Nguvu ya neno "Hapana"

Nguvu ya neno "Hapana"

Son of Gamba

JF-Expert Member
Joined
Oct 26, 2012
Posts
4,718
Reaction score
6,979
Neno HAPANA lina maana kubwa sana kwenye maisha ya kila mwanadamu chini ya jua. Neno hili hapana kama likitumiwa sehemu sahihi na wakati sahihi basi huwa linaamua mustakabali wa maisha ya mtu husika.

Kusema hapana ni kukataa, na kila binadamu, maisha yake huwa yameathiriwa kwa namna moja ama nyingine kwa sababu katika kipindi fulani kwenye maisha yake alishindwa kuwa na uamuzi wa kukataa, alishindwa kusema HAPANA. Alishindwa kukataa vitu fulani fulani, VITU ambavyo leo hii vimeathiri kabisa mwelekeo wa maisha yake.

Kuna baadhi ya watu sababu ya kushindwa kusema “hapana” au sababu ya kuogopa macho ya watu na kushindwa kusema “hapana”, leo hii wameishia gerezani. Kuna wengine sababu hawakuwa na ujasiri wa kusema hapana, leo hii wamekuwa maskini wa kutupwa. Wengine sababu ya kuogopa kusema “hapana” wameishia kupata magonjwa yasiyotibika, magonjwa ambayo wasingepata kama tu wangekuwa na ujasiri wa kusema “HAPANA”. Wengine wamepata ulemavu wa kudumu, ulemavu ambao hawakuzaliwa nao, lakina sababu hawakuweza kusema hapana, wameishia kuwa walemavu. Wengine wameishia kupata mimba zisizotarajiwa kwa kushindwa kusema “hapana” na maisha yao yamebadilika kabisa na kuwa mabaya mno. Mbaya zaidi kuna baadhi ya watu wamepoteza maisha, sababu tu walishindwa kusema neno HAPANA, wakajikuta wanakubali kufanya vitu ambavyo mwisho wa siku, vimewasababishia wapoteza maisha yao.

Wengi wetu tulio hai leo hii huwa tunakumbuka ile siku, ile siku ambayo haiwezi kurudi tena katika maisha yetu, ile siku na ile saa ambayo tungesimama kwa ujasiri na kusema kwa sauti neno moja tu; “HAPANA”.

Wengi huwa wanakumbuka na kusema “kama siku ile ningesema “hapana”, leo hii maisha yangu yasingekuwa hivi. Kama siku ile ningekataa leo nisingekuwa hapa gerezani. Kama siku ile ningekataa, leo nisingekuwa na UKIMWI. Kama siku ile ningekataa leo nisingekuwa mlemavu. Kama siku ile ningesema “hapana” leo nisingekuwa kwenye ndoa hii ya mateso. Kama siku ile ningesema “hapana” leo hii ningekuwa bado niko na ajira yangu. Na mifano mingine mingi tu.

Neno “HAPANA” kama likitumiwa wakati sahihi na kwenye jambo la maana, basi linaweza kubeba kabisa mustakabali wa maisha yako yote. Lakini pia, neno hili hili “hapana,” likitumiwa vibaya pia huleta majuto makubwa sana baadaye. Kuna watu wengi tu leo hii wanajuta na wanasema kwanini nilipoambiwa niende shuleni nilisema “HAPANA”? Kwanini nilipoambiwa nifanye biashara nilikataa?

Kuna mifano mingi sana, ambayo siwezi kuitaja yote, lakini uwezo wa kukataa una maana kubwa sana kwenye maisha ya mwanadamu. Siku zote jifunze kukataa, kataa kabisa vitu visivyokuwa na maana kwako. Hasa hasa jifunze kuwa jasiri kukataa mbele ya marafiki, ndugu, na hata wazazi. Ukiona mtu anakushauri kufanya kitu ambacho wewe nafsi yako inakataa kabisa, basi kwa ujasiri kabisa sema “HAPANA”. Kamwe usifanye kitu chochote kile ili mradi tu umfurahishe yeye anayekushauri, usifanye kitu kwa kuogopa eti, nikikataa hivi watanionaje? Au nikikataa na kusema “HAPANA”,hivi rafiki yangu, shoga yangu, kaka, dada, mpenzi, mjomba, shangazi, bibi, babu, baba au mama atanifikiriaje? Kama ni sahihi kusema “HAPANA” basi sema hapana, tena, sema hapana kwa herufi kubwa.

Kwa watu tuliojaliwa kuwa na watoto, tunapaswa kuwafundisha watoto wetu kusema “HAPANA” mara tu wanapoanza kuongea. Tusisubiri mtoto akue na kuwa na ndevu na matiti ndio tuanze kumfundisha kusema “HAPANA”. Tunapaswa kuwafundisha watoto wetu wakiwa katika umri mdogo kusema “HAPANA”, tena tunapaswa kuwajengea watoto wetu ujasiri wa kusema hapana. Tuwafundishe watoto wetu wasimwogope mtu yeyote yule pale ambapo wanaona ni sahihi kusema HAPANA. Kwa kufanya hivi tutakuwa tunawaandalia watoto wetu uwezo wa kujiamini na uwezo wa kujiamulia vitu vyao wenyewe bila kusukumwa na watu wengine, uwezo wa kuchukua maamuzi sahihi.

Hebu jiulize, hivi ingekuwa vipi kama siku ile ungesema “HAPANA”? Nini kingetokea kama ungekataa na kusema “HAPANA”? Ungepoteza nini kwenye maisha yako? Leo hii ungekuwa wapi ikiwa tu siku ile ungesema “HAPANA”?

Tafakari…
 
Shukran Mkuu!
Umenena kweli tupu.
Na ni Jambo zuri/inapendeza sana kuwafundisha watoto wangali wadogo naamini itawasaidia haswa kuwa na msimamo wa jambo husika .

Neno 'ninge' huja mwisho wa safari.
 
mimi huwa nakwepa sna kusema Hapana zaidi huwa natafuta namna nyingine naepuka kumuuzi mtu
 
Huo ujasiri ninao peke yangu.. Wa kukuataa mambo ya kijinga.. Kusema hapana panapostahili...
Kwa mfano: bora ufe maskini huku ukitetea wanyonge au kuishi vyema huku wanyonge wakipata taabu sana..?

Tafadhali Naomba Jibu lako.
 
mimi huwa nakwepa sna kusema Hapana zaidi huwa natafuta namna nyingine naepuka kumuuzi mtu
Lakini isiwe tabia ya kila siku,
Kuna mambo mengine lazima use me hapana ukimaanisha huku ukiwa umekunja dinta.
 
Sema HAPANA kwa Uzinzi,HAPANA kwa Ulevi,HAPANA kwa Uongo,Wizi,Rushwa,Usengenyaji,Ufitini,Majungu,Tamaa,Uvivu,Ulaghai,Kiburi,Jeuri,Uzembe,Chuki,Wivu,Dharau,Majivuno,Kebehi sema HAPANA HAPANA HAPANA...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom