Muswada wa Katiba una matatizo mengi - Zitto

nice 2

JF-Expert Member
Aug 10, 2011
747
520
'Nimeona niwashirikishe wanaJF makala hii ya ndugu Zitto Kabwe kuhusu Katiba ambayo itatoka kesho katika magazeti na ameisambaza kwa wadau mbalimbali nikiwemo mimi'


Muswada wa Marekebisho ya Katiba ujenge Mwafaka wa Kitaifa

Zitto Kabwe, Mb

Kama kuna jambo moja ambalo huunganisha Taifa ni Katiba ya Taifa hilo. Katiba huweka misingi mikuu ya nchi na namna ya kujenga na kuendesha Taifa. Hivyo Katiba inapaswa kuwa ni matokeo ya mwafaka wa kitaifa kwenye masuala yote ya msingi ya nchi husika. Tanzania imekuwa ikiongozwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kabla ya hapo kulikuwa na Katiba ya Uhuru ambayo ilitokana na Mwafaka wa wapigania Uhuru wa nchi yetu, baadaye Katiba ya Jamhuri ya Tangayika na kisha Katiba ya muda ya Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kabla ya kubadili jina na kuitwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ukiachana na Katiba ya Uhuru, Katiba nyingine zote hazikutokana na mwafaka wa kitaifa bali matakwa ya tabaka la watawala. Katiba ya kudumu ya mwaka 1977 ni zao dhahiri kabisa la utawala wa chama kimoja ambacho kilikuwa na dhamira ya kushika hatamu za uongozi. Kutokana na hali hii haikuchukua muda kwa wasomi mnamo mwaka 1983 kuanza harakati za kuifanyia mabadiliko makubwa. Mabadiliko hayo yalizaa kuwemo kwa Haki za Msingi za Binaadamu katika Katiba katika mabadiliko ya mwaka 1984, miaka saba tu toka kuandikwa kwa Katiba ya kudumu.

Takribani mwaka mzima huu kumekuwa na madai ya kuandikwa kwa Katiba mpya. Madai haya sio mapya kwani huibuka na kusinyaa kila baada ya uchaguzi Mkuu. Itakumbukwa kwamba miaka ya Tisini mwishoni kundi la vyama vya siasa liliunda Kamati ya Mabadiliko ya Katiba (KAMAKA) ili kudai kuandikwa kwa Katiba mpya. Hata hivyo safari hii sauti ya mabadiliko imekuwa ni kubwa sana kiasi cha Serikali kusikia na hivyo kupeleka Bungeni muswada wa Marejeo ya Katiba kwa lengo la kuandika Katiba mpya ya nchi yetu. Muswada huu umeleta kelele nyingi na manung'uniko mengi sana kutoka kwa makundi mbalimbali ya jamii kuanzia vyama vya siasa, viongozi wa dini na Asasi za Kijamii. Baadhi ya Asasi za Kijamii zimeunda Jukwaa la Katiba ili kuweza kuratibu vizuri juhudi za kuandikwa kwa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sababu kubwa ya kupingwa kwa muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 ni kwamba mchakato umewekwa kwenye Dola mno na hasa kwenye Urais. Rais anateua Tume ya kukusanya maoni, Rais anateua Bunge la Katiba nk. Watu wengi tungependa kuona mchakato unakuwa kwa wananchi zaidi. Serikali imefanya marekebisho kadhaa na kupanua wigo wa mjadala wa Katiba na pia kumhusisha kikamilifu Rais wa Zanzibar katika mchakato.

Baadhi yetu tunaona kama nafasi ya Zanzibar katika mchakato imepewa nguvu kubwa kupita kiasi. Ninadhani Zanzibar inastahili kupata nafasi hii katika mchakato wa Katiba. Jambo ambalo ni vizuri tulitilie maanani ni kwamba Muungano wa Mwaka 1964 ulihusisha nchi mbili huru zenye hadhi sawa mbele ya sheria za kimataifa. Linapokuja suala la kuandika Katiba ya Muungano, pande mbili za Muungano zinakuwa na hadhi sawasawa. Kwamba Zanzibar ishiriki kwenye masuala ya Muungano tu ni hoja inayojadilika iwapo tu Katiba ya Muungano ingetofautisha kinagaubaga taasisi za kimuungano na zisizo. Kwa mfano Sura ya Bunge katika Katiba ni lazima ijadiliwe na pande zote mbili ingawa Bunge wakati mwingine hupitisha miswaada ambayo sio ya masuala ya Muungano. Aina ya Muungano wetu inatulazimisha kufanya hivi tunavyofanya sasa. Mkataba wa Muungano ni lazima uheshimiwe kama ulivyo sasa.
Katiba mpya yaweza kuweka makubaliano mapya lakini muswada wa sasa ni lazima utambue nafasi halali ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya sasa na Hati za Muugano. Suala hili ni suala la kisheria na sio suala la idadi ya watu au ukubwa wa eneo la nchi husika. Nchi ya Ushelisheli yenye watu 80,000 ina nafasi sawa na Tanzania yenye watu 42 milioni katika SADC, AU na UNO. Zote zina kura moja tu. Huu ndio ukweli na hatuna budi kukubaliana nao.

