RIWAYA:BIASHARA YA KIFO

RIWAYA:BIASHARA YA KIFO

NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi

“Nataka twende sehemu.”
“Wapi?”
“Kutembea! Unapenda kukaa hapa tu kwa siku zote tangu umefika?”
“Hapana! Ila sidhani, sijapazoea sana huku.”
“Unaogopa utapotea?”
“Ndiyo!”
Ethan alikuwa akizungumza na Annabel, alitaka kumchukua na kumtoa mtoko huku lengo lake kubwa likiwa ni kutaka kuzungumza naye juu ya kile kilichomfanya kuwa nchini Tanzania. Bado Ethan aliona kulikuwa na ugumu wa msichana huyo kukubaliana naye kwani kila alipojaribu kumchombeza kwa maneno ya haya na yale, ugumu ulionekana dhahiri.
Annabel hakuwa na maamuzi ya maisha yake, alikuwa na umri chini ya miaka kumi na nane, kila kitu kilichotakiwa kuamuliwa maishani mwake kilikuwa chini ya wazazi wake. Japokuwa kipindi hicho wazazi wake hawakuwepo lakini hakutaka kulisahau hilo, hakutaka kuondoka nyumbani hapo.
Bado Ethan alikuwa akimchombeza kwa maneno matamu ya mahaba, alitaka msichana huyo awe mpenzi wake kwanza, alale naye na ndipo ampeleke nchini Marekani kwa ajili ya kucheza filamu ya ngono kama ilivyokuwa imepangwa.
Wanawake wale kumi walikuwa tayari, walijiandaa na wengine kuaga kabisa lakini tatizo likawa kwa Ethan tu. Hakutaka kuondoka nchini Tanzania pasipo Annabel, alimpenda mno msichana huyo na alimhitaji kuliko mtu yeyote yule, kila alipomwangalia, cha zaidi ya yote alihitaji kufanya naye ngono.
“Why are you here?” (Kwa nini upo hapa?) aliuliza askofu Benedicto mara baada ya kufika nyumbani.
“Me?” (Mimi?)
Askofu akakasirika, alijua fika kwamba Ethan alijua kuwa alikuwa akiongea na yeye sasa ilikuwaje aanze tena kumuuliza kama alikuwa akiongea naye. Akaanza kukunja ndita usoni mwake, hakumpenda kijana huyo na alimchukia mno.
“I’m sorry sir, I want to take your daughter out,” (Samahani mkuu, ninataka kumtoa binti yako mtoko) alisema Ethan huku akijivika ujasiri mkubwa.
“Impossible.” (Haiwezekani)
Askofu hakutaka kukaa mahali hapo, moja kwa moja akaelekea chumbani kwake kwa kuamini kwamba mara unapoamua kumuua nyani haukutakiwa kumwangalia usoni. Ethan akanyong’onyea, hakuamini kama baba yake Annabel angekataa kumruhusu binti yake kuondoka naye.
Alimwangalia Annabel usoni, kila alipomwangalia, mapenzi yalizidi kuchomoza moyoni mwake kiasi kwamba kuna wakati alijiona kutokujiweza kwa msichana huyo, aliamua tu kumchukua na kuwa naye huku lile lengo la kutaka kumpeleka nchini Marekani kwa ajili ya kuigiza filamu za ngono aachane nalo.
“Naomba unisamehe,” alisema Ethan.
“Umenifanyia nini kibaya?”
“Hakuna! Ila naomba unisamehe.”
Moyo wa Ethan ulikuwa kwenye maumivu makali mno, kutokana na mapenzi makubwa yaliyougubika moyo wake, hapo ndipo alipogundua kwamba alifanya kosa kubwa kutaka kumchukua Annabel na kumpeleka nchini Marekani kuigiza filamu zile za kikubwa.
Alijiona mkosaji na ndiyo maana wakati huo aliamua kumuomba msamaha msichana huyo kwa kile alichotaka kukifanya japokuwa hakumuweka wazi ni kitu gani.
“Utarudi Marekani?” aliuliza Ethan.
“Kurudi? Mmmh! Sijajua, ila sijui kama nitarudi, nitataka kukaa na wazazi wangu zaidi,” alisema Annabel.
Ethan hakutaka kurudi nchini Marekani peke yake, mtu aliyekuwa akimhitaji kurudi naye alikuwa Annabel tu. Kila siku akawa mtu wa kufika nyumbani hapo kwa ajili ya kumuona msichana huyo na kuzungumza naye mengi.
Japokuwa siku za nyuma askofu alikuwa akimchukia sana Ethan lakini mwisho wa siku akajikuta akimzoea kijana huyo na hatimaye chuki kuanza kupotea moyoni mwake. Wakaanza kukaa chini na kuzungumza mengi huku kila mmoja akijaribu kumficha mwenzake kile kilichokuwa kikiendelea katika maisha yake, yaani askofu akimfichana Ethan kama alikuwa askofu wa Kanisa la Kiroma huku kijana huyo akificha kazi aliyokuwa akiifanya kipindi hicho.
“Ninataka kumfanya Annabel kuwa mwanamke mwenye furaha kuliko wote duniani,” alisema Ethan huku akitoa tabasamu kubwa.
“Nyie vijana wa sasa hivi hamuaminiki kabisa.”
“Kwa nini tusaminike? Yaani hata wewe huniamini?”
“Hahaha! Siwezi kukuamini hivihivi.”
“Unataka nifanye nini ili uniamini?”
“Uanze kwenda kanisani.”
“Hahaha!”
Walizungumza kama marafiki, walizoeana mno na wakati mwingine walitaniana hapa na pale. Ethan alijisahau kabisa, akasahau kama alitumwa kwa ajili ya kuwachukua wanawake na kuwapeleka nchini Marekani, kwake, kile alichokuwa akikifikiria kwa kipindi hicho ni mapenzi tu.
Kutokana na ukaribu na familia hiyo, kila mmoja akamzoea Ethan kiasi kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa na hofu naye tena. Kwa kuwa alizoeleka, hivyo alichokifanya ni kuendelea kumsisitizia Annabel jinsi alivyokuwa akimpenda na kumuhitaji maishani mwake.
Alikataa na kukataa lakini mwisho wa siku akaona kama usumbufu hivyo kukubaliana naye na hivyo kuwa na uhusiano wa kimapenzi. Ilikuwa ni siri kubwa, wazazi hawakujua chochote kile, walifanyiana mambo ya chumbani kila muda ambao wazazi hao hawakuwepo nyumbani hapo.
Wazazi walipokuwepo, waliishi kama kaka na dada kitu kilichowatia upofu wazazi hao. Japokuwa aliaminika sana lakini Ethan hakuwa mtu wa kulala nyumbani hapo, alikuwa akifika asubuhi na kuondoka usiku, kurudi hotelini na kucheza kamari, mchezo aliopenda sana kuucheza kipindi hicho.
*****
“Ninataka mniletee Ethan mahali hapa!” ilisikika sauti ya mwanaume mmoja kutoka ndani ya nyumba moja ya kifahari.
“Sawa.”
“Ninataka mkamilishe kila kitu, ikiwezekana, mmuue kama tu ataleta ubishi,” alisikika mwanaume huyoi.
“Hakuna tatizo mkuu.”
Yalikuwa ni mangezi baina ya bwana Cook na vijana aliokuwa amewaita ndani ya nyumba yake. Alichanganyikiwa mno, biashara zake zilisimama kwa muda. Uchumi wake mkubwa ulitegemea biashara ya ngozi aliyokuwa akiiifanya, wasichana waliokuwa wakiletwa na kukataa ndiyo haohao ambao ngozi zao zilichunwa na kupelekwa nchini China.
Alichanganyikiwa, alijiona kama akikaribia kufilisika. Kijana wake wa kazi ambaye alimtuma nchini Tanzania, alizamia, kwa kipindi cha mwezi mmoja na nusu hakuwa amerudi nchini Marekani, mbaya zaidi, hakuwa akiwasiliana naye kama alivyofanya wakati alipokuwa akienda katika nchi nyingine.
Alikuwa na hasira mno, alichohisi ni kwamba Ethan alitaka kuachana na biashara hiyo kitu ambacho hakutaka hata kukisikia kwa kuona kwamba ni lazima kijana huyo angekwenda kutoa siri juu ya biashara ile iliyokuwa ikiendelea.
Hakutaka hilo litokee, alikuwa radhi kulizuia kwa nguvu zote. Alichokuwa akikitaka mahali hapo, huyo Ethan aletwe kwake ili afanye uamuzi mmoja, kama kumuua au kumuonya kwa kile alichokuwa akikifanya.
“Kwa hiyo?” aliuliza kijana mmoja.
“Mmuue hukohuko.”
“Sawa mkuu!” alisema kijana mmoja na kuanza kuondoka.
“Subirini kwanza. Au kama vipi mleteni huku nimuue kwa mkono wangu! Wakati wa kuja huku, tumieni meli ya mizigo ya Mediteranian Cargo,” alisema bwana Cook.
“Hakuna tatizo!”
Kila kitu kikaanza kufanyika, vijana wale wakapatiwa dola laki tano kwa ajili ya safari yao ya kwenda nchini Tanzania ndani ya Jiji la Dar es Salaam kwa ajili ya kumtafuta Ethan na kwenda naye nchini Marekani.
Hawakujua wangempata wapi lakini kwa kuwa walijua kwamba Ethan alikuwa miongoni mwa watu waliohusudu sana michezo ya kamari, wakataka kuhakikisha wanatembelea sehemu zote za michezo hiyo na kumkamata.
Hawakutakiwa kurudi nchini Marekani pasipokuwa na Ethan mikononi mwao, walitakiwa kufanya juu chini mpaka mwanaume huyo anapatikana na kupelekwa nchini Marekani katika mikono ya bwana Cook.
Mawasiliano na Meli ya Mediteranian Cargo iliyokuwa Mombasa yakaanza kufanyika, mara baada ya Ethan kutekwa, hakutakiwa kupelekwa Marekani kwa ndege, alitakiwa kubebwa kwenye meli kiusalama zaidi.
Hilo halikuwa tatizo, nahodha alipopewa taarifa hiyo tu, akageuza meli hiyo ya mizigo na safari ya kuelekea nchini jijini Dar es Salaam kuanza. Kwa ujumla, kila kitu kilikamilika, kutokana na fedha nyingi alizokuwa nazo, alifanya chochote alichokitaka, hata baadhi ya viongozi wa serikali ya Marekani walikuwa chini yake.
*****
Hakukuwa na kitu alichokuwa akikipenda katika maisha yake kama kucheza kamari. Hakuanza kipindi hicho, tangu alipokuwa kijana mdogo aliyeishi katika mtaa wa kimasikini wa Manhattan, Ethan alikuwa mtu wa kushinda vijiweni na kucheza kamari tu.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, haikujalisha kama alikuwa na fedha au hakuwa nazo, alifilisika au la, kitu alichokuwa akikifanya pasipo kujihukumu moyoni mwake kilikuwa ni kucheza kamari tu.
Kila nchi aliyokwenda, kitu cha kwanza kilikuwa ni kupanga hoteli zilizokuwa na cassino ili humo ndani aweze kucheza kamari kama kawaida yake. Kwenye kamari hizo, alikuwa akila sana lakini kuna wakati mwingine aliliwa mpaka kuhisi kufakufa.
Hapo New Africa hotel alipofikia, kulikuwa na ukumbi mkubwa ambao ulitengwa kwa ajili ya cassino, ndani yake kulikuwa na michezo mbalimbali ya kamari. Alipofika hotelini hapo siku ya kwanza, kitu alichokifanya hata kabla ya kula, ni kwenda cassino na kuangalia ni jinsi gani watu walikuwa wakicheza kamari hasa kwa kutumia karata ambao Wazungu waliuita Pokker.
Alijitahidi kucheza, alionekana kama mmoja wa vijana waliozaliwa na kipaji cha kucheza mchezo huo tu. Alipofika ndani ya ukumbi huo tayari kwa kucheza mchezo huo, aliwashinda wengi na kujikusanyia kiasi kikubwa cha fedha.
Kwa kipindi kifupi tu akajikuta akiwa mtu maarufu ndani ya cassino hiyo hali iliyomfanya kujiona kuwa bingwa wa mabingwa na kubatizwa jina la Mr Pokker. Wacheza kamari wakaanza kupeana taarifa kwamba kulikuwa na mtu mmoja ambaye alikuja katika Hoteli ya New Africa na kisha kuzama katika cassino iliyokuwa mahali hapo na kucheza kamari, alikuwa moto wa kuotea mbali hivyo mabingwa wengi kukusanyika hotelini humo kuona makali ya huyo mtu aliyekuwa gumzo.
“Anajua kucheza sana Pokker, kuna wengi amewashinda,” alisema jamaa mmoja simuni, alikuwa akizungumza na rafiki yake.
“Anajua kweli?”
“Ni hatari aiseee...unamjua Muingereza aliyetutesa yule kwenye kamari, Phillip Walker?”
“Ndiyo!”
“Amemla!”
“Duuh!”
“Unamjua Mc Regard, yule Mzungu kutoka Belgium?”
“Ndiyo!”
“Amemla!”
“Acha bwana!”
“Ni hatari sana.”
“Sasa hawezi kuja Las Vegas akutane na wakali wake?”
“Ngoja, nitazungumza naye.”
Watu waliotajwa hapo juu walikuwa hatari katika mchezo wa kamari, walijua kucheza kamari na kuweka gumzo kwa watu wengi waliokuwa wakienda katika Cassino mbalimbali jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kucheza kamari.
Hawakuwa wakiishi nchini Tanzania, walikuwa mabaharia ambao kila siku walisafiri kwa meli, walipofika nchi yoyote ile, kazi yao ilikuwa ni kucheza kamari kisha mizigo iliposhushwa au kupandishwa, waliendelea na kazi yao.
Waliwala fedha watu wengi, walikuwa Wazungu wenye uwezo mkubwa wa kucheza kamari, walijitengenezea majina na kuonekana hatari miongoni mwa wacheza kamari mbalimbali mpaka wengi kuogopa kucheza nao.
Pamoja na uwezo wao mkubwa wa kucheza kamari, kwa Ethan hawakufua dafu, wote hao walipokea vipigo mfululizo hali iliyowafanya kupoteza zaidi ya dola milioni moja kila mmoja.
Baada ya kucheza sana kamari na kujitengenezea jina kubwa ndani ya wiki mbili hapo ndipo alipoamua kuhama na kuhamia katika Cassino ya Las Vegas ambapo kuliaminika kuwa na wakali wa kucheza kamari.
Alipofika huko, bado moto wake ulikuwa uleule, aliendelea kuwala fedha zao na kujikuta akiwa biashara, yaani kila alipokuwa akicheza, watu walimpandia hela na kusema kwamba angeshinda, kweli alifanya hivyo.
Vijana wa bwana Cook walipofika nchini Tanzania, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kwenda katika kumbi za starehe kwa ajili ya kumtafuta Ethan kwani kwa jinsi walivyojua ilikuwa ni lazima kumkuta huko kwa kuwa ndiye alikuwa miongoni mwa watu waliopenda starehe katika vijana wote wa bwana Cook.
Walitembelea katika hoteli kubwa kwa lengo la kumtafuta lakini hawakuweza kumpata. Ndani ya wiki mbili nzima kazi yao kubwa ilikuwa ni kwenda huku na kule katika kumbi na hoteli kubwa lakini hawakuweza kumpata mwanaume huyo.
Kikafika kipindi wote watatu wakaonekana kukata tamaa, hawakuona kama wangeweza kumpata Ethan aliyekuwa amepotelea nchini Tanzania. Kuna kipindi wakahisi kwamba inawezekana Ethan hakuwepo nchini Tanzania hivyo walijadiliana kwenda sehemu nyingine kumtafuta hasa katika nchi jirani kama Kenya na Uganda.
“Mnaonaje?” aliuliza Thorn, mmoja wa vijana waliokuwa wametumwa.
“Nadhani twendeni Kenya, haiwezekani tukamkosa sehemu za starehe na wakati tunajua jinsi Ethan alivyo,” alisema Stephen.
“Sawa! Haina tatizo! Twendeni huko hata kesho!”
“Hebu subiri kwanza!” aliingilia Bruno.
“Una wazo?”
“Ndiyo! Kwa nini tusiendelee kumtafuta hapahapa?”
“Ila tumemkosa, na wewe umeona!”
“Bado! Kuna sehemu nyingi tunatakiwa kwenda,” alisema Bruno.
“Hatujakuelewa!”
“Kipi tena hamjanielewa hapo? Kwani tumemaliza sehemu zote?”
“Bado ila......”
“Jamani! Wote tunamjua Ethan kwamba alikuwa mtu wa kupenda starehe, si ndiyo?”
“Ndiyo!”
“Ila mnakumbuka kwamba hata kucheza kamari Ethan alikuwa balaa?”
“Ndiyo! Tena umenikumbusha, nahisi tukianza kumtafuta kwa staili hiyo itakuwa safi,” alisema Thorn.
“Hebu tujaribuni!”
Hawakuwa na jinsi, walikubaliana kwamba waendelee kumtafuta Ethan kama mcheza kamari. Walichokifanya ni kuanza kutembelea kumbi mbalimbali hasa kulipokuwa kwa wacheza kamari wengi kwa lengo la kumpata mtu waliyekuwa wakimtafuta.
Mpaka kufikia kipindi hicho, tayari mwezi ulikuwa umepita lakini bado hawakufanikiwa kumpata Ethan jambo lililowakera sana. Waliwasiliana na bwana Cook na kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea kwamba walikuwa na wazo la kumtafuta katika kumbi mbalimbali za kamari kwani walijaribu kwenda kwenye kumbi za starehe lakini hawakufanikiwa kumpata.
Bwana Cook akakubaliana nao hivyo kuanza kwenda huko. Haikuwa kazi kubwa, usiku hawakulala, muda wao wa kulala ulikuwa mchana, ulipoingia usiku, walikuwa na kazi ya kumtafuta Ethan tu.
Baada ya kukaa kwa kipindi cha miezi mwezi mmoja ndipo waliposikia kwamba kulikuwa na kumbi mbili tu ambazo zilikuwa na wacheza kamari wakubwa, kulikuwa na ile iliyokuwa New Africa na Las Vegas, hivyo wakaanza kwenda huko kwa kuanzia New Africa.
Kabla ya kuulizia, wakaanza kupita katika kila meza ya wacheza kamari wa mchezo wa Pokker na kuanza kuwaangalia wachezaji. Kila mmoja alikuwa makini kabisa kuwaangalia na katika meza kumi na nane zilizokuwa ndani ya cassino hiyo, Ethan hakuonekana kitu kilichowafanya kuuliza.
“Ethan! Who is he?” (Ethan! Ndiye nani?) aliuliza mwanaume mmoja aliyekuwa ameulizwa kuhusu Ethan.
Hapo ndipo walipoanza kumwambia kuhusu mwanaume huyo, walifafanua sana, jinsi alivyokuwa na utaalamu wake wa kucheza kamari lakini mwisho wa siku mtu huyo aliwaambia kwamba hakuwa akimfahamu kwani hapo kulikuwa na wacheza kamari wengi waliokuwa wakifika, hivyo kumfahamu ilikuwa ngumu.
“Tufanye nini?”
“Hebu tuwaulizeni wengine.”
Hapo ndipo wakaanza kuwauliza watu mbalimbali waliokuwa ndani ya cassino hiyo. Jina walilokuwa wakiuliza lilikuwa Ethan kiasi kwamba ilikuwa ngumu sana kwa wengine kumfahamu.
“Unamuulizia mtaalamu wa kucheza kamari hapa?”
“Ndiyo!”
“Unataka kucheza?”
“Kama yupo mkali!”
“Unaweza nikuwekee dau?”
“Kiasi! Kuna wakali kwanza hapa?”
“Wakali wamepungua, wamehamia Las Vegas, kuna mmoja anaitwa Mr Pokker, huyo ndiyo balaa!” alisema mwanaume huyo.
“Hebu kwanza nianze na hawa, nikiwashinda utanipeleka kwa huyo Mr Pokker,” alisema Thorn na kupelekwa kwenye meza iliyojaa wacheza kamari, akapanda dau la dola elfu kumi kwanza kupima upepo.

