Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 43,037
- 34,741
Mgombea Ubunge Jimbo la Arumeru Mashariki, Siyoi Sumari
Siasa za kushutumiana, kupakana matope zimeendelea kutawala kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Arumeru Mashariki, mkoani Arusha na safari hii, wazee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Kata ya Akeri, wakiwalalamikia walimu wa shule za msingi na sekondari kwamba wamekigeuka chama hicho na kushabikia Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa kuwafundisha wanafunzi wao kutumia msemo unaotumiwa na Chadema wa
'peoples power'
Kadhalika, wazee hao wamelaani wafuasi wa Chadema, kwa kupiga yowe kwenye mikutano ya kampeni na kila wanapoona wafuasi wa CCM waliovalia sare za chama.
Wakizungumza na waandishi wa habari katika tawi la CCM la Patandi lililopo eneo la Tengeru, wazee hao walisema jana kuwa mila na desturi za Kimeru zinazua yowe kupigwa bila sababu hasa kama hakuna msiba, lakini inashangaza kuona
kwamba hata watoto wadogo wanapiga yowe na kuonyesha alama ya vidole viwili pindi wanapoona wafuasi wa CCM.
Mweyekiti wa Jumuiya ya wazazi wa CCM Kata ya Akeri, Ndewariyo Kaaya, alisema: Inasikitisha kwamba hadi watoto
wadogo wa shule wakiona mtu amevaa nguo zetu (CCM) wanapiga yowe kitu ambacho ni kibaya kwani ni uchuro na ni laana mbaya sana, labda pengine serikali yetu itusaidie.
Tunatukanwa hadi na watoto wadogo kabisa, ukipita wanasema peoples power na kuonyesha vidole viwili, aliongeza mzee huyo.
Mzee Benard Kaaya, mjumbe wa Kamati ya Siasa katika kata hiyo, alisema sehemu kubwa ya watu wanaopiga yowe ni vijana pamoja na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari na kuwataka wazazi wawakanye watoto wao kushiriki jambo hilo.
Walimu tena hapa sekondari ya Akeri, badala ya kuwafundisha watoto wetu masomo, wanawafundisha peoples power, wanawafundisha siasa, hebu tukemee vitendo hivi jamani, nawaomba mabalozi mliopo hapa tusiruhusu yowe tena kwenye kata yetu, alisema Mzee Kaaya na kuongeza: Hata leo asubuhi watoto wadogo wamenionyesha alama ya Chadema.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM (UWT) tawi la Akeri, Luyana Sikawa, alisema: Hawa walimu wamesahau kwamba wapo kwenye ajira ya CCM, wametugeuka na hawapo kabisa na sisi, hili ni jambo baya sana.
Alimlaani mgombea wa Chadema, Joshua Nassari, kwa kutangaza kwamba atafuta ushuru unaolipwa mara mbili mbili kwenye soko la Tengeru akieleza kwamba tangazo lake limeibua vurugu sokoni hapo.
Mgombea wa Chadema asilete vita pale sokoni, amekuwa akitangaza kufuta ushuru kitu ambacho hakiwezekani, yeye ametamka pale sokoni matokeo yake nimekuwa nikizomewa kila mahali ninapopita, watu wananipigia yowe kila wanaponiona, alisema Sikawa, ambaye pia ni mwenyekiti wa soko hilo.
LEMA AONYWA TENA
Mzee Kaaya alimwonya mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema, akimtaka asikanyage Arumeru Mashariki kwa kuwa wazee watawaamuru vijana wa CCM wampige. Lema aache tabia yake ya kuchochea vita na tunamwambia asije hapa, maana atapata janga na tunasema kabisa akija hapa atapigwa kweli, alisema.
CHADEMA YAANZA KUTUMIA HELIKOPTA
Chadema kimeanza rasmi kutumia helikopta katika mikutano kampeni huku Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbroad Slaa, akiendelea kuishutumu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na kudai kuwa Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji Mstaafu Damian Lubuva, ameanza vibaya kwa kuchakachua daftari la wapiga kura.
Hayo aliyasema jana alipokuwa akihutumbia mikutano wa hadhara katika vijiji vya Ngurudoto, Ngarananyuki na Sakila, huku umati mkubwa wa watu ukiwa umezunguka eneo hilo wakiangalia helikopta iliyoanza kutumika jana.
Alisema kuwa Nec imeanza mtihani huo vibaya kwa kutoa daftari jipya la wapiga kura, ambalo limechakachuliwa na kuongezwa vituo hewa zaidi ya 50.
Kama hawatarekebisha hili, safari hii hatutakubaliana na hili suala la kuibeba CCM kwa wazi, mtageuza Arumeru kuwa chanzo cha machafuko kama ilivyo Tunisia, alisema.
Dk. Slaa aliongeza kuwa mbali na kuchakachua daftari hilo, pia Nec iliwapatika CCM barua ya orodha ya wapiga kura siku saba kabla, lakini wao na vyama vingine hawajapata wakati wako katika orodha moja ya kucheza mpira wa uchaguzi.