Muswada unampa mamlaka Rais wa Tanzania na Rais wa Zanzibar kuteua Tume ya Katiba. Tume hii maRais hawatapata ushauri wa mtu mwingine yeyote kwa mujibu wa kifungu cha (6) na vifungu vidogo (1), (2) na (3). Wanasiasa wakiwemo Wabunge, Wawakilishi, viongozi wa vyama wa Ngazi za Taifa, Mkoa au Wilaya hawatakuwa na sifa za kuteuliwa.
Inawezekana kabisa waandishi wa muswada walikuwa na mantiki ya kuuondoa mchakato kwenye mikono ya wanasiasa. Nia hii njema haikufikiriwa vizuri hata kidogo. Njia hii haijengi mwafaka. Tume hii sio ya Wataalamu, ni Tume inayopaswa kuwa na sura ya kitaifa. Nafasi ya wanasiasa katika mchakato wa kukusanya maoni ni muhimu sana katika kuhalalisha mchakato wenyewe. Tume lazima ionekane ni Tume ya Taifa na sio Tume ya maRais. Hivyo kipengele hiki cha kuwanyima sifa wanasiasa kinapaswa kufutwa katika muswada. Wabunge na Wawakilishi kwa kuwa ni sehemu ya Bunge la Katiba wasiwemo katika Tume, lakini viongozi wengine wa kisiasa wawe na haki ya kuteuliwa kuwa wajumbe.

Lakini pia Rais ateue Tume kutokana na maoni kutoka katika makundi yenye maslahi ya karibu na Katiba ya nchi na hivi ni vyama vya siasa. Ninapendekeza kwamba katika Wajumbe 30 wa Tume ya kukusanya maoni ya Katiba, 10 watokane na vyama vya siasa vyenye Wabunge kwa uwiano wa CCM 2, CHADEMA 2, CUF 2, NCCR 2, TLP 1 na UDP 1. Kila chama cha siasa chenye Wabunge kupitia kiongozi wake Bungeni kipeleke majina ya watu wanaowapendekeza kuwa katika Tume ya Katiba na kutokana na Mapendekezo hayo Rais atawateua kuwa wajumbe. Masharti mengine ya nusu kutoka kila upande wa Muungano yazingatiwe.

Muswada unapendekeza kuwepo kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Kifungu cha cha 7 kifungu kidogo (1), (2) na (3) kinaweka utaratibu wa kupatikana kwa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Tume. Muswada unasema UTEUZI wa Mwenyekiti na Makamu utazingatia kwamba mmoja atoke uapnde mmoja wa Muungano na mwingine upande wa Pili wa Muungano. Ingawa Muswada hausemi waziwazi lakini ni dhahiri kwamba Mwenyekiti wa Tume atateuliwa na Rais baada ya kushauriana na kukubaliana na Rais wa Zanzibar. Sitaki kujenga hoja kwamba Mwenyekiti na Makamu wachaguliwe na wajumbe wa Tume kutoka miongoni mwao lakini ni dhahiri Mwenyekiti wa Tume anapaswa kuwa mtu mwenye heshima kubwa hapa nchini. Ningependekeza kwamba maRais wateue Wenyeviti wenza badala ya Mwenyekiti na Makamu wake ili kuweka nafasi sawa kwa pande mbili za Muungano. Hapa nchini tunao Watanzania ambao wamefanya kazi iliyotukuka katika nyadhifa mbalimbali na sasa ni wastaafu wasio na nia yeyote ya madaraka ya kisiasa wanaoweza kuongoza vizuri kabisa Tume hii. Ni pendekezo langu kwamba Dkt. Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Sinde Warioba wawe wenyeviti wenza wa Tume ya Katiba. Uzoefu wao katika uongozi na kuijua kwao nchi kutasaidia sana kuhakikisha kwamba mchakato wa kukusanya maoni na kisha kuandika Katiba unakuwa na mafanikio kwa kuzingatia misingi ya Taifa letu.

Muswada unapendekeza kwamba Hadidu rejea za Tume zitolewe na maRais. Kifungu cha nane na muswada kuhusu hadidu rejea nadhani hakina mantiki sana. Madhumuni ya muswada yanasema pamoja na mambo mengine muswada unaweka masharti kuhusu Hadidu rejea za Tume. Wakati huo huo muswada unasema Hadidu rejea zitakuwa ni hati ya kisheria itakayozingatiwa na Tume katika kazi zake.
Mantiki ni kwamba Hadidu rejea zinapaswa kuwa sehemu ya Muswada kama ‘schedule' ili kuzipa nguvu ya kisheria badala ya tangazo katika gazeti la Serikali. Hadidu rejea zikiwa ni sehemu ya Muswada zitajadiliwa na Bunge na kupitishwa hivyo kuwa ni jambo ambalo limefikiwa kwa mwafaka wa wawakilishi wa wananchi.

Muswada katika kifungu cha 22 unazungumzia kuhusu Katibu wa Bunge la kutunga Katiba. Muswada unatamka kwamba Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano na Katibu wa Baraza la Wawakilishi mmoja atakuwa Katibu wa Bunge la kutunga Katiba na Mwingine atakuwa Naibu wake kutokana na kwamba Spika wa Bunge atakuwa anatoka upande gani Muungano. Sharti hili halina maana yeyote na limewekwa katika Muswada kufurahisha tu upande fulani wa Muungano. SekretariatI ya Bunge la kutunga Katiba sio chombo cha Maamuzi, ni chombo cha kutunza kumbukumbu tu za Bunge la kutunga Katiba. Sekretariati sio chombo cha kisiasa bali ni chombo cha kitaalamu hivyo kukiwekea masharti ya kisiasa ni makosa makubwa sana. Inatosha kwamba Spika wa Baraza la kutunga Katiba akiwa anatoka Zanzibar Naibu wake atoke Bara. Muswada utamke tu kwamba Sekretariati ya Bunge la Muungano itakuwa ndio sekretariati ya Bunge la Kutunga Katiba na kwamba Katibu wa Bunge la Muungano atakuwa Katibu wa Bunge la kutunga Katiba. Kama kuna haja ya kuwa na Naibu wa Katibu wa Bunge la Katiba, basi Rais kwa kushirikiana na Rais wa Zanzibar aweza kumteua Katibu wa Baraza la Wawakilishi kuwa Naibu huyo. Pia katika utendaji wa Kazi za sekretariati, Bunge la kutunga Katiba litazingatia kuwatumia watumishi wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar katika sekretariati yake. Muswada usithubutu hata kidogo kulifanya Bunge la Jamhuri ya Muungano ni sawa na Baraza la Wawakilishi Zanzibar. Hiki ni chombo za Muungano chenye wajumbe kutoka pande zote za Muungano na Ofisi pia pande zote za Muungano na ndicho chombo pekee chenye uwezo na rasilimali za kuweza kuwa sekretariati ya Bunge la kutunga Katiba. Huu ndio ukweli na hakuna haja ya kuridhishana katika jambo la kitaalamu kama hili.

Muswada unataka uamuzi wa kura ya maoni kuhusu Katiba uwe ni kukubaliwa na nusu ya Watanzania katika kila upande wa Muungano. Nadhani hapa tunacheza na Katiba ya nchi. Katiba ya nchi inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura wa pande zote za Muungano yaani kila upande theluthi mbili. Hii itaipa Katiba ‘legitimacy' na hivyo kuheshimiwa na wananchi na watawala. Kuna woga gani uliopo kutaka katika ikubalike na nusu ya wapiga kura? Mifano ya nchi nyingi duniani Katiba inapaswa kukubaliwa na theluthi mbili ya wapiga kura. Hata jirani zetu wa Kenya ilikuwa hivyo na hata kura ya maoni kuhusu mwafaka huko Zanzibar ilikuwa hivyo. Kwa kuwa Katiba ni chombo cha mwafaka wa kitaifa, muswada utamke kwamba Katiba mpya itakuwa imepita iwapo theluthi mbili ya wapiga kura watapiga kura ya ndio.

mwisho
 
Asante Nice2.
Kwanza, Mh: yu buheri wa afya? Bila shaka anaendelea vema. Apone arudi kuendeleza harakati za ukombozi wa Tz.

Pili, hii hoja ya Katiba Mpya kwa sasa ni ya kisiasa zaidi and it doom to failure. Sasa wakati ukifika (kuwa sasa imeshindikana kupata katiba kwa matakwa ya wananchi wote wa Tz) unafikiri njia gani zitumike na kwa nini?
 
Lakini pia Rais ateue Tume kutokana na maoni kutoka katika makundi yenye maslahi ya karibu na Katiba ya nchi na hivi ni vyama vya siasa. Ninapendekeza kwamba katika Wajumbe 30 wa Tume ya kukusanya maoni ya Katiba, 10 watokane na vyama vya siasa vyenye Wabunge kwa uwiano wa CCM 2, CHADEMA 2, CUF 2, NCCR 2, TLP 1 na UDP 1. Kila chama cha siasa chenye Wabunge kupitia kiongozi wake Bungeni kipeleke majina ya watu wanaowapendekeza kuwa katika Tume ya Katiba na kutokana na Mapendekezo hayo Rais atawateua kuwa wajumbe. Masharti mengine ya nusu kutoka kila upande wa Muungano yazingatiwe.

.

mwisho

sijajua vigezo gani vimetumika kupata idadi hii, na kwanini tutenge vyama visivyo na wabunge kwa kudhani katiba ni mali ya vyama vyenye wabunge. nadhani hatutatenda haki kwa vyama vingine visivyo na wabunge
 
Zitto thinks miles of you, licha ya ugonjwa amekaa chini na kujadili katiba na kuweka hoja za kuboresha muswada, Mwanahalisi na JF wanajadili NCCR!
 
Hapo kwa Jaji Sinde Warioba hapana. Kuna majaji wenye kuheshimika kama jaji mstaafu Robert Kisanga anaweza kutusaidia kuliko Warioba.
 
Zitto, ungetulia kwanza ukapona, umefanyiwa operation ya kichwa kwa nini usitulie kwanza?
Hii nchi wako watu wazuri wengi hakitaharibika kitu usipocomment.
Tunakutakia mema upone ila kwa sasa pumzika ndg.
 
Nilikuwa mwanzoni nimepuza haya yaliyo andikwa kwa kuona ni mtu yuleyule anayetumiwa na watu walewale.

Lakini huu mswada wa katiba ulivyo letwa unamakosa mengi tu, ni kama tunalazimishwa, chama kwa kutumia mwenyekiti wake ambaye ni rais kinaendelea kushika hatamu katika kutupatia katiba mpya.

Sio kweli kuwa katiba ya wakati wa uhuru inatofauti yeyote ya maana na katiba ya mwaka 77, walioindaa ya wakati wa uhuru ndio walikuwa na madaraka na sauti katika kuiandaaya mwaka 77.

Hao tunao shawishiwa hapa tuwakubali ndio wawa wajumbe na viongozi katika kusimamia uundwaji wa katiba mpya ni kwamba kwa sehemu kubwa watatumika kutetetea maslahi ya watawala wetu wa sasa. Kwa mfano mtu anaesema vyama vya siasa kama cdm, tlp,nk watoe wawakilishi 2wa2,hebu jaribu kufikiri kidogo tu kati ya hao wawili kwa kila chama itokee awepo mrema. shibuda, cheyo, na sasa zitto (kumbuka hawa wanaushawishi na lobbing kubwa tu ktk vyama vyao) unategemea ni maslahi ya nani yatakayo tetewa kwenye hiyo katiba mpya.


Tunatakiwa tutafute utaratibu wa kupata katiba mpya ambayo itatokana na matakwa na kusimamiwa na wananchi wenyewe sio huu mchakato wa sasa ambao unamfanya rais kama mhusika mkuu wa kuwapatia wananchi katiba mpya inayo wakilisha matwaka ya watawala. Zitto unatumiwa kwa mengi hatutapenda uendelee kutumiwa tukielewa hivyo, tena tukanyamaza.
 
mawazo ni mazuri ila ushauri wangu ama maoni yangu ni vikundi vilivyoanza tayari mchakato wa maoni kama vya akina Deus Kibamba visiachwe nyuma hata hao wanasheria wakongwe watakapowekwa..
 
Zitto, tatizo lake huwa anaandikiwa vitu na kuviweka kama vya kwake ,

Huyu mzee wetu Salim ana uzoefu gani katika katiba ? bora hata ungesema watu kama wakina Shivji, Khamis Bakary , Jaji Ramadhan Agustino, Jaji Jandu na wengineo na sio huyu mzee ambaye wewe na yeye mlitengeneza kamtandao kenu ka kumuingiza Ikulu kakafeli.....

Warioba , huyu ana lipi jipya? Huyu naye ni fisadi kwenye Mwananchi Gold na kule BOT mpaka sasa huyu hana udhu. Mbona kuna watu wenye heshima zao wengi tuu kama wakina Jaji Kisanga, Jaji Samata, Jaji Kipenka na wengineo wengi tuu ? Huyu abaki kwenye kundi la wanansiasa naye akatoe maoni kama wengine wanavyofanya.

Kuhusu ZNZ kuwa na idadi sawa ya wajumbe , this is cheap politics your playing .........hoja yako hapo ni kutaka kuungwa mkono na wazanzibari ili upingane na mawazo ya Lissu? na hapo ndipo naona kuwa Warioba kakutuma kwani kwenye kamati siku hiyo nilikuwepo na hojua za Lissu zilikuwa nzito sana kiasi cha Warioba kukosa majibu ya kiina so usikubali kutumiwa its better ukawa kimya kwenye suala controversial.

This is my advice to you.
 
Zitto kumtaja Warioba unatuhuzunisha, ni huyu mzee juzi kaibuka toka mafichoni anadai ni haki DOWNS kulipwa amenisikitisha sana huyu mheshimiwa na watanzania wenzangu.Huyu ameamua kutoka kifisadi huwezi kulipa DOWNS ambayo haina mwenyewe, tunamlipa nani.Zito bora Sema Jaji Kisanga na angalu Mvungi wa UDSM
 
zITTO inavyoonekana si mgonjwa ana shughuli zake India, Haiwezekani kwa mgonjwa anayehitaji total bed rest anaibukia tena kwenye mitandao kujadili mambo mazito kama haya.STRESS anazidhibiti vipi??? tena bado hata discharge hospital haijatoka na bado uko chini ya uangalizi wa nurses and dr.
Ni vema waangalizi wamdhibiti huu kijana isije kuwa ni symptoms za kuchanganyikiwa.
 
Zitto kumtaja Warioba unatuhuzunisha, ni huyu mzee juzi kaibuka toka mafichoni anadai ni haki DOWNS kulipwa amenisikitisha sana huyu mheshimiwa na watanzania wenzangu.Huyu ameamua kutoka kifisadi huwezi kulipa DOWNS ambayo haina mwenyewe, tunamlipa nani.Zito bora Sema Jaji Kisanga na angalu Mvungi wa UDSM

Katika nyakati na sehemu tofauti zitto kama ilivyo jaji warioba walitetea dowans ilipwe malipo yake kwa hoja za kawaida tu. Sasa zitto anamtaja warioba kwa kupendekeza ati awe ni mmoja wa viongozi katika baraza la kutupatia wananchi katiba mpya. Nawanaomba wananchi hasa mnaopinga wizi na uonevyu wa watawala wetu mafisadi mtie akili wapi tunapelekwa katika hiki tunachokiita mchakato wa kupata katiba mpya. Tuukataie huu ulaghai kwa nguvu zetu zote.
 
Zito kwa uzoefu wako na exposure uliyonayo unatakiwa kushauri namna kupata ushiriki mpana zaidi wa wananchi juu ya uundwaji wa katiba mpya!! hapa Zitto umekuwa mbinafsi, mawazo yako yamekuwa conclusive! una tabia ya ubinafsi ingawa wewe ni kiongozi mzuri, jirekebishe ktk hilo kaka. Tunahitaji ushirikishwaji wa vyombo vyote vinavyowakilisha wananchi na sio vyombo na taasisi za serikali, HUO MUSWADA HAUFAI NA TUTAUKATAA KWA NGUVU ZOTE!!!!!!!!!!!!
 
Back
Top Bottom