Kufukuza watu ni moja ya hatua za kushughulikia ufisadi lakini ndogo sana hasa ukizingatia jinsi nchi yetu ilivyokuwa ikiendeshwa toka juu (Ikulu) kwa mfumo wa kifisadi. Kuna watumishi wengi tu waliolazimika "kufanikisha" ufisadi wa wakubwa wao ili wadumu kazini au wapandishwe vyeo. Wapo waliofukuzwa kazi kwa kujifanya "wanoko" sana.
Kazi kubwa sana inayotakiwa kufanywa kwa haraka ni kuminya mianya kadhaa iliyotegwa huko nyuma inayoliibia taifa kiasi kikubwa cha fedha za umma. Kwa mfano mkataba wa (IPTL) ni janga la taifa usipositishwa mapema. Mingine kama ya Symbion/Richmond, gesi, madini nayo ichunguzwe na kuwekwa sawa asap. Kwa bahati mbaya waliohusika kuandaa mikataba yenye ufisadi mkubwa unaoibana serikali ni kama vile hawagusiki (the untouchables)!
Kuziba mianya hiyo kukiambatana na kuwachukulia hatua za kisheria wahusika wakuu (mafisadi papa) ndipo tutakapoanza kupata mabadiliko ya kweli tunayotarajia. Kutimua watendaji wa umma kumesaidia kutoa ujumbe kwamba Ikulu ya safari hii ni nyingine lakini bila mianya kudhibitiwa ni suala la muda tu tutarudi kulekule. Halafu inawezekana pia kuna wahanga wengi waliotimuliwa wakitekeleza matakwa ya mabosi wao kwa jinsi navyoifahamu serikali.
La muhimu zaidi ni kukamilisha Katiba itakayoondoa fursa za kifisadi na kusimamia haki za wananchi wote.