Hivi inawezekanaje mpira unachezwa pamoja wa Simba na Yanga, halafu timu moja inapendelewa na refa, alafu wengine wakaangaia tu, lazima itatokeo vurugu, kuepuka hili Tume iangalie maana tumewashitukia, alisema Dk. Slaa.
Aidha, alisema ni vema kama serikali walitaka CCM ishinde uchaguzi huo na nyingine, vema wasingeleta uchaguzi kiini macho kwani wanavifunika mablanketi vyama vingine kwa lengo la kuipa ushindi CCM.
Katika hatua nyingine, Dk. Slaa alimjibu Mkuu wa Operasheni ya Uchaguzi wa Jeshi la Polisi, Isaya Mngulu, kuwa yeye amesomea sheria na hajasomea siasa na hakuna shule ya kusomea siasa.
Huyu Mngulu anasema eti kama tunataka Polisi tuachie wenyewe waliosomea sababu sisi tumesomea siasa, mimi namwambia siasa haisomewi bali nilichosomea sheria na nikachaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama, ila mimi kilio changu Polisi watende haki na sio kuibeba CCM, alisema.
NASSARI AJINADI
Mgombea wa chama hicho, Joshua Nassari, aliomba kupigiwa kura, ili awe mbunge wa wananchi atakayetatua kero zao zilizoshindikana kwa miaka 50 ya Uhuru.
Nassari pia aliwaambia wapiga kura wake kuwa hawahitaji uchawi Arumeru wala muujiza wowote, bali wanahitaji mkombozi wa kweli, ambaye ni yeye mwenye dhamira madhubuti ya kuwatoa wananchi kwenye hatua moja kwenda nyingine.
SIOI AOMBA KURA
Mgombea wa CCM, Sioi Sumari, ameahidi kutatua kero mbalimbali, ikiwemo ya kuiboresha shule ya sekondari ya wasichana ya Songoro.
Sioi alitoa ahadi hiyo wakati akiomba kura katika vijiji vya Mulala, Songoro, na Sura. Alisema kuna changamoto mbalimbali zinazoikabili shule hiyo ikiwemo upungufu wa vifaa vya maabara na kwamba wamchague ili kusimamia uboreshaji wa shule hiyo kwenda kwa wakati.
Mkinipa ridhaa ya kuwa mbunge wenu nitahakikisha nasimamia uboreshaji wa shule ya Songoro na mradi huu unakamilika kwa wakati, alisema.
Alisema pia atahakikisha anasimamia ukamilishaji wa ujenzi ya zahanati iliyopo kijiji cha Mulala kwa kuwa tayari fedha zimetengwa kwa ajili ya kumalizia zahanati hiyo.
NEC: FANYENI KAMPENI KWA UTULIVU
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imevitaka vyama katika jimbo la Arumeru Mashariki kufanya uchaguzi kwa amani na utulivu na kufuata maadili na kanuni za uchaguzi.
Nec pia imesisitiza kutofanya uandikishaji upya wa wapiga kura katika jimbo hilo badala yake litatumika daftari lililotumika mwaka 2010.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Lubuva alisema kampeni za uchaguzi zikiendeshwa kwa amani na utulivu hata siku ya kupiga kura wananchi nao watakuwa huru kwa kumchagua kiongozi wamtakaye.
Vyama vyote tuliwekeana saini ya kuendesha kampeni kwa amani na utulivu na watafuata maadili ya Tume ya Uchaguzi, pasipo kuwa na matusi yoyote, hivyo navitaka vyama vyote kulizingatia hilo, alisema Jaji Lubuva.
Lubuva aliongeza kuwa Tume imebaini kasoro mbalimbali zilizojitokeza katika daftari la uandikishwaji katika uchaguzi wa 2010 hivyo kutafanyika marekebisho kwa ajili ya uchaguzi wa sasa Arumeru Mashariki, lakini hakutakuwa na uandikishaji upya.
Alisema Tume imeshafanya marekebisho hayo na kuwaingiza wapiga kura 54 ambao taarifa zao haziwepo katika daftari la wapiga kura na kubaini wapiga kura 28 waliojiandikisha zaidi ya mara moja katika daftari lililotumika katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
WANAHARAKATI WATUMA WAANGALIZI
Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu (LHRC) kimepeleka timu ya waangalizi wa katika Jimbo la Arumeru Mashariki kama utafanyika katika mazingira huru na haki bila ukiukwaji wa haki za binaadamu.
Mratibu wa Uchaguzi kituo cha Sheria wa LHRC, Merick Luvinga, aliliambia NIPASHE kuwa timu hiyo iliondoka jana kwenda Arusha.
Alisema leo atatoa idadi kamili ya wamaharakati waliokwenda sambamba na maeneo ambayo watasambazwa.
Imeandikwa na Restuta James, Charles Ole Ngereza, Cynthia Mwilolezi, Arusha, Gwamaka Alipipi na Emmanuel Kimweri, Dar.
CHANZO: NIPASHE