Je, nini kitaendelea?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Unasuasua sana jamaa yangu..shukrani lakini.
 
Safi sana...

Huyu Annabel mtoto wa mchungaji namfananisha na wa kwenye simulizi fulani hivi, ambae mama yake alikua anatembea na mchungani mpaka kuzalishwa...


Cc: mahondaw
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi na Moja.

Ili kumpata Ethan ilitakiwa kutumia fedha nyingi, wote walikubaliana kwamba Thorn aanze kucheza kamari, hata kama angeliwa sana hilo wasingejari kwani lengo lao mwisho wa siku lilikuwa kumpata mtu wao waliyemfuata nchini Tanzania.
Thorn hakuona hatari kumwaga fedha, alikuwa tayari kwa kila kitu. Alijua kucheza kamari ya Pokker lakini hakuwa na uwezo kama watu wengine ambao walionekana kuwa moto wa kuotea mbali.
Siku ya kwanza aliliwa sana, siku ya pili, hakukubadilika kitu, aliliwa kama kawaida kiasi kwamba akakaa chini na wenzake na kujadili ni kitu gani walitakiwa kufanya kwani hali ilionekana kuwa mbaya kwa upande wao.
“Tuwe wadhamini,” alisema Bruno.
“Kivipi?”
“Tuwe mabosi, kamari zetu ziwe za kuwapandia watu, ila kazi hiyo aifanye Stephen. Kila nikikaa na kufikiria, moyo unaniambia kwamba tutampata huyu mjinga,” alisema Bruno.
“Basi sawa. Kwa hilo hakuna tatizo.”
Wakapanga mipango yao, ilipopangika vizuri, kesho yake wakarudi tena katika cassino iliyokuwa kwenye Hoteli ya New Africa ambapo huko kama kawaida Stephen akaanza kufanya kama alichokuwa ameagizwa.
Kama inavyokuwa katika michezo mingi ya kamari hasa kunapokuwa na ushindani mkubwa huwa kunakuwa na watu wenye kazi ya kuwekeana madau pembeni ndivyo ilivyokuwa ndani ya cassino hiyo.
Wachezaji wanne walijikusanya katika meza moja ambayo walipenda sana kuitumia, pale, Stephen akaanza kazi ya kumwaga fedha huku akimuwekea kila mtu aliyemuona kuwa mkali kwamba angeibuka mshindi katika mchezo huo.
Wakati mwingine alikuwa akiliwa lakini wakati mwingine alikuwa akila. Kutokana na kiasi kikubwa cha fedha alichouwa akikiweka, wengi wakamuonea huruma na kumtaka kubadilisha mazingira kwa kuwawekea watu waliojua kucheza mchezo huo ili apate faida vinginevyo angeliwa kila siku.
“Unaliwa sana fedha zako,” alisema jamaa mmoja, alimsogelea kisiri.
“Daah! Sasa nifanye nini na wakati wachezaji wenyewe wanazingua?” alihoji Stephen.
“Unataka nikuonyeshe chimbo?”
“Itakuwa poa sana.”
“Twende sehemu fulani hivi kwenye Cassino ya Las Vegas, pale kuna jamaa anajua sana mpaka wakampa jina la Mr Pokker, muwekee huyo dau lako, utakuwa tajiri,” alisema jamaa huyo.
“Iko wapi hiyo?”
“Si mbali sana! Una usafiri?”
“Tunaweza kukodi.”
“Haina noma! Twende.”
Hakukuwa na haja ya kuendelea kusubiri mahali hapo, walichokifanya ni kuondoka kwenda huko Las Vegas, njiani, walikuwa wakizungumza kana kwamba walikuwa marafiki wa muda mrefu.
Katika kipindi chote cha safari, jamaa yule aliendelea kumwambia Stephen kwamba huyo jamaa ambaye walikwenda kumuwekea dau alikuwa mtu hatari sana, mtu asiyefungika, aliyekuwa akicheza sana mchezo wa Pokker kana kwamba kauanzisha yeye.
Kutoka Posta Mpya mpaka Upanga hakukuwa mbali sana, walitumia dakika tano tu wakawa wamekwishafika katika cassino kubwa iliyokuwa na umaarufu mkubwa jijini Dar es Salaam. Dereva akapaki gari katika sehemu ya maegesho na kisha watu hao wawili kuteremka na kuanza kuelekea katika Cassino hiyo ilikuwa na ukimya mkubwa kwa nje ila kwa ndani kulifunguliwa na mziki mkubwa ambao haukuwa ukisikika kwa nje.
Wakati wote walipokuwa wakielekea huko, Bruno na Thorn walikuwa kwa nyuma wakiwafuatilia. Hawakujua watu hao walipokuwa wakielekea lakini waliendelea kuwafuata mpaka gari liliposimama nje ya jengo kubwa lililoandikwa Las Vegas Cassino kwa nje.
Hapo ndipo walipogundua kwamba mbali na cassino nyingine nyingi walizowahi kuzitembelea, kumbe kulikuwa na cassino kubwa ambayo hawakudhani kama ingekuwa nchini Tanzania. Wakateremka na kuendelea kuwafuatilia ambapo wakapitia katika mlango mkubwa wa mbele na kisha kuteremka ngazi kwani cassino hiyo ilikuwa chini ya ardhi, hivyo wakaanza kwenda huko.
Walichokikuta, hakikutofautiana na cassino mbalimbali zilizokuwa nchini Marekani. Watu wengi walikuwa wamejazana, kulikuwa na meza zaidi ya thelathini, mbali na kamari ya Pokker, kulikuwa na kamari nyingine
Kulikuwa na idadi kubwa ya wanawake waliokuwa wakicheza utupu kwa kudanndia kwenye vyuma vilivyokuwa ndani ya cassino hiyo ambapo wanaume walikuwa na kazi ya kuwatunza fedha na kisha kuwashikashika tu.
Hawakutaka kufuatilia kitu chochote kile, hawakufika ndani ya cassino hiyo kwa ajili ya kucheza kamari au kuwaangalia wanawake wale, walchokuwa wakikitaka ni kuona mahali alipokuwa akipelekwa Stephen.
“Wako wapi?” aliuliza Bruno.
“Wale kule.”
“Hebu tuwahi wasije wakatupotea, watu wengi sana humu,” alisema Bruno na hivyo kupiga hatua za kasi zaidi.
Safari ya Stephan na mwanaume yule waliishia pembeni ya meza iliyokusanya wacheza kamari wanne waliokuwa wamezungukwa na watu wengi ambao walikuwa wakiufuatilia mchezo waliokuwa wakicheza.
Kila aliyekuwa akicheza kamari ya Pokker alikuwa na miwani myeusi usoni mwake ambayo waliitumia katika kuchungulia karata za wachezaji wengine pasipo kugundulika lakini pamoja na hayo, walitakiwa kuwa makini kutokana na miwani ile kuonyesha taswira ambayo ingezifanya karata zao kuonekana kwa wachezaji wengine.
“Unamuona yule?”
“Yupi?”
“Yule wa upande ule!”
“Aliyevaa miwani mikubwa?”
“Hapana! Yule wa pembeni yake.”
“Namuona! Ndiye nani?”
“Yule ndiye Mr. Pokker, ndiye mtaalamu mwenyewe wa kumuwekea hela. Hata wale watu waliokuwa nyuma yake, wamemuwekea yeye,” alisema jamaa yule.
Alichokifanya Stephen ni kumwangalia vizuri mwanaume yule aliyeonyeshewa, sura yake haikuwa ngeni kabisa, alionekana kushtuka lakini alitaka kujihakikishia zaidi kama ndiye yule aliyekuwa akimfahamu au alikuwa mtu mwingine.
“Ethan!” alisema Stephen mara baada ya kumuona vizuri mwanaume huyo.
Mapigo yake ya moyo yakamdunda mno, hakuamini kama mwanaume aliyekuwa akimwangalia kwa wakati huo alikuwa Ethan, mtu waliyekuwa wamemtafuta sana. Hakutaka kumwangalia kwa mbali, alitaka kujihakikishia kama alikuwa mwenyewe au alimwangalia kiwange, akasogea zaidi kule, Ethan hakuweza kumuona kwani muda wote macho yake yalikuwa kwenye karata tu.
“Ndiye yeye!” alisema Stephen huku akionekana kushtuka mno. Alichokifanya ni kugeuka nyuma ambapo macho yake yakatua kwa mwenzake waliokuwa wakimwangalia, hapohapo akawapa ishara ya kuangalia kule alipokuwa akiangalia, nao, wakamuona Ethan, mioyo yao ikafurahi, ikarukaruka kwa furaha, kazi kubwa waliokuwa nao, waliona ikiwa imekamilika.
*****
Mtu waliyekuwa wamemfuata nchini Tanzania, alikuwa mbele yao akiwa bize kucheza kamari ya karata. Walimwangalia huku wakati mwingine wakitaka kupata uhakika juu ya kile walichokuwa wakikiona, walichokifanya ni kumsogelea, wakaamini kwamba alikuwa yeye.
Wakashusha pumzi ndefu, wakafurahia kile walichokuwa wamekiona. Hawakuamini kwamba baada ya kipindi kirefu kupita hatimaye walikuwa wamefanikiwa kumpata mwanaume huyo aliyekuwa bize, hakuangalia hata pembeni, macho yake, muda wote yalikuwa yakiziangalia karata tu.
“Ndiye yeye! Kwa hiyo tumfuate?”
“Hapana! Hatutakiwi kuwa na presha, hapa ni cassino, lazima ukumbuke hilo,” Thorn alimwambia Bruno aliyeonekana kuwa na presha.
Walichokifanya ni kwenda pembeni, wakaanza kumfuatilia Ethan pasipo kugundulika, muda ulikuwa ukienda, walimwangalia jinsi alivyokuwa akicheza, kazi yake kubwa ilikuwa ni kukusanya hela kwani watu wote waliouwa wakikaa, aliwafunga kana kwamba alikuwa akicheza na watu wasiojua.
Ilipofika saa kumi alfajiri, Ethan akainuka, akachukua fedha zake na kuagizwa dereva aletwe mule ndani tayari kwa kuondoka, hakutaka kuzibeba fedha hizo bali alichokifanya ni kuziingiza kwenye akaunti zake kupitia kwa mtu wa mahesabu aliyekuwa hapo ndani, kiasi alichobaki nacho ni shilingi laki tano kwa ajili ya matumizi yake tu.
Dereva alipoletwa, akatoka naye na kwenda nje ya cassino hiyo ambapo huko akachukua teksi na kuondoka pasipo kujua kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wakimfuatilia, walichotaka kujua ni mahali alipokuwa akiishi.
Waliendelea kuifuata teksi ile mpaka ilipofika katika Hoteli ya New Africa ambapo Ethan akateremka na kuelekea ndani. Wakaridhika, kwa kuwa walihitaji kuwa naye karibu zaidi, walichokifanya ni kuteremka.
“Kumbe alikuwa akiishi katika hoteli tunayoishi...daaah!” walishangaa kwani nao walichukua vyumba ndani ya hoteli hiyo.
Hawakutaka kuchelewa, walichokifanya ni kuelekea ndani ya hoteli hiyo na kisha kusubiria siku inayofuata ambapo waliamini kwamba ilikuwa ni lazima Ethan kutoka, hapo ndipo wangefanikiwa kumteka na kufanya walichotaka kukifanya, likiwemo suala la kumrudisha nchini Marekani.
Walichokifanya usiku huo ni kuwasiliana na bwana Cook na kumwambia ukweli kwamba tayari walikuwa wamefanikiwa kwani mtu waliyekuwa wameagizwa walifanikiwa kumuona na hivyo kilichokuwa kimebaki ni suala lao la kumteka na kumrudisha nchini Marekani.
“Mnajua kwamba meli imekwishafika huko?”
“Ndiyo bosi! Tulipewa taarifa.”
“Basi jueni mnaosubiriwa ni nyie tu, niwape muda gani?”
“Kama siku mbili, utapata majibu.”
“Sawa. Hakikisheni mnafanya kazi kwa wakati.”
“Hakuna tatizo bosi.”
Walichokifanya siku iliyofuata ni kuanza kumfuatilia mwanaume huyo. Wala haikuwa kazi kubwa sana kwa kuwa walikuwa katika hoteli moja. Alichokifanya Bruno ni kukaa kwenye makochi ya mapokezi na kuanza kumsubiria Ethan ambaye ilipofika saa sita mchana, akatoka huku akizungumza na simu.
Alichokifanya ni kuwashtua wenzake ambao wakatokea mahali hapo na kuanza kumfuatilia kwa nyuma. Hawakutaka kuwa naye karibu, walimuacha mpaka anafika umbali fulani na ndipo nao wakachukua teksi na kuanza kumfuatilia.
Walihisi kwamba kulikuwa na sehemu alipokuwa akielekea, hawakujua ni wapo na alikuwa akifuata nini huko. Hawakutaka kuacha, kwa sababu walikuwa wamedhamiri kumfuata, waliendelea kusonga mbele.
Walimfuatilia mpaka alipofika Gongo la Mboto ambapo mbele kabisa kama kilometa tatu wakafika Pugu Kajiungeni ambapo hapo kulikuwa na barabara iliyokata kushoto ambayo ilikuwa ikielekea Chanika na nyingine ilikuwa ikinyooka, huko ndipo kulipokuwaKisarawe.
“Where is he going?” (Anakwenda wapi huku?) aliuliza Thorn.
“I don’t know, ask him,” (Sijui! Muulize) alijibu Bruno, akimaanisha amuulize dereva ambapo Thorn akafanya hivyo.
“Kisarawe...”
“Okey!”
Safari ilikuwa ndefu lakini hawakukuwa na mtu aliyetaka kusimama, waliendelea mbele kwa kuamini kwamba ilikuwa ni lazima wampate mwanaume huyo na hivyo kumteka na kurudi naye nchini Marekani.
Katika njia hiyo waliyokuwa wakipita, kulikuwa na nyumba chache mno ambazo zilionekana kuwa mpya na nyingine zikiwa zinaendelea na ujenzi. Barabara haikuwa nzuri, hakukuwa na lami, hali iliyokuwepo ilionyesha kabisa kwamba wakati wa mvua kali, barabara ile ilichimbika sana.
Waliendelea mbele, walikuwa wakipandisha milimani, idadi kubwa ya minara ilikuwepo huko Kisarawe, kila mmoja alionekana kubabaika kwani kwa jinsi umbali ule ulivyokuwa, walifikiria jinsi hali itakavyokuwa endapo mafuta yangewaishia.
Waliendelea kumfuata mpaka alipofika sehemu iliyokuwa na nyumba nyingi nzuri, wakaona gari lile likisimama nje ya jumba moja kubwa kisha Ethan kumlipa dereva yule kiasi cha fedha alichotaka na kuingia ndani.
Nao hawakutaka kuendelea na safari, walichokifanya ni kuteremka na kuanza kuelekea katika nyumba ile ambapo Ethan alikuwa ameingia. Walichokipanga ni kumvamia kisha kumteka, hawakutaka kusikia kitu chochote kile, maelezo waliyokuwa wamepewa ni kumteka mwanaume huyo tu, maelezo mengine yangeelezwa mbele ya safari.
Walipolifikia geti kubwa la nyumba ile, wakatoa bastola zao na kuzishika vilivyo kisha kuanza kugonga geti lile. Walijifanya kuwa watu wema na hata ugongaji wa geti hilo ulikuwa ni wa kistaarabu sana, baada ya dakika moja, geti likafunguliwa na msichana, alikuwa Annabel.
“How are you!” (Habari yako!) alimsalimia Thorn.
“Cool! What can I help you?” (Salama! Niwasaidie nini?)
“We want the man who got in here,” (Tunamtaka mtu aliyeingia humu ndani) alijibu Thorn huku akiachia tabasamu pana.
“Who? Nobody got in here!” (Nani? Hakuna aliyeingia) alisema Annabel.
Hawakufika pale kupoteza muda, walikuja kwa ajili ya kufanya kazi moja tu, kumchukua mtu wao na kuondoka naye. Walichokifanya ni kumsukumia Annabel ndani kisha kuingia. Hawakutaka kumuacha mahali hapo kwa kuhisi kwamba angeweza kutoa taarifa kwa watu wengine kwa kupiga kelele, hivyo wakaanza kuondoka naye.
“Let’s get in, don’t shout out,” (Twende ndani, usipige kelele) alisema Thorn huku akionekana kumaanisha alichokuwa akikizungumza. Annabel akawa kimya, hofu ikamjaa moyoni.
Walipoufikia mlango wa kuingia sebuleni, Thorn akausukuma na Annabel kutangulia ndani, kitu kilichoonekana kumshtua hata Annabel mwenyewe, sebuleni hakukuwa na mtu yeyote yule, yaani yule Ethan aliyekuwa amemuacha pale kochini, hakujua alikwenda wapi.
Akapigwa na mshangao!

