Kwa jina lake manani, muumba wa vyote vitu
Mola aso mfanani, halinganishwi na mtu
Amenipa mtihani, na leo si mali kitu
NINATANGAZA MSIBA , MAMA AMENITOKA
Kwa 'kwikwi' najililia, msiba umenipata
Sina pakushikilia, nimejawa na matata
Mama katoka dunia, ni wapi nitakamata
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Machozi yabubujika, nimejawa na huzuni
Mama alivyofutika, ni kama niko ndotoni
Uhai umezimika, na sasa mimi ni duni
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Maradhi yalimwandama, akawa yu kitandani
Akakosa raha mama, Afya ikawa tabuni
wanawe tulishikana, kujua chanzo ni nini
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Sukari ikawa juu, kifua kilimbana
Akavimba na miguu, Dawa zilishindikana
Pumzi ikakata puu, kaitwa kwa maulana
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Alikuwa ni rafiki, na mengi aliusia
Nisipende unafiki, na maovu ya dunia
Dunia ina mikiki, ni vyema kuzingatia
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Nishikane na ibada, mama alisisitiza
Niheshimu wangu dada, nisipende kujikweza
Leo sina msaada, mwenzenu mie nawaza
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Ewe mola rahmani, msitiri mama yangu
Atulie kaburini, asipatwe na machungu
Muepushe ya motoni, mpe mema kwa mafungu
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
Na hapa ninasimama, moyoni bado nalia
Kaondoka wangu mama, naona chungu dunia
siwezi hata kusema, unyonge umezidia
NINATANGAZA MSIBA, MAMA AMENITOKA
"INNA LILAH WAINNA ILAYH RAJ'UUN"