Ni kweli watawala wanapendelea walikozaliwa

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
[h=1][/h]

picture-73.jpg

Na Nyaronyo Kicheere - Imechapwa 01 February 2012




WIKI iliyopita niliandika makala iliyohusu mambo mawili. Jambo la kwanza lilihusu umuhimu wa barabara ya Musoma – Arusha inayokatisha hifadhi ya Serengeti; na pili upendeleo unaoonekana kufanywa na watawala wa sasa kwa maeneo wanayotoka.


Makala hayo yamepokewa kwa hisia tofauti. Baadhi wameunga mkono na wengine wamedai kwamba miradi niliyotaja ilikuwapo kwenye mipango na kwamba watawala niliowalalamikia wanatekeleza tu mipango waliyokuta imekwishaandaliwa. Lakini kabla ya kulijadili hili kwa undani, nianze na barabara ya Serengeti.

Mwanzo tulipata mwekezaji, kampuni ya TATA kutoka India ikitaka kuwekeza kwenye ujenzi wa kiwanda cha magadi ziwa Natron. Mwekezaji akawa tayari kujenga barabara ya lami na reli kutoka Arusha hadi Ziwa Natron kuwezesha uwekezaji huo.


Wakajitokeza wanaojiita wanamazingira na vyama vyao kutoka Kenya vinavyofadhiliwa na Wazungu wenye miradi ya mahoteli kwenye hifadhi za Kenya kupinga huku wakiungwa mkono na wanamazingira wa Tanzania ambao hawafanyi vikao mpaka wenye mahoteli Kenya watoe ruzuku.


Baada ya mradi wa magadi kuyeyuka “wanamazingira” hao hao wa Ulaya wenye mahoteli Kenya wamezuka sasa kupinga ujenzi wa barabara ya Musoma – Arusha wakidai eti itaharibu mazingira na hasa uhamaji wa nyumbu kutoka Serengeti kwenda Masai Mara nchini humo. Lakini ni lini maendeleo hayakuharibu mazingira duniani hapa?


Huko Ulaya Wakenya wanajitangaza kwamba hifadhi zao zinafikika nyakati zote za mwaka kwa barabara za lami na kwamba hifadhi za Tanzania hazina miundombinu mizuri, zinafikika kwa ndege tu na hivyo ni ghali kuzitembelea. Hifadhi za Kenya zimejengwa barabara na reli, za Afrika Kusini zimejengwa barabara, reli na viwanja vya ndege ila za Tanzania zisijengwe miundombinu kwani inaharibu mazingira!


Wakati umefika Watanzania tufuate mfano wa Russia. Wanamazingira walipopinga ujenzi wa barabara kupitia msitu wa Khimki, Rais wa Russia, wakati huo, Vladmir Putin alisema, “Haijawahi kutokea maendeleo ya binadamu yakafanyika bila kuingiliana na mazingira.


Kila wakati maendeleo ya binadamu yalipewa umuhimu. Ukijenga nyumba, ukilima shamba, ukichimba madini, lolote utakalofanya lazima mazingira yataathirika ili kufanikisha maendeleo ya binadamu.” Na barabara hiyo ilijengwa. Nasi tujenge barabara ya Arusha – Musoma.


Hoja kwamba watawala wazaliwa wa Mara hawakupendelea mkoa wa Mara lakini watawala waliofuata baada ya utawala wa akina Julius Nyerere na Joseph Warioba wanajenga makwao kwanza na kutoa picha ya upendeleo wa waziwazi kwa maeneo wanayotoka.


Mifano niliyotoa ni uundwaji wa wilaya ya Mwanga na kupatiwa maji, umeme na barabara harakaharaka wakati mwingine ikabidi kuhamisha nguzo za umeme kutoka Ifakara na kuzipeleka Mwanga kukamilisha miradi iliyojengwa nyakati za Waziri Mkuu Mstaafu Cleopa Msuya ambaye ni mzaliwa wa Mwanga.


Pia nilitoa mifano ya miradi iliyojengwa au kutekelezwa mkoani Arusha wakati Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye akiwa madarakani ikiwa pamoja na upanuzi wa uwanja wa ndege wa Arusha na uhamishaji wa mradi wa maji wa Singida mjini na kuupeleka wilayani Hanang alikozaliwa.


Sikusahau pia ujenzi wa daraja la Mkapa kuvuka mto Rufiji wakati wa utawala wa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa na miradi ya barabara inayotekelezwa sasa mikoani Rukwa na Katavi pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege wa Mpanda alikozaliwa Waziri Mkuu Mizengo Kayanza Peter Pinda.


Kutokana na mifano hiyo ya utekelezaji wa mipango na miradi ya maendeleo wakati viongozi kutoka mikoa husika wakiwa madarakani, niliita mtindo huo kuwa ni “kutesa kwa zamu” na nikataarifu kuwa wakazi wa Mara, Monduli na Ngorongoro wangependa Rais Jakaya Kikwete agombee tena 2015 ili akamilishe ujenzi wa barabara ya Musoma – Arusha.


Wasomaji kadhaa kutoka Mara na Arusha hasa wilaya za Ngorongoro na Monduli wameniunga mkono lakini wasomaji wa wilaya ya Karatu nayo ya mkoa wa Arusha wamenipinga wakidai barabara ya kukatisha Serengeti itaharibu mazingira.


Wasomaji kutoka Kusini wamenilaani wakidai kuwa mikoa yao imenyanyasika kwa miaka mingi na kwamba Mkapa aliikuta mipango ya kujenga daraja hilo kuvuka Rufiji wakati wasomaji kutoka Rukwa wameniambia “mkuu ungekuwa umepita huko ungeshukuru kuwa Watanzania wenzako tunakombolewa.”


Katika makala ile sikusema kwamba daraja la Mkapa si muhimu. Ninacholalamikia mimi ni kuwepo mipango ya kujenga daraja hilo linalotuunganisha Watanzania wa kaskazini na wa kusini kwamba haikutekelezwa kwa miaka dahari mpaka pale alipoinigia madarakani mtu aliyezaliwa kusini!


Pia ninatambua umuhimu wa Watanzania wakazi wa Laela, Nkasi, Sumbawanga na Mpanda kupata usafiri wa uhakika na kuaminika wakati wote wa mwaka badala ya kutegemea reli ya Mpanda – Kaliua ambayo haiaminiki na treni hupatikana mara moja kwa wiki au wiki mbili.


Ninacholalamikia mimi ni kuwepo kwenye makabrasha ya serikali mipango mingi ya ujenzi wa barabara mkoani Rukwa na uwanja wa ndege Mpanda lakini haikutekelezwa hadi anapoteuliwa mtu aliyezaliwa Mpanda kuwa Waziri Mkuu, Pinda.


Nafahamu umuhimu wa uwanja wa ndege wa Arusha Mjini kwa utalii katika ukanda wa Kaskazini. Lakini nasema kwa serikali enzi za Sumaye kuacha kuendeleza viwanja vya ndege vya Songwe na Mwanza kufikia viwango vya kimataifa badala yake ikanunua mashamba ya Burka na kupanua uwanja wa Arusha (mkoani kwao wakati huo) ni uhuni.


Ukweli utabaki pale pale kwamba picha inayojengeka ni ya kila anayeteuliwa kushika wadhifa fulani mkubwa kutekeleza mipango ya maendeleo ya mkoa anakotoka kwanza jambo ambalo halijengi picha ya umoja wa kitaifa kwa sasa.


Tena yote haya yanatendeka wakati Waziri wa Ujenzi John Magufuli kapindisha barabara kongwe ya Geita – Biharamulo – Bukoba. Barabara hiyo imepindishwa Bwanga inapitia Chato nyumbani kwa Magufuli alikozaliwa kwenda Bukoba!


Kama mipango ya miradi hiyo ya maendeleo ilikuwapo na wameikuta, kwanini Magufuli ajenge kipande cha barabara akipindisha barabara ya Biharamulo kuelekea kwao? Kwanini Mkapa ndiye ajenge daraja muhimu la kwenda Kusini nyumbani kwao na siyo Ali Hassan Mwinyi au Julius Nyerere?


Kwanini Uwanja wa Mpanda pamoja na barabara za Sumbawanga zijengwe wakati Pinda akiwa Waziri Mkuu na siyo wakati wa Msuya au Sumaye? Mbaya zaidi, Sumaye na Msuya wahamishie kwao miradi ya maji na umeme kutoka Singida na Ifakara!


Wanamazingira si ndio walikataa ujenzi wa hoteli ya Sheraton iliyokuja kuitwa Royal Palm, Movenpick na sasa Serena? Hivi wanamazingira hawafanyi vikao katika hoteli hiyo sasa?


Hoja yangu inabaki pale pale kwamba watawala waache kupendelea kwao na binadamu ni muhimu kuliko nyumbu hivyo barabara kukatisha Serengeti ijengwe tena ijengwe mwaka huu 2012.


0785-788727/0718582755 kicheere@gmail.com





 
Only Julius Nyerere was not greedy was not selfish was real Tanganyikan... Others Just Me Me Me Me Leaders....
 
Usilaumu upendeleo, maana Sumbawanga au Mpanda wamekuwa wakilisha nchi tangu Uhuru lakini hawakuwa na barabara hata moja ya LAMI.

Tatizo ni sisi wenyewe kuanzia humuhumu JF tumekuwa na tabia ya kushabikia mambo na maamuzi ya nchi za jirani kwa kila kitu hata kama lengo lao ni kuendelea kutududumiza kiuchumi....(mfano mradi wa MGADI na barabara ya Serengeti)...:A S-coffee:
 
Kwa hilo la sisi kushindwa kujenga kile kiwanda cha magadi cha lake Natron nahisi Wakenya huwa wanatucheka kwa hilo.
 
Hilo liko wazi,
2005 JK aliwaahidi wananchi wa kanda ya ziwa kuwa atajenga kiwanda cha Cement Shinyanga ili bei ya Cement iwe chini kanda ya ziwa matokeo yake tumeshuhudia upanuzi wa Twiga cement Dar.
Hii ni tabia mbaya sana.
Tuzinduke
Tuamue
Tuchukue hatua
 
Back
Top Bottom