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumanne.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi na Mbili.

Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilikuwa furaha kwake, hakuamini kama maisha yake yangebadilika na kuwa kama yalivyokuwa, kiasi ambacho kila siku alikuwa akikipata kutoka kwa wacheza kamari wenzake kilimfanya kuashau kabisa majukumu yaliyomfanya kuwa nchini Tanzania.
Alipokuwa akiishi nchini Tanzania, wakati mwingine alijisikia kuwa kama nchini Marekani, alikuwa akipata kila kitu alichokitaka, kuwaona wanawake wazuri na hata kuingiza kiasi kikubwa cha fedha, kwa kifupi, hakuwa na mawazo ya kurudi nchini Marekani, na hata ile kazi aliyokuwa amepewa, hakutaka kuendelea nayo tena.
Mara baada ya kuamka kutoka usingizini, kitu cha kwanza kabisa kilichokuja kichwani mwake ni msichana Annabel tu. Alimpenda mno binti huyo, alimthamini na hakuwa tayari kuona akimpoteza mikononi mwake, alichokuwa amekipanga kwa wakati huo ni kumfuata nyumbani kwao tu.
Akachukua simu yake na kumpigia kisha kumpa taarifa kwamba alikuwa akianza safari kuelekea nyumbani kwao. Alibaki akizungumza naye mpaka alipodhuka mapokezi ambapo akaacha funguo na kisha kuondoka.
Nje, akachukua teksi na safari kuanza. Ilikuwa safari ndefu, kila siku alikuwa akiitumia teksi hiyohiyo kwa ajili ya kumpeleka Kisarawe. Muda wote huo, Ethan hakujua kama alikuwa akifuatiliwa, magari yote aliyoyaona nyuma, hayakumtia wasiwasi hata kidogo.
Walipofika Gongo la Mboto, wakaunganisha, walipoanza kuchukua barabara ya kuelekea Kisarawe, kwa mbali nyuma yake aliliona gari moja ndogo, hakuwa na wasiwasi nalo hata kidogo.
Baada ya kupita ile njia ya kuelekea Chanika, alipoona lile gari likizidi kuwafuata hapo ndipo alipoanza kuwa na wasiwasi kwamba inawezekana gari lile lilikuwa likiwafuata wao. Alichokifanya ni kumwambia dereva aongeze mwendo, nalo likaongeza.
Walipofika, akateremka na kuangalia nyuma kiwizi, aliliona gari lile likisogea taratibu na kisha kusimama, mpaka hapo alikuwa na uhakika kwamba watu waliokuwa ndani ya lile gari walikuwa wakimfuatilia, alichokifanya ni kumlipa dereva fedha zake kisha kwenda ndani huku akijifanya kutokuwa na wasiwasi.
“Nisikilize,” alisema Ethan mara baada ya kuingia ndani.
“Kuna nini?” aliuliza Annabel.
“Kama kuna yeyote atakuja kuniulizia, mwambie sipo,” alisema Ethan.
“Nani anakuja kukuulizia?”
“Wewe fanya kama nilivyokwambia.”
“Kwani ku...” alitaka kuuliza Annabel lakini hata kabla hajamalizia swali lake, akasikia mlango ukigongwa, Ethan akakaa kochini.
“Fanya kama nilivyokwambia.”
“Kwani ni nani?”
“Hatuna muda Annabel, fanya kama nilivyokwambia,” alisema Ethan huku akijiweka sawa kochini.
Annabel hakujali sana, alichokifanya ni kutoka nje na kisha kuelekea kule getini. Ethan akasimama na kuchungulia dirishani, alitaka kufahamu ni nani alikuwa akimfuatilia. Mara akaona Annabel akisukumiwa ndani kisha wanaume watatu kuingia, alikuwa akiwafahamu vilivyo.
“Thorn....” alisema Ethan, hapohapo akajua kilichokuwa kikiendelea.
Hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka sebuleni pale na kuelekea bafuni, alitaka kuruka kupitia katika kidirisha kidogo kisha kuelekea nje. Bafuni hapo, alikiangalia kidirisha hicho, kilikuwa kidogo mno, alichokifanya ni kutoka na kuelekea jikoni.
Kila kitu alichokuwa akikifanya, alikifanya kwa harakaharaka, alipofika jikoni mlango haukuwa umefungwa, hivyo alichokifanya ni kuuparamia ukuta na kurukia nje, akaanza kukimbia, hakujua alipokuwa akielekea, alichokiomba ni kukutana na usafiri wowote ule, hasa pikipiki.
*****
“Where is he?” (Yupo wapi?) aliuliza Thorn kwa sauti kubwa.
“Who is he?” (Ndiye nani huyo?)
“I give you the last chance, tell us where he is by now,” (Ninakupa nafasi ya mwisho, tuambie yupo wapi sasa hivi) alisema Thorn huku akionekana kukasirika.
Bado msichana Annabel hakutaka kuwapa jibu walilokuwa wakilitaka na badala yake alikuwa akiwauliza walimzungumzia nani kwani ndani mule alikuwa peke yake. Kila mmoja alikasirika, hawakutegemea kupata majibu kama yale, alichokifanya Thorn ni kukoki bastola yake.
Annabel hakuonekana kuhofia kitu chochote kile, hata alipowekewa bastola kichwani, bado aliendelea kuuliza watu hao walikuwa wakimzungumzi nani kwani humo ndani hakuwa na mtu yeyote zaidi yake, sasa wao walikuwa wakimuulizia nani?
“Unatuletea jeuri siyo!”
“Jeuri gani sasa? Nyie mnamuulizia nani?”
“Ethan!”
“Ndiye nani?”
“Mbona unamchelewesha Thorn! Hebu ngoja nikuonyeshee dawa ya kiburi,” alisema Bruno huku akichukua bastola yake, kwa mbali Annabel akaanza kuhofia kwani kwa jinsi Bruno alivyoonekana, hakuwa mtu wa kuletewa utani.
Bruno hakutaka kuchelewa, alionekana kuwa mwenye hasira mno, kitendo cha msichana Annabel kuwajibu kile alichokuwa akiwajibu kilimkasirisha mno. Alikuwa tayari kumpiga risasi kwani alileta jeuri na wakati walijua kwamba alifahamu kila kitu.
“Subiri kwanza Bruno.”
“Hatuna muda wa kupoteza Thorn, hataki kusema, unahisi tunatakiwa kufanya nini? Hakuna, bora tumuue tu,” alisema Bruno.
“Usiwe na wasiwasi, huyu ndiye wa kutuletea mtu huyo,” alisema Thorn.
Walichokifanya ni kumchukua Annabel na kisha kuondoka naye nyumbani hapo, japokuwa msichana huyo alikuwa akililia aachiwe lakini hawakutaka kufanya hivyo. Walichokuwa wakikifahamu ni kwamba lingekuwa jambo jepesi sana kwa Ethan kuwafuata kule walipokuwa endapo tu wangemwambia kwamba walikuwa na msichana huyo.
Wakatoka nje ambapo wakachukua gari lile walilokuja nalo na kuondoka mahali hapo. Njiani, Annabel aliendelea kulia, alitaka aachiwe ili arudi nyumbani kwani aliendelea kusisitiza kwamba hakuwa amemuona mtu aliyekuwa ameuliziwa.
“Hakuna tatizo, wala usijali, kuna kazi kubwa tunataka kufanya naye,” alisema Thorn.
Walikwishaambiwa kwamba tayari meli ile iliyotakiwa kumchukua Ethan ilikuwa imekwishawasili jijini Dar es Salaam hivyo wakaanza kuwasiliana na nahodha ambaye aliwaambia mahali alipokuwa amepaki, bandarini na kwenda huko.
Walichukua muda wa masaa mawili mpaka kufika, wakamchukua Annabel na kumuingiza ndani ya meli na kuwekewa ulinzi mkali. Msichana huyo alilia na kulia huku akitaka aachwe lakini hakukuwa na mtu aliyemsikiliza, walichokuwa wakikitaka ni kumuona Ethan akijisalimisha tu.
“Jamani! Kwani nimefanya nini?” aliuliza Annabel.
“Haujafanya kitu, tumejisikia tu kukuteka,” alisema Thorn huku akiachia tabasamu pana.
“Naomba mniache niondoke, naomba mniache.”
“Kivipi? Hatujamaliza kazi yetu, hauwezi ukaondoka mpaka tumpate mtu tunayemtaka, wewe si umekataa kumtaja, sawa, hakuna tatizo, utakaa mpaka atakapopatikana, asipopatikana, tunakutupa baharini,” alisema Thorn huku uso wake tu ukionyesha nijinsi gani alikuwa akimaanisha alichokuwa akikizungumza.
Annabel hakutaka kuzungumza ukweli, kila alipoulizwa kuhusu Ethan alisema kwamba hakuwa akimfahamu mwanaume waliyekuwa wakimuulizia. Ethan hakutaka kujali sana, kwa kuwa msichana huyo alipinga kwamba hakuwa akimfahamu, walichokifanya ni kumfungia ndani ya chumba kilichokuwa na giza nene.
Kilikuwa ni chumba kilichokuwa na mateso makali, pamoja na giza lililokuwemo ndani humo lakini pia sakafu yake ilikuwa na unyevuunyevu huku kwa mbali zikisikika sauti za panya zilizomfanya Annabel kuogopa mno.
Alilia sana, hakujua ni kitu gani kingetokea, hakujua ni jinsi gani angeweza kujikomboa na kuondoka katika chumba kile kilichokuwa na giza nene. Alilia siku nzima, si Thorn wala wenzake waliokuja kumjulia hali, walimuacha mulemule chumbani akiendelea kuteseka.
“Umeshinda usiku mzima ndani ya chumba hiki, hii ni saa tisa usiku,” alisema Thorn, aliufungua mlango huo huku akiwa na tochi mkononi. Annabel alikuwa akilia tu.
“Sikiliza, tunahitaji tumpate Ethan, unaweza kutusaidia katika hilo?” aliuliza Thorn.
“Simjui, sijawahi kumuona mwanaume huyo.”
“Sawa. Hakuna tatizo,” alisema Thorn na kuufunga mlango.
Watu hao walikuwa wabaya, walionekana kuwa watu wenye roho mbaya, alijua fika kwamba walimtaka Ethan kwa kuwa walitaka kumuua. Hakutaka kuona hilo likitokea, hakutaka kuona mwanaume aliyekuwa akimpenda akiuawa kwa kuwa tu alitaja mahali alipokuwa.
Moyo wake uliumia, alipata mateso makali kwa sababu ya mapenzi tu, gharama ya kupenda ndiyo iliyomfanya siku hiyo kuwa katika hali hiyo. Aliteseka, usiku kucha hakulala, alibaki akilia tu huku matumaini ya kutoka ndani ya chumba hicho yakiwa madogo. Wakati akiwa kwenye indi la mawazo, mlango ukafunguliwa, tayari ilikuwa saa moja asubuhi ila kama kawaida chumba hicho kilikuwa na giza nene.
“Utatuambia yupo wapi?” aliuliza Thorn.
“Nani? Mimi simjui mtu yeyoteyule,” alisema Annabel.
“Sawa,” alisema Thorn na kufunga mlango ule. Annabel akaanza kulia kwa sauti kubwa.

Kwa wale ambao wanahitaji kuimalizia haraka wanaweza kuja WhatsApp kwa namba 0718069269 kuinunua kwa sh. 2000 mpaka mwisho.

Namba ya kutuma pesa 0763986156. Kwa ambao hawana...tuendelee kuisubiri hapahapa.

Itaendelea Ijumaa.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI.
BIASHARA YA KIFO.
0718069269.

Sehemu ya Tano..

