Na Maggid Mjengwa,
KUNA kisa cha mwana wa gavana katika Misri ya Kale. Mwana yule alitembea akijivunia cheo cha baba yake. Akajawa kiburi kufikia siku moja kumdhalilisha mwalimu wa shule mtaani huku watu wazima na watoto wengine wakiangalia.
Ndio, mwana yule alimchapa bakora ya matakoni mwalimu yule, hadharani. Mwalimu alifedheheshwa sana, maana hata kosa lake hakulijua. Mwalimu yule akafunga safari ndefu kwenda kuarifu jambo lile kwa mfalme wa nchi . Huko akapokelewa, akaeleza yaliyomsibu.
Mfalme akaamuru mwana yule wa gavana aletwe haraka kujibu shauri akimbatana na baba yake, gavana. Baada ya kusikiliza shauri lile, mtawala yule akajiridhisha kuwa mwana yule wa gavana alifanya kosa. Akamwamuru mwalimu yule achukue bakora na kumchapa mwana yule wa gavana bakora mbili. Bakora za matakoni.
Mwalimu aliinua bakora akaanza; moja, ikaja ya pili. Akatamka; Mfalme wangu, nimemaliza. Mfalme akatamka; Bado, chukua tena bakora mchape gavana bakora tatu za matakoni.
Ewe Mfalme wangu, gavana hajanitendea kosa lolote, ni mwanawe. Alitamka mwalimu yule.
Mfalme akamwambia; Nimekwambia mchape gavana bakora tatu kwa kuwa bila ya yeye mwanawe asingetenda kosa hilo!. Na hilo ni Neno La Leo.
Maggid, Iringa
mjengwa