Boniphace Kichonge
JF-Expert Member
- Jul 31, 2017
- 1,605
- 1,957
TUME ya Taifa ya Uchaguzi nchini (NEC) imesema bado inaendelea kulifanyia kazi sakata la mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye Jimbo la Korogwe Vijijini mkoani Tanga, Timotheo Mnzava kupita bila kupingwa kwenye uchaguzi mdogo ujao. Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Dk Athumani Kihamia, alilieleza Habari- Leo jana kuwa muda ukifika, watalitolea maelezo jambo hilo, lakini kwa sasa hawezi kusema lolote kwa vile linafanyiwa kazi.
Sakata hilo la Mnzava kuwa mgombea pekee wa ubunge kwenye jimbo hilo, limekuja baada ya fomu ya mgombea huyo kuwa pekee iliyorudishwa kwa wakati katika ofisi ya Msimamizi wa Uchaguzi wa jimbo hilo saa 10 jioni Agosti 20, mwaka huu. Wagombea wengine kutoka vyama vya upinzani kikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), walidaiwa kushindwa kurejesha fomu zao ndani ya muda huo.
Wagombea walioshindwa kurejesha fomu zao kwa wakati na vyama vyao kwenye mabano ni Amina Saguti (Chadema), Abdulazizi Abdallah Mahamoud (AAFP), Josephine Mpalahingwe (DP), Shabani Karata (ACT), Nurdin Mshangama (CUF), Catherini Mpalahingwe (SAU) na Juma Gao (ADA-TADEA). Wakati Dk Kihamia akisema kuwa suala la Mnzava kupita bila kupingwa litatolewa maelezo baadaye, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Kwame Daftari, alinukuliwa na gazeti hili juzi akisema kuwa wagombea hao, wana nafasi ya kufuata ngazi za kisheria ili kuwasilisha malalamiko yao. Kwa mujibu wa Daftari, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, ilipofika saa 10 jioni ya Agosti 20, mgombea aliyekuwa amerejesha fomu alikuwa ni mmoja tu, ambaye ni Mnzava wa CCM.
HABARI LEO