Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,482
Ahmed Rajab Raiamwema
KUNAFUKUTA chini kwa chini Zanzibar na wakuu wa serikali pamoja na wanasiasa wasipochukua hadhari tunaweza tukashuhudia marejeo ya matumizi ya nguvu, ugandamizaji wa wapinzani na ghasia kwa jumla.
Kwa ufupi, mafanikio yote yaliyopatikana tangu Oktoba 2010, hasa utulivu wa hali ya kisiasa, yanaweza yakenda arijojo.
Wiki iliyopita Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idi, akiwa Dodoma, alinukuriwa akisema kwamba "ametangaza vita kwa mtu yeyote anayepanga njama za kuvuruga mchakato wa Rasimu ya Pili ya Katiba".
Wakati huohuo alimkebehi Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa chama cha Civic United Front (CUF).
Siku chache kabla ya Balozi Idi kutoa hayo matamshi yake ya "kutangaza vita" Hamad alikariri tena msimamo wa chama chake kuhusu muundo wa Muungano. Akihutubia mkutano wa hadhara huko Kibandamaiti, Unguja, Machi 26, alisema kwamba chama chake hakitounga mkono muundo wa Muungano wa Serikali mbili na wala hotuba aliyoitoa Rais Jakaya Kikwete katika ufunguzi wa Bunge la Katiba.
Balozi Idi alinukuliwa akisema kwamba hali ikiendelea hivyo - yaani ikiwa Hamad ataendelea kudai pawepo Muungano wa Serikali tatu - basi Serikali ya Mapinduzi haitasita "kuwashughulikia" watu wote wa aina hiyo.
"Kuwashughulikia" maana yake ni kuwachukulia hatua zisizopendeza kama vile kuwatia ndani, kuwatesa au kuwafanyia mambo mengine ya kukirihisha.
Inasikitisha kusikia kwamba mtu mwenye hadhi kama ya Balozi Idi anatumia lugha kama hiyo ya vitisho wakati wa mjadala kuhusu Katiba mpya. Na huyu ni mwanadiplomasia wa siku nyingi mwenye uzoefu wa miaka mingi wa jinsi mambo yalivyo duniani. Anachotuambia ni kwamba ni sawa yeye kuutetea muundo wa Muungano wa serikali mbili lakini wenye kutaka muundo wa Muungano wa serikali tatu hawana haki ya kufanya hivyo. Ni wasaliti wanaostahiki "kushughulikiwa".
Matamshi kama hayo huashiria kwamba mwenye kuyatamka ana nia ya kuwadhuru watu wengine. Mamlaka nyingi za kisheria huviona vitisho aina hiyo kuwa ni vitendo vyenye kuhalifu sheria. Na wenye kutoa vitisho vya aina hiyo wanaweza wakafikishwa mbele ya mahakama na kushtakiwa kwa makosa ya jinai.
Wakuu wanapokuwa wanatoa vitisho vya aina hiyo huwa wanaamini kwamba lazima watumie vitisho na mabavu (utumizi wa nguvu) kuwatia hofu wananchi ili hao wananchi wasalimu amri na wakubali yale serikali inayoyataka.
Utumiaji wa nguvu na vitisho ni miongoni mwa mbinu zinazotumiwa kuwashurutisha watu, hasa wapinzani, wafuate msimamo au sera za serikali. Mbinu aina hizo hutumiwa sana na serikali katika nchi zenye mfumo wa demokrasia isiyopevuka. Mfano mzuri ni hapa kwetu.
Vitisho aina hiyo vinaweza hatimaye vikawa sababu ya kuzuka kwa mauaji ya kimbari, kukamatwa watu wasio na hatia kwa sababu za kisiasa, kutekwa nyara kwa wapinzani na baadaye kupotea wasijulikane walipo na mauaji ya wapinzani.
Tukiangalia historia ya hivi karibuni ya nchi kadhaa zenye mfumo wa demokrasia isiyopevuka tunaona kwamba viongozi wa serikali wenye midomo mirefu ya kutoa vitisho dhidi ya wapinzani, aghalabu, huwa ni viongozi walio dhaifu.
Viongozi hao huwa na tabia ya kuzidi kutoa vitisho vikali pale wanapohisi kwamba madaraka huenda yakawaponyoka, kwamba tawala zao zinayumbayumba na kwamba wapinzani wanaweza wakakishinda chama kinachotawala katika uchaguzi.
Kushindwa kwa serikali kuyaridhia matakwa ya wananchi wake mara nyingi husababisha mfumo wa kisiasa katika nchi uoze. Kuoza huko ndiko kunakowafanya watawala wakimbilie kutumia nguvu dhidi ya wapinzani ili kuunusuru utawala wao.
Kwa kweli nchi kama zetu zenye demokrasia isiyo imara zimo hatarini kwani serikali zao hazioni ajizi kuwagandamiza wapinzani kwa vile zinawaona wapinzani kuwa ni kitisho kwa madaraka yao. Kwa hivyo, viongozi wao nao hutumia vitisho vya nguvu za dola dhidi ya wapinzani. Hali huzidi kuwa mbaya pale wapinzani wanapokuwa wanatoa madai yenye kuungwa mkono na wengi wa wananchi lakini yenye kwenda kinyume na sera za chama kinachotawala.
Mfano mzuri ni huu tunaouona sasa Zanzibar ambako, kwa mujibu wa Tume ya Katiba, wananchi wengi hawautaki Muungano wa serikali mbili.
Kila pengo linapokuwa kubwa baina ya madai ya wapinzani na msimamo wa chama kinachotawala basi huwa ni vigumu kwa pande hizo mbili kuridhiana. Na madai au matakwa ya wapinzani yanapokuwa yanaungwa mkono na wengi wa wananchi basi hapo kunakuwa hatari ya kuzuka hali ya kisiasa isiyo thabiti na uwezekano mkubwa wa serikali kuanza kuwakandamiza wapinzani, na wakati mwingine, hata wasio wapinzani.
Hali inakuwa hivyo katika nchi zenye mfumo wa kidemokrasia isiyokamilika kwa sababu taasisi za dola, kwa mfano, mahakama au jeshi la polisi, zinakuwa hazina nguvu au uwezo wa kujiamulia mambo yao bila ya kuingiliwa na wakuu wa serikali. Ndiyo maana baada ya Balozi Idi kutoa matamshi yake ya vitisho tumesikia ya kuwa Jeshi la Polisi la Zanzibar limeanza uchunguzi wa kukichungua kikundi kinachojiita ‘Gaza' kinachosemekana kwamba kimewatahadharisha wajumbe wa Bunge la Katiba kutoka Zanzibar wasirudi kwao endapo wataisaliti Zanzibar kwa kukubaliana na muundo wa Muungano wa Serikali mbili.
Kamishna wa Polisi wa Zanzibar, Hamdan Omar Makame, ananukuriwa akisema kwamba tayari jeshi lake limekwishaanza kazi ya kuzipitia kanda za video za maandamano yaliyofanywa na kikundi hicho katika mitaa kadhaa Unguja hadi kwenye ule mkutano wa hadhara wa CUF huko Kibandamaiti. Dhamiri ya uchunguzi huo, alisema, ni kukichukulia hatua za kisheria kikundi hicho.
Shtuma zilizotolewa ni kwamba kikundi hicho kilibeba bango lililokuwa na hayo maandishi ya kuwataka Wabunge wa Katiba kutoka Zanzibar wataokubali muundo wa Serikali mbili wasirudi Zanzibar. Inasemekana kwamba bango hilo lilitembezwa mitaani na halafu likapokewa na Maalim Seif Sharif Hamad, aliyekuwa mgeni rasmi katika mkutano huo.
Kamishna Hamdan amesema kwamba ameagiza matamshi yote ya mkutano yapitiwe "ili kuangalia makosa ya jinai yaliyotendeka kabla ya kuchukua hatua za kisheria."
Kwa matamshi yake Kamishna Hamdan alikwishaamua kwamba makosa ya jinai yalitendeka hata kabla ya uchunguzi kumalizika.Tuseme Kamishna anajipendekeza kwa serikali au anatii tu amri ya wakuu fulani wa serikali tunayoambiwa kuwa ni Serikali ya Umoja wa Taifa?
Polisi ya Zanzibar haina historia nzuri. Huu ni ukweli usiofichika. Ukatili wa polisi dhidi ya wapinzani wa serikali unajulikana na jumuiya zote za kimataifa zenye kupigania haki za binadamu, zikiwa pamoja na Amnesty International na Human Rights Watch.
Ripoti mbalimbali za mashirika kama hayo pamoja na ripoti za wizara ya mambo ya nje ya Marekani kuhusu haki za binadamu Tanzania zimetaja jinsi jeshi hilo la polisi lilivyokiuka haki za binadamu katika nyakati mbalimbali, hasa tangu kurejelewa nchini kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.
Ni dhahiri kutokana na mambo yanavyokwenda Zanzibar hivi sasa kwamba Maalim Seif Sharif Hamad na wafuasi wake wanategewa mitego iwanase. Majaribio yalifanywa na yanaendelea kufanywa ya kukihusisha chama chake na ugaidi wa kimataifa lakini majaribio hayo yameshindwa nguvu kwa kukosekana ushahidi. Jaribio la sasa ni la kukifunganisha chama cha CUF na hicho kikundi cha Gaza.
La kushangaza ni kwamba hao vijana wa kikundi cha Gaza wanachunguzwa na polisi harakaharaka wakati viongozi fulani wa CCM wamekuwa wakipanda kwenye majukwaa wakiwatukana wapinzani wao kwa matusi yenye kashfa tupu na hawakuchukuliwa hatua zozote, si za kisheria au hata za kukemewa na viongozi wakuu wa chama chao si huko Zanzibar wala si Dodoma.
Wakereketwa wenginewa CCM wamekuwa wakisema wazi kwamba Wapemba waondoke Unguja na warudi kwao Pemba, wakisahau kama Rais Ali Mohamed Shein na wakereketwa kadhaa wengine wa CCM nao ni Wapemba.
Hao wanaotaka Wapemba wafukuzwe Unguja nao pia hawakuchunguzwa wala kukemewa na viongozi wakuu wa CCM. Wala polisi hawakuwachukulia hatua yoyote ilhali matamshi kama hayo yanaweza kusababisha mfarakano mkubwa katika jamii na hata mauaji ya kimbari.
Huu sio tena wakati wa kutishana. Wala si wakati wa viongozi wa serikali kujaribu kuzipima nguvu zao. Kiongozi yeyote yule anayefanya hivyo anakuwa kama mtu anayekikabili kioo akiwa amefunga macho eti ili aweze kujiona anakuwaje anapolala.
Chanzo: Raia mwema