“Ethan, stop,” (Ethan, acha) ilisikika sauti ya mama yake kutoka nyuma.
Ethan hakutaka kuiachia bastola ile, alikuwa amedhamiria kumuua baba yake wa kambo, hakumpenda kabisa, alimchukia mno, kitendo cha kumuona kila siku katika maisha yake kilimkasirisha.
Alijiandaa kumfyatulia risasi na kumuua kabisa, lakini hata kabla hajafanya hivyo, mama yake akamsogelea na kisha kumzuia kubonyeza kitufe cha bastola ile. Hiyo ikaonekana kuwa bahati ya mtende kwa mzee George, kwa jinsi alivyomwangalia Ethan, alikuwa amedhamiria kumuua kabisa.
Ethan akaondoka mahali hapo, kundi lile la watu lililokuwa limewazunguka nao likaondoka kuendelea na kazi zao kama kawaida.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, alichukiwa na kila mtu kwa kuwa alikuwa mtemi, japokuwa alikuwa na miaka kumi na sita lakini tayari Ethan alijifunza maisha ya mitaani hasa ya kutumia bastola katika maisha yake.
Alikuwa mtu wa fujo, alijulikana sehemu kubwa hapo Manhattan huku akianzisha kundi lake kubwa la kihuni lililojulikana kama The Mobb. Lilikuwa na vijana ishirini, walioshindikana katika maisha yao, walikuwa watumiaji wazuri wa bastola, walikuwa wavuta bangi na hata wakati mwingine kutumia madawa ya kulevya.
Walikuwa vijana wadogo lakini wale ambao hawakuwa na huruma hata kidogo. Polisi wa hapo Manhattan waliliogopa kundi hili, hawakuyathamini maisha yao, kwao, kupigwa risasi na kufa lilikuwa jambo jema tu kwani waliamini kwamba kulikuwa na mungu wao wa kisela ambaye angewapokea na kuwaingiza katika mbingu yao iliyokuwa na makontena makubwa ya madawa ya kulevya na bangi.
Wakati kundi hilo likiendelea kukua, likiwapiga watu na hata wakati mwingine kuwaua, hapo ndipo walipotumwa polisi waliokuwa na hasira, polisi waliotoka nje ya Manhattan kwa ajili ya kufanya jambo moja tu, kuwakamata vijana hao na hata kama wataleta ubishi au kufanya chochote kilicho kibaya cha kuhatarisha maisha yao, basi wawaue.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kumaliza magenge hayo, vijana wengi walikamatwa na kufungwa gerezani lakini kwa Ethan, akatoroka jijini New York na kuhamia Washington DC ambapo maisha yake yakaendelea.
Hakutaka kuwa mhuni kama alivyokuwa, hakutaka kufanya usela wa mitaani alichokifanya kwa wakati huo ni kujikita katika uuzaji wa madawa ya kulevya kwa kuyasafirisha sehemu moja kwenda nyingine.
Hapo ndipo alipokutana na wale watu aliokuwa akiwasikia kwamba walikuwa wauzaji wazuri wa madawa ya kulevya na walikuwa watu wenye kuogopwa sana. Alipofikishwa kwa mzee mmoja aliyekuwa na asili ya Mexico, mzee Sanchez El Paso, akamchukua na kumfanya mfanyakazi wake ambaye kazi yake kubwa ilikuwa ni kusafirisha madawa nchini Marekani.
“Ukifanya kazi na mimi, utakuwa tajiri mno,” alisema mzee Sanchez.
“Nitatajirika vipi?”
“Utafahamiana na watu wengi, nisingependa ufanye kazi kwangu milele, pia ningependa baadaye ufanye kazi wewe kama wewe,” alisema mzee Sanchez.
“Ili nifikie ndoto ya kufanya biashara zangu mwenyewe, natakiwa kufanya nini?”
“Kujitoa kazini, hakuna cha zaidi, ila epuka sana wizi, ukiiba na kugundulika, nitakuua,” alisema mzee huyo maneno yaliyomtia hofu mkubwa.
“Siwezi kufanya hivyo! Umenitoa mbali, hakika nitaendelea kukuheshimu na sitokufanyia ujinga,” alisema Ethan.
Alimheshimu mzee huyo kwa kuwa ndiye aliyekuwa akimfanyia mambo mengi na kukutana na watu ambao hakutegemea kukutana nao katika maisha yake. Kila siku alikuwa mtu wa kutoka, hakutulia sehemu moja, leo alikuwa akienda California, kesho Texas na kesho kutwa sehemu nyingine.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake, kila siku alikuwa akibadilisha muelekeao wake ambapo kote huko kazi kubwa aliyokuwa akiifanya ni kusafirisha madawa ya kulevya tu. Jina lake likaanza kukua, mnyororo mkubwa aliokuwa nao mzee Sanchez ukamsaidia mno na hata katika viwanja vya ndege mbalimbali hakuwa akipata usumbufu wowote ule.
“What do you want?” (Unataka nini?) aliuliza mzee mmoja.
“What do I want? What do you mean?” (Nahitaji nini? Unamanisha nini?)
“For how long have you been doing this work?” (Kwa kipindi gani umekuwa ukifanya kazi hii?)
“Three years?” (Miaka mitatu)
“Ok!” (Sawa)
Alikuwa akizungumza na mzee mmoja aliyekuwa amekaa naye ndani ya ndege. Hakujua ni nani alimwambia kuhusu biashara ya madawa ya kulevya aliyokuwa akiifanya, mzee huyo alianza kumuuliza maswali mengi kiasi kwamba akaanza kuogopa kwani hata humo ndani ya ndege alipokuwemo, alikuwa na mzigo mkubwa aliokuwa akiupeleka Los Angeles.
“Lakini wewe ni nani?” aliuliza Ethan huku akionekana kushikwa na hofu.
“Ninaitwa Boyle Cook,” alijibu mzee yule.
“Umejua vipi kama ninafanya kazi hii?”
“Hauwezi kunificha, ninawajua kwa kuwaangalia, umekuwa na amani katika kufanya kazi hii?” aliuliza bwana Cook.
“Kiasi, si sana, wakati mwingine unakuwa na hofu kubwa.”
“Utakuwa tayari kama nikikupa kazi nyingine, nzuri tu?”
“Kazi gani?”
“Ninataka uwe na amani, siwezi nikakupa kazi ngumu. Niambie, upo tayari?” aliuliza bwana Cook.
“Mmmh!”
“Usijali! Chukua hii, ukiwa tayari niambie,” alisema bwana Cook na kisha kumpa business card yake iliyokuwa na mawasiliano yote.
Mpaka kufikia hatua hiyo Ethan alichanganyikiwa, alikuwa akimwangalia mzee huyo mara mbilimbili, hakumfahamu alikuwa nani, hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza kukutana naye, tena walizungumza kwa muda mchache kabla ya mzee huyo kubaki kimya mpaka ndege ilipotua Jijini Los Angeles na kisha kuteremka.
Hawakuzungumza chochote kile, kila mmoja akaendelea na kazi zake zilizomleta ndani ya jiji hilo la starehe. Ethan akaondoka na kupeleka mzigo alipoelekezwa kwani hata kuutoa pale uwanja wa ndege hakukuwa na kazi kubwa kwani kila kitu kiliwekwa tayari.
Kichwa chake kikawa na maswali mengi, alikuwa akijiuliza kuhusu mzee yule ambaye alionekana kumfahamu mno, hakuishia hapo, aliendelea kufikiria hata ile kazi aliyotaka kumpa, hakujua ilikuwa kazi gani ila alimwambia kwamba endapo angekuwa tayari basi amtafute.
Uuzaji wa madawa ya kulevya ilikuwa biashara mbaya na yenye hatari mno lakini hakutaka kuiacha kwani ilimpa kisasi fulani cha fedha na kuanza kuyabadilisha maisha yake. Alichokifanya ni kumpuuzia bwana Cook na yeye kuendelea na maisha yake kama kawaida ingawa mara nyingi mno alikuwa akijiuliza kuhusu mzee yule na kukosa jibu.
****
Biashara ilimwendea vizuri, japokuwa hakuwa bosi lakini kwa kiasi fulani kila kitu kilikwenda kama alivyokuwa akitaka. Yeye ndiye alikuwa msafirishaji mkuu wa madawa hayo kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
Aliaminika mno kwa kuwa kila mzigo aliokuwa akitumwa ulifika salama mikononi mwa mtu aliyekuwa akihitajika kuupata mzigo huo. Siku zikaendelea kukatika, akaanza kuwa na maendeleo makubwa lakini tatizo lilikuja pale alipoanza kufanya starehe.
Kiasi kikubwa cha fedha alichokuwa akikipata kutoka katika biashara zile, alikiweka katika mstari wa starehe zake. Kila siku Ethan alikuwa mtu wa kubadilisha wanawake na kubadilisha viwanja kiasi kwamba kiasi cha fedha alichokuwa akikipata wakati mwingine hakikutosha kabisa.
Alisahau alipotoka, alisahau kama kule Manhattan alipokuwa kulikuwa na rundo la watoto masikini, watu wasiojiweza ambao kila siku maisha yao yalikuwa pembeni ya mapipa ya takataka. Alisahau kila kitu, aalichokuwa akikifanya kwa wakati huo kilikuwa ni starehe tu.
Wanawake walimopapatikia kwa kuwa hakuwa mchoyo, alichokuwa akikipata aligawana nao na hivyo kutengeneza jina kubwa masikioni mwao. Siku zikakatika na kukatika mpaka pale aliposikia taarifa kwamba bosi wake aliyekuwa akimuweka mjini, bwana Sanchez alikuwa hoi kitandani.
Kilichomlaza kilikuwa ni saratani ya damu, alikuwa akiugua kila siku kwa kutokwa na damu puani na mdomoni. Ugonjwa huo ulimuanza kwa kasi hali ambayo ilimfanya kupelekwa hospitali ambapo madaktari wakawaambia ndugu zake kwamba asingeweza kupona.
“Hawezi kupona ugonjwa huu, ni lazima afe,” alisema daktari, aliamua kuwaambia ukweli kwamba mgonjwa waliyekuwa wamempeleka ilikuwa lazima afe.
“Hawezi kupona?”
“Hawezi. Ni lazima afe.”
Kansa yake ilisababishwa na ubwiaji mkubwa wa madawa ya kulevya, hakuwa na nafuu hata kidogo walichokifanya ndugu zake ni kumchukua na kumrudisha nyumbani kumuuguza katika kipindi cha mwisho.
Walipomfikisha huko, wakamfungia chumbani kwake. Hawakutaka kumuacha hata kidogo na hawakutaka kumficha juu ya kile alichokisema daktari kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kufa hivyo kama alitaka kufanya vitu vyake kwa mara ya mwisho, alitakiwa kufanya kwa wakati huo.
“Nitagawa utajiri kwa watoto wangu! Niitieni mwanasheria wangu,” alisema bwana Sanchez.
Mwanasheria wake akaitwa na kisha kuandika kile alichotakiwa kuandika, mirathi ikagaiwa kwa watoto wote. Kitu ambacho hakukiamini Ethan ni kwamba hakukuwa na mali yoyote aliyoachiwa japokuwa yeye alikuwa mtu wa karibu sana na mzee huyo.
Bwana Sanchez alipofariki hapo ndipo maisha yalipomgeukia, akaanza kurudi kule alipotoka, bisahara zikakata, mitego yote aliyokuwa ametega ikaharibika vibaya, marafiki zae ambao kila siku alifanya nao starehe wakamkimbia kwani waliona kwamba hakuwa na kitu tena.
Aliogopa kurudi New York katika mtaa aliozaliwa kwa kuhisi kwamba bado alikuwa akitafutwa sana, hivyo alichokifanya ni kukimbilia Texas, sehemu iliyokuwa na mpaka mkubwa wa kuingilia nchini Mexico.
Huku akiwa huko ndipo alipokumbuka kwamba mara ya mwisho alikutana na mzee mmoja ndani ya ndege ambaye alimwambia sana kuhusu biashara ile ya madawa kwamba haikuwa nzuri hivyo alitakiwa kuachana nayo.
“Namba yake niliiweka wapi?” alijiuliza.
Hicho ndicho kilichomuumiza kichwa wakati huo, hakukumbuka mahali alipoihifadhi namba ile, alikumbuka vilivyo kwamba alipewa na kurudi nayo nyumbani, baada ya hapo, hakukumbuka aliiweka wapi kwani kilipita kipindi kirefu mno na hata kumbukumbu zake zikawa zimepotea kabisa.
“Nilirudi nyumbani nikiwa nacho, nikakaa kitandani, baada ya pale nilikiweka wapi? Mhh! Hapana! Mbona sikumbuki vizuri?” alijiuliza lakini akakosa jibu.
Aliendelea kupigika mitaani, maisha yakampiga sana. Alipoona kwamba kila kitu kinakwenda kombo hapo ndipo alipoingia katika biashara ya kuuza magari, yaani walikuwa wakiiba magari nchini Marekani, wanayapitisha kwa njia za panya kuelekea Mexico na kuyauza huko.
Hakuwa na jinsi, japokuwa ilikuwa ni kazi ya hatari iliyohatarisha maisha yake lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kupambana ili atoke katika umasikini mkubwa uliompigia hodi mlangoni.
“Ushawahi kuiba Lambonghin?”
“Hapana!”
“Sasa leo tunakwenda kuiiba, kama tukifanikiwa, sisi matajiri,” alisema jamaa yake, walikuwa wezi wakubwa hapo Texas.
“Hakuna noma, ila hatuwezi kukamatwa?”
“Tutakamatwa vipi? Kama tumewahi kuiba magari zaidi ya mia tano, tutakamatwaje kwa gari moja?” aliuliza rafiki yake huyo.
“Basi sawa. Lipo wapi?”
Huo ndiyo mpango waliopanga siku hiyo, walitaka kuiba gari ya thamani na kisha kuisafirisha kwa njia za panya mpaka nchini Mexico. Kuhusu kuiba, hilo wala halikuwa tatizo kabisa, waliweza kufanya hivyo ila kazi kubwa waliyokuwa nayo mahali hapo ni kulitoa gari hilo sehemu lilipokuwa na kulipeleka huko walipotaka kulipeleka.
