira zilimshika maradufu. Hakuwa na namba ya Daudi Chochoro ambaye pengine angemsaidia kujua kinachoendelea. Akahisi kudhalilika na kusumbuka kwa tamaa ya pesa za haraka. Wakati akiwaza cha kumjibu yule mlinzi. Simu yake ikaita, alikuwa Fatumata.
Moyo ukafunguka haraka, hata kabla ya mwito wa simu ile kuchanganyia akaipokea.
“Mpuuzi wewe na huyo Uchochoro wako!” Alisonya. “Hivi mnadhani mie kipande cha mti kukaa hapa nawangojea kiama na msiniambie mko wapi?”
Morena hakuwa na muda wa kumsikiliza Fatumata aliyekuwa akiongea wakati Morena akigomba. “Mie mgeni huku halafu hamnambii kinachoendelea mkitegemea nini? Nimekoswa koswa kisu cha utumbo we’ unalalana tu uko…”
Alisonya msonyo mrefu zaidi wa kilo za kutosha kiasi cha kumfanya mlinzi atabasamu.
“Sipajui hapa… niendeje?... Mwenzangu mwisho usiku huu nitokezee Matombo Morogoro bure kwa kukatiza katiza… Kwa hiyo?” Morena aliuliza akiinama kidogo na kuanza kuvaa viatu vyake. Ni kama vile sasa alipata suluhisho la namna ya kuondoka pale.
Alipomaliza kuongea na Fatumata, alinyanyuka. Alimshukuru yule mlinzi. Aliitoa ile elfu mbili yake aliyokuwa nayo. Alimpatia mlinzi. Kwa uungwana wake, mlinzi akaikataa akidai kumsitiri pale ilikuwa ihsani tu.
Huenda alishikwa na imani vile alivyoitoa hela pekee toka kwenye kitambaa kidogo kilichokuwa kwenye sidiria. Wakazungumza mawili matatu. Mlinzi akavunja kanuni za ulinzi. Alimsindikiza Morena mpaka karibu na ile njia panda. Dakika tatu tu, mwanga wa gari ukaonekana ukikata kona kuja eneo lile.
Morena akashukuru. Wakaagana.
“Unajua una mishe ya hatari halafu unachukua gari bovu, la kazi gani mzee?” Morena alinung’unika wakati akiingia kwenye teksi ya Daudi Chochoro baada ya kuelezwa sababu ya kuchelewa kwake.
Daudi alikuwa mtu mzima wa makamo. Mvi lukuki zilizompatia shikamoo nyingi za hiari. Huo utu uzima wake ndiyo uliopelekea Morena amfanyie staha ya kutomporomoshea maneno ya shombo. Vinginevyo, njia nzima angeipata pata.
Kwa ule umri wake, ilimpasa kuwa nyumbani akiogelea kwenye bahari ya usingizi wa raha. Tena, baada ya uchovu wa kucheza na wajukuu kutwa nzima. Lakini, uhalisia wa maisha ulimpiga ngwara matata sana. Nazo shida za dunia hii zikampora yote yampasayo.
Alikuwa barabarani usiku huu akitafuta senti za ziada. Senti za kupeleka mkono kinywani kwake na kwa familia yake kubwa ya wana na wajukuu. Familia iliyomtegemea yeye kwa kila kitu.
“Magari hayana muamana mwanangu!” Mzee Daudi alijitetea akitabasamu. Tabasamu lililovaa uchovu wa kutwa nzima. Mwendo wa gari ukaongezeka.
***Hii safari ya kukifuata Kiroba inazidi kuwa ndefu aisee!
 
Namkumbuka Morena alivyojitoa muhanga kuhakikisha uhai kati yake na rafiki yake unadumu.
Tariki kijana tajiri anaishi miaka mingiu akiwa hafahamu kuhusu siri ya ramani iliyoachwa na baba yake.
Fatuma mwanadada wa mjini wa mjanja mjanja lakini hajui kusoma.
 
Tatizo la watu wanaopost story humu huwa wanataka waonekane kama Miungu watu sasa mtu unamuuliza na yuko online anapiga kimya kama haoni msiwe mnapost story zenu kama mnajua haziish
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom