Uchaguzi 2020 Prof. Lipumba: Ni kwanini naomba ridhaa ya kuliongoza taifa?

CUF Habari

JF-Expert Member
Dec 12, 2019
239
234
IMG_20200916_181536_339.jpg


NI KWA NINI NAOMBA RIDHAA YA KULIONGOZA TAIFA? PROF.LIPUMBA​

Na Profesa Ibrahim Haruna Lipumba

"Tunahitaji kuwekeza kwa watu, ili watu wawekeze kwenye vitu”

Tangu uhuru hakuna uwekezaji wowote wa maana ambao umefanywa kwa watu ili hatimaye watu waweze kuwekeza kwenye maendeleo ya vitu.

Maadui wakuu watatu wa taifa wa tangu uhuru – yaani ujinga, maradhi na umaskini – hadi leo, miaka 59 baadaye, bado wanatuandama; tena kwa kiwango cha juu.

Ukichunguza kwa umakini sababu ya haya yote ni uwekezaji mdogo ambao umekuwa ukifanyika kwa watu.

Raslimali watu imepuuzwa. Upuuzaji huu unatuletea matatizo makubwa sana kama taifa.

Ujinga tuliodhamiria kuupiga vita tangu tunapata uhuru leo umekuwa kama sehemu ya utamaduni wetu. Leo tuna vijana waliomaliza sekondari na vyuo ambao hata kuandika vizuri ni matatizo.

Kila sekta imejaa watumishi ambao uwezo wao ni mdogo – hawana viwango.

Elimu yetu iko katika hali mbaya, inahitaji kukwamuliwa.

Bila elimu bora, tena kwa watu walio wengi, tutabaki kuwa taifa la majaribio na linaloendeshwa kwa kubahatisha kila siku! Tunahitaji mapinduzi makubwa katika sekta ya elimu ili kujenga taifa lenye ushindani katika jumuiya ya kimataifa.

Miaka 59 baada ya uhuru bado Watanzania wanakabiliwa na tatizo kubwa la utapiamlo. Lishe duni, ambayo wakati mwingine haishibishi pia, imekuwa ni sehemu ya utamaduni wa Kitanzania. Hali hii imesababisha Watanzania wengi kupata udumavu wa mwili, mtindio wa ubongo na uwezo mdogo wa kukabiliana na maradhi mbalimbali.

Nguvu kazi ambayo haina afya bora ya kimwili na kiakili haiwezi kufanya kazi kwa tija na ufanisi. Sehemu kubwa ya umasikini wetu unatokana na uzalishaji mdogo. Uzalishaji mdogo ni zao la tija na ufanisi mdogo.

Kwa mujibu wa takwimu za serikali, leo Watanzania wanaokabiliwa na umasikini wa kutupwa (wanaoishi kwa shilingi 50,000/- kwa mwezi au chini ya hapo) ni zaidi ya milioni 14!
Mtu maskini haoni thamani ya chochote zaidi ya kuishi leo.

Tumeshuhudia watu waking’oa vyuma vya reli, vyuma vya madaraja na mifuniko ya chemba za barabarani ili wakauze kwenye chuma chakavu!

Tumeshuhudia wavuvi maskini wakitumia sumu na mabomu kuvua samaki bila kutafakari kwamba wanachokifanya kinaweza kuwaondolea hata hicho kipato kidogo wanachokipata sasa, baada ya miaka michache tu.

Kuna maeneo watu wamegawiwa vyandarua vya bure kwa ajili ya kujikinga na mbu wanaosambaza malaria, wao wamevigeuza kuwa nyavu za kuvulia dagaa!

Tunashuhudia utendaji mbaya kabisa ndani ya taasisi za umma kwa sababu tu watumishi wanahitaji rushwa ya kujikimu.

Mifano ya jinsi umasikini unavyoiharibu jamii yetu na kuifanya kuwa jamii ya hovyo ni mingi sana na haiwezekani kuitaja yote hapa. Itoshe tu kusema kwamba suala la umasikini haliwezi kuendelea kufumbiwa macho.

Ni muhimu tukajua kuwa hatutaweza kuondoa umaskini bila kubadili kwanza namna tunavyofikiri. Tunahitaji kutambua kuwa maendeleo ya kweli yanaanzia kwa watu ndipo yaende kwenye vitu na siyo kinyume chake.

Kwa mara nyingine tena ifikapo Oktoba 2020 wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tutapiga Kura kuchagua Rais, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wa nchi yetu. Huu utakuwa ni Uchaguzi Mkuu wa sita (6) kufanyika nchini chini ya mfumo wa vyama vingi.

Tunaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wakati nchi yetu ikiwa njia panda, Watanzania wamechoshwa na hadaa na ngulai za CCM.

Umasikini unaongezeka, ajira zimetoweka, ufisadi na rushwa bado havijatoweka na Mafisadi waliostahili kufikishwa Mahakama ya Ufisadi leo wanajisafisha kwa tendo la kubadili vyama tu.

Serikali ya CCM imeshindwa kuboresha maisha ya Mtanzania. Hali ya maisha imezidi kuwa ngumu mpaka vijana wameanzisha msamiati mpya wa "Vyuma Vimekaza".

Wafanyakazi wana hali mbaya kutokana na serikali kushindwa kuboresha mishahara na stahiki zao nyingine kuendana na kupanda kwa gharama za maisha.

Ufisadi na rushwa zinaendelea kuimarika nchini na CCM imegawika mapande mapande. CCM kila uchao inazidi kuhama kutoka kuwa chama cha siasa na kuelemea zaidi kuwa chama Dola. Ni ukweli usio na shaka kwamba bila dola CCM itasambaratika.

Watanzania tutajuta ikiwa tutaruhusu ufisadi mkubwa wa wizi wa kura na kuipa fursa CCM ya kuendelea kutawala.

CCM haina dira ya kuongoza nchi na kusimamia utawala bora. Imeshindwa kutumia utajiri mkubwa tulionao wa rasilimali na maliasili ya taifa kwa manufaa ya wananchi wote na badala yake leo Tanzania imeendelea kuwa omba omba wa kimataifa.

Kumbuka jinsi tulivyonyukana na hata kutamani kuuana kwa sababu ya Mkopo wa Bilioni 500 kutoka Benki ya Dunia katika kipindi cha Januari na Aprili 2020.

Mapato ya ndani hayakidhi kulipia matumizi ya kawaida pamoja na kulipia madeni ya ndani na ya nje. Kimsingi bajeti ya maendeleo inategemea mikopo na misaada.

Malengo ya Maendeleo Endelevu yaliyowekwa na Umoja wa Mataifa mwaka 2015 yana nia ya kufuta umaskini katika nyanja zake zote ifikapo mwaka 2030, kwa kutekeleza kwa vitendo haki za kiuchumi, kijamii, kisiasa na kimazingira.

Inatia moyo sana kwamba hata kabla ya Jumuiya ya Kimataifa kuyakubali na kuyatangaza Malengo ya Maendeleo Endelevu, tayari sera za CUF za haki Sawa na furaha kwa Wote zilishajikita katika kufanikisha malengo hayo haraka iwezekanavyo.

Hivyo basi, Ilani ya CUF, pamoja na mambo mengine inafafanua, sanjari na kupendekeza hatua stahiki, ili kufanikisha Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Dunia 2030.

Malengo haya ni kuwa ifikapo 2030 tuwe na Tanzania ambayo:-

1. Haina umaskini

2. Wananchi hawana njaa. Wanapata chakula cha kutosha na lishe bora

3. Wana huduma za msingi za afya na ustawi bora

4. Watoto wanapata elimu bora na wananchi wana fursa ya kujiendeleza kielimu katika maisha yao yote.

5. Kuna usawa wa jinsia. Haki za wanawake zinalindwa.

6. Wananchi wote wanapata maji safi na salama na wanaishi katika mazingira masafi

7. Wananchi wanatumia nishati safi na salama kwa sayari yetu, lakini yenye gharama nafuu

8. Wananchi wanapata ajira stahiki kutokana na Uchumi unaokua vizuri na kwa kasi

9. Inaendeleza Viwanda vya kisasa, Inachochea ubunifu na Inajenga Miundombinu yenye kukidhi haja

10. Inanyanyua pato la mwananchi wa kawaida kwa kasi ili kupunguza tofauti za mali na vipato kati ya Wananchi

11. Inaendeleza Miji bora kwa vigezo vya kisasa

12. Ina Matumizi na uzalishaji wenye kukidhi mahitaji ya kiuchumi ya Wananchi na Taifa.

13. Imechukua hatua za kuhuisha na kulinda Mazingira

14. Inalinda uhai wa viumbe wa Majini - mito, maziwa na bahari

15. Inalinda uhai wa viumbe wa Juu ya ardhi - misitu,wanyama na viumbe wengine

16. Ina Amani, Haki, Furaha na Taasisi za kiutawala zilizo bora na imara

17. Inashirikiana kwa karibu na Jumuia ya kimataifa kufikia malengo.

Wachambuzi wengi wa maendeleo ya uchumi na jamii wanaamini kuwa kuongezeka kwa furaha ya wananchi kwa ujumla wao ndiyo kipimo mahsusi cha maendeleo ya uchumi na jamii.

Mambo muhimu yanayowafanya wananchi kuwa na furaha ni pamoja na jamii inayojaliana, yenye uhuru, yenye ukarimu, yenye kuaminiana, ambayo watu wake wana afya njema, ambayo watu wake wana kipato kizuri, na yenye utawala bora.

Tangu mwaka 2012, Taarifa ya Furaha Duniani - World Happiness Report - imekuwa ikitolewa kila mwaka kusaidia kazi za Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Viongozi wa Juu kuhusu Maisha Bora na Furaha.

Taarifa ya Furaha Duniani - World Happiness Report 2020 inaonyesha kuwaTanzania ni nchi ya 148 kati ya nchi 153 kwa kuwa na furaha duniani.

Watanzania hatuna furaha kwa sababu ya hali ngumu ya maisha, huduma mbovu za afya, mazingira ya kutoaminiana, uvunjifu wa haki za binadamu na ukosefu wa uhuru na utawala bora.

Watanzania wenye kutafakari mambo kwa kina wameweka matumaini yao kwa Chama cha CUF na misingi ya sera zake ya "Haki Sawa na Furaha kwa wote" na "Kujenga uchumi imara unaoongeza ajira na utakaoleta neema na tija kwa wote".

Nchi yetu imerudi katika Mfumo wa Vyama Vingi muda mrefu sasa na CCM imeendelea kutawala.Wananchi wanaendelea kuteseka kwa kuona matatizo yao yakizidi kuongezeka bila kuchukuliwa kwa hatua za msingi kuyatatua. Hali hii imewafanya wananchi wengi - hasa vijana na wanawake - kuwa na shauku kubwa ya kuona utawala wa nchi yetu unabadilishwa kwa amani, kupitia sanduku la kura.

CUF kwa kutambua nafasi yake katika kuyaongoza mabadiliko yanayohitajika, hususan kutokana na mjengeko wake wa kuwa kweli ni Chama cha kitaifa chenye kukubalika na chenye mtandao mpana katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano, imeibuka na sera zilizojikita katika msingi na kauli mbiu ya HAKI SAWA NA FURAHA KWA WOTE.

Msingi huu ni Dira ya mabadiliko na ndiyo kitovu cha ILANI yetu ya uchaguzi.

Msingi huu chini ya Serikali ya CUF utaibeba Tanzania mpya inayojali haki sawa kwa wote na kuwahakikishia wananchi wote FURAHA.

Mambo muhimu yaliyobebwa na Ilani hii ni haya yafuatayo:-

1. KUUNDA SERIKALI YA UMOJA WA KITAIFA

Nchi yetu imejaa ufisadi, ubinafsi, migawanyiko, kuumizana, ubaguzi, kutokuaminiana, chuki, kukata tamaa na huzuni. Haya ni majeraha yanayohitaji kutibiwa na kuwarejeshea wananchi matumaini.

Tumefikia hapa tulipo kutokana na Tanzania kukosa taasisi imara za kusimamia uendeshaji wake. Taasisi zilizoko uimara wake ni wa kinadharia kuliko wa kuhalisia. Katika mazingira haya mustakabali wa nchi umekuwa ukitegemea zaidi haiiba na matakwa ya rais aliyeko madarakani kuliko taratibu za kitaasisi.

CUF inataka nchi iwe na taasisi imara zinazounda mfumo madhubuti ambao utahakikisha kuwa nchi iko salama bila kujali ni chama gani kiko kwenye nadaraka.

Kuunda mfumo huu kunahitaji nguvu ya pamoja na ushirikishwaji wa kila Mtanzania. Kwa sababu hii CUF inapendekeza serikali ya umoja wa kitaifa. Serikali hii jumuishi itakuwa na jukumu la kujenga mfumo unaohitajika.

Serikali ya Umoja wa Kitaifa chini ya CUF itaweka misingi ya kuhakikisha kuwa taifa linakuwa na Demokrasia ya kweli. Serikali ya umoja wa kitaifa itakamilisha mchakato wa kupata katiba mpya yenye misingi imara ya demokrasia na utawala bora. Katiba ambayo pamoja na mambo mengine itatenganisha kikamilifu mamlaka na nguvu za mihimili mbalimbali, italinda misingi ya ushindani wa kisiasa, itapanua na kukuza haki za kiraia, na itahakikisha uwepo wa uhuru wa kutosha wa vyombo vya habari na fursa ya kujieleza.

Tunahitaji kuwa na katiba nzuri inayompa kila Mtanzania uhuru wa kweli wa kuchagua na au kuchaguliwa. Tunahitaji kuwa na Muungano wa Watanganyika na Wazanzibari usio na mashaka ndani yake kwa pande zote mbili. Tunahitaji Umoja wa Kitaifa wa kweli ambapo ubaguzi wa aina yoyote iwe ni wa jinsia, rangi, dini au ulemavu utakuwa ni jinai inayoadhibiwa kwa mujibu wa sheria. Aidha tunahitaji kuwa na katiba inayojilinda isivunjwe na wanasiasa walioko madarakani kwa ajili ya maslahi yao binafsi na maslahi ya makundi wanayoshabikia.
Katiba ya sasa haikidhi vigezo vinavyohitajika ili kuchochea maendeleo ya demokrasia nchini mwetu.

Chini ya Sera za HAKI SAWA NA FURAHA KWA WOTE, serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itaandaa utaratibu unaofaa wa kupata Katiba Mpya ya wananchi.

2.KUTOKOMEZA NJAA NA KUHAKIKISHA LISHE BORA KWA WAJAWAZITO NA WATOTO

Kuhakikisha kuwa kila mwananchi anakuwa na uwezo au kuwezeshwa kupata milo mitatu kwa siku. Hatua za makusudi zitachukuliwa kuhakikisha kuwa kina mama wajawazito na watoto wachanga wanapata lishe bora itakayowasaidia watoto kujengeka vizuri katika viungo vya mwili, kinga ya mwili na ubongo, ili waweze kushiriki kikamilifu katika kujielimisha na kujiendeleza.

3. KUTOA HUDUMA BORA YA AFYA NA KUDHIBITI VIFO VYA WAJAWAZITO NA WATOTO

Kuhakikisha kuwa Bajeti ya Wizara ya Afya inapanda na kufikia asilimia 15 ya Bajeti ndani ya miaka 10 ijayo. Ongezeko la bajeti litawezesha katika kuandaa miundombinu ya kisasa, wataalam, vifaa tiba na vipimo vya kutosha kwa maradhi yote.

Aidha ongezeko la bajeti litawezesha kutenga fungu maalum kwa ajili ya kukabili maradhi ya milipuko kama COVID-19 kwa kadri yatakavyojitokeza. Ili kuhakikisha kuwa kila raia ana haki na anapata huduma za msingi za afya, Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itahakikisha asilimia 70 ya Watanzania wote wana Bima ya Afya ifikapo 2025 na asilimia 100 ifikapo 2028.

Hatua maalumu zitachukuliwa kuhakikisha kuwa huduma za uzazi bila malipo zinapatikana kwa kila mama mjamzito ili kupunguza vifo vingi vinavyotokea ambavyo vinadhibitika.

4. KUWAHU
DUMIA WAZEE WALIOLITUMIKIA TAIFA LETU

Kuweka utaratibu wa kitaifa wa hifadhi ya wazee itakayohusisha jamii nzima kuwalea wazee wetu ambao wengi wao baada ya kulitumikia Taifa letu kwa muda mrefu wanaishi katika dimbwi la umasikini wa kutisha. Hatua kwa hatua kila mzee atakuwa na haki ya kulipwa kila mwezi fao la uzee kwa ajili ya hifadhi yake.

5. KUWASAIDIA WALEMAVU NA KUWAWEZESHA KUPATA ELIMU NA AJIRA

Serikali itakayoongozwa na CUF itatenga fungu maalum la kuwasaidia walemavu wapate elimu, matibabu na vifaa vya kuwapunguzia dhiki ya ulemavu walionao pamoja na kutoa mafunzo stahiki waweze kuajirika na kuajiriwa katika fani mbalimbali kwa mazingira bora zaidi kuliko ilivyo sasa.

Hii inatokana na ukweli kwamba zaidi ya asilimia 10 ya Watanzania wote ni watu wenye ulemavu. Watu wenye ulemavu wana mahitaji ya msingi sawa na watu wengine na wana mahitaji ya ziada kulingana na aina ya ulemavu walionao.

6. USIMAMIZI WA ELIMU BORA NA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA YA HABARI NA MAWASILINO

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itahakikisha kuwa watoto wote wa Tanzania wanakuwa na haki ya kupata elimu bora ya msingi, elimu ya sekondari na elimu ya juu.

Kila raia atahimizwa kujiendeleza kielimu hasa kwa kutumia vizuri teknolojia ya habari na mawasiliano.

Serikali ya umoja wa kitaifa itakayoundwa na CUF itatoa kipaumbele maalum katika kuwaendeleza kielimu wasichana na kujenga misingi imara ya kuendeleza elimu za hisabati, sayansi na teknolojia. Aidha, Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itahakikisha kwamba ifikapo 2025 asilimia 50 ya Shule za Umma nchini zinakuwa na Uwezo wa Kufundisha wanafunzi wake kwa njia ya TEHAMA na asilimia 100 ifikapo 2028. Hili litawezesha wanafunzi wengi kuendelea na masomo hata pale shule zitakapofungwa kwa dharura kama tulivyojifunza kupitia janga la CORONA

7. KUSIMAMIA MAENDELEO YA KIUCHUMI NCHINI

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itajenga uchumi wa kisasa wenye ushindani kimataifa na utakaohimili misukosuko ya utandawazi, unaokuwa kwa kasi bila kuharibu mazingira, na ambao utakuwa na manufaa kwa wananchi wote. Kukua kwa uchumi kunahitaji uongozi imara
na utawala makini, mikakati na mipango mizuri ya maendeleo na utekelezaji mzuri wa mikakati na mpango hiyo.

Kujenga mazingira mazuri ya kuwekeza, kufanya biashara na ushirikiano wa kimataifa bila kuathiri uhuru wa nchi yetu. Kuweka misingi ya utawala bora na utekelezaji wa sera utakaohakikisha kuwa uchumi unakuwa kwa asilimia 8 - 10 kwa miaka kumi ijayo na kufanikisha kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu mwaka 2030.

8. USIMAMIZI MAKINI KATIKA SEKTA YA KILIMO NA MAENDELEO YA VIWANDA

Dira ya Mabadiliko ya CUF inakipa kilimo nafasi ya pekee katika mikakati ya kukuza uchumi na hivyo kuwaondolea umasikini wananchi wengi na hasa wa vijijini, na kuhakikisha Taifa linakuwa na chakula cha kutosha na ziada ya kuuza nje ya nchi.

Katika miaka mitano ijayo, bajeti ya sekta ya kilimo itakayoandaliwa na serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itakuwa kati ya asilimia 10-15 ya bajeti yote, na italenga katika kuimarisha maeneo yafuatayo:

• Utafiti na elimu kwa wakulima na huduma za ugani;

• Upatikanaji wa mbolea na pembejeo nyingine kwa bei nafuu;

• Masoko ya uhakika;

• Bei nzuri kwa wakulima;

• Kutengeneza barabara za vijijini; na

• Kusambaza umeme vijijini kwa kutumia nishati mbadala
kama vile biogas inayotokana na mabaki ya mimea na vinyesi vya mifugo, jua na upepo.

Wakulima watahamasishwa kutumia TEHAMA kupata taarifa za masoko ya mazao na pembejeo, hali ya hewa na mafunzo ya kilimo bora.

Dira ya mabadiliko ya CUF inakusudia kuasisi Mapinduzi ya kweli ya kilimo nchini, yatakayoongeza uzalishaji na tija kwa kuijenga upya sekta ya maendeleo ya viwanda.

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itaweka mkakati madhubuti wa kuanzisha na kuendeleza viwanda vinavyotumia malighafi ya ndani ya nchi na kuajiri watu wengi - kama vile viwanda vya nguo na mavazi, viatu na bidhaa za ngozi, vifaa vya matumizi ya nyumbani na vifaa vya umeme na elektroniki.

9. KUIMARISHA MIUNDO MBINU NA KUHAMASISHA UWEKEZAJI

Mafaniko ya kiuchumi kwa Taifa lolote lile hutegemea mfumo wa kisera na uwekezaji wa serikali katika sekta muhimu.

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itawekeza kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha miundo mbinu - biarabara, reli, bandari, mawasiliano, nishati, maji, elimu na afya.

Hii itasaidia kuvutia sekta binafsi kuwekeza katika shughuli za uzalishaji na biashara.

10. USIMAMIZI WA RASILIMALI ZA TAIFA NA NIDHAMU YA MATUMIZI YA FEDHA ZA UMMA

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itajenga mfumo mzuri wa usimamizi na nidhamu ya matumizi ya fedha za umma, itaondoa misamaha holela ya kodi na itabana myanya ya ukwepaji wa kodi. Aidha, itahakikisha kwamba sekta ya madini inachangia asilimia 30 ya thamani ya mauzo ya madini kwenye mapato ya serikali.

Serikali ya umoja wa kitaifa chini ya CUF itapambana na rushwa na ufisadi kwa kuweka mfumo imara wa kutambua viashiria na itahakikisha kuwa maliasili na rasilimali za Taifa zinatumiwa kwa umakini mkubwa na kwa manufaa ya wananchi wote.

Mimi binafsi kama Mgombea wa Urais kwa tiketi ya CUF nawaahidi Watanzania nikichaguliwa kuwa Rais nitajiwekea lengo la kuijengea heshima nchi yangu kwa kuimarisha utawala bora na uadilifu na kukuza uchumi unaotoa ajira kwa wingi na kuleta neema kwa wananchi wote.

Kazi hii nitaifanya kwa uadilifu wa hali ya juu na kuhakikisha kuwa kwa mara ya kwanza Rais wa Tanzania atakapostaafu ataingia kwenye nafasi bora ya kupata tuzo ya Mo Ibrahim inayotolewa kwa kuongoza nchi vizuri kwa kuheshimu na kulinda haki za binadamu, kupambana na ufisadi kwa mafanikio, kukuza uchumi na kuutokomeza umasikini.
 
Nataka nione ushujaaa wa Lipumba baada ya uchaguzi pale ambapo hatakuwa hana mbunge hata 1 na hana ruzuku.

Waliingizwa mkenge yeye na Mama Tanzania sasa wanajuta,utadhani hawakujua mchezo wa siasa unabadilika,na kule Vunjo kimei kamkalia kooni.
 
Ukisoma maelezo yake wana vitu vya maana vinavyonyesha tofauti yao na chama tawala ila kwa kuwa wengi tumekalia ushabiki na uvivu wankusoma tutaishia kutoa kejeli
 
Back
Top Bottom