Saa mbili usiku wakakutana karibu kabisa na ukumbi mmoja wa starehe, mbele yao kulikuwa na magari mengi lakini miongoni mwa magari hayo, kulikuwa na gari moja la thamani sana lililokuwa na gharama zaidi ya dola mioni tano, zaidi ya bilioni moja, ilikuwa Lambonghin nyekundu iliyoonekana kuwa mpya kabisa.
Walikuwa wazoefu wa kuiba magari, hata kuiba gari hilo wala haikuwasumbua kabisa. Kwa sababu Ethan alikuwa mtaalamu mkubwa wa kuendesha magari, akakaa sehemu ya dereva, kwa kutumia utundu kwa kuunganisha nyaya, wakaunganisha na gari kuwaka, kilichobakia ni sauti za watu huko nyuma.
Hapo ndipo walipoanza safari ya kuelekea mpakani kwa njia za panya ili waweze kuliingiza gari hilo nchini Mexico. Walipanga kwamba huo ndiyo ungekuwa wizi wao wa mwisho hivyo baada ya hapo wangeacha kabisa kwani ilikuwa moja ya kazi ya hatari kabisa kuwahi kuifanya.
“Hivi unakanyaga mafuta kweli?”
“Ndiyo!”
“Upo ngapi hapo?”
“180 kwa saa!”
“Gari mwisho ngapi?”
“400 kwa saa!”
“Sasa hizo nyingine unamuachia nani?”
“Ebwana tutakufa.”
“Kama kufa acha tufe, kuna raha gani ya kuishi, kama kufa tutakufa hata ukiendesha 1 kwa saa, kanyaga moto kaka,” alisema rafiki yake.
Mwendo aliokuwa akiendesha ulikuwa ni wa kasi mno, gari lilikuwa likijiweza kwa kasi hivyo Ethan hakuwa na jinsi, akaanza kukanyaga mafuta mpaka kuhisi kwamba gari hilo lingeweza kupaa.
Kutokana na kuwa usiku mwingi, barabarani hakukuwa na magari kabisa, walitembea kwa mwendo waliotaka tena kwa kasi zaidi na baada ya masaa mawili walitaraji kufika karibu na mpaka huo ambapo wangechukua njia za panya na kuingia Mexico.
Wakati wamebakiza kilometa tatu kabla ya kuingia katika kituo cha mafuta cha Gapco, kwa mbali wakaanza kuyaona magari ya polisi yakiwa yamesimama barabarani huku taa zikiwaka.
Kwanza wakaogopa, kwa kasi waliyokuwa wakienda nayo walijua kwamba endapo wangeyagonga magari yale basi ingekuwa kifo chao hivyo alichokifanya Ethan ni kupunguza kasi na kisha kuchukua barabara nyingine ya vumbi, magari yale ya polisi yakawashwa na kanza kuwafuata.
“Kanyaga mafuta!”
“Haiwezekani! Hakuna lami huku,” alisema Ethan.
Walikwenda na gari hilo kwa umbali mrefu mpaka mafuta yalipowaishia. Hawakuwa na jinsi, wasingeweza kubaki na wakati polisi waliendelea kuwasogelea kule walipokuwa, walichokifanya ni kuteremka na kisha kuanza kukimbia huku wakiwa wamelitelekeza gari lile.
Walikimbia kwa umbali mrefu, mbele kabisa wakakutana na korongo kubwa, lilionyesha kwamba mchana huwa kunakuwa na watu wanaochimba kokoto kutokana na ardhi ya Texas kuwa na kokoto nyingi, walichokifanya ni kuingia katika korongo lile na kuendelea na safari yao.
Hawakutaka kusimama sehemu yoyote ile, walichokuwa wakikitaka ni kufika walipotaka kufika pasipo kugundua kwamba polisi wale wa nyuma walipoona wezi wale kule walipokimbilia, wakawasiliana na polisi wa mpakani na kuwapa taarifa, nao wakaanza kusogea kule walipoambiwa wezi wale walipokimbilia, kwa maana hiyo, kadiri Ethan na rafiki yale walivyokuwa wakipiga hatua, ilikuwa ni sawa na kuwasogelea polisi hao waliotoka mpakani.

Je, nini kitaendelea?

Kwa wanaotaka kujiunga na kundi la simulizi, kuchati kwa sana na kujuana, bonyeza hii link chini, kama hutaki meseji meseji tafadhali usije.

Hadithi na Chattin'

Sent using Jamii Forums mobile app
Mbona inagoma?

Air HOSTAGE
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi na Tatu.

Askofu Benedicto alionekana kuwa na furaha, kila kilichokuwa kikiendelea kilimfurahisha mno. Alimpenda sana binti yake zaidi ya kitu chochote kile, kila alipomuona amekaa sehemu yoyote ndani ya nyumba yake, alimfuata na kukaa karibu naye.
Japokuwa alikuwa na mapenzi makubwa kwake lakini kila siku alikuwa mkimya, msiri mkubwa ambaye hakutaka kumuweka wazi kwamba alikuwa askofu baada ya kupitia upadri kwa kipindi kirefu.
Siku hii, alikuwa akitoka nyumbani kwake, alijaribu kumpigia simu Annabel na kumpa taarifa kwamba alikuwa njiani, tatizo likatokea kwamba msichana huyo hakuwa akipokea simu. Alishangaa, haikuwa kawaida hata kidogo, alijua kwamba wakati mwingine binti yake anakuwa bize na mambo mengine, lakini anapoona kwamba alipigiwa simu, ilikuwa ni lazima kupiga ili asikie alitaka kuambiwa nini.
Aliendesha gari kwa kasi huku kila wakati akijaribu tena na tena kumpigia simu lakini majibu yalikuwa yaleuale kwamba simu haikuwa ikipatikana. Alichanganyikiwa lakini hakuwa na jinsi, alijiona kutokufika haraka nyumbani, foleni za kizushi zilizokuwa zikitokea njiani nazo zilimuongezea hasira zaidi.
“Ninakupenda binti yangu, pokea simu,” alisema Askofu huyo huku akiendesha gari kwa kasi.
Ilipofika saa saba mchana ndiyo muda ambao aliingia nyumbani, kama kawaida akateremka na kufungua geti. Aliuzoea ukimya, hata alipoona kukiwa kimya, hakujiuliza sana, akaingia ndani.
Hali ya ndani ndiyo ikamshtua zaidi, ukimya ulikuwa maradufu, televisheni ilizimwa, kitu ambacho haikuwa kawaida hata mara moja, aliopozunguka huku na kule, hakumuona mtu yeyote yule, alichokifanya ni kujaribu kumuita Annabel, majibu yalikuwa yaleyale, ukimya mkubwa ulitawala.
Jina la mtu aliyemjia kichwani lilikuwa moja tu, naye alikuwa Etha, alichohisi ni kwamba inawezekana binti yake alikuwa na mwanaume huyo, hivyo akaanza kumpigia simu. Simu iliita na kuita, haikupokelewa kitu kilichomchanganya sana.
Akashusha pumzi ndefu na kutulia kochini, alionekana kuwa na mawazo mengi mno juu ya binti yake. Huku akijifikiria kuhusu Annabel, mara akasikia simu yake ikiita, alipoichukua na kuangalia kioo, alikuwa Ethan, harakaharaka akaipeleka sikioni.
“Ethan...” aliita.
“Naaam!”
“Upo na Annabel?”
“Hapana! Sipo naye!”
“Yupo wapi?”
“Nyumbani hayupo?”
“Hayupo, sijakuta mtu yeyote yule.”
“Mmmh!”
“Ulikuja nyumbani?”
“Ndiyo, nilifika hapo!”
“Ulimkuta?”
“Ndiyo!”
“Yupo wapi sasa?”
“Naomba tukutane sehemu tuzungumze.”
“Tuzungumze kuhusu nini?”
“Annabel!”
“Yupo wapi?”
“Kuna mengi ya kuzungumza, naomba tukutane tuongee,” alisema Ethan na kukata simu huku akimpa maelekezo juu ya mahali walipotakiwa kuonana.
Askofu akachanganyikiwa, maneno ya Ethan yalimchanganya mno, hakujua ni kitu gani Ethan alitaka kuzungumza naye mpaka kuhitaji kuonana naye. Akatulia kichwani, alichokifanya ni kujaribu kupiga simu ya binti yake, majibu hayakubadilika, yalikuwa yaleyale kwamba simu haikupatikana.
Alichokifanya ni kuondoka nyumbani hapo na kumfuata Ethan kule alipomwambia waonane, alitaka kusikiliza ni kitu gani alitaka kumwambia. Hakutaka kumpa Irakoze taarifa kwani alijua kwamba angechanganyikiwa, alihitaji kumuona kwanza Ethan ili wajue ni kitu gani walitakiwa kufanya.
Alipofika katika Hoteli ya Kilimanjaro, akateremka garini na kuanza kupiga hatua sehemu iliyokuwa na meza nyingi, kulikuwa na mghahawa ambapo hapo akapiga macho huku na kule, yakatua kwa Ethan aliyekuwa akinywa juisi, akaanza kumfuata.
“Kwanza niambie nini kinaendelea,” alisema askofu mara baada ya salamu.
“Subiri kwanza, kuna jambo linaendelea ila tunatakiwa kulifanya kwa umakini sana.
“Jambo gani Ethan? Binti yangu yupo wapi?” aliuliza askofu Benedicto, alionekana kuchanganyikiwa.
“Yupo!”
“Wapi?”
“Ametekwa!”
“Ametekwa! Na nani?”
“Subiri kwanza, usiwe na presha.”
“Ni lazima niwe na presha, ni nani amemteka?”
Ethan hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kumuelezea askofu kile kilichokuwa kimetokea, tangu maisha yake yalivyokuwa mpaka muda huo. Askofu alibaki kimya, alimsikiliza Ethan kwa umakini, alionekana kuwa kijana mpole lakini mambo aliyokuwa akiyaeleezea kwa mzee huyo yalimsikitisha mno.
“Ethan!”
“Ndiyo!”
“Pole sana, ila nitampata vipi binti yangu? Huyo Cook ni nani?” aliuliza askofu.
“Huwezi kumfahamu! Wanaomtaka si binti yako bali ni mimi,” alijibu Ethan huku akimwangalia askofu huyo usoni.
“Nitampata vipi binti yangu?”
“Usijali, utampata, nitakwenda kumuokoa.”
“Naomba ufanye hivyo! Au tukatoe taarifa polisi?”
“Hahah! Huwezi kumpata, wale watu ni hatari, ukitoa taarifa polisi utakuwa unajisumbua tu, ule mtandao wao ni wa kimataifa,” alisema Ethan huku akimwangalia Askofu usoni.
Tumaini la askofu Bonedicto lilikuwa kwa Ethan tu, kila alipokaa alikuwa akimuomba kumsaidia kumpata binti yake tu, hakuwa na uhakika mahali alipokuwa, alitamani kwenda polisi kushtaki, ila kama aangekwenda huko ingekuwaje? Angemtambulisha Annabel kama nani? Binti yake? Lilikuwa jambo lisilowezekana hata mara moja.
“Naomba unisaidie,” alisisitiza aaskofu.
“Usijali, nitafanya hivyo,” alijibu Ethan.
*****
Usiku mzima Annabel alikuwa akilia, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea, alibaki akisononeka sana, hakujua wale watu walimteka walikuwa nani na walihitaji nini. Hapo ndipo maswali mengi kuhusu Ethan yalipoanza kumjia kichwani mwake.
Yule Ethan alikuwa nani? Na kwa nini alikuwa akitafutwa vile, kila alipojiuliza alikosa jibu. Ndani ya chumba kile kulikuwa na mateso makubwa, kitendo cha kukaa mule huku kukiwa hakuna mwanga na hata sakafu kuwa na unyevuunyevu kilionekana kuwa mateso makubwa.
Ilipofika mchana, mlango ukafunguliwa na Thorn kuingia ndani, alionekana kuwa na kitu alichotaka kumwambia Annabel, alichokifanya ni kumuita na kumwambia amfuate, Annabel akafanya hivyo.
Wakaelekea mpaka katika ehemu moja iliyokuwa pembeni kabisa, aliliona jiji la Dar es Salaam huku jengo kubwa la The Prince likionekana pale alipokuwa. Mahali hapo melini alipokuwa amepelekwa, kulikuwa na Wazungu wengine wawili, Bruno na Stephen, akawekwa kati.
“Tunamtaka Ethan,” alisema Thorn, alionekana kuwa na hasira mno. Annabel akanyamaza.
“Ungependa kuendelea kukaa kwenye meli hii zaidi?” aliuliza Bruno.
“Hapana!”
“Basi tuambie Ethan yupo wapi.”
“Aliondoka.”
“Kwenda wapi?”
“Sijajua! Kwani amefanya nini?”
“Hautakiwi kujua. Tunaomba namba yake,” alisema Bruno.
Hilo ndilo walilolitaka, kukaa na Annabel ndani ya meli ile halikuwa lengo lao, walichokita ni kumpata Ethan ambaye mpaka muda huo hawakujua alikuwa wapi. Aliteseka sana, alilia usiku kucha, kitendo cha kuambiwa kwamba ni namba ya Ethan ndiyo iliyokuwa ikihitajika, hilo halikuwa tatizo, akawapa.
“Asante,” alisema Thorn.
Akaichukua ile namba na kisha kuanza kupiga simu. Muda wote huo Annabel alikuwa akitoa kilio cha chini kilichojaa kwikwi, hakutaka kutoa namba ya Ethan lakini kutokana na mateso makubwa aliyokutana nayo ndani ya chumba kile, hakuwa na jinsi.
“Ethan, unazungumza na Thorn, tunakuhitaji wewe kabla ya saa tisa, kama hautofika, huyu msichana hautoweza kumuona tena,” alisema Thorn mara baada ya simu kupokelewa.
“Thorn, nisikilize, huyo msichana hajawafanya kitu, mwacheni aende zake,” alisikika Ethan simuni huku akilalamika.
“Ataondoka utakapokuja.”
“Thorn.....”
“Tukutane kwenye Hoteli ya Kingstar, jirani na hapo ulipo saa kumi jioni, utakaokuja, tutamwacha huru,” alisema Thorn, Ethan akashusha pumzi nzito, hapohapo Thorn akakata simu.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumatatu.

Kwa wanaoitaka yote kwa pamoja waje Whatsapp kwa namba 0718069269 ila waje na 2000.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO
0718069269

Japokuwa Ethan alikuwa na hofu kukutana na Wazungu wale waliokuwa wamemfuata nchini Tanzania lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kuonana nao ili mpenzi wake, Annabel aachwe huru na yeye kufikishwa huko walipotaka kumfikisha.
Kwenda katika Hoteli ya Kingstar halikuwa tatizo na kwa sababu haikuwa mbali na hoteli aliyokuwa amefikia, alihakikisha anafika huko muda aliopangiwa pasipo kuchelewa. Alijua kwamba alifanya kosa kubwa, kitendo cha kufanya kazi ile huku akijua kwamba aliagizwa na ndiyo ilikuwa kazi iliyomuingizia kiasi kikubwa bosi wake, lilikuwa kosa lisiloweza kuvumilika kwa bosi huyo.
Ilipofika saa tisa na nusu alasiri, tayari alikuwa katika hoteli hiyo ambapo baada ya dakika chache Thorn akatokea huku akiwa peke yake kitu ambacho hakikuwa makubaliano yao.
“Vipi?” aliuliza Ethan.
“Vipi nini?”
“Mpenzi wangu yupo wapi?”
“Subiri kwanza! Usiwe na presha.”
“Ninataka kumuona Annabel kwanza, vinginevyo siendi popote pale,” alisema Ethan huku akionekana kumaanisha alichokuwa akisema.
“Usiwe na haraka sana, sikuweza kumleta mahali hapa, inuka tuondoke, hakuna muda wa kupoteza,” alisema Thorn huku akimwangalia Ethan.
“Hapana! Siwezi kwenda popote pasipo Annabel.”
“Kweli?” aliuliza Thorn huku akionyesha bastola iliyokuwa kiunoni mwake.
Hicho ndicho kilichomuogopesha, alimfahamu vilivyo Thorn, alionekana kuwa mwanaume mpole, mwenye tabasamu wakati wote lakini roho yake ilikuwa tofauti na muonekano wake wa nje. Alikuwa mtu aliyependa sana kuua, alipenda kuwatesa watu na hata alipokuwa akipewa amri ya kuua, alilitekeleza suala hilo kwa haraka sana.
Alipoonyeshewa bastola ile, hakuwa na jinsi, hakutaka kukataa, aliamini kwamba endapo angekataa basi kungekuwa na kitu kingine kabisa na inawezekana historia ya maisha yake ikabadilikia hapo, alichokifanya ni kusimama na kuanza kuondoka na mwanaume huyo.
Walizungumza kama marafiki, Ethan hakutakiwa kuonyesha hofu yoyote ile, walipofika barabarani wakachukua teksi na kuanza kuelekea sehemu ilipokuwa boti ndogo ambayo wangeichukua na kuelekea kule ilipopaki meli ile ya mizigo.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika ufukweni, wakateremka na kuanza kuelekea katika boti moja iliyokuwa imepakiwa pembeni, wakapanda na safari ya kuifuata meli iliyoonekana kwa mbali kuanza.
Kichwa cha Ethan kilifikiria mambo mengi, alijiwa na wazo la kutoroka kwa kuzama baharini na mwisho wa siku kupiga mbizi ili aweze kuondoka mikononi mwa Thorn ya watu hao lakini kitu kilichomsumbua moyoni mwake ni uwepo wa Annabel katika mikono ya watu hao tu.
Hakuwa tayari kurudi nchini Marekani, aliyazoea maisha ya Tanzania, alitaka kuhakikisha hapelekwi nchini Marekani kirahisi kama walivyotaka kufanya watu hao. Alitakiwa kupambana kama mwanaume lakini kitu kilichoonekana kuwa kigumu ni kwamba alikuwa na msichana Annabel tu.
“Siwezi kufanya kazi yenu tena,” alisema Ethan huku akimwangalia Thorn usoni.
“Una uhakika?”
“Ndiyo!”
“Basi tutawasiliana na mzee tumwambie, yeye atatuambia tufanye nini! Kama kukuua kwa mikono yake au atuachie sisi tukuue,” alisema Thorn.
Mashine ilizidi kuunguruma na boti ilizidi kusonga mbele, muda wote huo Ethan alikuwa akifikiria kutoroka mikononi mwa Thorn tu. Bado moyo wake haukutaka kuwa tayari kujiona akiingia nchini Marekani na kukabidhiwa mikononi mwa bwana Cook, kama mwanaume, alitakiwa kupambana, hata kama angeuawa wakati akipambana, kwake ingekuwa fahari.
Hawakuchukua dakika nyingi wakawa wamekwishafika katika meli ile ambapo wakapewa kamba ambayo wakaishika na kuanza kuingia melini mule. Bruno na Stephan walipomuona Ethan, nyuso zao zikajaa tabasamu pana, kazi kubwa waliyokuwa wamepewa ilionekana kukamilika.
“Mmeshanipata, muacheni Annabel aondoke,” alisema Ethan.
“Haondoki mtu hapa!”
“Sasa mnataka mumpeleke Marekani akafanye nini? Hili ni suala langu na nyie, yeye hausiki na chochote kile,” alisema Ethan huku akianza kuingiwa na hasira.
“Usijali, hatofika Marekani, tutamtupa baharini, ngoja tufike kina kirefu, tukimwacha, atatoa siri na hivyo kukamatwa,” alisema Thorn.
Walichokifanya ni kumchukua Ethan na kisha kumpeleka katika chumba kile alichofungwa Annabel, alipoingizwa, hakumuona Annabel kutokana na giza nene lililokuwemo mule ndani. Giza lile tu, kwake likaonekana kuwa mateso makubwa, hakujua Annabel alikuwa wapi, alichokifanya ni kuanza kumuita.
“Annabel...” alimuita msichana huyo huku akiwasha simu yake, hata kabla msichana huyo hajaitikia, Ethan alishtukia akipigwa kibao kimoja kizito mpaka simu kumdondoka, alikuwa Annabel.
“Kwa nini umenifanyia hivi?’ aliuliza Annabel huku akimshika fulana Ethan.
“Nisikilize kwanza mp....” alisema lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, akashtukia akipigwa kibao kingine.
“Kwa nini? Kwa nini?” aliuliza msichana huyo, alionekana kuwa na hasira mno.
“Mpenzi! Naomba unisamehe.”
“Wewe ni nani?”
“Ethan.”
“Nakuuliza wewe ni nani?”
“Annabel subiri, punguza hasira, tutazungumza mengi,” alisema Ethan.
“Niambie kwanza, wewe ni nani na hawa ni wakina nani?’ aliuliza Annabel.
Ethan hakuzungumza kitu, alibaki kimya huku akimwangalia msichana huyo kwa msaada wa mwanga wa simu yake, ni kweli alijiona kufanya kosa kubwa, kitendo cha kumficha msichana huyo kwamba alikuwa nani na wale watu walikuwa wakina nani kilimuumiza sana.
Annabel alilia na kulia, Ethan akamsogela na kisha kumkumbatia, alikuwa msichana wake, aliyemthamini, msichana aliyekuwa na nguvu kubwa katika maisha yake, hakutaka kumuona akilia, kitendo cha kububujikwa na machozi mashavuni mwake kilimuumiza mno.
“Nisamehe mpenzi,” alisema Ethan huku akiwa amemkumbatia.
“We..we ni n..an..i..?” aliuliza Annabel kwa sauti ya kilio kilichojaa kwikwi.
“Kuna mengi ya kuzungumza ila amini kwamba umeubadilisha moyo wangu Annabel,” alisema Ethan huku akiwa amemkumbatia msichana huyo.
“Niambie wewe ni nani.”
“Mimi ni muuaji mstaafu.”
“Umemuua nani?”
“Nimeua watu wengi kabla ya kukutana na wewe ambaye umeyabadilisha maisha yangu,” alijibu Ethan kwa sauti ndogo.
“Naomba usinidanganye.”
“Siwezi kukudanganya, mimi ni muuaji,” alisema Ethan.
Hapo ndipo Ethan alipoanza kumsimulia Annabel historia fupi ya maisha yake namna alivyokuwa akifanya kazi kwa mzee Sanchez mpaka alipoacha baada ya mzee huyo kufariki na hatimaye kuhamia kwa bwana Cook ambaye aliamua kuachana naye mara baada ya kukutana na msichana huyo mrembo.
Hakutaka kumficha kitu chochote, aliona kwamba huo ndiyo ulikuwa muda wa kumwambia ukweli juu ya kila kitu alichokuwa amekifanya, vitu vilivyomfanya kuwa mahali hapo kipindi hicho.
Annabel alilia sana, alimlalamikia mno kwa kumwingiza katika matatizo, lakini katika yote hayo, aligundua kwamba kama kutokea, tayari mambo yote hayo yalikuwa yametokea na kilichobaki ni kupanga nini cha kufanya baada ya hapo.
Akamsamehe kwa kila kitu, walichokubaliana ilikuwa ni lazima watoroke, hawakutaka kufika Marekani, Ethan alimfahamu bwana Cook, alikuwa mtu mwenye roho mbaya ambaye kwenye mambo ya biashara hakuonekana kuwa na mchezo hata kidogo.
“Sitaki kufika Marekani, ikitokea ikawa hivyo, ni lazima tutauawa,” alisema Ethan huku akimshika Annabel.
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Ni lazima tutoroke.”
“Tutaweza?”
Yote niachie mimi, hatufiki Marekani salama, kama kutuua, bora watuue ila si kufika mikononi mwa bwana Cook,” alisema Ethan, muda huo tayari meli ikang’oa nanga na safari ya kuelekea nchini Marekani kuanza kwa kupitia Afrika Kusini.
*****
Mpango uliokuwepo ni wa kutoroka ndani ya meli ile, hawakujua ni jinsi gani wangetoroka lakini kitu pekee walichokijua ni kwamba hawakutakiwa kufika nchini Marekani. Unyevuunyevu wa ndani ya chumba kile uliwaweka kwenye wakati mgumu, hakukuwa na mtu aliyekaa chini, walibaki wakiwa wamesimama na kila miguu ilipochoka, walikuwa wakichuchumaa tu.
Bahari ilitulia, walisikia upepo ukipiga kwa nje huku kelele ya injini ikisikika chumbani mule walipokuwa. Hawakuwa wakijua Kaskazini ulikuwa upande gani, Magharibi wala pande nyingine za dunia.
Ndani ya meli hiyo, Thorn na wenzake walikuwa na furaha mno, hawakutegemea kama wangefanikiwa kumpata Ethan ambaye kwao alionekana kuwa lulu zaidi ya madini yoyote yale.
Walichokifanya ni kusherehekea tu, walitoa mizinga ya pombe kali na kuanza kunywa, walipongezana na kugongesheana glasi zao, kila kitu kilichokuwa kikiendelea ilikuwa ni shangwe tele.
“Hatimaye tumefanikiwa, ni lazima tutapiga hela sana tukifika,” alisema Thorn kwa sauti ya kilevi.
“Ndiyo hivyo! Kwanza tukifika Afrika Kusini tumtupe baharini yule mwanamke,” alisema Bruno.
“Sawasawa. Hakuna tatizo, hatakiwi kufika Marekani kabisa,” alisema Stephan huku akionekana kuwa mwenye furaha tele.
Hiyo ndiyo ilikuwa mipango yao, Annabel hakutakiwa kufika nchini Marekani, iwe isiwe ilikuwa ni lazima kutupwa baharini na sehemu ambayo walikuwa wameipanga ilikuwa ni Afrika Kusini, sehemu ambapo bahari mbili za Indi na Atlantiki zilipokuwa zikikutana.
Mtu ambaye alikuwa akihitajika alikuwa Ethan tu na si mwingine, kila walipokuwa wakisherehekea walikumbuka kile walichotaka kukifanya. Baada ya siku mbili, huku wakiingia na kutoka ndani ya chumba kile kwa ajili ya kuwapa chakula, wakafika nchini Malawi ambapo hawakutaka kusimama, waliunganisha na kuanza kuitafuta Msumbiji.
“Tukifika Afrika Kusini, kitu cha kwanza ni kununua pombe,” alishauri Bruno.
“Hakuna tatizo, tena pale kuna pombe nyingi, zenye ulevi wa hali ya juu, hakuna tatizo,” alisema Thorn huku kila mmoja akionekana kuwa na furaha.
Upande wa pili Ethan hakutaka kutulia, alikuwa akihangaika huku na kule, kazi kubwa aliyokuwa nayo ni kutafuta njia ya kuweza kutoka ndani ya chumba kile kilichoonekana kuwa na mateso makali.
Kulikuwa na maboksi mengi, hawakuelewa yalikuwa ni maboksi ya nini, waliachana nayo, waliyasogeza huku na kule na mishemishe za kutafuta jia ya kutokea kuendelea. Waliangalia kila sehemu ili kuona kama wangeweza kuona tundu au kitu chochote kile na waweze kujitoa lakini hawakuambulia kitu.
Kuna kipindi walikata tamaa, wakaona kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kufika nchini Marekani. Ethan akaonekana kuchoka, hakujua ni kipi kingine alitakiwa kufanya kwani chumba kilionekana kutimia.
Meli ilizidi kusonga mbele, kila baada ya masaa sita, mmoja wa Wazungu wale aliingia ndani na kisha kuwapatia chakula na kuondoka zake. Wakati mwingine kitu alichokuwa akikifikiria Ethan ni kupambana na yeyote ambaye angewaletea chakula na hatimaye kuondoka melini humo, ila swali kubwa lililomjia kichwani, wangetorokaje na wakati walikuwa katikati ya bahari?
“Haya maboksi yana nini?” aliuliza Annabel.
“Mmmh! Hebu subiri,” alisema Ethan, hapohapo akaanza kufungua boksi moja baada ya jingine, alichokikuta ndani hakuamini, kulikuwa na dola nyingi zilizokuwa zikisafirishwa kuelekea nchini Marekani, kwa maana hiyo aliona kwamba kama wangefanikiwa kulichukua hata boksi moja, basi wangekuwa matajiri.
“Utajiri huu,” alisema Ethan huku akionekana kushtuka.
“Fedha za nani hizi?”
“Atakuwa bwana Cook! Ni mtu anayejishughulisha na biashara nyingi haramu, bila shaka hizi ni fedha zake zilizotoka Afrika na Asia, kama itawezekana, tunaondoka na zote,” alisema Ethan.
“Kivipi? Tutaweza?”
“Niachie mimi.”
*****
Askofu Benedicto alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, akili yake haikutulia, mawazo yalimsonga sana na muda wote alikuwa akimfikiria binti yake tu. Hakujua mahali alipokuwa, kitendo cha Ethan kumsimulia historia ya maisha yake ilimuogopesha na kubaki akijiuliza huyo bwana Cook alikuwa nani.
Kitu alichokifikiria na ambacho kilikuja kwa haraka kichwani mwake ilikuwa ni lazima aende kituo cha polisi na kutoa taarifa juu ya kupotea kwa binti yake, swali pekee lililokuja kichwani mwake, akifika huko aseme nani aliyepotea? Binti yake? Ugumu ukawa hapo.
Japokuwa alikuwa na swali hilo gumu lakini hakutaka kujali, alichotaka kukiona ni binti yake akiwa mikononi mwake tu. Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilikuwa siri yake, hakutaka kumpa taarifa Irakoze kwa kuamini kwamba angechanganyikiwa katika masomo yake, alipoulizwa kwamba Annabel aliendeleaje, alimwambia anaendelea vizuri.
“Karibu baba askofu,” alisema polisi mmoja aliyekuwa kaunta.
“Asante sana, nimekuja kutoa taarifa,” alisema askofu Benedicto.
“Taarifa gani askofu?”
“Mtoto wa dada yangu ametekwa,” alijibu askofu.
Hapohapo polisi akachukua daftari na kuanza kuandika maelezo ya askofu Benedicto. Alikuwa mtu mwenye jina kubwa, aliyejulikana sana hata zaidi ya masupastaa wengine, kuwa kiongozi wa dini katika dhehebu kubwa kulimfanya kuwa na jina Afrika Mashariki nzima.
Polisi wengine ambao walimuona mahali pale wakamsogelea na kuanza kuzungumza naye, kila mmoja alijisikia fahari kuwa karibu na askofu huyo kiasi kwamba wengine wakadiriki hata kupiga naye picha za ukumbusho kwani kumuona tofauti na kanisani lilikuwa jambo gumu.
“Hakuna tatizo askofu, tutaanza kufanya kazi,” alisema polisi yule.
“Nitashukuru sana. Ila kwanza anzeni na huyu Ethan, kuna mengi anafahamu,” alisema askofu.
Katika maelezo aliyoyatoa kituoni hapo alimwandika mpaka Ethan na kuwaambia mahali alipokuwa akipatikana, alipanga katika Hoteli ya New Africa iliyokuwa Posta jijini Dar es Salaam. Walipoambiwa hivyo, hapo ndipo walipoanza kufuatilia, wakawaita polisi wawili ambao walishughulika sana na masuala ya kipelelezi na kuwaambia waanze kufuatilia huko ili kujua ni wapi pa kuanzia.
Walipofika huko, wakamuulizia Ethan ambapo wakaambiwa kwamba alikuwepo ila mchana wa siku iliyopita aliondoka kuelekea katika Hoteli ya Kingstar ambapo hakukuwa mbali na hapo ilipokuwa hoteli hiyo.
Wakaelekea katika hoteli hiyo, vyote hivyo walitaka kufahamu mahali alipokuwa Ethan, walipofika na kujitambulisha kisha kuulizia, wakachuuliwa na kupelekwa katika chumba kimoja kilichokuwa na kompyuta tano na kisha kuambiwa wakae vitini.
Hapo, wakaanza kuonyeshewa video kadhaa za siku iliyopita kutoka katika kamera za CCTV zilizokuwa katika maeneo makubwa ya hoteli hiyo. Walimwona mwanaume mmoja akizungumza na Mzungu, walikuwa ni watu pekee waliokuwa wakizungumza katika muda huo walioambiwa.
Walichokifanya ni kuanza kuwafuatilia kwa ukaribu ili kuona baada ya hapo ni kitu gani kilifuata. Walizungumza kadhaa, walionekana kama kutokukubaliana kitu fulani. Polisi wale wakawaangalia vizuri ndipo walipomuona Mzungu yule akimuonyeshea bastola Ethan kwa siri.
“Kuna kitu,” alisema polisi mmoja.
“Hata mimi! Hebu tucheki kwanza,” alisema polisi mwingine.
Waliendelea kufuatilia kila hatua, waliwaona watu wale wakisimama na kuondoka, wakajua kwamba kulikuwa na sehemu waliyokuwa wakienda na Ethan alikuwa akifuata kwa kuwa alionyeshewa bastola.
Kwa mbali wakawaona wakiingia kwenye teksi moja na kuondoka mahali hapo, walipoelekea, hawakujua palikuwa wapi. Hawakutaka kukaa mahali hapo, walichokifanya ni kutoka na kuelekea kule kulipokuwa na teksi.
Walitaka kufahamu kile kilichokuwa kimeendelea baada ya hapo, walitaka kufahamu mahali walipoelekea, walichokifanya ni kumuuliza dereva teksi mmoja katika ya wengi waliokuwepo mahali hapo.
“Mzungu! Jana, labda aulizwe Ahmad,” alisema dereva teksi mara baada ya kuulizwa kuhusu Mzungu wa jana yake.
“Huyo Ahmad yupo wapi?”
“Yupo kule mbele. Teksi ile kule,” alijibu huku akiionyooshea kidole.
Walichokifanya ni kumfuata huyo Ahmed na kuanza kumuuliza kuhusu Mzungu wa jana ambaye alimkodi kwenye teksi yake akiwa na kijana mmoja wa Kiafrika.
“Mmmh! Kuna nini jamani? Gaidi nini?” aliuliza Ahmed.
“Kwa nini?”
“Jana yule Mwafrika hakuwa akijiaminiamini, nyie nao mnanitia wasiwasi,” alijibu Ahmed.
“Uliwapeleka kuelekea wapi?”
“Coco Beach!”
“Mmmh! Kufanya nini huko?”
“Sijui! Niliachana nao hapo, wakawa wameelekea ufukweni, sijui walikwenda kuogelea!” alijibu Ahmed.
“Hebu tupeleke huko,” alisema polisi mmoja, wakaingia ndani ya teksi ile na kuanza kuelekea huko Coco Beach, kila walipojifikiria sababu iliyowafanya kwenda ufukweni, wakakosa jibu.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumatano

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi na Tano.

Wapelelezi wale hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokifanya ni kuondoka kuelekea ufukweni huko ili waone kama wangeweza kupata kitu chochote ambacho kingeweza kuwasaidia. Walipofika Osterbay, wakaanza kuelekea katika ufukwe wa Coco.
Huko, hawakuona dalili zozote za kuwepo kwa watu hao, walichokifanya ni kuwauliza vijana fulani ambao makazi yao makubwa yakiwa huko huku vichwa vyao vikiwa na mipango ya kuzamia na kwenda Ulaya au Marekani, vijana hawa walijiita Beach Boys.
“Nani huyo?” aliuliza kijana mmoja mara baada ya kuulizwa kuhusu Ethan na Mzungu yule.
“Kijana mmoja alifika hapa akiwa na Mzungu!”
“Mmh! Wala sijamuona, ilikuwa lini?”
“Jana!”
“Sijui kwa kweli, kawaulize beach boys wengine, wale pale,” alisema kijana mmoja huku akiwanyooshea vidole wenzake.
Wapelelezi wale hawakuwa na jinsi, walichokifanya ni kuwasogelea vijana hao wengine na kuwauliza, hawakuwa wamewaona watu hao, waliuliza na kuuliza na mwisho wa siku kuamua kuondoka zao.
“Kwa hiyo!”
“Tukatoe taarifa kwamba tunaendelea, tutampata tu,” alisema mpelelezi mmoja wakati wakiwa wanarudi.
*****
Meli iliendelea kukata mawingu, mateso ndani ya chumba ile yalikuwa makubwa mno. Ethan hakutaka kuendelea kubaki ndani ya chumba kile, kitu alichokifikiria kwa kipindi hicho ni kutoroka huku akiwa na mpenzi wake, Annabel na fedha zilizokuwa kwenye maboksi waliyokuwa nayo ndani ya chumba kile.
Bado akili yake ilikuwa ikisumbuka ni kwa namna gani angeweza kufanikiwa kutoka ndani ya chumba kile salama, aliendelea kupekua huku na kule lakini kikafika kipindi akachoka, hakutaka kuendelea tena, akaacha kwa kuamini kwamba singeweza kufanikiwa.
“Vipi?” aliuliza Annabel.
“Yaani nimeshindwa kujua chochote kile,” alisema Ethan.
“Kwa hiyo tumeshindwa?”
“Inawezekana.”
“Na kwa hiyo tunarudi Marekani?”
“Kurudi haiwezekani, hata kama tumeshindwa, sawa, ila kurudi Marekani, haiwezekani,” alisema Ethan.
Walitumia wiki nzima na ndipo meli ikaanza kuingia Afrika Kusini. Thorn na wenzake walifurahi sana kwani waliamini baada ya hapo, wangeanza safari nyingine ya kuelekea Marekani kwani wangafanikiwa kutoka kwenye Bahari ya Indi na kuingia kwenye Bahari ya Atlantika ambayo ndiyo ilikwenda mpaka nchini Marekani.
Walipofika umbali wa kilometa ishirini kabla ya kuifikia Bahari ya Atlantiki, walichokifanya ni kushusha boti walizokuwa nazo kisha kuelekea nchi kavu kwa ajili ya kununua pombe na kunywa. Walipofika katika Mji wa Nangame katika Jimbo la Kwa Zulu Natal, wakanunua pombe kali huku wakitumia siku hiyo kulala na wanawake ambao kwao waliwapa kipaumbele huku kule melini wakiwa wamewaacha nahodha na wafanyakazi wake kwa kuamini kwamba ulinzi ungeimarishwa.
Ndani ya meli bado Ethan alikuwa akijifikiria namna ya kutoka ndani ya meli hiyo, chumba kilikuwa na giza mno, hakuweza kujua mahali walipokuwa na walikuwa wakielekea wapi. Walipofika karibu na Nangame, sehemu ambayo meli ile ilisimama kwa siku nzima, Ethan akashtuka, haikuwa kawaida meli kusimama, tena injini zikiwa zimezimwa kabisa, hapo akajua kwamba walikuwa wamefika sehemu na kuweka kituo.
“Meli imesimama?” aliuliza Ethan.
“Umejuaje?”
“Unasikia injini ikilia?”
“Hapana!”
“Itakuwa imesimama, inamaanisha kwamba tumefika kwenye kituo,” alisema Ethan.
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Kama tupo kwenye kituo, hawa watu hawatakuwepo, hebu subiri,” alisema Ethan.
Alichokifanya ni kuusogelea mlango na kisha kuanza kuugonga. Aliugonga kwa dakika kadhaa mara akasikia sauti za miguu ya mtu ikija kule walipokuwa, alichokifanya ni kusikilizia mpaka pale sauti zile zilipoacha kusikika mara baada ya kuufikia mlango ule.
“Kuna mtu humu?” ilisikika sauti ikiuliza.
“Ndiyo! Kuna mtu.”
“Wewe ni nani? Mzamiaji?”
“Hapana!”
“Kumbe wewe ni nani?”
Ethan hakujibu kitu, kwanza akabaki kimya, kitu kilichomjia kichwani mwake ni kwamba mtu huyo hakujua uwepo wao ndani ya meli ile na ndiyo maana alikuwa na maswali mengi ambayo ndiyo yaliyomuonyeshea kile alichokuwa amekifikiri.
“Mimi ni mzamiaji kaka,” alisema Ethan.
“Si umesema wewe si mzamiaji?”
“Mimi ni mzamiaji kaka.”
“Sawa! Ulikuwa unakwenda wapi?”
“Popote pale, nilitaka kwenda Ulaya tu.”
“Haiwezekani! Ni lazima nikushushe,” alisema jamaa yule.
“Kwani hapa ni wapi?”
“Afrika Kusini.”
“Hapahapa kaka kunatosha, wewe nishushe tu kisiri, hata hapa natumaini nitaishi kama nipo Ulaya,” alisema Ethan.
“Unajua kupiga mbizi?”
“Najua sana tu, nisaidie kaka, naomba unisaidie” alisema Ethan.
Aliongea kwa kujiamini sana kiasi kwamba ingekuwa ngumu kugundua kwamba mtu huyo alikuwa akidanganya, kijana huyo, pasipo kujua uwepo wa watu hao humo ndani akawafungulia mlango huku lengo lake likiwa ni kumtorosha kisiri ili asiweze kuonekana na watu wengine kwa kujua kwamba angeweza kuuawa.
Ile alipofungua mlango tu, akajikuta akivutwa ndani, akazibwa mdomo wake, akabaki akikukuruka kwa kutaka kujitoa mikononi mwa Ethan lakini hakufanikiwa, alishikwa vilivyo.
“Nisikilize,” alisema Ethan.
“Nakusikiliza, naomba usiniue,” alisema kijana yule huku akiogopa.
“Sina haja ya kukuua, nisikilize, ninataka boti ya kuondoka humu ndani,” alisema Ethan.
“Boti...boti...haturuhusiwi kuzitoa.”
“Hapana! Lazima utoe hata moja, ninataka ufanye hivyo, ninahitaji kuondoka humu,” alisema Ethan, hata sauti yake aliibadilisha na kuwa nzito.
“Naomba usiniue,” alisisitiza kijana yule.
“Sihitaji kukuua. Nitakupa fedha ili unisaidie,” alisema Ethan.
“Sawa.”
Alichokifanya ni kuyafuata maboksi yale, akalichana boksi moja na kisha kutoa bunda moja la dola laki moja na kisha kumpelekea kijana yule na kumgawia. Zilikuwa fedha nyingi mno ambazo asingeweza kuzipata hata kama angefanya kazi mfululizo ndani ya meli ile. Tamaa ikamuingia.
“Ukinifanyia kazi yangu, nakupa nyingine.”
“Kazi gani? Nipo tayari.”
“Ninahitaji kupata boti kwanza,” alisema Ethan.
“Mmmh!”
“Ni ngumu kuipata?”
“Ni ngumu sana, niambie kingine.”
“Nataka kwenda kwenye chumba cha chini ambacho kitanifanya niyaone maji vizuri kwa kupitia kwenye dirisha dogo,” alisema Ethan.
“Sawa. Ila ili iweje?”
“Unataka hela hutaki?”
“Nataka!”
“Subiri!” alisema Ethan na kisha kulifuata boksi lile na kutoa bunda jingine la fedha na kumpatia kijana yule.
“Inawezekana?”
“Bila shaka, inawezekana,” alisema kijana yule.
“Nitataka uje kunifungulia mlango wakati meli inaanza kuondoka,” alisema Ethan.
“Hakuna tatizo.”
Kila kitu kilichokuwa kikifanyika ndani ya meli hiyo ilikuwa siri kubwa. Bwana Cook alikuwa akijihusisha na biashara nyingi haramu za madawa ya kulevya na ngozi za binadamu, hakukuwa aliyekuwa akilifahamu hilo katika meli ile zaidi ya nahodha ambaye alimwamini sana.
Ndani ya meli ile kulikuwa na maboksi matano, yote yalijaa fedha kutokana na malipo aliyokuwa amelipwa barani Asia na Afrika. Fedha hizo alitaka kuzisafirisha kwa kutumia meli kwani aliogopa kutumiwa benki kwa kuhofia kushtukiwa hivyo kufuatiliwa.
Wafanyakazi wengine hawakujua hilo, walichokuwa wakikijua ni kwamba wao walikuwa wavuvi wa samaki wakubwa. Uwepo wa Ethan na Annabel ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa mno, hakukuwa na aliyekuwa akifahamu zaidi ya nahodha tu.
Hata uwepo wa maboksi yale yaliyokuwa na fedha ilikuwa siri kubwa, hakutakiwa mtu yeyote afahamu hilo kutokana na uaminifu kuwa mdogo. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya kijana yule kudanganyika kirahisi kwamba Ethan alikuwa mzamiaji aliyetaka kuelekea Marekani au Ulaya.
Alipopewa fedha zile, alishangaa, zilikuwa nyingi, ilikuwaje mzamiaji awe na fedha nyingi kiasi kile? Hakutaka kujiuliza maswali mengi, alichokiagalia ni fedha tu, hivyo akataka kufanya kama vile Ethan alivyotaka afanye, wakati meli inaondoka, akamchukua na kumpeleka katika moja ya vyumba vilivyokuwa chini ambapo huko tungesema kwamba kilikuwa chini ya bahari.
****
Siku ya kwanza ikakatika, ya pili kuingia na hatimaye wiki nzima, bado hakukuwa na taarifa za kuridhisha kutoka kwa polisi juu ya kile kilichokuwa kimeendelea katika upepelezi wao juu ya Annabel.
Kila alipokuwa akienda kituoni kuulizia, askofu hakupewa majibu ya kueleweka, alikuwa akiambiwa hivi na vile, njoo kesho bado wapelelezi wetu wanaendelea kufuatilia. Hakuwa na amani, alikosa furaha, hakujua ni kitu gani alitakiwa kukifanya ili aweze kumpata binti yake.
Hakutaka kumwambia Irakoze kwani alijua ni kwa jinsi gani angechanganyikiwa, alichokifanya ni kufuatilia kimyakimya na mwanamke huyo kila alipokuwa akiuliza, jibu lilikuwa lilelile kwamba Annabel anaendelea vizuri.
“Naomba nizungumze naye mana’ke simuni hapatikani,” alisikika Irakoze.
“Amelala! Akiamka nitakupa uongee naye,” alisema askofu Benedicto.
Kila siku alikuwa akidanganya huku akifuatilia kituoni lakini majibu yalikuwa yaleyale. Kwa sababu polisi walimfahamu sana askofu Benedicto, walichokifanya ni kutoa taarifa katika vituo vingine na hata kwenye vyombo vya habari ambapo huko wakatangaza kwamba kulikuwa na msichana aliyekuwa ametekwa na kupelekwa pasipojulikana.
Watu wakashtuka, hawakuamini kama kweli katika Tanzania hii kungekuwa na mtu ambaye angetekwa kwani mambo kama hayo yalikuwa yakisikika nchi za nje tu.
Kitendo cha picha za Annabel kuanza kusambazwa kwenye magazeti mbalimbali, askofu akahofu na kuona kwamba Irakoze angegundua kile kilichokuwa kikiendelea, alichokifanya ni kumpa taarifa tu kwani hakuwa na jinsi.
“Unasemaje?”
“Annabel hajulikani alipo.”
“Tangu lini?”
“Majuzi, yaani hapa nimechanganyikiwa,” alisema askofu.
“Nakuja,” alisikika Irakoze na kukata simu.
Hakuwa na jinsi, alitakiwa kufanya kile alichokifanya, alijua kwamba Irakoze angeumia sana lakini hakukuwa na jinsi, alitakiwa kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Baada ya masaa mawili, Irakoze alifika nyumbani hapo, macho yake yalikuwa mekundu kwa sababu ya kulia sana.
“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze huku akibubujikwa na machozi.
“Subiri kwanza.”
“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze na kuanza kulia kwa sauti kubwa.
Askofu akapata kazi kubwa ya kuanza kumbembeleza, ni kweli alitakiwa kulia, mapenzi mazito aliyokuwa nayo kwa binti yake yalimfanya kuumia mno pale aliposikia kwamba alikuwa ametekwa na watu wasiojulina.
Alichokifanya askofu ili kujiondoa lawama ni kumwambia Irakoze kila kitu kilichokuwa kimetokea hasa kuhusu Ethan aliyeonekana kuwa chanzo cha kila kitu. Irakoze akajikuta akichukia, akamchukia Ethan kuliko mtu yeyote yule, hakuamini kama uwepo wa mwanaume yule ndiyo ungemfanya binti yake kutekwa na kutokujulikana mahali alipokuwa.
Alipouliza kuhusu Ethan, hata naye hakuwa akijulikana alipokuwa, hilo likamuumiza zaidi na kuona kama tayari binti yake alikuwa ameuawa na watu hao. Akajilaumu kwa kitendo cha kumwamni Ethan na kumpa nafasi ya kufika nyumbani pale huku wakati mwingine wakimwacha na binti yao.
Hawakujua wafanye nini, huo haukuwa muda wa kulaumiana au kujutia kile kilichokuwa kimefanyika, walichotakiwa kukifanya kwa wakati huo ni kukubaliana na ukweli kwamba binti yao hakuwa mikononi mwao.
Irakoze hakurudi tena chuoni, akaamua kuachana na masomo hayo na kuwa mwanamke wa nyumbani tu. Kichwa chake kilichanganyikiwa mno, kila wakati alikuwa mtu wa majonzi na hakuweza kunyamaza, alikuwa mtu wa kububujikwa na machozi tu.
Siku ziliendelea kukatika, Askofu Benedicto hakutaka kundoka nyumbani hapo, hakutaka kwenda kanisani na siku zte alitoa udhuru kwamba kulikuwa na kitu alichokuwa akikifanya hivyo asingeweza kwenda kanisani kitu ambacho hakikuwa na tatizo lolote lile.
“Annabel atarudi tu, atapatikana wala usiwe na wasiwasi,” alisema askofu huku akimwangalia Irakoze usoni. Mwanamke huyo hakuzungumza kitu zaidi ya kulia tu.
*****
Walipomaliza kunywa pombe na wanawake wao, wakawachukua na kwenda nao hotelini ambapo huko wakalala huku wakifanya nao anasa usiku mzima. Asubuhi na mapema waliamka huku pombe zikiwa kichwani, hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokitaka ni kuondoka kuelekea nchini Marekani, safari ndefu ambayo ingewachukua hata miezi miwili baharini.
Walipoondoka hotelini, wakaelekea ufukweni ambapo wakachukua boti zao na kuanza kurudi kule ilipokuwa meli yao, umbali wa kilometa mbili kutoka pale walipokuwa. Ndani ya boti walikuwa na mizinga ya pombe kali, walikuwa wakisherehekea huku wakigongesheana chupa zao kwa furaha kubwa.
Walichukua dakika kumi kuifikia meli ile ambapo wakarushiwa kamba na kisha kuingia melini huku wafanyakazi hao wakifanya machakato mzima wa kuipandisha boti ile melini.
“Wale wapumbavu wapo?” aliuliza Thorn kwa sauti ya kilevi, alikuwa akimuuliza nahodha.
“Wapo!”
“Mmewapa chakula?”
“Hapana!”
“Kawapeni! Yule mwanamke hana muda mrefu atakufa, tunataka kumtupa baharini katika mpaka wa bahari,” alisema Thorn.
“Sawa!”
Kwa kuwa uwepo wa watu hao ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa, nahodha akaenda peke yake huku akiwa ameshika sinia lililokuwa na chakula, alipofika nje ya mlango ule, aliufungua kisha kulitupia sinia lile ndani na kisha kuufunga na kurudi.
“Tayari?” aliuliza Thorn.
“Ndiyo! Nishawatupia.”
“Sawa.”
Usiku ulikuwa umeingia, safari ya kuelekea nchini Marekani ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Walikuwa wamebakiza umbali wa kilometa kama kumi ili kufika katika eneo ambalo bahari ya Indi ilikuwa ikikutana na Bahari ya Atlantiki, sehemu pekee ambayo walipanga kumtupa Annabel na kuendelea na safari yao.
Kila mmoja melini alionekana kuwa na furaha tele, walikuwa wakigongesheana chupa zao na kuendelea kunywa huku wakipiga kelele ambazo zilionekana kuwa kero kwa wafanyakazi ambao hawakuwa wakinywa kama wao.
Kijana ambaye tayari mfukoni mwake alikuwa na dola laki mbili kila wakati alikuwa akiangalia saa yake tu, alikuwa akisubiri muda ambao angekwenda kumtoa Ethan na kumpeleka katika chumba ambacho alitaka kwenda.
Ilipofika saa mbili usiku, harakaharaka akaelekea katika chumba kile, alichokifanya ni kuufungua mlango na Ethan kutoka huku akiwa amelivua shati lake na kulifunga kiunoni tayari kwa kufanya kile alichotaka kukifanya.
“Vipi?”
“Nipo tayari! Twende.”
Kijana yule akamchukua Ethan kisiri tena huku wakati mwingine akijificha kila aliposikia watu wakija upande waliokuwepo, walitembea mpaka walipofika katika mlango mkubwa ambapo hapo alimfungulia na kumwambia aingie ndani.
“Tuingie wote.”
“Kwa nini?”
“Wewe tuingie,” alisema Ethan na kijana yule kuingia naye.
Walipofika ndani, Ethan hakutaka kujificha, alimwambia kijana yule kile alichotaka kukifanya, alimwambia dhahiri kwamba hakuwa mzamiaji kama alivyomwambia bali alikuwa mtu aliyetekwa ambaye alikuwa akirudishwa nchini Marekani tayari kwa kuuawa.
Kijana yule alibaki kimya akimsikiliza. Yeye mwenyewe akabaki akishangaa kwani ndani ya meli ile hakukuwa hata na mfanyakazi mmoja aliyekuwa akijua kama humo ndani kulikuwa na mtu ambaye alikuwa akipelekwa nchini Marekani.
“Huyo mwanamke yupo wapi?”
“Nimemuacha ndani,” alijibu Ethan.
“Sawa! Kwa hiyo unataka kufanya nini mpaka umeniambia nikulete humu?” aliuliza kijana yule.
“Nataka kuzamisha meli.”
“Unasemaje?”
“Nataka kuzamisha meli, sipo tayari kurudi nchini Marekani,” alisema Ethan.
“Utaizamishaje?”
“Unakiona kidirisha kile cha kioo?”
“Ndiyo!”
“Unayaona yale maji?”
“Ndiyo! Basi ndivyo nitakavyofanya, kwa kuwa chumba hiki kipo chini, yaani chini ya bahari kwa chini, nikipasua kioo kile, maji yataingia, basi na meli itazama,” alisema Ethan.
“Mmmh!”
“Ndiyo hivyo, andaa boya lako, hakuna kurudi Marekani hapa, baada ya hapa, mimi, wewe na mke wangu tutaondoka, nenda kaandae boti tayari kwa kuondoka nayo, meli itakapoanza kuzama, njoo na boti katika upande wa chumba chetu, baada ya hapo, nakuahidi utakwenda kuwa milionea. Sawa?” aliuliza Ethan.
“Sawa!”
Kazi ikabaki kwa Ethan, akaanza kukivunja kioo kile kigumu kwa kutumia kipande cha chuma kilichokuwa pembeni. Japokuwa kilipiga kelele sana lakini hakukuwa na mtu aliyesikia kutoka na chumba kile kuwa karibu na injini ya meli hiyo.
Wala hazikupita dakika nyingi, kioo kile kikaanza kutoa ufa, Ethan hakuacha, aliendelea kukipiga zaidi na zaidi na baada ya muda fulani, kioo kile kikaachia na maji kuanza kuingia ndani ya meli ile, hakutaka kukaa hapo, alichokifanya ni kuufungua mlango na kuanza kutoka kwa kunyata kuelekea ndani ya chumba kile alichokuwemo Annabel.
“Vipi?”
“Tayari! Jiandae, yafunge maboksi hayo vizuri, kuna boti itakuja upande wa huku, tutatakiwa kutoka kisha kuingia botini,” alisema Ethan.
Upande wa pili, Thorn na wenzake walikuwa wakiendelea kuimba na kupiga kelele, walikuwa wamekunywa mno na walionekana kuzidiwa na ulevi, muda wote, mizinga ya pombe kali ilikuwa mikononi mwao, nyimbo walizoimba, hazikueleweka kabisa.
Hakukuwa na wafanyakazi waliokuwa wakiwafahamu wale walikuwa wakina nani, kadiri walivyoendelea kuwa ndani ya meli ile walizidi kuwa na maswali zaidi, hawakuonekana kuwa watu wazuri hata mara moja kutokana na yale waliyokuwa wakiyafanya.
Baada ya dakika kama kumi, ghafla wakaanza kuhisi kwamba meli ile ilianza kuzama. Wafanyakazi wote wakashtuka, hawakuwa na uhakika juu ya kile walichokuwa wamekihisi, walichokifanya ni kwenda kwenye vyumba vyote kuangalia.
Walipokuwa wakielekea katika chumba kile, ghafla wakaona maji mengi yakitoka kutokea mlangoni na walipoufungua mlango tu, chumba kizima kilikuwa kimejaa maji, hivyo kitendo cha kuufungua tu, maji yakawa kama yameruhusiwa.
Kila mtu alichanganyikiwa, maji yaliendelea kuingia na kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele na ndivyo meli ile ilivyoendelea kuzama. Kila mmoja akaanza kuhangaika huku na kule, walikuwa wamefika mbali mno na nchi kavu hakukuonekana, walikuwa wakiukaribia mpaka wa bahari mbili za Indi na Atlantiki.
“Chukueni maboya,” alisema nahodha huku akionekana kuchanganyikiwa, giza lilikuwa limetanda kila kona.
Kilichofanyika, wafanyakazi wakachukua maboya, kijana yule ambaye alikuwa amekwishafanya mipango na Ethan, akachukua boti iliyokuwa imefungwa nyuma ya meli ile, akaifungua kamba, ikaelekea baharini, hapohapo hakutaka kuchelewa, alichokifanya ni kujirusha majini na kuanza kupiga mbizi kuifuata boti ile, alipoifikia, akaipanda, akaiwasha na kuelekea katika upande ule aliokuwepo Ethan na Annabel ambapo napo chumba chao kilianza kujaa maji, maboksi yale matano yaliyojaa hela yalianza kuelea.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Ijumaa.
Kumbuka hadithi yangu ya UTAJIRI WENYE UCHUNGUimeanza kwenye kundi la SIMULIZI TAMUTAMU.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
NYEMO CHILONGANI
BIASHARA YA KIFO

Sehemu ya Kumi na Tano.

