Kabla sterling wa Tegeta Escrow Account Saga, Zitto Kabwe hajarudi kusambaratisha majibu ya serikali yaliyosomwa leo na Waziri wa Nishati na Madini, sospeter Muhongo.
Au kabla komando David Kafulila hajashuka na ile style yake ya kushambulia kama tumbili, hebu kwanza nami nimjibu Muhongo kwa kifupi...
Utetezi kwamba Tanesco inadaiwa sana, eti wakaona fedha za Tegeta Escrow zitolewe kwa PAP ni pumba.
HOJA: Kuchotwa kwa fedha za Tegeta Escrow, hakusaidii madeni yaliyotajwa na Muhongo kufutwa.
Yataendelea kuwepo, vilevile Tanesco itaendelea kudaiwa. Msingi wake ni kwamba zile pesa zilitolewa kwa PAP kama fedha zake stahili baada ya kughushi nyaraka za kujihalalisha umiliki wa IPTL.
Hata kama ingekuwa hivyo, wapi yalipo maandishi kuwa kuchotwa kwa fedha za Tegeta Escrow, kutasidia kuondoa madeni ambayo ameyataja? Au aliyataja kama stori ya kutapatapa?
Ukweli unabaki kuwa fedha za Tegeta Escrow ni za Watanzania. Zilichotwa kifisadi.
Utetezi kwamba waliamua fedha za Tegeta Escrow zitoke ili kujinasua na mzigo wa kuwalipa mawakili ni dhaifu sana.. tena sana!
HOJA:
Ni mtu asiyejali peke yake ndiye anaweza kuruhusu hazina ya taifa ichotwe, eti kwa sababu ya kuona mawakili wanaoitetea Tanesco dhidi ya tozo kubwa la IPTL, wanalipwa fedha nyingi. Yaani umenunua bidhaa dukani, baadaye unagundua mwenye duka alikutoza fedha nyingi kinyume na uhalisia.
Unamtuma mtu akakudaie, yule mtu anakuomba nauli. Eti kwa kujiuliza kwa nini umlipe yule mtu nauli, unaamua kumsusia fedha zote mwenye duka, wakati ilikuwa wazi kuwa mwenye duka alipaswa kurejesha fedha zote za ziada alizokutoza na fidia juu. Hoja ya pili ni kuwa kwa nini serikali haikutumia njia nyingine kuhakikisha haki ya Tanesco haipotei? Ni wazi uamuzi uliochukuliwa ni uzembe na ufisadi.
Wakati wa Bunge la Bajeti mwaka huu, Muhongo, Werema (mwanasheria mkuu wa serikali) na Pinda (waziri mkuu), kwa nyakati tofauti walisema fedha za Tegeta Escrow ni za wanahisa wa IPTL, na kwamba akaunti hiyo ilifunguliwa kutokana na mgogoro wa wabia wa IPTL.
Leo, Muhongo amekubali kuwa akaunti ya Tegeta Escrow, ilifunguliwa kutokana na Tanesco kulalamika kuwa IPTL inaitoza tozo kubwa la capacity charges. Utetezi wote wa Muhongo umeshindwa kujibu hoja kuwa fedha za Tegeta Escrow Account ni za umma, na kwamba zilichotwa kifisadi.
Hajajibu pia kwa nini katika Bunge la Bajeti, kwa kushirikiana na Werema pamoja na pinda, walilidanganya bunge na umma kuwa akaunti ya Tegeta Escrow, ilifunguliwa kutokana na mgogoro wa wabia wa IPTL?
Kuhusu Mwanasheria wa Tanesco aliyefukuzwa kazi kwa kutoa ushauri wa kuikataza serikali isimuamini Sethi (Singasinga), Muhongo ametetea, lakini hajajibu hoja ni kwa nini bodi ya Tanesco na wizara ya nishati na madini, hawakufanyia kazi ushauri ambao mwanasheria huyo alitoa kwamba uuzaji wa hisa kutoka Piper Links kwenda PAP ni magumashi kwa sababu katika mauziano, makampuni hayo mawili yaliwakilishwa na mtu mmoja ambaye ni Sethi. Kwa nini hili hawakuzingatia?
Muhongo hajajibu hoja ya Kamati ya PAC kuwa Piper Links ni kampuni hewa, usajili wake hautambuliki kwenye nchi yoyote duniani, sasa serikali iliiamini kwa ushahidi upi ikiwa ni kampuni hewa?
Muhongo hajajibu hoja kwa nini serikali iliruhusu PAP ichukue fedha za Tegeta Escrow wakati hukumu ya Jaji Utamwa haitamki popote kuwa kampuni hiyo ipewe fedha hizo? Na kwamba Jaji Utamwa aliridhia PAP ikabidhiwe mitambo ya IPTL tu. Kwa nini fedha zimetoka? Hajajibu.
Hajatoa majibu ni kwa nini PAP iliaminiwa na serikali wakati haikuwa na hati halisi za hisa 7 (asilimia 70) ambazo mmiliki wake halali ni Kampuni ya Menchmar ya Malaysia?
Muhongo hajajibu pia serikali itafanya nini endapo Menchmar wataishtaki serikali kwa kuikumbatia PAP na kuipa rasilimali zake wakati haijaiuzia hisa zake saba (asilimia 70).
Muhongo amejitetea kuwa yeye si dalali aliyeyakutanisha makampuni ya PAP na VIP. Ila hajamkana MD wa VIP, Rugemalira aliyeiambia kamati ya PAC na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu Hesabu za Serikali (CAG), kuwa Muhongo ndiye aliyewakutanisha Sethi na Rugemalira kisha kusimamia mauziano ya hisa tatu (asilimia 30) za VIP kwenda PAP.
Muhongo hajajibu ni kwa nini mtu mwenye mtaji wa shilingi milioni 500, anaweza kupewa shilingi bilioni 321 bila kuzifanyia kazi?
Hajajibu ni kwa nini PAP ililipwa fedha za Tegeta Escrow kwanza kisha ndiyo ikapata uwezo wa kununua hisa asilimia 30 za VIP?
Muhongo hajawafanya Watanzania wafunge midomo yao, maana tangu jana Ripoti ya PAC kuhusu Tegeta Escrow Account Scandal iliposomwa, wamebaki midomo wazi kwa mshangao, iweje hisa asilimia 30 zinunuliwe kwa dola milioni 75 (karibu shilingi bilioni 124) wakati hisa asilimia 70 za Menchmar, eti PAP ilizinunua kwa shilingi milioni sita tu (6,000,000)? Uwiano hapo upo wapi kama si wizi?
Muhongo akasema issue ya kukwepa kodi na kuikosesha mapato serikali katika tukio zima la uchotwaji fedha za Tegeta Escrow, eti PAP ipo, inaweza kudaiwa kodi wakati wowote na italipa.
Muhongo anajifanya hajui kama kesi ya kukwepa kodi si ya kudaiwa kodi. Ukwepaji kodi ni uhujumu uchumi na adhabu yake ni kifungo jela na hata kufilisiwa. Muhongo hajui hili? Au analeta sanaa kwenye jumba la sanaa?
Kamishna wa TRA na CAG, wamesema kwa hoja za kitaalamu na kimahesabu kama walivyohojiwa na Kamati ya PAC kuwa fedha za Tegeta Escrow Account ni za Watanzania, Muhongo anakuja na blah! Blah!
Kwa kifupi Muhongo hajajibu hoja za msingi, isipokuwa alijitahidi kuupaka sukari utetezi wake ili uwe mtamu kwa wasikilizaji lakini imeshindikana.
Ila salute kwa Muhongo; Tofauti na wanasiasa wengi ambao wanaposhambuliwa au kubanwa kwa hoja hupaniki, hupayuka na hata hutukana, Muhongo ni tofauti sana, ana uwezo mkubwa wa kujieleza bila jazba, tena kwa utulivu. Ndiyo maana mara nyingi huko nyuma, wabunge waligeuka mashabiki wake, hata pale alipodanganya au kukashifu wenzake kwa sababu ya kipawa hicho alichojaliwa. Huongea kwa upole na ni rahisi kuteka wasikilizaji kuamini na kushangilia kila anachokisema.
Hata leo, wabunge licha ya kumzomea mara nyingi, alikuwa imara kuzungumza. Hiki hasa ni kipaji cha Muhongo.
By Luqman Maloto (The Gladiator)