Wapelelezi wale hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokifanya ni kuondoka kuelekea ufukweni huko ili waone kama wangeweza kupata kitu chochote ambacho kingeweza kuwasaidia. Walipofika Osterbay, wakaanza kuelekea katika ufukwe wa Coco.
Huko, hawakuona dalili zozote za kuwepo kwa watu hao, walichokifanya ni kuwauliza vijana fulani ambao makazi yao makubwa yakiwa huko huku vichwa vyao vikiwa na mipango ya kuzamia na kwenda Ulaya au Marekani, vijana hawa walijiita Beach Boys.
“Nani huyo?” aliuliza kijana mmoja mara baada ya kuulizwa kuhusu Ethan na Mzungu yule.
“Kijana mmoja alifika hapa akiwa na Mzungu!”
“Mmh! Wala sijamuona, ilikuwa lini?”
“Jana!”
“Sijui kwa kweli, kawaulize beach boys wengine, wale pale,” alisema kijana mmoja huku akiwanyooshea vidole wenzake.
Wapelelezi wale hawakuwa na jinsi, walichokifanya ni kuwasogelea vijana hao wengine na kuwauliza, hawakuwa wamewaona watu hao, waliuliza na kuuliza na mwisho wa siku kuamua kuondoka zao.
“Kwa hiyo!”
“Tukatoe taarifa kwamba tunaendelea, tutampata tu,” alisema mpelelezi mmoja wakati wakiwa wanarudi.
*****
Meli iliendelea kukata mawingu, mateso ndani ya chumba ile yalikuwa makubwa mno. Ethan hakutaka kuendelea kubaki ndani ya chumba kile, kitu alichokifikiria kwa kipindi hicho ni kutoroka huku akiwa na mpenzi wake, Annabel na fedha zilizokuwa kwenye maboksi waliyokuwa nayo ndani ya chumba kile.
Bado akili yake ilikuwa ikisumbuka ni kwa namna gani angeweza kufanikiwa kutoka ndani ya chumba kile salama, aliendelea kupekua huku na kule lakini kikafika kipindi akachoka, hakutaka kuendelea tena, akaacha kwa kuamini kwamba singeweza kufanikiwa.
“Vipi?” aliuliza Annabel.
“Yaani nimeshindwa kujua chochote kile,” alisema Ethan.
“Kwa hiyo tumeshindwa?”
“Inawezekana.”
“Na kwa hiyo tunarudi Marekani?”
“Kurudi haiwezekani, hata kama tumeshindwa, sawa, ila kurudi Marekani, haiwezekani,” alisema Ethan.
Walitumia wiki nzima na ndipo meli ikaanza kuingia Afrika Kusini. Thorn na wenzake walifurahi sana kwani waliamini baada ya hapo, wangeanza safari nyingine ya kuelekea Marekani kwani wangafanikiwa kutoka kwenye Bahari ya Indi na kuingia kwenye Bahari ya Atlantika ambayo ndiyo ilikwenda mpaka nchini Marekani.
Walipofika umbali wa kilometa ishirini kabla ya kuifikia Bahari ya Atlantiki, walichokifanya ni kushusha boti walizokuwa nazo kisha kuelekea nchi kavu kwa ajili ya kununua pombe na kunywa. Walipofika katika Mji wa Nangame katika Jimbo la Kwa Zulu Natal, wakanunua pombe kali huku wakitumia siku hiyo kulala na wanawake ambao kwao waliwapa kipaumbele huku kule melini wakiwa wamewaacha nahodha na wafanyakazi wake kwa kuamini kwamba ulinzi ungeimarishwa.
Ndani ya meli bado Ethan alikuwa akijifikiria namna ya kutoka ndani ya meli hiyo, chumba kilikuwa na giza mno, hakuweza kujua mahali walipokuwa na walikuwa wakielekea wapi. Walipofika karibu na Nangame, sehemu ambayo meli ile ilisimama kwa siku nzima, Ethan akashtuka, haikuwa kawaida meli kusimama, tena injini zikiwa zimezimwa kabisa, hapo akajua kwamba walikuwa wamefika sehemu na kuweka kituo.
“Meli imesimama?” aliuliza Ethan.
“Umejuaje?”
“Unasikia injini ikilia?”
“Hapana!”
“Itakuwa imesimama, inamaanisha kwamba tumefika kwenye kituo,” alisema Ethan.
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Kama tupo kwenye kituo, hawa watu hawatakuwepo, hebu subiri,” alisema Ethan.
Alichokifanya ni kuusogelea mlango na kisha kuanza kuugonga. Aliugonga kwa dakika kadhaa mara akasikia sauti za miguu ya mtu ikija kule walipokuwa, alichokifanya ni kusikilizia mpaka pale sauti zile zilipoacha kusikika mara baada ya kuufikia mlango ule.
“Kuna mtu humu?” ilisikika sauti ikiuliza.
“Ndiyo! Kuna mtu.”
“Wewe ni nani? Mzamiaji?”
“Hapana!”
“Kumbe wewe ni nani?”
Ethan hakujibu kitu, kwanza akabaki kimya, kitu kilichomjia kichwani mwake ni kwamba mtu huyo hakujua uwepo wao ndani ya meli ile na ndiyo maana alikuwa na maswali mengi ambayo ndiyo yaliyomuonyeshea kile alichokuwa amekifikiri.
“Mimi ni mzamiaji kaka,” alisema Ethan.
“Si umesema wewe si mzamiaji?”
“Mimi ni mzamiaji kaka.”
“Sawa! Ulikuwa unakwenda wapi?”
“Popote pale, nilitaka kwenda Ulaya tu.”
“Haiwezekani! Ni lazima nikushushe,” alisema jamaa yule.
“Kwani hapa ni wapi?”
“Afrika Kusini.”
“Hapahapa kaka kunatosha, wewe nishushe tu kisiri, hata hapa natumaini nitaishi kama nipo Ulaya,” alisema Ethan.
“Unajua kupiga mbizi?”
“Najua sana tu, nisaidie kaka, naomba unisaidie” alisema Ethan.
Aliongea kwa kujiamini sana kiasi kwamba ingekuwa ngumu kugundua kwamba mtu huyo alikuwa akidanganya, kijana huyo, pasipo kujua uwepo wa watu hao humo ndani akawafungulia mlango huku lengo lake likiwa ni kumtorosha kisiri ili asiweze kuonekana na watu wengine kwa kujua kwamba angeweza kuuawa.
Ile alipofungua mlango tu, akajikuta akivutwa ndani, akazibwa mdomo wake, akabaki akikukuruka kwa kutaka kujitoa mikononi mwa Ethan lakini hakufanikiwa, alishikwa vilivyo.
“Nisikilize,” alisema Ethan.
“Nakusikiliza, naomba usiniue,” alisema kijana yule huku akiogopa.
“Sina haja ya kukuua, nisikilize, ninataka boti ya kuondoka humu ndani,” alisema Ethan.
“Boti...boti...haturuhusiwi kuzitoa.”
“Hapana! Lazima utoe hata moja, ninataka ufanye hivyo, ninahitaji kuondoka humu,” alisema Ethan, hata sauti yake aliibadilisha na kuwa nzito.
“Naomba usiniue,” alisisitiza kijana yule.
“Sihitaji kukuua. Nitakupa fedha ili unisaidie,” alisema Ethan.
“Sawa.”
Alichokifanya ni kuyafuata maboksi yale, akalichana boksi moja na kisha kutoa bunda moja la dola laki moja na kisha kumpelekea kijana yule na kumgawia. Zilikuwa fedha nyingi mno ambazo asingeweza kuzipata hata kama angefanya kazi mfululizo ndani ya meli ile. Tamaa ikamuingia.
“Ukinifanyia kazi yangu, nakupa nyingine.”
“Kazi gani? Nipo tayari.”
“Ninahitaji kupata boti kwanza,” alisema Ethan.
“Mmmh!”
“Ni ngumu kuipata?”
“Ni ngumu sana, niambie kingine.”
“Nataka kwenda kwenye chumba cha chini ambacho kitanifanya niyaone maji vizuri kwa kupitia kwenye dirisha dogo,” alisema Ethan.
“Sawa. Ila ili iweje?”
“Unataka hela hutaki?”
“Nataka!”
“Subiri!” alisema Ethan na kisha kulifuata boksi lile na kutoa bunda jingine la fedha na kumpatia kijana yule.
“Inawezekana?”
“Bila shaka, inawezekana,” alisema kijana yule.
“Nitataka uje kunifungulia mlango wakati meli inaanza kuondoka,” alisema Ethan.
“Hakuna tatizo.”
Kila kitu kilichokuwa kikifanyika ndani ya meli hiyo ilikuwa siri kubwa. Bwana Cook alikuwa akijihusisha na biashara nyingi haramu za madawa ya kulevya na ngozi za binadamu, hakukuwa aliyekuwa akilifahamu hilo katika meli ile zaidi ya nahodha ambaye alimwamini sana.
Ndani ya meli ile kulikuwa na maboksi matano, yote yalijaa fedha kutokana na malipo aliyokuwa amelipwa barani Asia na Afrika. Fedha hizo alitaka kuzisafirisha kwa kutumia meli kwani aliogopa kutumiwa benki kwa kuhofia kushtukiwa hivyo kufuatiliwa.
Wafanyakazi wengine hawakujua hilo, walichokuwa wakikijua ni kwamba wao walikuwa wavuvi wa samaki wakubwa. Uwepo wa Ethan na Annabel ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa mno, hakukuwa na aliyekuwa akifahamu zaidi ya nahodha tu.
Hata uwepo wa maboksi yale yaliyokuwa na fedha ilikuwa siri kubwa, hakutakiwa mtu yeyote afahamu hilo kutokana na uaminifu kuwa mdogo. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya kijana yule kudanganyika kirahisi kwamba Ethan alikuwa mzamiaji aliyetaka kuelekea Marekani au Ulaya.
Alipopewa fedha zile, alishangaa, zilikuwa nyingi, ilikuwaje mzamiaji awe na fedha nyingi kiasi kile? Hakutaka kujiuliza maswali mengi, alichokiagalia ni fedha tu, hivyo akataka kufanya kama vile Ethan alivyotaka afanye, wakati meli inaondoka, akamchukua na kumpeleka katika moja ya vyumba vilivyokuwa chini ambapo huko tungesema kwamba kilikuwa chini ya bahari.
****
Siku ya kwanza ikakatika, ya pili kuingia na hatimaye wiki nzima, bado hakukuwa na taarifa za kuridhisha kutoka kwa polisi juu ya kile kilichokuwa kimeendelea katika upepelezi wao juu ya Annabel.
Kila alipokuwa akienda kituoni kuulizia, askofu hakupewa majibu ya kueleweka, alikuwa akiambiwa hivi na vile, njoo kesho bado wapelelezi wetu wanaendelea kufuatilia. Hakuwa na amani, alikosa furaha, hakujua ni kitu gani alitakiwa kukifanya ili aweze kumpata binti yake.
Hakutaka kumwambia Irakoze kwani alijua ni kwa jinsi gani angechanganyikiwa, alichokifanya ni kufuatilia kimyakimya na mwanamke huyo kila alipokuwa akiuliza, jibu lilikuwa lilelile kwamba Annabel anaendelea vizuri.
“Naomba nizungumze naye mana’ke simuni hapatikani,” alisikika Irakoze.
“Amelala! Akiamka nitakupa uongee naye,” alisema askofu Benedicto.
Kila siku alikuwa akidanganya huku akifuatilia kituoni lakini majibu yalikuwa yaleyale. Kwa sababu polisi walimfahamu sana askofu Benedicto, walichokifanya ni kutoa taarifa katika vituo vingine na hata kwenye vyombo vya habari ambapo huko wakatangaza kwamba kulikuwa na msichana aliyekuwa ametekwa na kupelekwa pasipojulikana.
Watu wakashtuka, hawakuamini kama kweli katika Tanzania hii kungekuwa na mtu ambaye angetekwa kwani mambo kama hayo yalikuwa yakisikika nchi za nje tu.
Kitendo cha picha za Annabel kuanza kusambazwa kwenye magazeti mbalimbali, askofu akahofu na kuona kwamba Irakoze angegundua kile kilichokuwa kikiendelea, alichokifanya ni kumpa taarifa tu kwani hakuwa na jinsi.
“Unasemaje?”
“Annabel hajulikani alipo.”
“Tangu lini?”
“Majuzi, yaani hapa nimechanganyikiwa,” alisema askofu.
“Nakuja,” alisikika Irakoze na kukata simu.
Hakuwa na jinsi, alitakiwa kufanya kile alichokifanya, alijua kwamba Irakoze angeumia sana lakini hakukuwa na jinsi, alitakiwa kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Baada ya masaa mawili, Irakoze alifika nyumbani hapo, macho yake yalikuwa mekundu kwa sababu ya kulia sana.
“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze huku akibubujikwa na machozi.
“Subiri kwanza.”
“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze na kuanza kulia kwa sauti kubwa.
Askofu akapata kazi kubwa ya kuanza kumbembeleza, ni kweli alitakiwa kulia, mapenzi mazito aliyokuwa nayo kwa binti yake yalimfanya kuumia mno pale aliposikia kwamba alikuwa ametekwa na watu wasiojulina.
Alichokifanya askofu ili kujiondoa lawama ni kumwambia Irakoze kila kitu kilichokuwa kimetokea hasa kuhusu Ethan aliyeonekana kuwa chanzo cha kila kitu. Irakoze akajikuta akichukia, akamchukia Ethan kuliko mtu yeyote yule, hakuamini kama uwepo wa mwanaume yule ndiyo ungemfanya binti yake kutekwa na kutokujulikana mahali alipokuwa.
Alipouliza kuhusu Ethan, hata naye hakuwa akijulikana alipokuwa, hilo likamuumiza zaidi na kuona kama tayari binti yake alikuwa ameuawa na watu hao. Akajilaumu kwa kitendo cha kumwamni Ethan na kumpa nafasi ya kufika nyumbani pale huku wakati mwingine wakimwacha na binti yao.
Hawakujua wafanye nini, huo haukuwa muda wa kulaumiana au kujutia kile kilichokuwa kimefanyika, walichotakiwa kukifanya kwa wakati huo ni kukubaliana na ukweli kwamba binti yao hakuwa mikononi mwao.
Irakoze hakurudi tena chuoni, akaamua kuachana na masomo hayo na kuwa mwanamke wa nyumbani tu. Kichwa chake kilichanganyikiwa mno, kila wakati alikuwa mtu wa majonzi na hakuweza kunyamaza, alikuwa mtu wa kububujikwa na machozi tu.
Siku ziliendelea kukatika, Askofu Benedicto hakutaka kundoka nyumbani hapo, hakutaka kwenda kanisani na siku zte alitoa udhuru kwamba kulikuwa na kitu alichokuwa akikifanya hivyo asingeweza kwenda kanisani kitu ambacho hakikuwa na tatizo lolote lile.
“Annabel atarudi tu, atapatikana wala usiwe na wasiwasi,” alisema askofu huku akimwangalia Irakoze usoni. Mwanamke huyo hakuzungumza kitu zaidi ya kulia tu.
*****
Walipomaliza kunywa pombe na wanawake wao, wakawachukua na kwenda nao hotelini ambapo huko wakalala huku wakifanya nao anasa usiku mzima. Asubuhi na mapema waliamka huku pombe zikiwa kichwani, hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokitaka ni kuondoka kuelekea nchini Marekani, safari ndefu ambayo ingewachukua hata miezi miwili baharini.
Walipoondoka hotelini, wakaelekea ufukweni ambapo wakachukua boti zao na kuanza kurudi kule ilipokuwa meli yao, umbali wa kilometa mbili kutoka pale walipokuwa. Ndani ya boti walikuwa na mizinga ya pombe kali, walikuwa wakisherehekea huku wakigongesheana chupa zao kwa furaha kubwa.
Walichukua dakika kumi kuifikia meli ile ambapo wakarushiwa kamba na kisha kuingia melini huku wafanyakazi hao wakifanya machakato mzima wa kuipandisha boti ile melini.
“Wale wapumbavu wapo?” aliuliza Thorn kwa sauti ya kilevi, alikuwa akimuuliza nahodha.
“Wapo!”
“Mmewapa chakula?”
“Hapana!”
“Kawapeni! Yule mwanamke hana muda mrefu atakufa, tunataka kumtupa baharini katika mpaka wa bahari,” alisema Thorn.
“Sawa!”
Kwa kuwa uwepo wa watu hao ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa, nahodha akaenda peke yake huku akiwa ameshika sinia lililokuwa na chakula, alipofika nje ya mlango ule, aliufungua kisha kulitupia sinia lile ndani na kisha kuufunga na kurudi.
“Tayari?” aliuliza Thorn.
“Ndiyo! Nishawatupia.”
“Sawa.”
Usiku ulikuwa umeingia, safari ya kuelekea nchini Marekani ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Walikuwa wamebakiza umbali wa kilometa kama kumi ili kufika katika eneo ambalo bahari ya Indi ilikuwa ikikutana na Bahari ya Atlantiki, sehemu pekee ambayo walipanga kumtupa Annabel na kuendelea na safari yao.
Kila mmoja melini alionekana kuwa na furaha tele, walikuwa wakigongesheana chupa zao na kuendelea kunywa huku wakipiga kelele ambazo zilionekana kuwa kero kwa wafanyakazi ambao hawakuwa wakinywa kama wao.
Kijana ambaye tayari mfukoni mwake alikuwa na dola laki mbili kila wakati alikuwa akiangalia saa yake tu, alikuwa akisubiri muda ambao angekwenda kumtoa Ethan na kumpeleka katika chumba ambacho alitaka kwenda.
Ilipofika saa mbili usiku, harakaharaka akaelekea katika chumba kile, alichokifanya ni kuufungua mlango na Ethan kutoka huku akiwa amelivua shati lake na kulifunga kiunoni tayari kwa kufanya kile alichotaka kukifanya.
“Vipi?”
“Nipo tayari! Twende.”
Kijana yule akamchukua Ethan kisiri tena huku wakati mwingine akijificha kila aliposikia watu wakija upande waliokuwepo, walitembea mpaka walipofika katika mlango mkubwa ambapo hapo alimfungulia na kumwambia aingie ndani.
“Tuingie wote.”
“Kwa nini?”
“Wewe tuingie,” alisema Ethan na kijana yule kuingia naye.
Walipofika ndani, Ethan hakutaka kujificha, alimwambia kijana yule kile alichotaka kukifanya, alimwambia dhahiri kwamba hakuwa mzamiaji kama alivyomwambia bali alikuwa mtu aliyetekwa ambaye alikuwa akirudishwa nchini Marekani tayari kwa kuuawa.
Kijana yule alibaki kimya akimsikiliza. Yeye mwenyewe akabaki akishangaa kwani ndani ya meli ile hakukuwa hata na mfanyakazi mmoja aliyekuwa akijua kama humo ndani kulikuwa na mtu ambaye alikuwa akipelekwa nchini Marekani.
“Huyo mwanamke yupo wapi?”
“Nimemuacha ndani,” alijibu Ethan.
“Sawa! Kwa hiyo unataka kufanya nini mpaka umeniambia nikulete humu?” aliuliza kijana yule.
“Nataka kuzamisha meli.”
“Unasemaje?”
“Nataka kuzamisha meli, sipo tayari kurudi nchini Marekani,” alisema Ethan.
“Utaizamishaje?”
“Unakiona kidirisha kile cha kioo?”
“Ndiyo!”
“Unayaona yale maji?”
“Ndiyo! Basi ndivyo nitakavyofanya, kwa kuwa chumba hiki kipo chini, yaani chini ya bahari kwa chini, nikipasua kioo kile, maji yataingia, basi na meli itazama,” alisema Ethan.
“Mmmh!”
“Ndiyo hivyo, andaa boya lako, hakuna kurudi Marekani hapa, baada ya hapa, mimi, wewe na mke wangu tutaondoka, nenda kaandae boti tayari kwa kuondoka nayo, meli itakapoanza kuzama, njoo na boti katika upande wa chumba chetu, baada ya hapo, nakuahidi utakwenda kuwa milionea. Sawa?” aliuliza Ethan.
“Sawa!”
Kazi ikabaki kwa Ethan, akaanza kukivunja kioo kile kigumu kwa kutumia kipande cha chuma kilichokuwa pembeni. Japokuwa kilipiga kelele sana lakini hakukuwa na mtu aliyesikia kutoka na chumba kile kuwa karibu na injini ya meli hiyo.
Wala hazikupita dakika nyingi, kioo kile kikaanza kutoa ufa, Ethan hakuacha, aliendelea kukipiga zaidi na zaidi na baada ya muda fulani, kioo kile kikaachia na maji kuanza kuingia ndani ya meli ile, hakutaka kukaa hapo, alichokifanya ni kuufungua mlango na kuanza kutoka kwa kunyata kuelekea ndani ya chumba kile alichokuwemo Annabel.
“Vipi?”
“Tayari! Jiandae, yafunge maboksi hayo vizuri, kuna boti itakuja upande wa huku, tutatakiwa kutoka kisha kuingia botini,” alisema Ethan.
Upande wa pili, Thorn na wenzake walikuwa wakiendelea kuimba na kupiga kelele, walikuwa wamekunywa mno na walionekana kuzidiwa na ulevi, muda wote, mizinga ya pombe kali ilikuwa mikononi mwao, nyimbo walizoimba, hazikueleweka kabisa.
Hakukuwa na wafanyakazi waliokuwa wakiwafahamu wale walikuwa wakina nani, kadiri walivyoendelea kuwa ndani ya meli ile walizidi kuwa na maswali zaidi, hawakuonekana kuwa watu wazuri hata mara moja kutokana na yale waliyokuwa wakiyafanya.
Baada ya dakika kama kumi, ghafla wakaanza kuhisi kwamba meli ile ilianza kuzama. Wafanyakazi wote wakashtuka, hawakuwa na uhakika juu ya kile walichokuwa wamekihisi, walichokifanya ni kwenda kwenye vyumba vyote kuangalia.
Walipokuwa wakielekea katika chumba kile, ghafla wakaona maji mengi yakitoka kutokea mlangoni na walipoufungua mlango tu, chumba kizima kilikuwa kimejaa maji, hivyo kitendo cha kuufungua tu, maji yakawa kama yameruhusiwa.
Kila mtu alichanganyikiwa, maji yaliendelea kuingia na kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele na ndivyo meli ile ilivyoendelea kuzama. Kila mmoja akaanza kuhangaika huku na kule, walikuwa wamefika mbali mno na nchi kavu hakukuonekana, walikuwa wakiukaribia mpaka wa bahari mbili za Indi na Atlantiki.
“Chukueni maboya,” alisema nahodha huku akionekana kuchanganyikiwa, giza lilikuwa limetanda kila kona.
Kilichofanyika, wafanyakazi wakachukua maboya, kijana yule ambaye alikuwa amekwishafanya mipango na Ethan, akachukua boti iliyokuwa imefungwa nyuma ya meli ile, akaifungua kamba, ikaelekea baharini, hapohapo hakutaka kuchelewa, alichokifanya ni kujirusha majini na kuanza kupiga mbizi kuifuata boti ile, alipoifikia, akaipanda, akaiwasha na kuelekea katika upande ule aliokuwepo Ethan na Annabel ambapo napo chumba chao kilianza kujaa maji, maboksi yale matano yaliyojaa hela yalianza kuelea.

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Ijumaa.
Kumbuka hadithi yangu ya UTAJIRI WENYE UCHUNGUimeanza kwenye kundi la SIMULIZI TAMUTAMU.

Sent using Jamii Forums mobile app
Prince mambo ebu tuletee story mpya za nyemo alizopost fb mbili hii achana nayo nilishaileta humu nimeimaliza
 
Ntag nikaimalizie kusoma

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Thanks, Shunie
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom